Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kumkaribia “Msikiaji wa Sala”

Jinsi ya Kumkaribia “Msikiaji wa Sala”

Jinsi ya Kumkaribia “Msikiaji wa Sala”

“Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.”—ZABURI 65:2.

1. Ni jambo gani linalowatofautisha wanadamu na viumbe wengine walio duniani, na hilo linatuwezesha kufurahia pendeleo gani?

KATI ya maelfu ya viumbe walio duniani, ni wanadamu tu wanaoweza kumwabudu Muumba. Ni wanadamu tu wanaotambua kuwa wana uhitaji wa kiroho na kwamba wanahitaji kuutosheleza. Hilo linatuwezesha kufurahia pendeleo zuri la kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Baba yetu wa mbinguni.

2. Dhambi iliathirije sana uhusiano wa mwanadamu pamoja na Muumba wake?

2 Mungu alimuumba mwanadamu akiwa na uwezo wa kumkaribia Mtengenezaji wake. Adamu na Hawa waliumbwa bila dhambi. Hivyo, wangeweza kumkaribia Mungu kwa uhuru kama vile mtoto anavyomkaribia baba yake. Hata hivyo, walipoteza pendeleo hilo zuri walipofanya dhambi. Kwa sababu Adamu na Hawa hawakumtii Mungu, uhusiano wao wa karibu pamoja naye uliharibika. (Mwanzo 3:8-13, 17-24) Je, hilo linamaanisha kwamba wazao wa Adamu wasio wakamilifu hawawezi tena kuwasiliana na Mungu? Hapana, bado Yehova anawaruhusu wamkaribie maadamu wanatimiza matakwa fulani. Hayo ni matakwa gani?

Matakwa ya Kumkaribia Mungu

3. Wanadamu wenye dhambi wanapaswa kumkaribiaje Mungu, na ni mfano gani unaoonyesha jambo hilo?

3 Tukio fulani lililowahusu wana wawili wa Adamu linatusaidia kuona mambo ambayo Mungu anataka yatimizwe na mwanadamu asiye mkamilifu ambaye angependa kumkaribia. Kaini na Abeli walijaribu kumkaribia Mungu kwa kumtolea dhabihu. Toleo la Abeli lilikubaliwa, lakini la Kaini likakataliwa. (Mwanzo 4:3-5) Tofauti ilikuwa nini? Andiko la Waebrania 11:4 linasema hivi: “Kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini, imani ambayo kupitia hiyo alitolewa ushahidi kwamba yeye alikuwa mwadilifu.” Hivyo, ni wazi kwamba imani ni takwa la kumkaribia Mungu. Takwa lingine linaonyeshwa katika maneno ambayo Yehova alimwambia Kaini: “Ukigeuka utende mema, je, hutainuliwa?” Naam, Kaini angekubaliwa amkaribie Mungu ikiwa angegeuka na kutenda mema. Hata hivyo, Kaini alikataa shauri la Mungu, akamuua Abeli, na mwishowe akawa mtu aliyetengwa na jamii. (Mwanzo 4:7-12) Hivyo, mapema katika historia ya mwanadamu, ilikaziwa kwamba ni muhimu kumkaribia Mungu kwa imani na matendo mema.

4. Tunapaswa kutambua nini kuhusu kumkaribia Mungu?

4 Ikiwa tunataka kumkaribia Mungu, ni muhimu tutambue kwamba sisi ni watenda-dhambi. Wanadamu wote wana dhambi, na dhambi ni kizuizi cha kumkaribia Mungu. Nabii Yeremia aliandika hivi kuhusu taifa la Israeli: “Sisi wenyewe tumekosa . . . Umeweka kizuizi cha wingu kubwa usiweze kufikiwa, ili sala isiweze kupenya.” (Maombolezo 3:42, 44) Hata hivyo, katika historia yote ya wanadamu, Mungu ameonyesha kwamba yuko tayari kukubali sala za watu wanaomkaribia kwa imani wakiwa na nia nzuri na ambao wanashika amri zake. (Zaburi 119:145) Baadhi ya watu hao ni akina nani, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na sala zao?

5, 6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Abrahamu alivyomkaribia Mungu?

5 Mmoja wao ni Abrahamu. Mungu alikubali Abrahamu amkaribie, kwa kuwa Mungu alimwita “rafiki yangu.” (Isaya 41:8) Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Abrahamu alivyomkaribia Mungu? Mzee huyo mwaminifu alimuuliza Yehova kuhusu mrithi, akisema: “Utanipa nini, kwa sababu mimi naenda zangu bila mtoto?” (Mwanzo 15:2, 3; 17:18) Pindi nyingine, Abrahamu alitaka kujua ikiwa watu fulani wangeokolewa wakati ambapo Mungu angeleta hukumu dhidi ya waovu waliokuwa huko Sodoma na Gomora. (Mwanzo 18:23-33) Isitoshe, Abrahamu aliomba dua kwa ajili ya watu wengine. (Mwanzo 20:7, 17) Na, kama ilivyokuwa katika kisa cha Abeli, nyakati nyingine Abrahamu alimkaribia Mungu kwa kumtolea dhabihu.—Mwanzo 22:9-14.

