Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwa Hodari Kupitia Imani na Kumwogopa Mungu

Kuwa Hodari Kupitia Imani na Kumwogopa Mungu

Kuwa Hodari Kupitia Imani na Kumwogopa Mungu

“Uwe hodari na mwenye nguvu . . . Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe.”—YOSHUA 1:9.

1, 2. (a) Kwa maoni ya wanadamu, je, kulikuwa na matumaini yoyote kwamba Waisraeli wangewashinda Wakanaani? (b) Yoshua alipewa uhakikisho gani?

KATIKA mwaka wa 1473 K.W.K., taifa la Israeli lilikuwa tayari kuingia Nchi ya Ahadi. Kuhusiana na matatizo ambayo wangekabili, Musa aliwakumbusha watu hao hivi: ‘Leo mnavuka Yordani mwingie ndani na kuyafukuza mataifa makubwa zaidi na yenye nguvu zaidi kuliko ninyi, majiji makubwa na yenye ngome zinazofika mbinguni, watu wakubwa na warefu, wana wa Waanaki, ambao mmesikia ikisemwa juu yao, “Ni nani anayeweza kusimama imara mbele ya wana wa Anaki?”’ (Kumbukumbu la Torati 9:1, 2) Naam, mashujaa hao ambao walikuwa majitu walijulikana sana! Isitoshe, Wakanaani fulani walikuwa na majeshi yenye silaha za kutosha, pamoja na farasi na magari ya vita yenye miundu ya chuma kwenye magurudumu.—Waamuzi 4:13.

2 Kwa upande mwingine, hapo awali Israeli lilikuwa taifa la watumwa, nao walikuwa wamekaa nyikani kwa miaka 40. Hivyo, kwa maoni ya wanadamu, haikuonekana kwamba wangeshinda vita. Hata hivyo, Musa alikuwa na imani; angeweza ‘kumwona’ Yehova akiwaongoza. (Waebrania 11:27) Musa aliwaambia watu hivi: ‘Yehova Mungu wenu anavuka mbele yenu. Atawaangamiza hao, na yeye mwenyewe atawatiisha mbele yenu.’ (Kumbukumbu la Torati 9:3; Zaburi 33:16, 17) Baada ya kifo cha Musa, Yehova alimhakikishia Yoshua kwamba angemtegemeza, aliposema hivi: “Simama sasa, vuka huu mto Yordani, wewe na watu hawa wote, mwingie katika nchi ambayo ninawapa wao, wana wa Israeli. Hakuna yeyote atakayesimama imara mbele yako siku zote za maisha yako. Nitakuwa pamoja nawe, kama vile nilivyokuwa pamoja na Musa.”—Yoshua 1:2, 5.

3. Ni nini kilichomsaidia Yoshua kuwa na imani na uhodari?

3 Ili kupata msaada na mwongozo wa Yehova, Yoshua alipaswa kusoma na kutafakari Sheria ya Mungu na kuishi kulingana nayo. Yehova alisema hivi: “Kwa maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima. Je, mimi sikukuamuru wewe? Uwe hodari na mwenye nguvu. Usitetemeke wala usiwe na hofu, kwa maana Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe kila mahali unapoenda.” (Yoshua 1:8, 9) Kwa kuwa Yoshua alimsikiliza Mungu, alikuwa hodari, mwenye nguvu, naye alifanikiwa. Hata hivyo, watu wengi wa kizazi chake hawakusikiliza. Hivyo, hawakufanikiwa, nao walikufa nyikani.

Watu Wasio na Imani Wakosa Uhodari

4, 5. (a) Mtazamo wa wale wapelelezi kumi ulitofautianaje na ule wa Yoshua na Kalebu? (b) Yehova alitendaje watu hao walipokosa imani?

