Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mpendwa Wako Anapomwacha Yehova

Mpendwa Wako Anapomwacha Yehova

Mpendwa Wako Anapomwacha Yehova

MARK na Louise ni Mashahidi wa Yehova. * Waliwafundisha watoto wao Maandiko kwa upendo kama vile Biblia inavyowahimiza wazazi Wakristo kufanya. (Methali 22:6; 2 Timotheo 3:15) Kwa kusikitisha, si watoto wao wote walioendelea kumtumikia Yehova baada ya kuwa watu wazima. Louise anasema hivi: “Mimi huumia sana moyoni ninapowafikiria watoto wangu ambao wamemwacha Yehova. Nawezaje kujifanya kwamba siumii kila siku kwa sababu ya jambo hilo? Wengine wanapozungumza kuhusu wana wao, mimi huumia sana moyoni na inanibidi nijizuie nisilie.”

Naam, mtu anapoamua kumwacha Yehova na njia ya uzima inayoonyeshwa katika Maandiko, kwa kawaida, watu wa familia yao ambao ni waaminifu huhuzunika sana. Irene anasema hivi: “Nampenda sana dada yangu. Ningependa sana kuona akimrudia Yehova!” Maria, ambaye ndugu yake alimwacha Yehova kwa sababu ya mwenendo wake usio wa adili, anasema hivi: “Imekuwa vigumu kwangu kuvumilia jambo hilo kwa sababu amekuwa msaada mkubwa kwangu katika mambo mengine. Mimi humkosa sana hasa wakati wa karamu za familia.”

Kwa Nini Ni Vigumu Sana?

Kwa nini watu wa ukoo ambao ni Wakristo huumia sana wakati wanapompoteza kiroho mtoto wao au mpendwa wao? Ni kwa sababu wanajua kwamba Maandiko yanaahidi uzima wa milele katika paradiso duniani kwa wale ambao watabaki washikamanifu kwa Yehova. (Zaburi 37:29; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3-5) Wanatazamia kupata baraka hizo pamoja na wenzi wao, watoto wao, wazazi wao, ndugu na dada zao, na wajukuu wao. Wanaumia sana wanapofikiria kwamba huenda wapendwa wao ambao wameacha kumtumikia Yehova wakakosa baraka hizo! Hata kuhusu maisha yao ya sasa, Wakristo wanaelewa kwamba sheria na kanuni za Yehova ni kwa faida yao. Hivyo, Wakristo huumia moyoni wanapowaona wapendwa wao wakipanda kwa njia ambayo itawafanya wavune kwa uchungu.—Isaya 48:17, 18; Wagalatia 6:7, 8.

Huenda ikawa vigumu kwa wengine ambao hawajampoteza mpendwa kiroho kuelewa jinsi hali hiyo inavyoumiza sana. Karibu kila sehemu ya maisha inaathiriwa. Louise anasema hivi: “Imekuwa vigumu sana kuwa kwenye mikutano ya Kikristo na kuona wazazi wakicheka na kuzungumza na watoto wao. Ninapokuwa kwenye tukio lolote lenye kufurahisha, mimi huhuzunika kwa sababu ya kuwakosa wapendwa wangu.” Mzee mmoja Mkristo anakumbuka miaka minne ambapo binti ya mke wake hakushirikiana nao. Anasema hivi: “Mara nyingi, hata katika pindi zenye kufurahisha, tulihisi uchungu moyoni. Hata nilipompa mke wangu zawadi au kwenda matembezi pamoja naye mwishoni mwa juma, alilia alipokumbuka kwamba binti yake hakuwapo.”

Je, maoni ya Wakristo hao yamepita kiasi? La. Kwa kuwa wanadamu waliumbwa kwa mfano wa Yehova, huenda kwa kadiri fulani Wakristo hao wakawa wanaonyesha sifa zake. (Mwanzo 1:26, 27) Hilo linamaanisha nini? Yehova alihisije watu wake Israeli walipomwasi? Katika andiko la Zaburi 78:38-41, tunajifunza kwamba Yehova alihuzunishwa na kutiwa uchungu. Hata hivyo, aliwaonya kwa subira, akawatia nidhamu, na kuwasamehe tena na tena walipoonyesha toba. Bila shaka, Yehova anapenda sana viumbe wake, ‘kazi ya mikono yake,’ naye hawaachi kwa urahisi. (Ayubu 14:15; Yona 4:10, 11) Aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo huo pia wa kushikamana na wapendwa wao. Na watu wa familia wanaweza kupendana sana. Basi haishangazi kwamba wanadamu wanaweza kuhuzunika sana mtu wa ukoo anapomwacha Yehova.

