Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Tunaishi Katika “Siku za Mwisho”?

Je, Kweli Tunaishi Katika “Siku za Mwisho”?

Je, Kweli Tunaishi Katika “Siku za Mwisho”?

MABADILIKO ya aina mbili yanatusaidia kuelewa siku za mwisho zinazotajwa katika Biblia. Maandiko yalitabiri mambo ambayo yangetukia wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3) Pia, Biblia inazungumza kuhusu mabadiliko katika mielekeo na matendo ya watu wanaoishi katika “siku za mwisho.”—2 Timotheo 3:1.

Matukio ya ulimwengu pamoja na mwenendo na nyutu za watu zinathibitisha kwamba tunaishi katika siku za mwisho na kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaleta baraka za kudumu kwa ajili ya wale wanaompenda Mungu. Acheni tuanze kuchunguza mambo matatu ambayo Yesu alisema yangeonyesha siku za mwisho.

“Mwanzo wa Maumivu ya Taabu”

Yesu alisema hivi: “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine.” Kisha akaongeza hivi: “Mambo yote hayo ni mwanzo wa maumivu ya taabu.” (Mathayo 24:7, 8) Acheni tuchunguze ‘mambo hayo’ moja baada ya lingine.

Watu wengi sana walikufa kwa sababu ya vita na mapambano ya kikabila katika karne iliyopita. Kulingana na ripoti ya taasisi moja (Worldwatch Institute), “idadi ya watu waliokufa kwa sababu ya vita katika karne [ya 20] ni zaidi ya mara tatu ya wale waliokufa kutokana na vita tangu karne ya kwanza W.K. hadi mwaka wa 1899.” Katika kitabu chake (Humanity—A Moral History of the Twentieth Century), Jonathan Glover anaandika hivi: “Inakadiriwa kwamba tangu mwaka wa 1900 hadi 1989, watu milioni 86 walikufa kutokana na vita. . . . Idadi ya watu ambao wamekufa vitani katika karne ya 20 ni kubwa sana. Si sahihi kusema kwamba idadi ya vifo hivyo ilikuwa ileile katika kipindi hicho chote kwa karibu theluthi mbili ya watu hao (milioni 58) walikufa katika vita viwili vya ulimwengu. Lakini, ikiwa vifo hivyo vingetokea katika kipindi chote cha karne ya 20, watu 2,500 wangekufa kutokana na vita kila siku, yaani, watu zaidi ya 100 wangekufa baada ya kila saa moja, kwa miaka 90.” Je, unaweza kuwazia jinsi mamilioni ya watu wa ukoo na marafiki walivyohuzunika kwa sababu ya kupoteza watu wao?

Licha ya kwamba ulimwengu unatokeza chakula kingi, upungufu wa chakula ni mojawapo ya mambo ambayo yalitabiriwa yatatokea siku za mwisho. Watafiti wanasema kwamba katika miaka 30 iliyopita, kiasi cha chakula kinachozalishwa kimeongezeka haraka kuliko ongezeko la idadi ya watu. Hata hivyo, kuna upungufu wa chakula katika sehemu nyingi ulimwenguni kwa sababu watu wengi hawana mashamba ya kutosha ya kuzalisha chakula wala pesa za kununua chakula. Katika nchi zinazoendelea, watu bilioni 1.2 hivi huishi kwa dola moja (ya Marekani) kwa siku au chini ya dola moja. Kati yao, milioni 780 hivi hawapati chakula kwa muda mrefu. Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, watoto zaidi ya milioni tano hufa kila mwaka hasa kwa sababu ya kukosa chakula kinachofaa.

Namna gani matetemeko ya nchi ambayo yalitabiriwa? Kulingana na Shirika la Marekani la Uchunguzi wa Jiolojia, kwa wastani, kila mwaka tangu 1990, kumekuwa na matetemeko 17 ya nchi ambayo yanaweza kuharibu majengo. Kwa wastani, matetemeko ya nchi yanayoweza kuharibu majengo kabisa yametokea mara moja kila mwaka. Kulingana na chanzo kingine, “matetemeko ya nchi yamesababisha vifo vya mamia ya maelfu ya watu katika miaka 100 iliyopita.” Sababu moja ni kwamba tangu mwaka wa 1914, idadi ya watu imeongezeka sana katika sehemu zinazokumbwa na matetemeko ya nchi.

