Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Biblia Ina Sheria Nyingi Mno?

Je, Biblia Ina Sheria Nyingi Mno?

Je, Biblia Ina Sheria Nyingi Mno?

KIJANA mmoja huko Finland anasema hivi: “Nilipokuwa mtoto sikufundishwa kanuni zozote za Biblia. Mungu hakutajwa kamwe.” Wengi wamelelewa kwa njia hiyo leo. Watu wengi, hasa vijana, huiona Biblia kuwa imepitwa sana na wakati na ina sheria nyingi mno. Wale wanaotaka kuitii Biblia huonwa na wengine kuwa watu waliokandamizwa ambao wamelemewa na sheria na amri nyingi. Hivyo, wengi wanaona ni afadhali kutafuta mwongozo kwingineko badala ya kuisoma Biblia.

Watu wana maoni hayo kuhusu Biblia kwa sababu makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo yamewakandamiza watu kwa muda mrefu sana. Kwa mfano, katika kipindi ambacho wanahistoria fulani wanakiita Enzi za Giza, Kanisa Katoliki huko Ulaya liliongoza karibu sehemu zote za maisha ya watu. Mtu yeyote aliyethubutu kulipinga kanisa alikabili hatari ya kuteswa na hata kuuawa. Pia, makanisa ya Kiprotestanti yaliyotokea baadaye, yalikandamiza uhuru wa watu. Dini fulani za Kiprotestanti zinajulikana kuwa dini zinazotoa adhabu kali. Hivyo, kwa kuwa dini hizo zilikandamiza, watu wamekata kauli kimakosa kwamba mafundisho ya Biblia ni yenye kukandamiza.

Katika karne za karibuni, dini zimeshindwa kuongoza maisha ya watu katika nchi fulani. Watu wengi wanakataa mafundisho ya kawaida ya dini, nao wanaamini kwamba wana haki ya kujiamulia mema na mabaya. Matokeo? Ahti Laitinen, profesa wa elimu ya jinai na sosholojia ya kisheria, anasema hivi: “Watu wameacha kuheshimu mamlaka, na wanazidi kushindwa kutofautisha mambo yanayokubaliwa na yasiyokubaliwa.” Inastaajabisha kwamba hata viongozi wa dini wameathiriwa na maoni hayo. Askofu mmoja mashuhuri wa kanisa la Kilutheri alisema hivi: “Sikubaliani na maoni ya kwamba masuala ya kiadili yanaweza kusuluhishwa kwa kufuata mwongozo wa Biblia au chanzo fulani cha kidini chenye mamlaka.”

Je, Uhuru Usio na Mipaka Unafaa?

Huenda wazo la kuwa na uhuru usio na mipaka likawafurahisha watu, hasa vijana. Wengi hawapendi kuongozwa au kuwekewa sheria. Hata hivyo, je, kila mtu anapaswa kuwa huru kufanya lolote apendalo? Ili kujibu swali hilo, fikiria mfano huu. Wazia jiji lisilo na sheria za barabarani. Katika jiji hilo, mtu hahitaji kuwa na leseni ya kuendesha gari wala kufanya mtihani wa kuendesha gari. Watu wanaweza kuendesha gari kwa njia yoyote ile, hata wakiwa walevi, bila kujali mwendo uliowekwa kisheria, ishara za barabarani, taa za kuongoza magari, barabara za kuelekea upande mmoja, au sehemu za kuvukia barabara. Je, “uhuru” huo unafaa? Hapana! Hali hiyo inaweza kusababisha fujo, mvurugo, na misiba. Ingawa sheria za barabarani hudhibiti uhuru wa watu, tunaelewa kwamba sheria hizo huwalinda madereva na watu wanaotembea kwa miguu.

Vivyo hivyo, Yehova hutoa mwongozo kuhusu jinsi tunavyopaswa kuishi. Mwongozo huo hutufaidi. Bila mwongozo huo, ingetubidi tujifunze mambo kwa kujaribu-jaribu tu, na kwa kufanya hivyo, tungejiumiza na kuwaumiza wengine. Hali hiyo ya kukosa viwango vya maadili vya kutuongoza haipendezi na ni hatari kama vile kuendesha gari katika jiji ambalo halina sheria za barabarani. Ukweli ni kwamba, tunahitaji sheria za aina fulani, na watu wengi wanakubali jambo hilo.