6 Katika pindi zote hizo, Abrahamu aliongea na Yehova kwa uhuru. Lakini ingawa alikuwa na uhuru wa kusema, alitambua kwa unyenyekevu hali yake mbele za Muumba wake. Ona jinsi alivyoongea kwa heshima, kama inavyoonyeshwa katika Mwanzo 18:27: “Tafadhali, tazama nimejiamulia kusema na Yehova, hali mimi ni mavumbi na majivu.” Huo ni mtazamo mzuri kama nini!

7. Wazee wa ukoo walisali kwa Yehova kuhusu mambo gani?

7 Wazee wa ukoo walisali kuhusu mambo mbalimbali, na Yehova aliwasikia. Yakobo aliweka nadhiri kupitia sala. Baada ya kumwomba Mungu amtegemeze, Yakobo alitoa ahadi hii nzito: “Katika kila kitu utakachonipa bila shaka nitakupa wewe sehemu ya kumi.” (Mwanzo 28:20-22) Baadaye, alipokuwa karibu kukutana na ndugu yake, Yakobo alimsihi sana Yehova amlinde, akisema: “Nakuomba, unikomboe kutoka katika mkono wa ndugu yangu, kutoka katika mkono wa Esau, kwa sababu mimi ninaogopa.” (Mwanzo 32:9-12) Yule mzee wa ukoo Ayubu alisali kwa Yehova kwa niaba ya familia yake, huku akitoa dhabihu kwa ajili yao. Wakati marafiki watatu wa Ayubu walipotenda dhambi kwa kusema mambo yasiyofaa, Ayubu alisali kwa ajili yao, naye “Yehova akaukubali uso wa Ayubu.” (Ayubu 1:5; 42:7-9) Masimulizi hayo yanatusaidia kutambua mambo tunayoweza kutaja tunaposali kwa Yehova. Pia, tunajifunza kwamba Yehova yuko tayari kukubali sala za wale wanaomkaribia kwa njia inayofaa.

Wakati wa Agano la Sheria

8. Wakati wa agano la Sheria, mambo yalifikishwaje mbele za Yehova kwa niaba ya watu?

8 Baada ya Yehova kulikomboa taifa la Israeli kutoka Misri, aliwapa agano la Sheria. Sheria ilionyesha mpango wa kumkaribia Mungu kupitia makuhani waliowekwa rasmi. Baadhi ya Walawi walipewa mgawo wa kuwa makuhani kwa niaba ya watu. Mambo yaliyohusu taifa lote yalipozuka, mwakilishi wa watu, kama vile mfalme au nabii, alisali kwa Mungu kuhusu mambo hayo. (1 Samweli 8:21, 22; 14:36-41; Yeremia 42:1-3) Kwa mfano, wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu, Mfalme Sulemani alimkaribia Yehova katika sala ya kutoka moyoni. Kisha, Yehova akaonyesha kwamba amekubali sala ya Sulemani kwa kujaza utukufu Wake katika hekalu na kusema: “Masikio yangu yatasikiliza sala katika mahali hapa.”—2 Mambo ya Nyakati 6:12–7:3, 15.

9. Ni takwa gani lililopaswa kutimizwa ili kumkaribia Yehova kwa njia inayofaa katika patakatifu?

9 Katika Sheria ambayo Waisraeli walipewa, Yehova alitaja takwa la kumkaribia kwa njia inayokubalika katika patakatifu. Takwa gani? Kila asubuhi na kila jioni, zaidi ya kutoa matoleo ya wanyama, kuhani mkuu alipaswa kufukiza uvumba wenye manukato mbele za Yehova. Baadaye, hata makuhani wa cheo cha chini walifanya utumishi huo, isipokuwa katika Siku ya Upatanisho. Ikiwa makuhani hawangefanya tendo hilo la heshima, Yehova hangefurahia utumishi wao.—Kutoka 30:7, 8; 2 Mambo ya Nyakati 13:11.

10, 11. Tuna uthibitisho gani kwamba Yehova alikubali sala za mtu mmoja-mmoja?

