Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Maombi Yenu na Yajulishwe Mungu”

“Maombi Yenu na Yajulishwe Mungu”

“Maombi Yenu na Yajulishwe Mungu”

“Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.”—WAFILIPI 4:6.

1. Tuna pendeleo la kuwasiliana na nani, na kwa nini jambo hilo linastaajabisha sana?

IKIWA ungeomba uruhusiwe kukutana na mtawala wa nchi yenu, unafikiri ungepata jibu la aina gani? Labda ungepokea jibu la fadhili kutoka kwa wafanyakazi wake, lakini yaelekea sana hungeruhusiwa kuongea na mtawala huyo uso kwa uso. Hata hivyo, Yehova Mungu, yule Mtawala mkuu kuliko wote na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, ni tofauti. Tunaweza kuongea naye tukiwa mahali popote pale na wakati wowote ule. Sikuzote yeye husikia sala zinazokubalika. (Methali 15:29) Hilo ni jambo la kustaajabisha sana! Je, hatupaswi kuonyesha shukrani zetu kwa ajili ya jambo hilo kwa kusali kwa ukawaida kwa Yule ambaye kwa kufaa anaitwa “Msikiaji wa sala”?—Zaburi 65:2.

2. Ni jambo gani linalohitajiwa ili Mungu akubali sala?

2 Hata hivyo, huenda mtu akauliza, ‘Mungu hukubali sala za aina gani?’ Biblia inaeleza jambo moja ambalo linahitajiwa ili sala zikubaliwe: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Naam, kama ilivyoelezwa katika makala iliyotangulia, imani ni takwa muhimu la kumkaribia Mungu. Mungu yuko tayari kukubali sala za wale wanaomkaribia, lakini ni lazima wawe na imani wanapofanya hivyo, watende mema, wawe wanyoofu, na wawe na nia nzuri.

3. (a) Kama inavyoonyeshwa na sala za watumishi waaminifu wa kale, tunaweza kutaja nini katika sala? (b) Tunaweza kutoa sala za aina gani?

3 Mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo wa wakati wake: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.” (Wafilipi 4:6, 7) Biblia ina mifano mingi ya watu waliomweleza Mungu mahangaiko yao. Baadhi yao ni Hana, Eliya, Hezekia, na Danieli. (1 Samweli 2:1-10; 1 Wafalme 18:36, 37; 2 Wafalme 19:15-19; Danieli 9:3-21) Tunapaswa kuiga mfano wao. Pia, ona kwamba maneno ya Paulo yanaonyesha tunaweza kutoa sala za aina mbalimbali. Paulo alitaja kutoa shukrani, yaani, sala ya kueleza uthamini wetu kwa ajili ya mambo ambayo Mungu anatufanyia. Sala hiyo inaweza kutia ndani kutoa sifa. Dua ni sihi ya unyenyekevu inayotolewa kwa hisia nyingi. Na tunaweza pia kutoa maombi, au kuomba jambo fulani hususa. (Luka 11:2, 3) Baba yetu wa mbinguni yuko tayari kutukubali tunapomkaribia kupitia njia yoyote kati ya hizo.

4. Ingawa Yehova anajua mahitaji yetu, kwa nini sisi humjulisha maombi yetu?

4 Huenda wengine wakauliza, ‘Si Yehova tayari anajua mahitaji yetu yote?’ Ndiyo, anayajua. (Mathayo 6:8, 32) Basi, kwa nini anataka tumjulishe maombi yetu? Fikiria mfano huu: Mwenye duka anaweza kuamua kuwapa zawadi baadhi ya wateja wake. Hata hivyo, ili wateja hao waipokee, ni lazima wamwendee mwenye duka na kumwomba zawadi hiyo. Wateja wasiotaka kujitahidi kufanya hivyo wataonyesha kuwa hawaithamini. Vivyo hivyo, tusipotaja maombi yetu katika sala, tutaonyesha kwamba hatuthamini mambo ambayo Yehova anatuandalia. Yesu alisema hivi: “Ombeni nanyi mtapokea.” (Yohana 16:24) Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kuwa tunamtegemea Mungu.

Tunapaswa Kumkaribiaje Mungu?

5. Kwa nini tunahitaji kusali katika jina la Yesu?

5 Yehova hakuweka sheria nyingi ngumu za jinsi tunavyopaswa kusali. Hata hivyo, tunahitaji kujua njia inayofaa ya kumkaribia Mungu, ambayo inatajwa katika Biblia. Kwa mfano, Yesu aliwafundisha wafuasi wake hivi: “Mkimwomba Baba jambo lolote atawapa katika jina langu.” (Yohana 16:23) Hivyo, tunapaswa kusali katika jina la Yesu, tukitambua kwamba Yesu ndiye njia pekee ambayo Mungu anatumia kuwawezesha wanadamu wote wapate baraka zake.

