Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Tano cha Zaburi

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Tano cha Zaburi

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Tano cha Zaburi

HUENDA matajiri wakasema: “Wana wetu ni kama mimea michanga iliyokua wakati wa ujana wao, binti zetu ni kama nguzo za pembeni zilizochongwa kwa mtindo wa jumba la mfalme, maghala yetu yamejaa, . . . makundi yetu yanaongezeka kwa maelfu.” Isitoshe, huenda matajiri wakapaaza sauti hivi: “Wenye furaha ni watu ambao mambo yako hivyo kwao!” Hata hivyo, mtunga-zaburi anasema hivi: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!” (Zaburi 144:12-15) Naam, watu ambao Mungu wao ni Yehova wanatazamiwa kuwa wenye furaha. Yehova ni Mungu mwenye furaha, na wale wanaomwabudu ni wenye furaha pia. (1 Timotheo 1:11) Kweli hiyo inaonyeshwa wazi katika kitabu cha mwisho cha nyimbo zilizoongozwa kwa roho ya Mungu, yaani, Zaburi ya 107 hadi ya 150.

Kitabu cha Tano cha Zaburi kinakazia pia sifa bora za Yehova, kutia ndani fadhili zenye upendo, ukweli, na wema. Kadiri tunavyoufahamu vizuri zaidi utu wa Mungu, ndivyo tutakavyompenda na kumwogopa zaidi. Hilo ndilo hutuwezesha kuwa wenye furaha. Kitabu cha Tano cha Zaburi kina ujumbe wenye thamani kama nini!—Waebrania 4:12.

WENYE FURAHA KWA SABABU YA FADHILI ZENYE UPENDO ZA YEHOVA

(Zaburi 107:1–119:176)

Wayahudi walio uhamishoni wanaimba hivi wanaporudi kutoka utekwani Babiloni: “Watu na wamtolee Yehova shukrani kwa ajili ya fadhili zake zenye upendo na kwa ajili ya kazi zake za ajabu kwa wana wa binadamu.” (Zaburi 107:8, 15, 21, 31) Akimtukuza Mungu, Daudi anaimba hivi: “Ukweli wako [uko] mpaka angani.” (Zaburi 108:4) Katika muziki unaofuata, Daudi anasali hivi: “Unisaidie, Ee Yehova Mungu wangu; uniokoe kulingana na fadhili zako zenye upendo.” (Zaburi 109:18, 19, 26) Zaburi ya 110 ni unabii unaohusu utawala wa Masihi. Andiko la Zaburi 111:10 linasema hivi: “Kumwogopa Yehova ni mwanzo wa hekima.” Kulingana na zaburi inayofuata, “mwenye furaha ni mtu anayemwogopa Yehova.”—Zaburi 112:1.

Zaburi ya 113 hadi ya 118 zinaitwa Zaburi za Haleli kwa sababu zinarudia-rudia neno “Haleluya,” au “Msifuni Yah!” Kulingana na Mishnah, kitabu cha karne ya tatu chenye mapokeo ya kale yaliyopitishwa kwa mdomo, nyimbo hizo ziliimbwa wakati wa Pasaka na kwenye sherehe tatu za kila mwaka za Wayahudi. Zaburi ya 119, ambayo ndiyo zaburi ndefu zaidi na sura ndefu zaidi katika Biblia, hutukuza neno la Yehova lililofunuliwa, au ujumbe wake.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

109:23—Daudi alimaanisha nini aliposema: “Kama wakati kivuli kinapopungua, mimi nalazimika kwenda zangu”? Kwa njia ya kishairi, Daudi alikuwa akimaanisha kwamba alikuwa karibu kufa.—Zaburi 102:11.

110:1, 2—“Bwana [wa Daudi],” Yesu Kristo, alikuwa akifanya nini alipoketi kwenye mkono wa kuume wa Mungu? Baada ya kufufuliwa kwake, Yesu alipanda mbinguni na kungojea kwenye mkono wa kuume wa Mungu hadi mwaka wa 1914 ili kuanza kutawala akiwa Mfalme. Wakati huo, Yesu alikuwa akitawala juu ya wafuasi wake watiwa-mafuta na kuwaongoza katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Pia, alikuwa akiwatayarisha kutawala pamoja naye katika Ufalme wake.—Mathayo 24:14; 28:18-20; Luka 22:28-30.

