Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uhodari Waimarishwa kwa Upendo

Uhodari Waimarishwa kwa Upendo

Uhodari Waimarishwa kwa Upendo

“Mungu hakutupa sisi roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.”—2 TIMOTHEO 1:7.

1, 2. (a) Upendo unaweza kumchochea mtu kufanya nini? (b) Kwa nini uhodari wa Yesu ulikuwa wa pekee sana?

MUME na mke waliooana karibuni walikuwa wakipiga mbizi karibu na mji fulani ulio kwenye pwani ya mashariki ya Australia. Walikuwa karibu kutoka majini wakati samaki mkubwa anayeitwa papa aliposonga haraka kumwelekea mke. Kwa ushujaa, mume huyo alimsukuma mke wake kando, naye akaacha samaki huyo amshambulie. Mwanamke huyo alisema hivi wakati wa mazishi ya mume wake: “Alitoa uhai wake kwa ajili yangu.”

2 Naam, upendo unaweza kuwachochea wanadamu kuonyesha uhodari wa hali ya juu. Yesu Kristo mwenyewe alisema hivi: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Muda usiozidi saa 24 baada ya Yesu kusema maneno hayo, alitoa uhai wake, si kwa ajili ya mtu mmoja tu, bali kwa ajili ya wanadamu wote. (Mathayo 20:28) Isitoshe, Yesu hakutoa uhai wake kwa kushtukia. Alijua kimbele kwamba angedhihakiwa, angetendewa vibaya, angehukumiwa isivyo haki, na kuuawa kwenye mti wa mateso. Hata aliwatayarisha wanafunzi wake kwa ajili ya hilo, akisema: “Tazama, tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani, na waandishi, nao watamhukumia kifo na kumtia mikononi mwa watu wa mataifa, nao watamdhihaki, watamtemea mate, watampiga mijeledi na kumuua.”—Marko 10:33, 34.

3. Ni nini kilichomwezesha Yesu kuwa hodari sana?

3 Ni nini kilichomwezesha Yesu kuonyesha uhodari usio wa kawaida? Hasa ni kwa sababu ya imani na kumwogopa Mungu. (Waebrania 5:7; 12:2) Hata hivyo, zaidi ya yote, uhodari wa Yesu ulitokana na upendo wake kwa Mungu na kwa wanadamu wenzake. (1 Yohana 3:16) Tukisitawisha upendo kama huo pamoja na imani na kumwogopa Mungu, sisi pia tutakuwa hodari kama Kristo. (Waefeso 5:2) Tunaweza kusitawishaje upendo kama huo? Tunapaswa kutambua Chanzo cha upendo huo.

“Upendo Unatoka kwa Mungu”

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova ndiye Chanzo cha upendo?

4 Yehova ndiye mfano bora zaidi wa upendo na Chanzo cha sifa hiyo. Mtume Yohana aliandika hivi: “Wapendwa, acheni tuendelee kupendana, kwa sababu upendo unatoka kwa Mungu, na kila mtu ambaye hupenda amezaliwa kutokana na Mungu na hupata kumjua Mungu. Yeye ambaye hapendi hajamjua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:7, 8) Hivyo, mtu anaweza kusitawisha upendo kama wa Mungu ikiwa tu anamkaribia Yehova kupitia ujuzi sahihi na kutenda kulingana na ujuzi huo kwa kutii kutoka moyoni.—Wafilipi 1:9; Yakobo 4:8; 1 Yohana 5:3.

5, 6. Ni nini kilichowasaidia wafuasi wa Yesu wa mapema kusitawisha upendo kama wa Kristo?

5 Katika sala yake ya mwisho pamoja na mitume wake waaminifu 11, Yesu alionyesha uhusiano kati ya kumjua Mungu na kukua katika upendo aliposema hivi: “Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda nao upate kuwa ndani yao nami katika muungano pamoja nao.” (Yohana 17:26) Yesu aliwasaidia wanafunzi wake kusitawisha upendo kama ule uliokuwapo kati yake na Baba yake, akionyesha kwa maneno na kwa mfano kile ambacho jina la Mungu linawakilisha, yaani, sifa nzuri ajabu za Mungu. Hiyo ndiyo sababu Yesu alisema hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yohana 14:9, 10; 17:8.

