Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kwa Sababu Tu ya Mvulana Mwenye Umri wa Miaka Tisa”

“Kwa Sababu Tu ya Mvulana Mwenye Umri wa Miaka Tisa”

“Kwa Sababu Tu ya Mvulana Mwenye Umri wa Miaka Tisa”

WAKATI wowote Mashahidi wa Yehova walipokuja mlangoni pake, Wiesława, anayeishi kusini mwa Poland, aliwashukuru kwa upole na kukataa kuzungumza nao. Siku moja, Samuel, mwenye umri wa miaka tisa, alifika mlangoni pake akiwa na mama yake. Wakati huo, Wiesława aliamua kusikiliza ujumbe wao, naye akakubali gazeti lililozungumzia paradiso duniani.

Kwa kuwa Ukumbusho wa Kifo cha Yesu Kristo ulikuwa umekaribia, Samuel alitaka kumwalika Wiesława kwenye tukio hilo la pekee. Hivyo, akiwa pamoja na mama yake, mvulana huyo alimtembelea tena Wiesława, akiwa na mwaliko uliochapishwa. Kwa kuwa aliona kwamba mvulana huyo alikuwa amevalia vizuri, Wiesława aliomba wampe muda mfupi ili aende kuvaa vizuri. Aliporudi mlangoni, alimsikiliza Samuel, akakubali mwaliko, na akauliza hivi: “Je, nije peke yangu au nije na mume wangu?” Kisha akaongeza hivi: “Hata ikiwa mume wangu haji, mimi nitakuja. Nitafanya hivyo kwa sababu yako Samuel.” Alikuja kama alivyoahidi, na Samuel akafurahi sana.

Wakati hotuba ya Ukumbusho ilipokuwa ikiendelea, Samuel aliketi kando ya Wiesława na kumwonyesha maandiko ambayo yalikuwa yakizungumziwa. Hilo lilimshangaza sana. Alifurahia programu ya Ukumbusho na jinsi mawazo mazito yalivyofafanuliwa kwa njia rahisi. Pia, alifurahia ukaribishaji wenye shauku na fadhili alizoonyeshwa na kutaniko. Tangu hapo, Wiesława amependezwa zaidi na mambo ya kiroho, naye ameanza kushirikiana kwa ukawaida na Mashahidi wa Yehova. Hivi karibuni alisema hivi: “Ninaaibika kwamba mwanzoni sikuwasikiliza mlipokuja kwangu. Na ni lazima nikubali kwamba nilisikiliza ujumbe wenu kwa sababu tu ya mvulana mwenye umri wa miaka tisa, naam, kwa sababu ya Samuel.”

Kama Samuel huko Poland, vijana wengi Mashahidi wa Yehova wanamsifu Mungu kwa kuhubiri na kwa mwenendo wao mzuri. Ikiwa wewe ni kijana, wewe pia unaweza kuwasaidia watu wanyoofu wapendezwe na maadili ya kiroho.