6. Tunapaswa kuwa katika mkao gani tunaposali?

6 Tunapaswa kuwa katika mkao gani tunaposali? Biblia haitaji kihususa jinsi tunavyopaswa kukaa ili sala zetu zisikilizwe. (1 Wafalme 8:22; Nehemia 8:6; Marko 11:25; Luka 22:41) Jambo la maana ni kusali kwa Mungu kwa unyoofu tukiwa na nia nzuri.—Yoeli 2:12, 13.

7. (a) Neno “amina” linamaanisha nini? (b) Neno hilo hutumiwaje kwa njia inayofaa katika sala?

7 Namna gani kutumia neno “amina”? Maandiko yanaonyesha kwamba kwa kawaida huo ni umalizio mzuri wa sala zetu, hasa tunaposali mbele ya watu. (Zaburi 72:19; 89:52) Neno la Kiebrania ʼa·menʹ linamaanisha “hakika.” Kitabu kimoja (Cyclopedia cha McClintock na Strong) kinaeleza kuwa “Amina” husemwa mwishoni mwa sala ili “kukubaliana na maneno yaliyotangulia kusemwa, na kuomba yatimie.” Hivyo, mtu anapomalizia sala kwa kusema “Amina” kwa unyoofu, yeye huonyesha jinsi anavyohisi moyoni kuhusu mambo ambayo ametangulia kusema. Mkristo anayewakilisha kutaniko katika sala anapomalizia kwa neno hilo, wale wanaosikiliza wanaweza pia kusema “Amina” kimyakimya au kwa sauti ili kuonyesha kwamba wanakubaliana kabisa na yale ambayo yamesemwa.—1 Wakorintho 14:16.

8. Baadhi ya sala zetu zinawezaje kuwa kama sala ya Yakobo au Abrahamu, na hilo litaonyesha nini kutuhusu?

8 Nyakati nyingine, Mungu anaweza kuacha tuonyeshe uzito wa mambo tunayotaja katika sala. Huenda tukahitaji kuwa kama Yakobo wa kale, ambaye alipigana mweleka usiku kucha na malaika ili abarikiwe. (Mwanzo 32:24-26) Au katika hali fulani huenda tukahitaji kuwa kama Abrahamu, ambaye alimwomba Yehova tena na tena kwa niaba ya Loti na watu wengine waadilifu ambao wangepatikana Sodoma. (Mwanzo 18:22-33) Sisi pia tunaweza kumsihi Yehova kuhusiana na mambo tunayoyapenda sana, na kumwomba kwa msingi wa haki yake, fadhili zake zenye upendo, na rehema zake.

Tunaweza Kuomba Nini?

9. Tunapaswa kuhangaikia nini hasa tunaposali?

9 Kumbuka kwamba Paulo alisema hivi: “Katika kila jambo . . . maombi yenu na yajulishwe Mungu.” (Wafilipi 4:6) Hivyo, sala za kibinafsi zinaweza kuhusisha karibu sehemu zote za maisha. Hata hivyo, katika sala zetu tunapaswa kutanguliza mapenzi ya Yehova. Danieli aliweka mfano bora kuhusiana na jambo hilo. Wakati Waisraeli walipoadhibiwa kwa sababu ya dhambi zao, Danieli alimwomba Yehova aonyeshe rehema, akisema: “Usikawie, ee Mungu wangu, kwa ajili ya . . . jina lako!” (Danieli 9:15-19, Biblia Habari Njema) Je, sala zetu pia zinaonyesha kuwa tunahangaikia hasa kutakaswa kwa jina la Yehova na kutimizwa kwa mapenzi yake?

10. Tunajuaje kwamba inafaa kusali kuhusu mambo ya kibinafsi?

10 Hata hivyo, inafaa pia kuomba kuhusu mambo ya kibinafsi. Kwa mfano, kama mtunga-zaburi, tunaweza kusali ili tuelewe mambo mazito ya kiroho. Alisali hivi: “Unifanye nielewe, ili nipate kuishika sheria yako nami nipate kuishika kwa moyo wote.” (Zaburi 119:33, 34; Wakolosai 1:9, 10) Yesu “alitoa dua na pia maombi kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa kutoka katika kifo.” (Waebrania 5:7) Kwa kufanya hivyo, alionyesha kwamba inafaa kuomba nguvu wakati mtu anapokabili hatari au majaribu. Alipowafundisha wanafunzi wake ile sala ya mfano, Yesu alitia ndani mambo ya kibinafsi, kama vile kusamehe makosa na kupata chakula cha kila siku.