Kwa kweli, kumpoteza kiroho mpendwa ni mojawapo ya majaribu makali zaidi ambayo waabudu wa kweli hukabili. (Matendo 14:22) Yesu alisema kwamba kukubali ujumbe wake kungesababisha mgawanyiko katika familia fulani. (Mathayo 10:34-38) Hilo si kwa sababu ujumbe wa Biblia husababisha mgawanyiko katika familia. Badala yake, ni watu wa familia ambao si waamini au wasio waaminifu ndio husababisha mgawanyiko kwa kuukataa, kuuacha, au hata kuupinga Ukristo. Hata hivyo, tunamshukuru Yehova kwamba hawaachi waaminifu wake bila msaada wa kukabiliana na majaribu hayo. Ikiwa kwa sasa unahuzunika kwa sababu ya kumpoteza kiroho mpendwa wako, ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kukusaidia kuvumilia huzuni hiyo na kupata shangwe na uradhi wa kadiri fulani?

Kukabiliana na Hali Hiyo

“Kwa kujijenga wenyewe . . . , jitunzeni katika upendo wa Mungu.” (Yuda 20, 21) Ikitegemea hasa hali zako, huenda hakuna jambo lolote unaloweza kufanya wakati huu ili kumsaidia mtu wa familia ambaye ameacha kumtumikia Yehova. Hata hivyo, unaweza na unapaswa kujiimarisha mwenyewe kiroho na pia kuwaimarisha watu wengine wa familia ambao ni waaminifu. Veronica, ambaye wana wake watatu waliiacha kweli, anasema hivi: “Mimi na mume wangu tulikumbushwa kwamba tukibaki wenye nguvu kiroho, itakuwa rahisi zaidi kwetu kuwakaribisha wana wetu watakaporudiwa na fahamu zao. Ingekuwa vigumu kwa mwana mpotevu kurudi nyumbani ikiwa baba yake hangekuwa katika hali nzuri ya kumpokea tena.”

Ili uendelee kuwa mwenye nguvu kiroho, jishughulishe na mambo ya kiroho. Hilo linatia ndani kuwa na ratiba ya kujifunza Biblia kwa undani na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Uwe tayari kuwasaidia wengine kutanikoni kwa kadiri hali zako zinavyoruhusu. Ni kweli kwamba mwanzoni huenda ukaona ni vigumu kufanya mambo hayo. Veronica anakumbuka hivi: “Wazo lililokuja akilini kwa mara ya kwanza ni kujitenga na wengine kama mnyama aliyeumizwa. Lakini mume wangu alisisitiza kwamba tunapaswa kuendelea kuwa na ratiba nzuri ya mambo ya kiroho. Hivyo, alihakikisha kwamba tulihudhuria mikutano. Wakati ulipofika wa kuhudhuria kusanyiko la wilaya, nilihitaji ujasiri mwingi ili kwenda huko na kukutana na watu. Hata hivyo, programu ilitufanya tumkaribie zaidi Yehova. Mwana wetu aliyebaki mwaminifu aliimarishwa sana na kusanyiko hilo.”

Maria, aliyetajwa mwanzoni, anasema kwamba jambo linalomsaidia hasa ni kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri, na sasa anasaidia watu wanne kujifunza Biblia. Vivyo hivyo, Laura anasema hivi: “Ingawa bado mimi hulia kila siku, ninamshukuru Yehova kwamba hata ingawa sikupata mafanikio ambayo wazazi wengine wamepata kwa kuwalea watoto, nina ujumbe mzuri wa Biblia ambao unaweza kuzisaidia familia katika siku hizi za mwisho.” Ken na Eleanor, ambao wana watoto wakubwa walioliacha kutaniko, walipanga kuhamia katika eneo ambalo lina uhitaji wa wahubiri wa Ufalme ili kufanya utumishi wa wakati wote. Hilo limewasaidia kuona mambo kwa njia inayofaa na kuepuka kumezwa na huzuni.