4 Miaka 40 mapema Waisraeli walipokaribia Kanaani kwa mara ya kwanza, Musa aliwatuma wanaume 12 ili waipeleleze nchi. Kumi kati yao walirudi wakiwa na woga. Walipaaza sauti hivi: “Watu wote tuliowaona katikati yake ni watu wenye ukubwa usio wa kawaida. Na humo tuliwaona Wanefili, wana wa Anaki, waliotoka kwa Wanefili; hivi kwamba sisi tukawa machoni petu wenyewe kama panzi.” Je, kweli “watu wote” walikuwa majitu au ni Waanaki tu? Si watu wote waliokuwa majitu. Je, Waanaki walikuwa wazao wa Wanefili walioishi kabla ya Gharika? Hapana! Hata hivyo, kwa sababu ya kutilia chumvi, woga ulitanda kambini. Hata watu walitaka kurudi Misri, ambako walikuwa watumwa!—Hesabu 13:31–14:4.

5 Lakini, wapelelezi wawili Yoshua na Kalebu, walitamani kuingia Nchi ya Ahadi. Walisema hivi: “[Wakanaani] ni mkate kwetu. Ulinzi wao umegeuka kutoka juu yao, na Yehova yuko pamoja nasi. Msiwaogope.” (Hesabu 14:9) Je, uhakika wa Yoshua na Kalebu ulikuwa na msingi? Ndiyo! Wao pamoja na taifa lote, walikuwa wameona Yehova akifedhehesha taifa la Misri lenye nguvu na miungu yao kupitia Mapigo Kumi. Kisha, walimwona Yehova akimzamisha Farao na majeshi yake katika Bahari Nyekundu. (Zaburi 136:15) Ni wazi kwamba, wapelelezi kumi na wale walioathiriwa nao hawakupaswa kuogopa. Yehova alisema hivi kwa huzuni nyingi: “Watakosa kuniamini mpaka wakati gani ijapokuwa ishara zote ambazo nilifanya katikati yao?”—Hesabu 14:11.

6. Kuna uhusiano gani kati ya uhodari na imani, na hilo limeonekanaje katika nyakati za sasa?

6 Yehova alitaja chanzo cha tatizo, yaani, woga wa watu hao ulionyesha kwamba hawakuwa na imani. Naam, kuna uhusiano wa karibu sana kati ya imani na uhodari, hivi kwamba mtume Yohana aliandika hivi kuhusu kutaniko la Kikristo na vita vyake vya kiroho: “Huu ndio ushindi ambao umeushinda ulimwengu, imani yetu.” (1 Yohana 5:4) Leo, imani kama ya Yoshua na Kalebu imewezesha habari njema ya Ufalme ihubiriwe ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni sita, vijana kwa wazee, wenye nguvu na walio dhaifu. Hakuna adui ambaye amefaulu kunyamazisha jeshi hilo lenye nguvu na lililo hodari.—Waroma 8:31.

‘Usirudi Nyuma’

7. ‘Kurudi nyuma’ kunamaanisha nini?

7 Leo, watumishi wa Yehova wanahubiri habari njema kwa uhodari kwa sababu wana mtazamo kama wa mtume Paulo aliyeandika hivi: “Sisi si namna ya watu wanaorudi nyuma kwenye maangamizi, bali sisi ni namna ya watu walio na imani ya kuihifadhi hai nafsi.” (Waebrania 10:39) Kama Paulo alivyotaja ‘kurudi nyuma’ hakumaanishi kuogopa kwa muda mfupi, kwa kuwa kuna wakati ambapo watumishi wengi waaminifu wa Mungu wameogopa. (1 Samweli 21:12; 1 Wafalme 19:1-4) Badala yake, kamusi moja ya Biblia inasema kwamba kurudi nyuma kunamaanisha “kusonga nyuma, kuacha,” “kulegea katika kufuata kweli.” Pia, inasema kwamba huenda ikawa ‘kurudi nyuma’ ni maneno ya mfano yanayotokana na “kushusha tanga ya meli na hivyo kupunguza mwendo” katika utumishi wa Mungu. Bila shaka, wale walio na imani yenye nguvu hawafikirii kamwe “kupunguza mwendo” wakati matatizo yanapotokea, yawe ni mateso, magonjwa, au majaribu mengine. Badala yake, wanasonga mbele kwa kumtumikia Yehova, wakijua kwamba anawajali sana na anajua udhaifu wao. (Zaburi 55:22; 103:14) Je, una imani kama hiyo?