6 Upendo kama wa Kristo unatokana na roho takatifu ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Siku ya Pentekoste 33 W.K., wakati Wakristo wa mapema walipopokea roho takatifu iliyoahidiwa, hawakukumbuka tu mambo mengi ambayo Yesu aliwafundisha, bali pia walielewa zaidi maana ya Maandiko. Inaonekana kwamba ufahamu huo ulioongezeka uliimarisha upendo wao kwa Mungu. (Yohana 14:26; 15:26) Ikawaje? Hata uhai wao ulipokuwa hatarini, walihubiri habari njema kwa ujasiri na kwa bidii.—Matendo 5:28, 29.

Kuonyesha Uhodari na Upendo

7. Paulo na Barnaba walivumilia mambo gani katika safari yao ya umishonari?

7 Mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu hakutupa sisi roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.” (2 Timotheo 1:7) Paulo alikuwa akisema mambo aliyojionea. Fikiria yale yaliyompata yeye na Barnaba walipokuwa katika safari yao ya umishonari. Walihubiri katika majiji mengi, kutia ndani Antiokia, Ikoniamu, na Listra. Katika kila jiji, watu fulani walipata kuwa waamini, lakini wengine walikuwa wapinzani wakali. (Matendo 13:2, 14, 45, 50; 14:1, 5) Huko Listra, watu wenye hasira hata walimpiga Paulo kwa mawe na kumwacha wakifikiri kwamba amekufa! “Hata hivyo, wanafunzi walipomzunguka, akasimama na kuingia ndani ya jiji. Na siku iliyofuata akaondoka pamoja na Barnaba kwenda Derbe.”—Matendo 14:6, 19, 20.

8. Uhodari wa Paulo na Barnaba ulionyeshaje kwamba waliwapenda watu sana?

8 Je, jaribio hilo la kumuua Paulo lilimwogopesha yeye na Barnaba kuacha kuhubiri? Hapana! Baada ya “kufanya wanafunzi wengi” huko Derbe, wanaume hao wawili “wakarudi Listra na Ikoniamu na Antiokia.” Kwa nini? Ili kuwatia moyo wapya wabaki wakiwa imara katika imani. Paulo na Barnaba walisema hivi: “Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.” Ni wazi kwamba walikuwa hodari kwa sababu walipenda sana “wana-kondoo” wa Kristo. (Matendo 14:21-23; Yohana 21:15-17) Baada ya kuwaweka rasmi wazee katika kila moja ya makutaniko mapya, ndugu hao wawili walitoa sala na “kuwakabidhi kwa Yehova ambaye walikuwa wamemwamini.”

9. Upendo wa Paulo uliwachocheaje wazee wa Efeso?

9 Paulo alikuwa mtu mwenye upendo na uhodari hivi kwamba Wakristo wengi wa mapema walimpenda sana. Kumbuka yaliyotukia kwenye mkutano ambao Paulo alifanya pamoja na wazee wa Efeso, ambako alikuwa amekaa kwa miaka mitatu na kukabili upinzani mwingi. (Matendo 20:17-31) Baada ya kuwatia moyo kulichunga kundi la Mungu walilokabidhiwa, Paulo alipiga magoti pamoja nao na kusali. Kisha, “wote wakalia sana, nao wakamwangukia Paulo shingoni na kumbusu kwa wororo, kwa sababu waliumizwa hasa na neno alilosema kwamba hawangemwona uso wake tena.” Ndugu hao walimpenda Paulo sana! Kwa kweli, wakati wa kuagana ulipofika, ilibidi Paulo na wale waliosafiri pamoja naye ‘wajiondoe kwao.’ Naam, wazee wa huko hawakutaka kuwaruhusu waondoke.—Matendo 20:36–21:1.

