Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufaidika na Ushikamanifu wa Wapendwa Wangu

Kufaidika na Ushikamanifu wa Wapendwa Wangu

Simulizi la Maisha

Kufaidika na Ushikamanifu wa Wapendwa Wangu

LIMESIMULIWA NA KATHLEEN COOKE

ALIPOKUWA anawatembelea watu wa ukoo huko Glasgow, Scotland, mwaka wa 1911, nyanya yangu Mary Ellen Thompson, alisikiliza hotuba ya Charles Taze Russell, mshiriki mashuhuri wa Wanafunzi wa Biblia, kikundi ambacho baadaye kiliitwa Mashahidi wa Yehova. Nyanya yangu alifurahia habari alizosikia. Aliporudi Afrika Kusini aliwatafuta Wanafunzi wa Biblia. Mnamo Aprili 1914 alikuwa miongoni mwa watu 16 waliobatizwa katika kusanyiko la kwanza la Wanafunzi wa Biblia huko Afrika Kusini. Binti ya Nyanya, Edith, ambaye ndiye mama yangu, alikuwa na umri wa miaka sita wakati huo.

Baada ya kifo cha Ndugu Russell mwaka wa 1916, kulikuwa na kutoelewana miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia ulimwenguni pote. Idadi ya waaminifu huko Durban ilipungua kutoka 60 hadi 12 hivi. Nyanya yangu aliyemzaa baba, Ingeborg Myrdal, na mwana wake, Henry, waliwaunga mkono waaminifu. Henry alikuwa amebatizwa karibuni. Mwaka wa 1924, Henry akawa kolpota, kama watumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Alihubiri katika maeneo mengi ya kusini mwa Afrika kwa miaka mitano iliyofuata. Mnamo 1930, Henry na Edith walifunga ndoa, nami nikazaliwa miaka mitatu baadaye.

Familia Iliyopanuka

Tuliishi Msumbiji kwa muda, lakini mwaka wa 1939 tukahamia nyumba ya Babu na Nyanya Thompson huko Johannesburg. Babu yangu hakupendezwa na kweli za Biblia na wakati mwingine alimpinga Nyanya, lakini alikuwa mkarimu sana. Dada yangu, Thelma, alizaliwa mwaka wa 1940, nami pamoja naye tukajifunza kuwatunza watu wenye umri mkubwa. Mara nyingi wakati wa chakula cha jioni tulizungumza kwa muda mrefu kuhusu matukio ya siku na kukumbuka yaliyopita.

Familia yetu ilifurahia kukaa na Mashahidi waliotutembelea, hasa watumishi wa wakati wote. Wao pia walishiriki katika mazungumzo wakati wa chakula cha jioni, na maelezo yao yalituchochea tuthamini urithi wetu wa kiroho. Hiyo iliimarisha tamaa yangu na ya Thelma ya kuwa mapainia kama wao.

Tangu utotoni, tulizoezwa kufurahia kusoma. Mama, Baba, na Nyanya walitusomea vitabu vizuri vya hadithi au Biblia. Mikutano na huduma ya Kikristo ilikuwa muhimu sana katika maisha yetu. Baba alikuwa mtumishi wa Kutaniko (sasa mwangalizi msimamizi) la Johannesburg, hivyo ilitubidi sisi sote tufike mikutanoni mapema. Tulipokuwa na kusanyiko, Baba alisaidia katika kazi ya usimamizi, naye Mama aliwasaidia wageni kupata mahali pa kulala.

Kusanyiko Lililokuwa la Pekee Kwetu

Kusanyiko la mwaka wa 1948 huko Johannesburg lilikuwa la pekee. Kwa mara ya kwanza, washiriki wa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, walikuja. Baba alipewa mgawo wa kutumia gari lake kuwasafirisha Nathan Knorr na Milton Henschel kwa muda wote ambao walikaa huko. Nilibatizwa katika kusanyiko hilo.

Muda mfupi baadaye, Baba alishangaa wakati Babu alipomwambia kwamba anajuta kuwa kufuatia kifo cha Ndugu Russell, aliruhusu aathiriwe na wale waliojitenga na Wanafunzi wa Biblia. Babu alikufa miezi michache baadaye. Kwa upande mwingine, nyanya yangu, Myrdal, alibaki mshikamanifu hadi kifo mwaka wa 1955, akiwa na tumaini la kwenda mbinguni.