8, 9. (a) Yehova aliimarishaje imani ya Wakristo wa mapema? (b) Tunaweza kufanya nini ili tuimarishe imani yetu?

8 Wakati mmoja mitume walihisi kwamba imani yao ilikuwa imepungua, hivyo wakamwambia Yesu hivi: “Tupe imani zaidi.” (Luka 17:5) Ombi lao la unyoofu lilijibiwa, hasa siku ya Pentekoste 33 W.K., wakati roho takatifu iliyoahidiwa ilipokuja juu ya wanafunzi na kuwapa ufahamu mwingi wa Neno la Mungu na kusudi lake. (Yohana 14:26; Matendo 2:1-4) Imani ya wanafunzi hao ikiwa imeimarishwa, walianza kampeni ya kuhubiri, na licha ya upinzani walihubiri habari njema katika “uumbaji wote ulio chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23; Matendo 1:8; 28:22.

9 Ili kuimarisha imani yetu na kuendelea na huduma yetu, ni lazima sisi pia tujifunze na kutafakari kuhusu Maandiko na kusali ili tupate roho takatifu. Kama vile Yoshua, Kalebu, na wanafunzi Wakristo wa mapema, tukikazia kweli ya Mungu katika akili na moyo wetu tutapata imani inayotuwezesha kuwa hodari ili kuvumilia na kushinda katika vita vyetu vya kiroho.—Waroma 10:17.

Imani Si Kuamini Tu Kwamba Kuna Mungu

10. Imani ya kweli inahusisha nini?

10 Kama ilivyoonyeshwa na watu wa zamani wenye utimilifu, imani inayomsaidia mtu kuwa hodari na kuvumilia inatia ndani mengi kuliko kuamini tu kwamba kuna Mungu. (Yakobo 2:19) Imani hiyo inahusisha kumjua Yehova kuwa mtu halisi na kumwamini kabisa. (Zaburi 78:5-8; Methali 3:5, 6) Inamaanisha kuamini kwa moyo wetu wote kwamba tunafaidika sana tunapotii sheria na kanuni za Mungu. (Isaya 48:17, 18) Pia, imani inahusisha kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatimiza ahadi zake zote na kuwa “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:1, 6; Isaya 55:11.

11. Yoshua na Kalebu walibarikiwaje kwa sababu ya imani na uhodari wao?

11 Imani hiyo hukua. Inakua tunapoishi kulingana na kweli, ‘tunapoonja’ faida zake, ‘tunapoona’ sala zetu zikijibiwa, na kutambua mwongozo wa Yehova maishani mwetu kwa njia nyingine. (Zaburi 34:8; 1 Yohana 5:14, 15) Tunaweza kuwa na hakika kwamba imani ya Yoshua na Kalebu iliimarishwa walipoonja wema wa Mungu. (Yoshua 23:14) Fikiria mambo haya: Waliokoka safari ya miaka 40 nyikani kama Mungu alivyoahidi. (Hesabu 14:27-30; 32:11, 12) Walipewa kazi ya pekee wakati wa ile miaka sita ya kuteka Kanaani. Hatimaye, walifurahia maisha marefu na afya nzuri na hata wakapewa urithi wao. Yehova huwapa thawabu wale walio waaminifu na wanaomtumikia kwa uhodari!—Yoshua 14:6, 9-14; 19:49, 50; 24:29.

12. Yehova ‘hulitukuzaje neno lake’?

12 Fadhili zenye upendo ambazo Mungu aliwaonyesha Yoshua na Kalebu zinatukumbusha maneno haya ya mtunga-zaburi: “Umeyatukuza maneno yako hata juu ya jina lako lote.” (Zaburi 138:2) Yehova anapotumia jina lake kuonyesha uhakika wa ahadi fulani, utimizo wa ahadi hiyo ‘hutukuzwa’ katika maana ya kwamba ahadi hiyo hutimia hata zaidi ya vile inavyotarajiwa. (Waefeso 3:20) Naam, kamwe Yehova hawavunji moyo wale ambao ‘hupata furaha tele’ katika yeye.—Zaburi 37:3, 4.