10. Mashahidi wa Yehova leo wameonyeshaje kwa uhodari kwamba wanapendana?

10 Leo, waangalizi wanaosafiri, wazee wa makutaniko, na wengine wengi wanapendwa sana kwa sababu ya uhodari wanaoonyesha wanaposhughulikia kondoo za Yehova. Kwa mfano, katika nchi zinazokumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe au katika maeneo ambako kazi ya kuhubiri imepigwa marufuku, waangalizi wanaosafiri na wake zao wamehatarisha maisha yao na uhuru wao ili kuyatembelea makutaniko. Vivyo hivyo, Mashahidi wengi wameteswa na watawala wakatili pamoja na wafuasi wao kwa sababu wamekataa kuwasaliti Mashahidi wenzao au kusema mahali wanapotoa chakula cha kiroho. Maelfu ya Mashahidi wengine wameteswa, wamenyanyaswa, na hata kuuawa kwa sababu wamekataa kuacha kuhubiri habari njema au kukutana na waamini wenzao kwenye mikutano ya Kikristo. (Matendo 5:28, 29; Waebrania 10:24, 25) Acheni tuige imani na upendo wa ndugu na dada hao hodari!—1 Wathesalonike 1:6.

Usiache Upendo Wako Upoe

11. Shetani hutumia njia gani kupigana vita vya kiroho dhidi ya watumishi wa Yehova, nao wanahitaji kufanya nini?

11 Shetani alipotupwa duniani, aliazimia kuelekeza hasira yake kwa watumishi wa Yehova kwa sababu ‘wanashika amri za Mungu na wana kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.’ (Ufunuo 12:9, 17) Mojawapo ya mbinu za Ibilisi ni mateso. Hata hivyo, mara nyingi mbinu hiyo haifanikiwi kwa sababu inawafanya watu wa Mungu wawe na uhusiano wa karibu zaidi unaotegemea upendo wa Kikristo na inawachochea wengi wao kuwa na bidii zaidi. Mbinu nyingine ya Shetani ni kuchochea mielekeo ya wanadamu ya kutenda dhambi. Tunahitaji kuwa hodari kwa njia nyingine ili kushinda mbinu hiyo kwa sababu pambano letu ni la ndani, dhidi ya tamaa mbaya katika ‘moyo wetu wenye hila ambao ni hatari.’—Yeremia 17:9; Yakobo 1:14, 15.

12. Shetani anatumiaje “roho ya ulimwengu” ili kujaribu kudhoofisha upendo wetu kwa Mungu?

12 Shetani anatumia silaha nyingine yenye nguvu, yaani, “roho ya ulimwengu,” ambayo ni mwelekeo au uvutano wake wenye nguvu zaidi ambao unapinga moja kwa moja roho takatifu ya Mungu. (1 Wakorintho 2:12) Roho ya ulimwengu huchochea pupa na tamaa ya mali, naam, “tamaa ya macho.” (1 Yohana 2:16; 1 Timotheo 6:9, 10) Ingawa mali na pesa zenyewe haziwezi kutudhuru, tukizipenda badala ya kumpenda Mungu, basi Shetani atakuwa ameshinda. Nguvu au “mamlaka” ya roho ya ulimwengu, hutokana na jinsi inavyochochea mwili wenye dhambi, jinsi ilivyo yenye hila, jinsi inavyowachochea watu tena na tena, na jinsi inavyoenea sana kama hewa. Usiache roho ya ulimwengu iathiri moyo wako!—Waefeso 2:2, 3; Methali 4:23.