Matukio Yaliyobadili Maisha Yangu

Nilianza upainia wa kawaida Februari 1, 1949. Punde kukawa na msisimuko baada ya kutangazwa kwamba kutakuwa na kusanyiko la kimataifa huko New York City mwaka uliofuata. Tulitaka sana kwenda, lakini hatungeweza kugharimia safari hiyo. Kisha, Februari 1950, Babu Thompson alikufa, naye Nyanya akatumia pesa ambazo alikuwa amerithi ili kulipia gharama za usafiri kwa ajili ya sisi sote watano.

Majuma kadhaa kabla ya kuondoka, tulipokea barua kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York. Ilikuwa barua ya kunialika kuhudhuria darasa la 16 la shule ya umishonari ya Gileadi. Hilo lilikuwa tukio lenye kusisimua kama nini, kwa sababu sikuwa nimefikia umri wa miaka 17! Darasa hilo lilipoanza, nilikuwa miongoni mwa wanafunzi kumi kutoka Afrika Kusini, waliofurahia pendeleo hilo zuri.

Baada ya kuhitimu mnamo Februari 1951, wanane kati yetu tulirudi Afrika Kusini kutumikia tukiwa wamishonari. Kwa miaka michache iliyofuata, mimi na mwenzangu tulihubiri katika miji midogo ambapo Kiafrikana kilizungumzwa. Mwanzoni sikujua lugha hiyo vizuri. Nakumbuka siku moja nilirudi nyumbani nikiendesha baiskeli huku nikilia kwa sababu ya kupungukiwa katika huduma. Hata hivyo, baadaye nilijitahidi, na Yehova akabariki jitihada zangu.

Ndoa na Kazi ya Kusafiri

Mwaka wa 1955, nilimfahamu John Cooke. Alisaidia kuanzisha kazi ya kuhubiri huko Ufaransa, Ureno, na Hispania kabla na baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, naye akatumwa kutumikia akiwa mmishonari barani Afrika mwaka huo niliokutana naye. Baadaye aliandika hivi: “Nilipata mambo matatu yenye kushangaza katika juma moja . . . Ndugu mmoja mkarimu alinipa gari dogo; niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa wilaya; na nikampenda dada mmoja.” * Tulifunga ndoa Desemba 1957.

Wakati wa uchumba, John alinihakikishia kwamba maisha yetu pamoja yatakuwa yenye kufurahisha kila wakati, na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Tulitembelea makutaniko kotekote Afrika Kusini, hasa katika maeneo ya weusi. Kila juma, ilitubidi tupate kibali cha kuingia maeneo hayo na kulala huko usiku kucha. Katika pindi kadhaa tulilala kwenye sakafu katika duka moja lililokuwa bila kitu karibu na eneo la wazungu ambapo tulijaribu kujificha tusionekane na wapita njia. Kwa kawaida tulikaa karibu na Mashahidi wazungu walioishi mbali sana.

Pia, tulikabili tatizo la kukutana msituni katika sehemu zilizokuwa zimejengwa kwa ajili ya makusanyiko. Tulionyesha sinema zilizotayarishwa na Mashahidi wa Yehova ambazo ziliwasaidia watu kuthamini undugu wetu wa ulimwenguni pote. Tulibeba jenereta yetu kwa sababu maeneo hayo hayakuwa na umeme. Pia, tulikabili matatizo katika maeneo yaliyokuwa chini ya Uingereza ambapo vichapo vyetu vilikuwa vimepigwa marufuku. Isitoshe, tulihitaji kujifunza Kizulu. Hata hivyo, tulifurahia kuwatumikia ndugu zetu.

Mnamo Agosti 1961, John akawa mwalimu wa kwanza kufundisha Shule ya Huduma ya Ufalme ya majuma manne iliyofanywa Afrika Kusini. Shule hiyo ilikusudiwa kuwasaidia waangalizi wa makutaniko. Alikuwa stadi katika kazi ya kufundisha na alifikia mioyo kwa hoja zinazoeleweka kwa urahisi na mifano iliyo wazi. Kwa karibu mwaka mmoja na nusu, tulisafiri kutoka sehemu moja hadi nyingine kwa ajili ya darasa lililofuata la Kiingereza. John alipokuwa akifundisha, nilihubiri pamoja na Mashahidi wa eneo hilo. Kisha, tulishangaa tulipopata mwaliko wa kutumikia katika ofisi ya tawi ya Afrika Kusini karibu na jiji la Johannesburg, kuanzia Julai 1, 1964.