Matukio Mengine Makuu

Yesu alisema hivi: “Katika mahali pamoja baada ya pengine kutakuwa na tauni.” (Luka 21:11) Leo, kuliko wakati mwingine wowote kuna maendeleo makubwa katika sayansi ya tiba. Lakini bado, magonjwa ambayo yamekuwapo na mengine mapya yanaendelea kuwakumba wanadamu. Hati ya Baraza la Kitaifa la Ujasusi la Marekani inasema hivi: “Magonjwa 20 yanayojulikana sana kutia ndani ugonjwa wa kifua kikuu, malaria, na kipindupindu, yametokea tena au kuenea tangu mwaka wa 1973, na mara nyingi huwa sugu kiasi cha kutoweza kutibika. Angalau virusi 30 ambavyo havikujulikana zamani vimegunduliwa tangu mwaka wa 1973, kutia ndani virusi vya UKIMWI, Ebola, ugonjwa wa ini, na Nipah, na hakuna tiba.” Kulingana na ripoti ya Msalaba Mwekundu ya Juni 28, 2000, idadi ya watu ambao walikufa kutokana na magonjwa ya kuambukiza katika mwaka uliotangulia ni zaidi ya mara 160 ya idadi ya wale waliokufa kutokana na misiba ya asili.

“Kuongezeka kwa uasi-sheria,” ni jambo lingine muhimu linaloonyesha siku za mwisho. (Mathayo 24:12) Katika sehemu nyingi duniani leo, watu hufunga nyumba zao, na hawajihisi salama wanapotembea barabarani usiku. Namna gani kuhusu uchafuzi wa hewa, maji, na uharibifu wa mashamba ambao unatukia leo, mara nyingi kwa sababu ya matendo haramu? Hilo pia linatimiza yale yaliyotabiriwa katika Biblia. Kitabu cha Ufunuo kinazungumzia wakati uliowekwa rasmi na Mungu wa “kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.”—Ufunuo 11:18.

Tabia za Watu Wanaoishi Siku za Mwisho

Tafadhali fungua Biblia yako na usome andiko la 2 Timotheo 3:1-5. Mtume Paulo anaandika hivi: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Kisha anaorodhesha mambo 20 ambayo yangewatambulisha watu wasiomwogopa Mungu. Je, umeona watu wanaoishi katika jamii yenu wakifanya baadhi ya mambo hayo? Ona yale ambayo yamesemwa hivi karibuni kuhusu watu wa siku hizi.

“Wenye kujipenda wenyewe.” (2 Timotheo 3:2) “Leo [watu] wanasisitiza kuishi wapendavyo kuliko wakati mwingine wowote. [Wamekuwa] miungu na wanataka watendewe hivyo.”—Gazeti la Financial Times, Uingereza.

“Wenye kupenda pesa.” (2 Timotheo 3:2) “Hivi karibuni, roho ya kupenda mali imekuwa yenye nguvu kuliko roho ya kiasi. Ikiwa wewe si tajiri katika jamii, basi unaonwa kuwa hufai kitu.”—Gazeti la Jakarta Post, Indonesia.

“Wasiotii wazazi.” (2 Timotheo 3:2) “Wazazi hushangaa kuona mtoto wao mwenye umri wa miaka minne akiwaamurisha kama mfalme au mtoto wao mwenye umri wa miaka minane akisema, ‘Nawachukia!’”—Gazeti la American Educator, Marekani.

“Wasio washikamanifu.” (2 Timotheo 3:2) “Badiliko kubwa zaidi katika maadili katika kipindi cha [miaka 40 iliyopita] ni kwamba wanaume wako tayari zaidi kuacha wenzi wao wa ndoa na watoto wao.”—Gazeti la Wilson Quarterly, Marekani.

“Wasio na upendo wa asili.” (2 Timotheo 3:3) “Jeuri katika familia ni jambo linalotukia sana kila siku katika jamii ulimwenguni pote.”—Gazeti Journal of the American Medical Association, Marekani.

“Wasiojizuia.” (2 Timotheo 3:3) “Vichwa vingi vikuu vya habari kila asubuhi katika magazeti huonyesha kwamba watu hawajizuii, hawashikamani na maadili, wala hawana huruma kuelekea wanadamu wenzao na hata hawajihurumii. . . . Jamii yetu ikiendelea kupendelea jeuri kama ilivyo sasa, hivi karibuni itapoteza maadili kabisa.”—Gazeti la Bangkok Post, Thailand.

“Wakali.” (2 Timotheo 3:3) “Hasira kali na ghadhabu inaonekana miongoni mwa madereva, wakati watu wanapotendewa vibaya katika familia, . . . na kupitia jeuri isiyo na msingi ambayo mara nyingi huambatana na uhalifu. Jeuri hutokea wakati wowote na bila kutazamiwa na watu huhisi kuwa wametengwa na kwamba hawana ulinzi.”—Gazeti la Business Day, Afrika Kusini.

“Wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:4) “Watu wanapigania uhuru katika masuala ya ngono, na wanaona maadili ya Kikristo kuwa kizuizi.”—Boundless, gazeti la Intaneti.

“Wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.” (2 Timotheo 3:5) “[Mwanamke mmoja aliyekuwa kahaba huko Uholanzi] alisema kwamba vikundi vya dini hasa ndivyo vinavyopinga kuhalalisha [ukahaba]. Alitua kidogo kisha akasema kwa tabasamu kwamba alipokuwa kahaba, wateja wake wa kawaida walikuwa viongozi fulani [wa dini]. Kisha mwanamke huyo akasema hivi huku akicheka: ‘Makahaba husema kwamba watu wa dini ndio wateja wao bora.’”—Gazeti la National Catholic Reporter, Marekani.

Wakati Ujao Utakuwaje?

Leo ulimwengu umejaa taabu kama vile Biblia ilivyotabiri. Hata hivyo, unabii kuhusu ‘ishara ya kuwapo kwa Kristo na ya umalizio wa mfumo wa mambo,’ una jambo lenye kutia moyo. Yesu alisema hivi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:3, 14) Habari njema ya Ufalme wa Mungu inahubiriwa katika nchi zaidi ya 230. Zaidi ya watu milioni sita kutoka “mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,” wanafanya kwa bidii kazi ya kutangaza Ufalme. (Ufunuo 7:9) Bidii yao imetimiza nini? Imetimiza jambo hili: Karibu kila mtu duniani anaweza kupata habari kuhusu Ufalme, yale ambayo utafanya, na jinsi ya kupata baraka zake. Kwa hakika, ‘ujuzi wa kweli umekuwa mwingi wakati wa mwisho.’—Danieli 12:4.

Unapaswa kutafuta ujuzi huo. Fikiria yale yatakayotukia baada ya Yehova kuridhika na kuhubiriwa kwa habari njema. Yesu alisema: “Ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Utakuwa wakati wa Mungu kuondoa uovu wote duniani. Andiko la Methali 2:22 linasema hivi: “Waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.” Namna gani Shetani na roho wake waovu? Watatupwa katika abiso ambamo hawataweza kuyadanganya mataifa tena. (Ufunuo 20:1-3) Kisha, “wanyoofu . . . na wasio na lawama ndio watakaobaki” duniani. Nao watafurahia baraka za ajabu za Ufalme.—Methali 2:21; Ufunuo 21:3-5.

Unaweza Kufanya Nini?

Hakuna shaka yoyote. Mwisho wa mfumo wa Shetani unakaribia sana. Wale wanaopuuza uthibitisho wa kwamba tunaishi katika siku za mwisho watashtuka mwisho utakapokuja. (Mathayo 24:37-39; 1 Wathesalonike 5:2) Hivyo, Yesu aliwaambia hivi wasikilizaji wake: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wale wote wanaokaa juu ya uso wa dunia yote. Basi, endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.”—Luka 21:34-36.

Ni wale tu walio katika hali inayokubalika mbele za Mwana wa binadamu, Yesu, ndio watakaokuwa na tarajio la kuokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo. Ni muhimu kama nini tutumie wakati unaobaki kutafuta kibali cha Yehova Mungu na Yesu Kristo! Yesu alisema hivi aliposali kwa Mungu: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Basi, ni jambo la hekima ujifunze mengi zaidi kumhusu Yehova Mungu na matakwa yake. Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukusaidia kuelewa yale ambayo Biblia inafundisha. Tunakualika kwa uchangamfu uwasiliane nao au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

MATUKIO YA SIKU ZA MWISHO

MATUKIO MAKUU:

▪ Vita.—Mathayo 24:6, 7.

▪ Upungufu wa chakula.—Mathayo 24:7.

▪ Matetemeko ya nchi.—Mathayo 24:7.

▪ Tauni.—Luka 21:11.

▪ Kuongezeka kwa uasi-sheria.—Mathayo 24:12.

▪ Kuharibiwa kwa dunia.—Ufunuo 11:18.

WATU:

▪ Wenye kujipenda wenyewe.—2 Timotheo 3:2.

▪ Wenye kupenda pesa.—2 Timotheo 3:2.

▪ Wenye majivuno.—2 Timotheo 3:2.

▪ Wasiotii wazazi.—2 Timotheo 3:2.

▪ Wasio na shukrani.—2 Timotheo 3:2.

▪ Wasio washikamanifu.—2 Timotheo 3:2.

▪ Wasio na upendo wa asili.—2 Timotheo 3:3.

▪ Wasiojizuia.—2 Timotheo 3:3.

▪ Wakali.—2 Timotheo 3:3.

▪ Wanaopenda raha.—2 Timotheo 3:4.

▪ Wanafiki wa dini.—2 Timotheo 3:5.

WAABUDU WA KWELI:

▪ Wana ujuzi mwingi.—Danieli 12:4.

▪ Wanahubiri habari njema ulimwenguni pote.—Mathayo 24:14.

[Hisani]

UNITED NATIONS/Photo by F. GRIFFING