11. Sala inaweza kutusaidiaje tusianguke tunaposhawishiwa?

11 Katika sala hiyo ya mfano, Yesu alitoa ombi hili: “Usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mathayo 6:9-13) Baadaye, alitoa shauri hili: “Endeleeni kukesha na kusali sikuzote, ili msiingie katika jaribu.” (Mathayo 26:41) Sala ni muhimu tunapokabili vishawishi. Tunaweza kushawishiwa kupuuza kanuni za Biblia tunapokuwa kazini au shuleni. Watu ambao si Mashahidi wanaweza kutualika tushirikiane nao kufanya mambo yasiyofaa. Tunaweza kuombwa tufanye jambo lisilopatana na kanuni za uadilifu. Katika pindi hizo, inafaa tufuate shauri la Yesu la kusali, kabla ya kishawishi na pia wakati tunapokabiliwa nacho, ili kumwomba Mungu atusaidie tusianguke katika kishawishi.

12. Ni mambo gani yanayosababisha mahangaiko ambayo yanaweza kutuchochea kusali, nasi tunaweza kutarajia Yehova afanye nini?

12 Watumishi wa Mungu leo hukabili mikazo na mahangaiko mbalimbali. Wengi wanasumbuliwa hasa na magonjwa na mfadhaiko. Jeuri huchangia mkazo maishani. Matatizo ya kiuchumi hufanya iwe vigumu kupata riziki. Inafariji sana kujua kwamba Yehova huwasikiliza watumishi wake wanaomweleza mambo hayo! Zaburi 102:17 inasema hivi kumhusu Yehova: “Hakika ataielekea sala ya wale waliovuliwa kila kitu, naye hataidharau sala yao.”

13. (a) Inafaa kusali kuhusu mambo gani ya kibinafsi? (b) Simulia kisa kinachohusu sala ya aina hiyo.

13 Naam, inafaa kusali kuhusu jambo lolote linaloathiri utumishi wetu kwa Yehova au uhusiano wetu pamoja naye. (1 Yohana 5:14) Ikiwa unakabili maamuzi kuhusu ndoa, kazi, au kupanua utumishi wako, sema na Mungu kwa uhuru kuhusu mambo hayo na umwombe mwongozo wake. Kwa mfano, mwanamke mmoja nchini Ufilipino alitaka kuwa mtumishi wa wakati wote. Hata hivyo, hakuwa na kazi ambayo ingemtegemeza. Anasema hivi: “Jumamosi moja, nilisali kwa Yehova waziwazi kuhusu upainia. Baadaye siku hiyohiyo, nilipokuwa nikihubiri, nilimpa msichana mmoja kitabu. Kwa ghafula, msichana huyo akasema hivi: ‘Unapaswa kuja katika shule yetu Jumatatu asubuhi.’ Nikamuuliza, ‘Kwa nini?’ Akaniambia kwamba kuna nafasi ya kazi na mfanyakazi anahitajiwa haraka iwezekanavyo. Nilienda huko, nami nikaajiriwa papo hapo. Mambo yote hayo yalitendeka haraka sana.” Mashahidi wengi ulimwenguni pote wamejionea mambo kama hayo. Basi, usisite kumjulisha Mungu maombi yako ya kutoka moyoni!

Namna Gani Ikiwa Tumetenda Dhambi?

14, 15. (a) Kwa nini mtu hapaswi kusita kusali hata ikiwa ametenda dhambi? (b) Zaidi ya kutoa sala za kibinafsi, ni jambo gani lingine litakalomsaidia mtu aliyetenda dhambi apone?

14 Sala inaweza kumsaidiaje mtu aliyetenda dhambi? Huenda wengine waliotenda dhambi wakaona aibu kusali. Lakini hilo si jambo la hekima. Kwa mfano: Msafiri anajua kwamba akipotea, anaweza kuomba watu wengine wamwonyeshe njia. Hata hivyo, itakuwaje msafiri huyo akisita kuwaomba watu wamwonyeshe njia eti kwa sababu anaaibika kwamba amepotea? Hiyo inaweza kuwa hatari! Vivyo hivyo, mtu aliyetenda dhambi anaweza kuumia zaidi akiaibika kusali kwa Mungu. Kuaibikia dhambi hakupaswi kumzuia mtu asizungumze na Yehova. Mungu anawaalika wale waliotenda dhambi nzito wasali kwake. Nabii Isaya aliwahimiza watenda-dhambi wa siku zake wamwite Yehova, “kwa maana atasamehe kwa njia kubwa.” (Isaya 55:6, 7) Ni wazi kwamba mtu anahitaji ‘kuutuliza uso wa Yehova,’ kwanza kwa kujinyenyekeza, kuacha dhambi, na kutubu kikweli.—Zaburi 119:58; Danieli 9:13.