Kufikia wakati huo, John alikuwa na ugonjwa ambao ulitutia wasiwasi. Katika 1948 aliugua kifua kikuu, naye alikuwa dhaifu mara nyingi. Alikuwa na dalili kama za mafua na ilimbidi alale mara nyingi, naye hangeweza kufanya chochote wala kumwona yeyote. Daktari tuliyemwomba mashauri kabla ya kualikwa kwenye ofisi ya tawi alisema kwamba John ameshuka moyo.

Haikuwa rahisi kubadili maisha yetu, kama daktari alivyopendekeza. Kwenye ofisi ya tawi, John alifanya kazi katika Idara ya Utumishi, nami nikapewa kazi ya kukagua makala. Lilikuwa pendeleo kama nini kuwa na chumba chetu wenyewe! John alikuwa ametumika katika maeneo ya Kireno kabla hatujafunga ndoa. Hivyo mnamo 1967, tuliombwa tusaidie familia za Mashahidi Wareno katika eneo hilo ili kuwahubiria Wareno wengi walioishi ndani na nje ya Johannesburg. Hilo lilimaanisha nijifunze lugha nyingine tena.

Kwa kuwa Wareno walikuwa wametawanyika katika eneo kubwa, tulisafiri sana, wakati mwingine kufikia umbali wa kilometa 300 ili kuwatafuta wanaostahili. Wakati huo, Mashahidi waliozungumza Kireno kutoka Msumbiji walianza kututembelea wakati wa makusanyiko, na jambo hilo liliwasaidia wapya wengi. Kwa miaka 11 tuliyotumia katika eneo la Kireno, tuliona kikundi kidogo cha wahubiri 30 hivi kikipanuka na kuwa makutaniko manne.

Mabadiliko Nyumbani

Wakati huo, mabadiliko yalitokea nyumbani kwetu. Mwaka wa 1960, dada yangu, Thelma, aliolewa na John Urban, painia kutoka Marekani. Mnamo 1965 wakahudhuria darasa la 40 la Shule ya Gileadi, na wakatumikia kwa ushikamanifu wakiwa wamishonari nchini Brazili kwa miaka 25. Mnamo 1990 walirudi Ohio kuwatunza wazazi wa John waliokuwa wagonjwa. Licha ya mikazo ya kuwatunza wazazi wagonjwa, wanaendelea na utumishi wa wakati wote mpaka leo.

Nyanya Thompson alikufa mwaka wa 1965 akiwa na umri wa miaka 98. Alikufa akiwa mwaminifu kwa Mungu naye alikuwa na tumaini la kwenda mbinguni. Baba alistaafu mwaka huohuo. Hivyo mimi na John tulipoombwa tusaidie kuhubiri katika eneo la Kireno, Mama na Baba walijitolea kujiunga nasi. Waliimarisha kikundi hicho sana na baada ya miezi michache, kutaniko la kwanza lilianzishwa. Muda mfupi baadaye, Mama aliugua kansa, naye akafa mwaka wa 1971 kutokana na ugonjwa huo. Baba alikufa miaka saba baadaye.

Kukabiliana na Ugonjwa wa John

Kufikia miaka ya 1970, ilikuwa wazi kwamba afya ya John iliendelea kuwa mbaya. Hatua kwa hatua, ilibidi aache baadhi ya mapendeleo yake ya utumishi, kutia ndani kuongoza funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma na mazungumzo ya Biblia ya asubuhi kwenye ofisi ya tawi. Alipelekwa kwenye Idara ya Utumishi, kisha katika ofisi ya barua, halafu kwenye bustani.

Kwa kuwa John hakukata tamaa kwa urahisi, ilikuwa vigumu kwake kufanya mabadiliko. Niliposisitiza kwamba anahitaji kupumzika, alisema kwa mzaha kwamba mimi ni kizuizi kwake, kisha akanikumbatia kwa upendo. Hatimaye tuliona ni afadhali tutoke katika eneo la Kireno na kutumikia katika kutaniko lililokutana kwenye Jumba la Ufalme la ofisi ya tawi.

