Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitihada za Mwanadamu za Kupata Uzima wa Milele

Jitihada za Mwanadamu za Kupata Uzima wa Milele

Jitihada za Mwanadamu za Kupata Uzima wa Milele

TANGU zamani za kale, wanadamu wametamani sana kuishi milele. Hata hivyo, tamaa hiyo haijatimizwa kwa kuwa hakuna mtu ambaye amepata njia ya kukomesha kifo. Lakini, hivi karibuni utafiti wa kitiba umewafanya watu watumaini tena kwamba huenda ikawezekana kurefusha maisha ya wanadamu. Ona jitihada zinazofanywa katika nyanja mbalimbali za uchunguzi wa kisayansi.

Wanabiolojia wanafanya majaribio kwa kutumia kimeng’enya fulani (telomerase) ili kuwezesha chembe zijifanyize upya mara nyingi zaidi. Wanasayansi wanajua kwamba chembe nzee zilizodhoofika huondolewa na badala yake chembe mpya hufanyizwa. Kwa kweli, sehemu kubwa ya mwili hufanyizwa upya mara kadhaa katika maisha ya mwanadamu. Watafiti wanafikiri kwamba ikiwa utaratibu huo wa kufanyizwa upya kwa chembe unaweza kutokea mara nyingi zaidi, “mwili wa mwanadamu unaweza kujifanyiza upya kwa muda mrefu sana, hata milele.”

Inadhaniwa kwamba utaalamu wa kufanyiza kiumbe bila kufanya ngono, ambao umezua ubishi, utawawezesha wagonjwa kupata ini, figo, au moyo wa kupandikizwa bila tatizo lolote. Viungo hivyo vinaweza kufanyizwa kwa kutumia chembe fulani za mgonjwa mwenyewe.

Watafiti wa teknolojia ya kutengeneza vifaa vidogo sana wanasema kwamba kuna wakati ambapo madaktari wataingiza vidude vidogo sana kama chembe ndani ya mishipa ya damu ili kugundua na kuangamiza chembe za kansa na bakteria hatari. Wengine wanaamini kwamba hatimaye, sayansi hiyo na matibabu ya kutumia chembe za urithi yatawezesha mwili wa mwanadamu ujifanyize upya milele.

Wataalamu fulani hugandisha miili ya wale waliokufa. Wanafanya hivyo ili kuhifadhi miili hiyo mpaka wakati ambapo maendeleo ya kitiba yatawawezesha madaktari kuponya magonjwa, kukomesha uzee, na kuwawezesha wafu kuishi tena na kuwa na afya nzuri. Gazeti fulani (American Journal of Geriatric Psychiatry) linasema kwamba hiyo ni “mbinu ya kisasa inayofanana na desturi ya Wamisri wa kale ya kuhifadhi maiti.”

Jitihada za muda mrefu za wanadamu za kuishi milele zinaonyesha jinsi ilivyo vigumu kwa mtu kukubali kwamba anaweza kufa. Je, inawezekana wanadamu wapate uzima wa milele? Biblia inasema nini kuhusu jambo hilo? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.