Usikate tamaa. Upendo “hutumaini mambo yote.” (1 Wakorintho 13:7) Ken, aliyetajwa hapo juu, anasema hivi: “Watoto wetu walipoiacha njia ya kweli, niliona ni kana kwamba wamekufa. Lakini baada ya kifo cha dada yangu, maoni yangu yalibadilika. Ninashukuru kwamba watoto wangu hawakufa kihalisi na kwamba Yehova anaendelea kuacha njia ikiwa wazi ili wamrudie.” Mambo ya hakika yameonyesha kwamba wengi ambao wameiacha kweli mwishowe hurudi.—Luka 15:11-24.

Shinda hisia za kujilaumu. Huenda wazazi wakafikiria wakati uliopita na kujuta kwamba hawakushughulikia mambo fulani kwa njia nzuri. Hata hivyo, wazo kuu linaloonyeshwa katika andiko la Ezekieli 18:20 ni kwamba Yehova humhesabia mtenda-dhambi kuwa ndiye mwenye hatia kwa sababu ya uamuzi wake mbaya, bali si wazazi wake. Inapendeza kujua kwamba ingawa kitabu cha Methali kinazungumzia sana wajibu wa wazazi wa kuwalea watoto wao katika njia inayofaa, mashauri ambayo vijana wanapewa ili wawasikilize na kuwatii wazazi wao ni mara nne zaidi ya yale ambayo wazazi wanapewa. Naam, watoto wana daraka la kukubali mazoezi yanayotegemea Biblia ambayo yanatolewa na wazazi wao wasio wakamilifu. Yaelekea wakati huo ulishughulikia mambo kwa kadiri ulivyoweza. Lakini, hata ingawa unahisi kwamba ulifanya makosa fulani na kwamba wewe ndiye uliyekosea, hilo halimaanishi kwamba makosa yako ndiyo yaliyosababisha mpendwa wako aiache kweli. Vyovyote vile, hatupati faida yoyote kwa kujilaumu kwa maneno kama “laiti ningefanya hivi au vile.” Jifunze kutokana na makosa yako, azimia kutoyarudia, na sali kwa Yehova ili akusamehe. (Zaburi 103:8-14; Isaya 55:7) Kisha, kazia macho yako wakati ujao, wala si wakati uliopita.

Waonyeshe wengine subira. Huenda ikawa vigumu kwa wengine kujua jinsi ya kukutia moyo au kukufariji, hasa ikiwa hawajawahi kupatwa na jambo unalokabili. Isitoshe, watu wana maoni tofauti kuhusu mambo ambayo yanaweza kuwatia moyo au kuwafariji wengine. Hivyo, wengine wakisema mambo ambayo yanakukasirisha, tumia shauri la mtume Paulo kwenye Wakolosai 3:13: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”

Heshimu mpango wa Yehova wa nidhamu. Ikiwa mtu wa ukoo ametiwa nidhamu na kutaniko, kumbuka kwamba hiyo ni sehemu ya mpango wa Yehova na ni kwa faida ya wote, kutia ndani mkosaji. (Waebrania 12:11) Hivyo, pinga mwelekeo wa kulaumu wazee walioshughulikia kisa hicho au maamuzi waliyofanya. Kumbuka kwamba matokeo mazuri yanatokana na kufanya mambo kulingana na njia za Yehova, lakini kupinga mipango ya Yehova huzidisha tu matatizo.

Baada ya Waisraeli kukombolewa kutoka Misri, mara nyingi Musa alitumikia akiwa mwamuzi. (Kutoka 18:13-16) Kwa kuwa hukumu iliyotolewa kwa faida ya mtu mmoja ingemwadhibu mtu mwingine, inaeleweka kwamba wengine hawakufurahia maamuzi ya Musa. Huenda kulaumu-laumu maamuzi ya Musa kulichangia kwa kadiri fulani uasi dhidi ya uongozi wake. Lakini, Yehova alimtumia Musa kuwaongoza watu Wake, na Yehova hakumwadhibu Musa, bali waasi na watu wa familia zao ambao waliwaunga mkono. (Hesabu 16:31-35) Tunaweza kujifunza kutokana na tukio hilo kwa kujitahidi kuheshimu na kuunga mkono maamuzi yanayofanywa na wale walio na mamlaka ya kitheokrasi leo.