110:4—Yehova ‘ameapa bila kujuta’ kuhusu jambo gani? Kiapo hicho ni agano ambalo Yehova alifanya pamoja na Yesu Kristo ili Yesu atumikie akiwa Mfalme na Kuhani Mkuu.—Luka 22:29.

113:3—Ni katika njia gani jina la Yehova litasifiwa “kutoka mapambazuko ya jua mpaka kutua kwake”? Hilo halihusishi tu kikundi cha watu wachache wanaomwabudu Mungu kila siku. Miale ya jua huangaza juu ya dunia yote, kuanzia wakati jua linapochomoza mashariki hadi linapotua magharibi. Vivyo hivyo, Yehova anapaswa kusifiwa duniani pote. Hilo haliwezekani bila kufuata utaratibu fulani. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tuna pendeleo zuri la kumsifu Mungu na kushiriki kwa bidii katika kazi ya kutangaza Ufalme.

116:15—Ni katika njia gani ‘kifo cha washikamanifu wa Yehova ni chenye thamani machoni pake’? Yehova anawaona waabudu wake kuwa wenye thamani sana hivi kwamba ni hasara kubwa kwake kuwaruhusu wafe wakiwa kikundi. Ikiwa Yehova angeruhusu jambo hilo, hiyo ingeonyesha kwamba maadui wake wana nguvu nyingi kuliko yeye. Isitoshe, hakuna mtu ambaye angebaki duniani ili afanyize msingi wa dunia mpya.

119:71—Kuteseka kuna faida gani? Shida zinaweza kutufunza kumtegemea Yehova zaidi, kusali kwa bidii zaidi, na kuwa wenye bidii zaidi kujifunza Biblia na kutumia mashauri yake. Isitoshe, jinsi tunavyokabiliana na mateso kunaweza kufunua kasoro za utu wetu ambazo zinahitaji kurekebishwa. Mateso hayatatufanya tuwe wenye kinyongo tukiyaruhusu yatusafishe.

119:96—Maneno “mwisho wa ukamilifu wote” yanamaanisha nini? Mtunga-zaburi anazungumzia ukamilifu kulingana na maoni ya kibinadamu. Yaelekea alikuwa anamaanisha kwamba maoni ya mwanadamu kuhusu ukamilifu yana mipaka. Kwa upande mwingine, amri ya Mungu haina mipaka. Mwongozo wake unahusu sehemu zote za maisha. Tafsiri ya Union Version inasema hivi: “Nimeona ukamilifu wote kuwa na mwisho, bali agizo lako ni pana mno.”

119:164—Inamaanisha nini kumsifu Mungu “mara saba wakati wa mchana”? Kwa kawaida, namba saba humaanisha ukamili. Hivyo, mtunga-zaburi anaonyesha kwamba Yehova anastahili kupewa sifa zote.

Mambo Tunayojifunza:

107:27-31. Hekima ya ulimwengu ‘itavurugika’ wakati wa Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Haiwezi kumwokoa yeyote asiharibiwe. Ni wale tu wanaomtegemea Yehova kwa ajili ya wokovu ndio watakaoishi ili ‘wamtolee shukrani kwa ajili ya fadhili zake zenye upendo.’

109:30, 31; 110:5. Kwa kawaida, mkono wa kuume wa askari ambao ulichukua upanga haukulindwa na ngao ambayo ilishikwa kwa mkono wa kushoto. Kwa njia ya mfano, Yehova yuko “kwenye mkono wa kuume” wa watumishi wake ili kuwapigania. Hivyo, yeye huwalinda na kuwasaidia, na hilo linatupa sababu nzuri ya ‘kumsifu sana.’

113:4-9. Yehova yuko juu sana hivi kwamba anahitaji kujishusha ili ‘kuzitazama hata mbingu.’ Hata hivyo, yeye ni mwenye huruma kwa mtu wa hali ya chini, maskini, na mwanamke tasa. Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ni mnyenyekevu naye anataka waabudu wake wawe hivyo pia.—Yakobo 4:6.

114:3-7. Tunachochewa sana tunapojifunza kuhusu kazi za ajabu ambazo Yehova aliwatendea watu wake kwenye Bahari Nyekundu, kwenye Mto Yordani, na kwenye Mlima Sinai. Wanadamu, ambao wanawakilishwa na “dunia,” wanapaswa kustaajabu, au katika njia ya mfano, wanapaswa kuwa katika “maumivu makali” kwa sababu ya Bwana.