10 Katika Israeli la kale, je, watu wangeweza kumkaribia Mungu kupitia wawakilishi walioteuliwa tu? Hapana, Maandiko yanaonyesha kwamba Yehova alifurahi kukubali sala za kibinafsi za mtu mmoja-mmoja. Alipokuwa akisali wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu, Sulemani alimsihi Yehova, akisema: “Sala yoyote, ombi lolote la kutaka kibali ambalo huenda likatolewa na mwanadamu au na watu wako wote Israeli, . . . wakati anaponyoosha mikono yake kuelekea nyumba hii, basi na usikie ukiwa mbinguni.” (2 Mambo ya Nyakati 6:29, 30) Simulizi la Luka linatuambia kwamba wakati Zekaria, baba ya Yohana Mbatizaji, alipokuwa akifukiza uvumba katika patakatifu, umati wa waabudu wa Yehova ambao hawakuwa makuhani ulikuwa “ukisali nje.” Inaonekana kwamba ilikuwa desturi ya watu kukusanyika nje ya patakatifu ili kusali huku uvumba ukifukizwa mbele za Yehova kwenye madhabahu ya dhahabu.—Luka 1:8-10.

11 Hivyo, wakati watu walipomkaribia Yehova kwa njia inayofaa, alikuwa tayari kukubali maombi ya wale waliowakilisha taifa zima na wale waliomkaribia kibinafsi. Leo, hatuko chini ya agano la Sheria. Hata hivyo, tunaweza kujifunza mambo fulani muhimu kuhusu sala kutokana na njia ambazo Waisraeli wa kale walitumia ili kumkaribia Mungu.

Wakati wa Mpango wa Kikristo

12. Ni mpango gani ulioanzishwa ili kuwawezesha Wakristo wamkaribie Yehova?

12 Leo tuko chini ya mpango wa Kikristo. Hakuna tena hekalu halisi lenye makuhani wanaowakilisha watu wote wa Mungu au ambalo tunaweza kulielekea tunaposali kwa Mungu. Lakini, bado Yehova amefanya mpango unaotuwezesha kumkaribia. Mpango gani? Katika mwaka wa 29 W.K., wakati ambapo Kristo alitiwa mafuta na kuwekwa rasmi kuwa Kuhani Mkuu, hekalu la kiroho lilianza kufanya kazi. * Hekalu hilo la kiroho ndio mpango mpya wa kumkaribia Yehova katika ibada kwa msingi wa dhabihu ya upatanisho ya Yesu Kristo.—Waebrania 9:11, 12.

13. Kuhusiana na sala, kuna ulinganifu gani mmoja kati ya hekalu lililokuwa Yerusalemu na hekalu la kiroho?

13 Mambo mengi katika hekalu la Yerusalemu yanawakilisha maandalizi ya hekalu la kiroho, kutia ndani maandalizi yanayohusiana na sala. (Waebrania 9:1-10) Kwa mfano, ni jambo gani linalowakilishwa na uvumba uliofukizwa asubuhi na jioni juu ya madhabahu ya uvumba ndani ya Patakatifu pa hekalu? Kulingana na kitabu cha Ufunuo, “uvumba unamaanisha sala za watakatifu.” (Ufunuo 5:8; 8:3, 4) Daudi aliongozwa kwa roho ya Mungu kuandika hivi: “Sala yangu na itayarishwe kama uvumba mbele zako.” (Zaburi 141:2) Hivyo, katika mpango wa Kikristo, uvumba wenye harufu tamu unawakilisha sala na sifa zinazokubalika ambazo zinatolewa kwa Yehova.—1 Wathesalonike 3:10.

14, 15. Tunaweza kusema nini kuhusu jinsi (a) Wakristo watiwa-mafuta wanavyomkaribia Yehova? (b) “kondoo wengine” wanavyomkaribia Yehova?

14 Ni nani wanaoweza kumkaribia Mungu katika hekalu hilo la kiroho? Katika hekalu halisi, makuhani na Walawi walikuwa na pendeleo la kutumikia katika ua wa ndani, lakini ni makuhani tu ndio wangeweza kuingia ndani ya Patakatifu. Wakristo watiwa-mafuta ambao wana tumaini la kwenda mbinguni wanafurahia hali ya pekee ya kiroho iliyowakilishwa na ua wa ndani na Patakatifu. Hali hiyo huwawezesha kusali na kumsifu Mungu.

15 Namna gani “kondoo wengine” ambao wana tumaini la kuishi duniani? (Yohana 10:16) Nabii Isaya alionyesha kuwa watu wa mataifa mengi wangekuja kumwabudu Yehova “katika siku za mwisho.” (Isaya 2:2, 3) Pia, aliandika kwamba “wageni” wangejiunga na Yehova. Akionyesha kuwa yuko tayari kuwakubali wanapomkaribia, Mungu alisema hivi: ‘Nitawafanya washangilie ndani ya nyumba yangu ya sala.’ (Isaya 56:6, 7) Andiko la Ufunuo 7:9-15 linatoa habari zaidi linapozungumza kuhusu “umati mkubwa” kutoka “mataifa yote” ambao unakusanyika kumwabudu Mungu na kusali kwake “mchana na usiku” huku ukisimama katika ua wa nje wa hekalu la kiroho. Inafariji kama nini kujua kwamba watumishi wote wa Mungu leo wanaweza kumkaribia Mungu kwa uhuru huku wakiwa na uhakika kabisa kwamba atawasikia!