Kuhusiana na hilo, Delores anakumbuka jinsi ilivyokuwa vigumu kwake kuwa na maoni yenye kusawazika binti yake alipotiwa nidhamu na kutaniko. Delores anasema hivi: “Kilichonisaidia ni kusoma tena na tena makala zilizoonyesha kwamba mipango ya Yehova ni yenye usawaziko. Nilikuwa na kitabu cha pekee ambamo niliandika mambo makuu niliyosikia katika hotuba au mambo niliyosoma katika makala fulani ambayo yangenisaidia kuvumilia na kuendelea kumtumikia Yehova.” Kuna jambo lingine muhimu linaloweza kutusaidia kukabiliana na hali hiyo.

Eleza jinsi unavyohisi. Huenda ukaona inafaa kuzungumza jambo hilo pamoja na rafiki mmoja au wawili ambao unawatumaini. Hivyo, chagua marafiki ambao watakusaidia kudumisha mtazamo unaofaa. Hata hivyo, njia yenye matokeo zaidi ni ‘kumimina moyo wako’ kwa Yehova katika sala. * (Zaburi 62:7, 8) Kwa nini? Kwa sababu Yehova anaelewa kwa undani zaidi jinsi unavyohisi. Kwa mfano, huenda ukahisi kuwa hukupaswa kupatwa na hali hiyo. Vyovyote vile, si wewe uliyemwacha Yehova. Mweleze Yehova jinsi unavyohisi, na umwombe akusaidie uwe na maoni yanayofaa kuhusu hali hiyo.—Zaburi 37:5.

Kadiri muda unavyopita, yaelekea utaweza kuvumilia vizuri zaidi hisia zako. Wakati huohuo, usiache kujitahidi kumpendeza Baba yako wa mbinguni, na usihisi kamwe kwamba jitihada zako ni za bure. (Wagalatia 6:9) Kumbuka kwamba ikiwa tutamwacha Yehova, bado tutakuwa tu na matatizo. Kwa upande mwingine, tunapobaki washikamanifu kwake, anatusaidia tukabiliane na majaribu. Basi, uwe na hakika kwamba Yehova anaelewa vizuri hali yako naye ataendelea kukupa nguvu unazohitaji kwa wakati unaofaa.—2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:13; Waebrania 4:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 19 Kuhusu kusali kwa ajili ya mtu wa ukoo aliyetengwa na ushirika, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 2001, ukurasa wa 30-31.

[Sanduku katika ukurasa wa 19]

Jinsi ya Kukabiliana na Hali Hiyo

◆ “Kwa kujijenga wenyewe . . . , jitunzeni katika upendo wa Mungu.” Yuda 20, 21.

◆ Usikate tamaa.1 Wakorintho 13:7.

◆ Shinda hisia za kujilaumu. Ezekieli 18:20.

◆ Waonyeshe wengine subira. Wakolosai 3:13.

◆ Heshimu mpango wa Yehova wa nidhamu.Waebrania 12:11.

◆ Eleza jinsi unavyohisi.Zaburi 62:7, 8.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Je, Umemwacha Yehova?

Ikiwa ndivyo, hata uwe na sababu gani, uhusiano wako pamoja na Yehova na matarajio yako ya milele yako hatarini. Labda unakusudia kumrudia Yehova. Je, unajitahidi sana kufanya hivyo sasa? Au je, unaahirisha hilo hadi wakati unaodhania kuwa utakufaa? Kumbuka kwamba Har–Magedoni inakaribia sana. Isitoshe, maisha katika mfumo huu ni mafupi na yanaweza kubadilika wakati wowote. Huwezi hata kujua ikiwa utakuwa hai kesho. (Zaburi 102:3; Yakobo 4:13, 14) Mtu mmoja aliyegunduliwa ana ugonjwa wa kufisha, alisema hivi: “Nilipata ugonjwa huo nikiwa mtumishi wa Yehova wa wakati wote, nami sikuwa nimeficha jambo lolote. Ninafurahi sana kuhisi hivyo.” Lakini, wazia ikiwa mtu huyo angepata ugonjwa huo huku akiendelea tu kusema, “Siku moja, nitamrudia Yehova!” Ikiwa umemwacha Yehova, huu ndio wakati mzuri zaidi wa kurudi.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kujishughulisha na mambo ya kiroho kunaweza kukusaidia kuwa na maoni yanayofaa