15 Sala ni muhimu kwa njia nyingine wakati mtu anapotenda dhambi. Mwanafunzi Yakobo anasema hivi kuhusu mtu anayehitaji msaada wa kiroho: “Na awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, nao wasali juu yake, . . . na Yehova atamwinua.” (Yakobo 5:14, 15) Naam, mtu anapaswa kuungama dhambi yake mbele za Yehova katika sala, lakini anaweza pia kuwaomba wanaume wazee wasali kwa ajili yake. Hilo litamsaidia kupona kiroho.

Majibu kwa Sala

16, 17. (a) Yehova hujibuje sala? (b) Ni mambo gani yaliyoonwa yanayoonyesha kwamba sala na kazi ya kuhubiri zinahusiana sana?

16 Sala hujibiwaje? Nyingine zinaweza kujibiwa haraka na kwa njia inayoonekana wazi. (2 Wafalme 20:1-6) Nyingine zinaweza kujibiwa baada ya muda fulani, na huenda zisijibiwe kwa njia inayoonekana wazi. Kama ilivyoonyeshwa katika mfano wa Yesu kuhusu mjane aliyemwendea mwamuzi tena na tena, huenda tukahitaji kusali kwa Mungu tena na tena. (Luka 18:1-8) Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tunaposali kupatana na mapenzi ya Mungu, Yehova hatatuambia kamwe: ‘Acheni kunisumbua.’—Luka 11:5-9.

17 Watu wa Yehova wameona sala zao zikijibiwa mara nyingi. Hilo limeonekana mara nyingi katika kazi yetu ya kuhubiri. Kwa mfano, dada wawili Wakristo nchini Ufilipino walikuwa wakigawa vichapo vya Biblia katika eneo la mbali. Walipompa mwanamke mmoja trakti, mwanamke huyo alitokwa na machozi. Alisema hivi: “Jana usiku nilimwomba Mungu anitumie mtu wa kunifundisha Biblia, nami nafikiri kwamba sala yangu imejibiwa.” Muda mfupi baadaye, mwanamke huyo alianza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Katika sehemu nyingine ya Kusini-Mashariki mwa Asia, ndugu mmoja Mkristo alikuwa na wasiwasi kuhusu kuhubiri katika jengo lenye ulinzi mkali. Hata hivyo, ndugu huyo alisali kwa Yehova, akajipa ujasiri, na kuingia ndani ya jengo hilo. Alipogonga mlango mmoja, mwanamke mmoja akatokea. Ndugu huyo alipomweleza kusudi lake la kufika hapo, mwanamke huyo alianza kulia. Mwanamke huyo alisema kwamba amekuwa akiwatafuta Mashahidi wa Yehova na kwamba alikuwa amesali awapate. Ndugu huyo alimsaidia kuwasiliana na kutaniko la karibu la Mashahidi wa Yehova.

18. (a) Sala zetu zinapojibiwa, tunapaswa kutendaje? (b) Tunaweza kuwa na uhakika gani tukisali kila wakati?

18 Kwa kweli, sala ni zawadi bora sana. Yehova yuko tayari kusikiliza na kujibu. (Isaya 30:18, 19) Hata hivyo, tunapaswa kuwa macho kuona jinsi Yehova anavyojibu sala zetu. Nyakati nyingine, huenda tukajibiwa kwa njia tofauti na ile tunayotarajia. Lakini, tunapotambua mwongozo wake, hatupaswi kamwe kusahau kumshukuru na kumsifu. (1 Wathesalonike 5:18) Isitoshe, sikuzote kumbuka shauri hili la mtume Paulo: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.” Naam, tumia vizuri kila nafasi kuzungumza na Mungu. Ukifanya hivyo, utaendelea kujionea ukweli wa yale ambayo Paulo anasema kuhusu watu wanaojibiwa sala zao: “Amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.”—Wafilipi 4:6, 7.

Je, Unaweza Kujibu?

• Tunaweza kutoa sala za aina gani?

• Tunapaswa kusali jinsi gani?

• Tunaweza kutaja mambo gani katika sala zetu?

• Sala humsaidiaje mtu aliyetenda dhambi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Sala ya kutoka moyoni hutusaidia tusianguke tunaposhawishiwa

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kupitia sala, tunamshukuru Mungu, tunamweleza mahangaiko yetu, na kumwomba