119:97-101. Kupata hekima, ufahamu, na uelewaji kutoka katika Neno la Mungu hutulinda na madhara ya kiroho.

119:105. Neno la Mungu ni taa ya miguu yetu katika maana ya kwamba linaweza kutusaidia kukabiliana na matatizo ya sasa. Pia, kwa njia ya mfano, linatuangazia njia yetu, kwa kuwa linatabiri kusudi la Mungu kuhusu wakati ujao.

WENYE FURAHA LICHA YA TAABU

(Zaburi 120:1–145:21)

Tunaweza kukabilianaje na hali ngumu na kuvumilia taabu? Zaburi ya 120 hadi ya 134 zinajibu waziwazi swali hilo. Tunavumilia taabu na kudumisha shangwe yetu kwa kutegemea msaada wa Yehova. Zaburi hizo, zinazoitwa Nyimbo za Mipando, huenda ziliimbwa wakati Waisraeli walipopanda kwenda Yerusalemu kwa ajili ya sherehe zao za kila mwaka.

Zaburi ya 135 na ya 136 zinaonyesha Yehova kuwa Mtendaji wa kila jambo linalompendeza, tofauti na miungu isiyo na maana. Zaburi ya 136 ilitungwa ikiwa na kiitikio, na sehemu ya mwisho ya kila mstari iliimbwa ili kuitikia sehemu ya kwanza. Zaburi inayofuata inaeleza huzuni ya Wayahudi waliokuwa Babiloni ambao walitaka kwenda kumwabudu Yehova huko Sayuni. Zaburi ya 138 hadi ya 145 zilitungwa na Daudi. Daudi anataka ‘kumsifu Yehova kwa moyo wake wote.’ Kwa nini? “Kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha,” asema Daudi. (Zaburi 138:1; 139:14) Katika zaburi tano zinazofuata, Daudi anasali ili alindwe dhidi ya watu wabaya, anasali kuhusu makaripio ya uadilifu, anasali ili akombolewe kutokana na watesi wake, na pia anasali ili kupata mwongozo kuhusiana na mwenendo. Anazungumzia hasa furaha ya watu wa Yehova. (Zaburi 144:15) Baada ya kuzungumza tena kuhusu ukuu na wema wa Mungu, Daudi anasema hivi: “Kinywa changu kitasema sifa za Yehova; na wote wenye mwili na walibariki jina lake takatifu mpaka wakati usio na kipimo, hata milele.”—Zaburi 145:21.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

122:3—Yerusalemu lilikuwaje jiji ‘lililounganishwa pamoja kwa umoja’? Kama ilivyokuwa kawaida katika majiji ya kale, nyumba katika jiji la Yerusalemu zilikaribiana sana. Jiji hilo lilikuwa imara na hivyo ilikuwa rahisi kulilinda. Isitoshe, kukaribiana kwa nyumba kulifanya iwezekane kwa wakaaji wa jiji hilo kusaidiana na kulindana. Hilo lilionyesha umoja wa kiroho wa makabila 12 ya Israeli yalipoungana katika ibada.

123:2—Mfano kuhusu macho ya watumishi unamaanisha nini? Watumishi na wajakazi wanatazama mkono wa bwana wao au bimkubwa wao kwa sababu mbili: ili kutambua matakwa yake na kupata ulinzi na vitu vya lazima maishani. Vivyo hivyo, macho yetu yanamwelekea Yehova ili kutambua mapenzi yake na kupata kibali chake.

131:1-3—Ni kwa njia gani Daudi ‘aliituliza na kuinyamazisha nafsi yake kama mtoto aliyeachishwa kunyonya juu ya mama yake’? Kama mtoto anayejifunza kutulia na kupata uradhi mikononi mwa mama yake, Daudi alijifunza kutuliza na kunyamazisha nafsi yake “kama mtoto aliyeachishwa kunyonya juu ya mama yake.” Jinsi gani? Kwa kuepuka kuwa na moyo na macho yenye kiburi, na kwa kutotafuta mambo makuu maishani mwake. Badala ya kutafuta umashuhuri, sikuzote Daudi alitambua udhaifu wake na hivyo akaonyesha unyenyekevu. Ni jambo la hekima kuiga mtazamo wake, hasa tunapojitahidi kufikia mapendeleo kutanikoni.