Afya ya John ilipoendelea kuzorota, nilitiwa moyo kuona akiwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Wakati John alipoamka katikati ya usiku akiwa ameshuka moyo sana, tulizungumza pamoja mpaka alipotulia na tukasali ili kumwomba Yehova msaada. Hatimaye, aliweza kukabiliana na hali hizo mbaya akiwa peke yake kwa kujilazimisha kukariri polepole maneno haya ya Wafilipi 4:6, 7: “Msihangaike juu ya kitu chochote . . .” Kisha angetulia kiasi cha kuweza kusali. Mara nyingi nilikuwa macho na ningetazama akifungua mdomo wake huku akimsihi Yehova kwa unyoofu.

Kwa kuwa ofisi yetu ya tawi ilikuwa ndogo sana, ujenzi wa ofisi kubwa ya tawi ulianza nje ya jiji la Johannesburg. Mimi na John tulitembelea mahali hapo penye utulivu mara nyingi, mbali na kelele na uchafu wa jiji. John alifurahi sana tuliporuhusiwa kuishi huko katika makao ya muda mpaka ofisi mpya ilipokamilika.

Matatizo Mengine Yatokea

Kadiri uwezo wa John wa kufikiri ulivyoendelea kuzorota, ndivyo ilivyokuwa vigumu zadi kutimiza migawo yake. Nilitiwa moyo sana nilipoona jinsi wengine walivyomsaidia John. Kwa mfano, ndugu alipotembelea maktaba ya umma ili kufanya utafiti, angeandamana na John. John alijaza trakti na magazeti katika mifuko yake alipokwenda matembezi hayo. Hilo lilimsaidia John kuhisi kwamba anahitajiwa na anatimiza jambo fulani.

Mwishowe, kwa sababu ya ugonjwa wa kupungua akili (ugonjwa wa Alzheimer), John hangeweza kusoma. Tulifurahi kuwa na kanda za vichapo vya Biblia na nyimbo za Ufalme. Tulizisikiliza tena na tena. Mara nyingi John angekasirika kama singeketi na kusikiliza pamoja naye, hivyo basi nikatumia pindi hizo kushona. Hiyo ilituwezesha kuwa na nguo nyingi za baridi na mablanketi!

Hatimaye, nilihitaji kumtunza John zaidi kwa sababu hali yake ilizidi kuwa mbaya. Ingawa mara nyingi nilichoka sana na singeweza kusoma wala kujifunza, lilikuwa pendeleo kumtunza mpaka mwisho. Mwisho huo ulifika mwaka wa 1998 John alipokufa akiwa amelala kwa utulivu mikononi mwangu muda mfupi baada ya kufikia umri wa miaka 85, akiwa mshikamanifu mpaka mwisho. Ninatarajia kumwona wakati wa ufufuo akiwa na afya nzuri ya kimwili na ya kiakili!

Kuburudishwa

Baada ya kifo cha John, haikuwa rahisi kuishi peke yangu. Hivyo, mnamo Mei 1999, nilienda Marekani kumtembelea dada yangu, Thelma, na mume wake. Nilifurahi sana kukutana na marafiki wengi washikamanifu, hasa tulipotembelea makao makuu ya Mashahidi wa Yehova, huko New York! Nilifurahi sana kutiwa moyo kiroho.

Ninapofikiria maisha ya wapendwa wangu washikamanifu ninakumbuka mambo mengi ambayo yamekuwa yenye faida kwangu. Kupitia maagizo yao, mifano, na msaada, nilijifunza kuwapenda watu wa mataifa na jamii tofauti-tofauti. Nilijifunza subira, uvumilivu, na kubadilika kulingana na hali. Zaidi ya yote, Yehova, ambaye ni Msikiaji wa sala, alinitendea kwa fadhili. Ninahisi kama mtunga-zaburi aliyesema: “Mwenye furaha ni yule unayemchagua na kumfanya akaribie, ili apate kukaa katika nyua zako. Hakika tutashiba mema ya nyumba yako.”—Zaburi 65:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1959, (Kiingereza) ukurasa wa 468-472.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Nyanya na binti zake

[Picha katika ukurasa wa 9]

Nikiwa na wazazi wangu nilipobatizwa mwaka wa 1948

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nikiwa pamoja na Albert Schroeder, msajili wa Shule ya Gileadi, na wanafunzi wengine tisa kutoka Afrika Kusini

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nikiwa na John mwaka wa 1984