Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Siku za Mwisho” Zinamaanisha Nini?

“Siku za Mwisho” Zinamaanisha Nini?

“Siku za Mwisho” Zinamaanisha Nini?

JE, WEWE hujiuliza maisha yako na ya wapendwa wako yatakuwaje wakati ujao? Watu wengi husikiliza habari kwa makini ili kuona jinsi matukio ya ulimwengu yanavyoweza kuathiri maisha yao. Hata hivyo, kuchunguza Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho hutupa ufahamu wa kweli. Hiyo ni kwa sababu zaidi ya kutabiri mambo yanayotukia sasa duniani, Biblia pia ilitabiri zamani za kale mambo ya wakati ujao.

Kwa mfano, Yesu Kristo alipokuwa duniani, alizungumza sana kuhusu Ufalme wa Mungu. (Luka 4:43) Bila shaka, watu waliomsikiliza walitaka kujua wakati ambapo Ufalme huo bora ungekuja. Kwa kweli, siku tatu kabla ya Yesu kuuawa isivyo haki, wanafunzi wake walimuuliza hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako [katika mamlaka ya Ufalme] na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Yesu aliwaambia kwamba Yehova Mungu peke yake ndiye anayejua wakati hususa ambapo Ufalme huo utatawala kwa ukamili juu ya dunia. (Mathayo 24:36; Marko 13:32) Hata hivyo, Yesu na wengine walitabiri mambo fulani ambayo yangetukia duniani kuonyesha kwamba Kristo anatawala katika mamlaka ya Ufalme.

Kabla hatujachunguza uthibitisho ulio wazi unaoonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo, acheni tuchunguze kwa ufupi jambo muhimu lililotukia katika makao ya kiroho. (2 Timotheo 3:1) Yesu Kristo alitawazwa kuwa Mfalme mbinguni mwaka wa 1914. * (Danieli 7:13, 14) Mara tu baada ya kupokea mamlaka ya Ufalme, Yesu alichukua hatua. Biblia inatuambia hivi: “Vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa, naye joka mkubwa na malaika zake wakapigana.” (Ufunuo 12:7) “Mikaeli, yule malaika mkuu” ni Yesu Kristo katika cheo chake mbinguni. * (Yuda 9; 1 Wathesalonike 4:16) Joka huyo mkubwa ni Shetani Ibilisi. Matokeo yalikuwa nini kwa Shetani na malaika waovu waliomuunga mkono, wanaoitwa roho waovu? Walishindwa katika vita hivyo nao “wakatupwa chini” au kuondoshwa mbinguni hadi duniani. (Ufunuo 12:9) Hivyo, ‘mbingu na wale wanaokaa ndani yake,’ yaani, wana wa roho wa Mungu ambao ni waaminifu, wakashangilia. Hata hivyo, wanadamu hawajashangilia. Biblia ilitabiri hivi: “Ole wa dunia . . . kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:12.

Akiwa na hasira kali, Shetani amesababisha ole, yaani, mateso, kwa wale wanaokaa duniani. Hata hivyo, ole hiyo ni ya muda mfupi, yaani, “kipindi kifupi cha wakati.” Biblia inataja kipindi hicho kuwa “siku za mwisho.” Tunaweza kufurahi kwamba hivi karibuni uvutano wa Ibilisi juu ya dunia utakomeshwa kabisa. Lakini, kuna uthibitisho gani unaoonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2006, ukurasa wa 6-7.

^ fu. 4 Unaweza kupata habari zaidi katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? ukurasa wa 218-219, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

COVER: Foreground: © Chris Stowers/Panos Pictures; background: FAROOQ NAEEM/AFP/Getty Images