Mtu ‘Aliyempendeza Mungu Vema’

13, 14. Kwa nini Enoko alihitaji imani na uhodari?

13 Tunaweza kujifunza mengi kuhusu imani na uhodari kwa kufikiria mfano wa shahidi mwingine wa kabla ya Ukristo, yaani, Enoko. Hata kabla ya kuanza kutoa unabii, huenda Enoko alijua kwamba imani na uhodari wake ungejaribiwa. Kwa nini? Kwa sababu Yehova alikuwa amesema katika Edeni kwamba kungekuwa na uadui au chuki kati ya wale wanaomtumikia Mungu na wale wanaomtumikia Shetani Ibilisi. (Mwanzo 3:15) Enoko alijua pia kwamba chuki hiyo ilikuwa imetokea mapema katika historia ya wanadamu wakati Kaini alipomuua Abeli ndugu yake. Adamu, baba yao, aliendelea kuishi miaka 310 hivi baada ya Enoko kuzaliwa.—Mwanzo 5:3-18.

14 Hata hivyo, licha ya mambo hayo, Enoko ‘aliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli’ kwa uhodari na kushutumu ‘mambo yenye kushtua’ ambayo watu walisema dhidi ya Yehova. (Mwanzo 5:22; Yuda 14, 15) Inaonekana msimamo huo thabiti kwa ajili ya ibada ya kweli ulifanya Enoko awe na maadui wengi na kuhatarisha maisha yake. Wakati huo, Yehova alimlinda nabii wake asipate maumivu ya kifo. Baada ya kumfunulia Enoko “kwamba amempendeza Mungu vema,” Yehova ‘alimhamisha’ toka uhai hadi kifo, huenda akiwa katika maono ya kinabii.—Waebrania 11:5, 13; Mwanzo 5:24.

15. Enoko aliwawekea watumishi wa kisasa wa Yehova mfano gani mzuri?

15 Mara tu baada ya kutaja jinsi Enoko alivyohamishwa, Paulo alikazia tena umuhimu wa imani aliposema hivi: “Zaidi ya hayo, bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema.” (Waebrania 11:6) Naam, kuwa na imani kulimwezesha Enoko kuwa hodari ili atembee pamoja na Yehova na kutangaza ujumbe wa Yehova wa hukumu kwa ulimwengu usiomwogopa Mungu. Kwa njia hiyo, Enoko alituwekea mfano mzuri. Tuna kazi kama hiyo katika ulimwengu unaopinga ibada ya kweli na uliojaa kila namna ya ubaya.—Zaburi 92:7; Mathayo 24:14; Ufunuo 12:17.

Kuwa Hodari kwa Kumwogopa Mungu

16, 17. Obadia alikuwa nani, naye alikabili hali gani?

16 Zaidi ya imani, kuna jambo lingine linalotuwezesha kuwa hodari, yaani, kumwogopa na kumheshimu Mungu. Acheni tuone mfano bora wa mtu aliyemwogopa Mungu, na ambaye aliishi katika siku za nabii Eliya na Mfalme Ahabu, aliyetawala ufalme wa kaskazini wa Israeli. Wakati wa utawala wa Ahabu, ibada ya Baali iliathiri sana ufalme wa kaskazini. Hata manabii 450 wa Baali na manabii wengine 400 wa mti mtakatifu, ambao ulikuwa ishara ya kiungo cha uzazi cha kiume, ‘walikula mezani pa Yezebeli,’ mke wa Ahabu.—1 Wafalme 16:30-33; 18:19.

17 Akiwa adui mkatili wa Yehova, Yezebeli alijaribu kukomesha ibada ya kweli nchini. Aliwaua baadhi ya manabii wa Yehova na hata akajaribu kumuua Eliya, ambaye kulingana na mwongozo wa Mungu alikimbia na kuvuka Mto Yordani. (1 Wafalme 17:1-3; 18:13) Je, unaweza kuwazia jinsi ambavyo ingekuwa vigumu kuunga mkono ibada safi katika ufalme wa kaskazini wakati huo? Namna gani ikiwa ungekuwa unafanya kazi katika jumba la mfalme? Obadia * alikabili hali hiyo. Alikuwa mtumishi wa nyumba ya Ahabu, naye alimwogopa Mungu.—1 Wafalme 18:3.