13. Uhodari wetu wa kudumisha usafi wa kiadili unaweza kujaribiwaje?

13 Hata hivyo, ili kupinga na kuchukia roho mbovu ya ulimwengu, tunahitaji kuwa hodari ili kudumisha usafi wa kiadili. Kwa mfano, uhodari unahitajiwa ili kuondoka kwenye jumba la sinema au kuzima kompyuta au televisheni wakati picha chafu zinapoonyeshwa. Tunahitaji kuwa hodari ili kukataa msongo wa marika na kuacha mashirika mabaya. Vivyo hivyo, tunahitaji kuwa hodari ili kufuata sheria na kanuni za Mungu licha ya kudhihakiwa na wanashule, wafanyakazi, majirani, au watu wa ukoo.—1 Wakorintho 15:33; 1 Yohana 5:19.

14. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tumeathiriwa na roho ya ulimwengu?

14 Basi, ni muhimu kama nini tuimarishe upendo wetu kwa Mungu na kwa ndugu na dada zetu wa kiroho! Chunguza miradi yako na maisha yako ili uone ikiwa roho ya ulimwengu imekuathiri kwa njia yoyote ile. Ikiwa imekuathiri, hata kwa kiasi kidogo, mwombe Yehova akupe uhodari ili uiondolee mbali kabisa na kutoiruhusu ikuathiri tena. Yehova hatapuuza maombi hayo ya unyoofu. (Zaburi 51:17) Isitoshe, roho yake ina nguvu zaidi kuliko roho ya ulimwengu.—1 Yohana 4:4.

Kukabili Majaribu kwa Uhodari

15, 16. Upendo kama wa Kristo unaweza kutusaidiaje kukabiliana na majaribu? Toa mfano.

15 Matatizo mengine ambayo watumishi wa Yehova wanakabili yanatia ndani matokeo ya kutokamilika na uzee, ambayo mara nyingi husababisha magonjwa, ulemavu, kushuka moyo, na matatizo mengine mengi. (Waroma 8:22) Upendo kama wa Kristo unaweza kutusaidia kukabiliana na majaribu hayo. Fikiria mfano wa Namangolwa aliyelelewa katika familia ya Kikristo huko Zambia. Alipokuwa na umri wa miaka miwili, Namangolwa alilemaa. Anasema hivi: “Nilikuwa nikijifikiria sana, nikifikiri kwamba watu watashtuliwa na umbo langu. Lakini ndugu zangu wa kiroho walinisaidia kuona mambo kwa njia tofauti. Kwa hiyo, niliacha kujifikiria sana, na baada ya muda nikabatizwa.”

16 Ingawa Namangolwa ana kiti cha magurudumu, mara nyingi yeye hulazimika kutembea kwa mikono na magoti anapokuwa kwenye barabara ya mchanga. Hata hivyo, yeye hufanya upainia msaidizi angalau miezi miwili kila mwaka. Mwenye nyumba mmoja alilia wakati Namangolwa alipomhubiria. Kwa nini? Kwa sababu alichochewa sana na imani na uhodari wa dada yetu. Yehova amembariki sana Namangolwa kwa kuwa watano kati ya wanafunzi wake wa Biblia wamebatizwa, na mmoja ni mzee wa kutaniko. Namangolwa anasema hivi: “Mara nyingi miguu yangu huniuma sana, lakini siachi jambo hilo linizuie.” Dada huyo ni mmoja wa Mashahidi wengi ulimwenguni walio dhaifu kimwili lakini wenye bidii nyingi kwa sababu wanampenda Mungu na jirani. Watu kama hao ni wenye kutamanika sana machoni pa Yehova!—Hagai 2:7.

17, 18. Ni nini huwasaidia wengi kuvumilia magonjwa na majaribu mengine? Toa mifano ya kwenu.