Ni Sala Gani Zinazokubalika?

16. Tunaweza kujifunza nini kuhusu sala kutokana na Wakristo wa mapema?

16 Wakristo wa mapema walisali kwa ukawaida. Walisali kuhusu mambo gani? Wazee Wakristo waliomba mwongozo walipochagua wanaume kwa ajili ya madaraka ya usimamizi. (Matendo 1:24, 25; 6:5, 6) Epafra alisali kwa ajili ya waamini wenzake. (Wakolosai 4:12) Washiriki wa kutaniko la Yerusalemu walisali kwa ajili ya Petro alipokuwa gerezani. (Matendo 12:5) Wakristo wa mapema walimwomba Mungu awape ujasiri walipokabili mateso, wakisema: “Yehova, viangalie vitisho vyao, na kuwawezesha watumwa wako kuendelea kusema neno lako kwa ujasiri wote.” (Matendo 4:23-30) Mwanafunzi Yakobo aliwahimiza Wakristo wamwombe Mungu hekima wanapokabili majaribu. (Yakobo 1:5) Je, wewe hutaja mambo kama hayo unaposali kwa Yehova?

17. Yehova hukubali sala za nani?

17 Mungu hakubali sala zote. Basi, tunawezaje kusali tukiwa na uhakika kwamba sala zetu zitakubaliwa? Watu waaminifu ambao Mungu aliwasikiliza zamani walimkaribia kwa unyoofu na kwa nia nzuri. Walionyesha kwamba wana imani kwa kutenda mema. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atawasikiliza wale wanaomkaribia kwa njia hiyohiyo leo.

18. Wakristo wanapaswa kutimiza takwa gani ili sala zao zisikiwe?

18 Kuna takwa lingine. Mtume Paulo alieleza takwa hilo, aliposema: “Kupitia yeye, sisi, . . . tunaweza kumkaribia Baba kwa roho moja.” Paulo alikuwa akizungumza juu ya nani alipoandika maneno haya, “kupitia yeye”? Alimaanisha Yesu Kristo. (Waefeso 2:13, 18) Naam, tunaweza kumkaribia Baba kwa uhuru kupitia Yesu tu.—Yohana 14:6; 15:16; 16:23, 24.

19. (a) Ni wakati gani ambapo Yehova alichukizwa na matoleo ya uvumba ya Waisraeli? (b) Tunaweza kuhakikishaje kwamba sala zetu ni kama uvumba wenye harufu tamu mbele za Yehova?

19 Kama ilivyotajwa tayari, uvumba uliofukizwa na makuhani Waisraeli unawakilisha sala zinazokubalika za watumishi waaminifu wa Mungu. Hata hivyo, nyakati nyingine, matoleo ya uvumba ya Waisraeli yalimchukiza Yehova. Ilikuwa hivyo wakati Waisraeli walipofukiza uvumba hekaluni huku wakiinamia sanamu. (Ezekieli 8:10, 11) Vivyo hivyo leo, sala za watu wanaodai kumtumikia Yehova huku wakitenda mambo yasiyopatana na sheria zake ni kama uvumba wenye kuchukiza kwake. (Methali 15:8) Basi, acheni tuendelee kuwa safi katika sehemu zote za maisha yetu ili sala zetu ziwe kama uvumba wenye harufu tamu mbele za Mungu. Yehova hufurahia sala za wale wanaofuata njia zake za uadilifu. (Yohana 9:31) Hata hivyo, kuna maswali mengine. Tunapaswa kusali jinsi gani? Tunaweza kusali kuhusu mambo gani? Na Mungu hujibuje sala zetu? Makala inayofuata itazungumzia maswali hayo na mengineyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2001, ukurasa wa 27.

Je, Unaweza Kueleza?

• Wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kumkaribiaje Mungu kwa njia inayokubalika?

• Tunaposali, tunaweza kuwaigaje wazee wa ukoo waaminifu?

• Tunajifunza nini kutokana na sala za Wakristo wa mapema?

• Ni wakati gani ambapo sala zetu huwa kama uvumba wenye harufu tamu mbele za Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kwa nini Mungu alikubali toleo la Abeli na kukataa la Kaini?

[Picha katika ukurasa wa 24]

“Mimi ni mavumbi na majivu”

[Picha katika ukurasa wa 25]

“Bila shaka nitakupa wewe sehemu ya kumi”

[Picha katika ukurasa wa 26]

Je, sala zako ni kama uvumba wenye harufu tamu mbele za Yehova?