18. Ni jambo gani lililomwezesha Obadia kuwa mwabudu wa pekee wa Yehova?

18 Bila shaka, Obadia alikuwa mwenye tahadhari na busara katika ibada yake kwa Yehova. Lakini, hakukana imani yake. Andiko la 1 Wafalme 18:3 linatuambia hivi: “Obadia alikuwa amejionyesha kuwa mtu anayemwogopa Yehova sana.” Naam, Obadia alimwogopa Mungu sana! Woga huo unaofaa ulimwezesha Obadia kuwa hodari sana, kama ilivyoonekana baada tu ya Yezebeli kuwaua manabii wa Yehova.

19. Obadia alifanya mambo gani yaliyoonyesha kwamba alikuwa hodari?

19 Tunasoma hivi: “Ikawa kwamba Yezebeli alipowakatilia mbali manabii wa Yehova, Obadia aliwachukua manabii 100, akawaficha wakiwa vikundi viwili vya watu 50 pangoni, naye akawapa mkate na maji.” (1 Wafalme 18:4) Kama unavyoweza kuwazia, ilikuwa hatari sana kuwalisha kisiri wanaume 100. Mbali na kuepuka kutambuliwa na Ahabu na Yezebeli, Obadia alipaswa pia kuepuka kugunduliwa na wale manabii wa uwongo 850 ambao walitembelea jumba la mfalme kwa ukawaida. Isitoshe, wale waabudu wengine wengi wa uwongo katika Israeli, kuanzia watu wa hali ya chini hadi wakuu, wangetumia nafasi hiyo kumfichua Obadia ili kupata kibali cha mfalme na malkia. Hata hivyo, Obadia aliwahudumia manabii wa Yehova kwa uhodari bila kuogopa kuonwa na waabudu hao wa sanamu. Naam, kumwogopa Mungu kunaweza kumwimarisha mtu sana!

20. Kumwogopa Mungu kulimsaidiaje Obadia, na mfano wake unakufaidije?

20 Kwa kuwa Obadia alionyesha uhodari kwa kumwogopa Mungu, inaonekana Yehova alimlinda dhidi ya maadui wake. Andiko la Methali 29:25 linasema hivi: “Kutetemeshwa na wanadamu ndiko huleta mtego, lakini yeye anayemtegemea Yehova atalindwa.” Obadia alikuwa mwanadamu tu kama sisi; aliogopa kukamatwa na kuuawa. (1 Wafalme 18:7-9, 12) Lakini, kumwogopa Mungu kulimwezesha awe hodari na kushinda woga wowote ambao angekuwa nao kuelekea wanadamu. Obadia ni mfano bora kwetu sote, hasa kwa wale wanaohatarisha uhuru wao au maisha yao ili wamwabudu Yehova. (Mathayo 24:9) Naam, acheni sisi sote tujitahidi kumtumikia Yehova “kwa woga wa kimungu na heshima.”—Waebrania 12:28.

21. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

21 Uhodari haupatikani tu kwa kuwa na imani na kumwogopa Mungu; upendo unaweza kutuimarisha hata zaidi. Paulo aliandika hivi: “Mungu hakutupa sisi roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.” (2 Timotheo 1:7) Katika makala inayofuata, tutaona jinsi upendo unavyoweza kutusaidia kumtumikia Yehova kwa uhodari katika siku hizi za mwisho zenye hatari.—2 Timotheo 3:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Huyo si yule nabii Obadia.

Je, Unaweza Kujibu?

• Ni nini kilichowasaidia Yoshua na Kalebu kuwa hodari?

• Imani ya kweli inahusisha nini?

• Kwa nini Enoko hakuogopa kutangaza ujumbe wa Mungu wa hukumu?

• Kumwogopa Mungu humsaidiaje mtu kuwa hodari?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Yehova alimwamuru Yoshua hivi: “Uwe hodari na mwenye nguvu”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Obadia aliwatunza na kuwalinda manabii wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 19]

Enoko alitangaza neno la Mungu kwa ujasiri