Mambo Tunayojifunza:

120:1, 2, 6, 7Uchongezi na maneno yenye kuumiza, yanaweza kuwataabisha sana wengine. Kuzuia ulimi wetu ni njia moja ya kuonyesha kwamba ‘tunasimama kwa ajili ya amani.’

120:3, 4Tukilazimika kumvumilia mtu mwenye “ulimi wenye ujanja,” tunaweza kufarijiwa kujua kwamba Yehova atanyoosha mambo kwa wakati wake. Wachongezi watataabika mikononi mwa “mwanamume mwenye nguvu.” Bila shaka, watapatwa na hukumu kali ya Yehova inayofananishwa na “makaa yanayowaka moto ya miretemu.”

127:1, 2Katika mambo yetu yote, tunapaswa kutegemea mwongozo wa Yehova.

133:1-3. Umoja wa watu wa Yehova unatuliza, unatia nguvu, na unaburudisha. Hatupaswi kuvuruga umoja huo kwa kutafuta-tafuta makosa, kugombana, au kunung’unika.

137:1, 5, 6Waabudu wa Yehova waliokuwa uhamishoni waliupenda sana mji wa Sayuni, ambao uliwakilisha tengenezo la Mungu. Namna gani sisi? Je, tunashikamana na tengenezo ambalo Yehova anatumia leo?

138:2. Yehova ‘anayatukuza maneno yake hata juu ya jina lake lote’ katika maana ya kwamba utimizo wa yote ambayo ameahidi katika jina lake utazidi matarajio yoyote ambayo huenda tukawa nayo. Kwa kweli, tuna matarajio mazuri sana.

139:1-6, 15, 16. Yehova anajua kazi zetu, mawazo yetu, na maneno yetu hata kabla hatujayatamka. Anatujua tangu kiini-tete chetu kilipofanyizwa, na hata kabla ya kila sehemu ya mwili wetu kuwa tofauti na nyingine. Ujuzi wa Mungu kuhusu kila mmoja wetu ni wa “ajabu mno” kueleweka. Inafariji kama nini kujua kwamba zaidi ya kuona hali ngumu tunayokabiliana nayo, Yehova anaelewa pia jinsi hali hiyo inavyotuathiri!

139:7-12. Hata tuwe wapi Mungu anaweza kutuimarisha.

139:17, 18. Je, tunapendezwa na kumjua Yehova? (Methali 2:10) Ikiwa ndivyo, basi tumepata chemchemi ya furaha yenye kudumu. Mawazo ya Yehova “ni mengi kuliko hata chembe za mchanga.” Sikuzote tutakuwa na mengi ya kujifunza kumhusu.

139:23, 24. Tunapaswa kutamani Yehova atuchunguze kwa undani ili kuona ‘njia zenye kuumiza’ kama vile mawazo, tamaa, na mielekeo isiyofaa, naye atusaidie kuziondoa. Kufanya hivyo kutatusaidia kuondoa mambo hayo katika moyo wetu.

143:4-7. Tunaweza kuvumiliaje matatizo magumu sana? Mtunga-zaburi anatupa suluhisho: Tutafakari utendaji wa Yehova, tuhangaikie sana kazi zake, na kumwomba msaada.

“Msifuni Yah!”

Kila kimoja cha vitabu vinne vya kwanza vya zaburi kinamalizia kwa maneno ya kumsifu Yehova. (Zaburi 41:13; 72:19, 20; 89:52; 106:48) Kitabu cha mwisho kinamalizia pia kwa maneno ya kumsifu Yehova. Andiko la Zaburi 150:6 linasema hivi: “Kila kitu kinachopumua—na kimsifu Yah. Msifuni Yah!” Maneno hayo yatatimizwa kihalisi katika ulimwengu mpya wa Mungu.

Tunapotazamia wakati huo wenye shangwe, tuna sababu nyingi sana za kumtukuza Mungu wa kweli na kulisifu jina lake. Tunapofikiria furaha tuliyo nayo kwa sababu ya kumjua Yehova na kuwa na uhusiano mzuri pamoja naye, je, hatuchochewi kumsifu kwa moyo wote?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kazi za ajabu za Yehova zinastaajabisha

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mawazo ya Yehova “ni mengi kuliko hata chembe za mchanga”