“Mzigo Wangu Ni Mwepesi”

Huenda sheria za barabarani zikahusisha orodha ndefu ya mambo ambayo hupaswi kufanya. Katika maeneo fulani, idadi ya sheria za kuegesha magari ni nyingi sana. Lakini, Biblia haina orodha ndefu ya sheria. Badala yake, ina kanuni za msingi ambazo si nzito wala hazikandamizi. Yesu Kristo aliwapa watu wa siku zake mwaliko huu wenye kuvutia: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:28, 30) Katika barua kwa kutaniko la Kikristo la Korintho, mtume Paulo aliandika hivi: “Mahali palipo na roho ya Yehova, pana uhuru.”—2 Wakorintho 3:17.

Hata hivyo, uhuru huo una mipaka. Yesu alisema waziwazi kwamba matakwa ya Mungu yanatia ndani amri fulani ambazo si nzito. Kwa mfano, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda ninyi.” (Yohana 15:12) Wazia jinsi ambavyo maisha yangekuwa ikiwa kila mtu angefuata amri hiyo! Hivyo, uhuru ambao Wakristo wanafurahia una mipaka. Mtume Petro aliandika hivi: “Iweni kama watu huru, lakini muwe na uhuru wenu, si kama kifuniko cha ubaya, bali kama watumwa wa Mungu.”—1 Petro 2:16.

Hivyo, hata ingawa Wakristo hawajawekewa orodha ndefu ya sheria, wao hawatendi kulingana na maoni yao kuhusu mema na mabaya. Wanadamu wanahitaji mwongozo ambao Mungu peke yake anaweza kutoa. Biblia inasema hivi waziwazi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Tukitii mwongozo wa Mungu, tutafaidika sana.—Zaburi 19:11.

Faida moja ni furaha. Kwa mfano, kijana aliyetajwa mwanzoni alikuwa mwizi na mwongo. Pia alikuwa mwasherati. Baada ya kujifunza viwango vya juu vya Biblia, alibadili maisha yake ili yapatane na viwango hivyo. Alisema: “Ingawa singeweza kufuata viwango vyote vya Biblia mara moja, nilielewa umuhimu wake. Maisha yangu ya awali hayakuniwezesha kuwa na furaha ambayo ninapata sasa. Kuishi kulingana na viwango vya Biblia hufanya maisha yako yawe rahisi. Unakuwa na kusudi maishani na unatambua mema na mabaya.”

Mamilioni ya watu wamejionea jambo hilo. Kati ya mambo mengine, mwongozo wa Biblia umewasaidia kuboresha uhusiano wao pamoja na watu wengine, kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu kazi, kuacha mazoea yenye kudhuru, na hivyo kuishi maisha yenye furaha. Kijana mmoja anayeitwa Markus, * ambaye wakati fulani hakufuata viwango vya Biblia, anasema hivi kuhusu maisha yake: “Kuishi kulingana na Biblia kumeniwezesha nijiheshimu zaidi.” *

Utachagua Nini?

Basi, je, Biblia ina sheria? Ndiyo, ina sheria zinazotufaidi sisi sote. Lakini, je, Biblia ina sheria nyingi mno? Hapana. Uhuru usio na mipaka husababisha matatizo. Viwango vya Biblia vina usawaziko, navyo vinatusaidia kuwa na hali njema na furaha. Markus anasema: “Kadiri wakati ulivyopita ndivyo nilivyotambua hekima ya kutumia Neno la Mungu maishani. Ingawa kwa njia nyingi maisha yangu ni tofauti na ya watu kwa ujumla, sijawahi kufikiri kwamba nimekosa kitu chochote muhimu maishani.”

Unapoanza kupata faida za kuishi kulingana na viwango vya Biblia, utalithamini zaidi Neno la Mungu. Hilo litakuwezesha kupata faida kubwa hata zaidi, yaani, utampenda Yehova Mungu aliye Chanzo cha Neno hilo. “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 Yohana 5:3.

Yehova ni Muumba wetu na Baba yetu wa mbinguni. Anajua kile kinachotufaa. Badala ya kutupa sheria zenye kulemea, anatupa mwongozo wenye upendo kwa faida yetu. Yehova anatumia lugha ya kishairi kutusihi hivi: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.”—Isaya 48:18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Jina limebadilishwa.

^ fu. 13 Ili upate habari zaidi kuhusu njia ya maisha inayopendekezwa na Biblia, ona sura ya 12 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yesu alisema kwamba matakwa ya Mungu yanaburudisha

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kutii mwongozo wa Mungu humwezesha mtu kupata furaha na kujiheshimu