17 Ugonjwa wa kudumu unaweza pia kumfanya mtu avunjike moyo, na hata kushuka moyo. Mzee mmoja wa kutaniko anasema hivi: “Katika funzo la kitabu ninalohudhuria, dada mmoja ana ugonjwa wa sukari na ugonjwa wa figo, mwingine ana kansa, wengine wawili wana ugonjwa wa baridi yabisi, na mmoja ana ugonjwa fulani wa misuli na ugonjwa mwingine (unaoitwa lupus). Wakati mwingine wao huvunjika moyo. Hata hivyo, wao hukosa mikutano wakati tu wanapokuwa wagonjwa sana au wanapolazwa hospitalini. Wote huhubiri kwa ukawaida. Wao hunikumbusha Paulo, aliyesema hivi: ‘Ninapokuwa dhaifu, ndipo ninapokuwa mwenye nguvu.’ Ninavutiwa na upendo wao na uhodari wao. Labda hali yao huwawezesha kuwa na maoni yanayofaa maishani na kutambua mambo yaliyo muhimu zaidi.” —2 Wakorintho 12:10.

18 Ikiwa unapambana na ugonjwa au tatizo lingine ‘sali bila kuacha’ upate msaada ili usivunjike moyo. (1 Wathesalonike 5:14, 17) Bila shaka, huenda ukavunjika moyo mara kwa mara, lakini jitahidi kukazia fikira mambo yanayofaa, yaani, mambo ya kiroho, hasa tumaini letu la Ufalme lenye thamani. Dada mmoja alisema hivi: “Ninaona kuhubiri kuwa dawa.” Kuwahubiria wengine habari njema humsaidia kudumisha mtazamo unaofaa.

Upendo Huwasaidia Wakosaji Kumrudia Yehova

19, 20. (a) Ni nini kinachoweza kuwasaidia wale ambao wametenda dhambi kupata uhodari ili kumrudia Yehova? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

19 Wengi ambao wamekuwa dhaifu kiroho au wametenda dhambi huona ni vigumu kumrudia Yehova. Lakini watapata uhodari unaohitajiwa ikiwa watatubu kikweli na kuanza tena kumpenda Mungu. Fikiria mfano wa Mario * ambaye anaishi Marekani. Mario aliacha kutaniko la Kikristo, akawa mlevi na akazoea kutumia dawa za kulevya, na baada ya miaka 20 akafungwa gerezani. Mario anasema hivi: “Nilianza kufikiri sana kuhusu wakati wangu ujao na kusoma Biblia tena. Baada ya muda, nilithamini sifa za Yehova, hasa rehema yake, ambayo nilimwomba mara nyingi. Baada ya kutoka gerezani, nilijiepusha na mashirika yangu ya zamani, nikahudhuria mikutano ya Kikristo, na mwishowe nikarudishwa. Ninavuna mwilini mwangu kile nilichopanda, lakini sasa angalau nina tumaini zuri ajabu. Ninamshukuru sana Yehova kwa huruma zake na msamaha wake.”—Zaburi 103:9-13; 130:3, 4; Wagalatia 6:7, 8.

20 Bila shaka, wale wanaokabili hali kama za Mario wanapaswa kujitahidi sana ili wamrudie Yehova. Lakini upendo wao uliochochewa upya kwa sababu ya kujifunza Biblia, kusali, na kutafakari, utawapa uhodari na bidii. Pia, Mario aliimarishwa na tumaini la Ufalme. Naam, zaidi ya upendo, imani, na kumwogopa Mungu, tumaini pia linaweza kutuchochea kutenda mema maishani. Katika makala inayofuata, tutachunguza kwa undani zawadi hiyo ya kiroho yenye thamani.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Jina limebadilishwa.

Je, Unaweza Kujibu?

• Upendo ulimsaidiaje Yesu kuwa na uhodari usio wa kawaida?

• Ni kwa njia gani upendo kwa ajili ya akina ndugu uliwawezesha Paulo na Barnaba kuwa na uhodari wa pekee?

• Shetani hutumia njia gani ili kujaribu kudhoofisha upendo wa Kikristo?

• Kumpenda Yehova kunaweza kutupa uhodari ili kuvumilia majaribu gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Paulo alivumilia kwa uhodari kwa sababu aliwapenda watu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Uhodari unahitajiwa ili kufuata viwango vya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Namangolwa Sututu