Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuishi Milele

Unaweza Kuishi Milele

Unaweza Kuishi Milele

WATU wengi wa dini mbalimbali ulimwenguni huvutiwa na tazamio la kupata uzima wa milele wa aina fulani. Huenda imani ya dini hizo kuhusu tazamio hilo ikatofautiana, lakini wana tumaini moja, yaani, kuishi kwa furaha katika hali nzuri bila kuogopa kufa. Je, inawezekana kwamba wewe pia unatamani jambo hilo? Kwa nini kuna tofauti hizo katika imani? Je, tarajio la kuishi milele litatimizwa wakati wowote?

Maandiko yanaonyesha kwamba Muumba aliweka tamaa ya kuishi milele ndani ya mwanadamu tangu mwanzo, tangu alipoumba mwanamume na mwanamke wa kwanza. Biblia inasema hivi: “Wakati usio na kipimo [Mungu] ameuweka ndani ya moyo wao.”—Mhubiri 3:11.

Hata hivyo, ili kutimiza tamaa hiyo ya kuishi milele, wenzi hao wa kwanza walipaswa kukubali mamlaka ya Mungu ya kuamua mema na mabaya. Ikiwa wangefanya hivyo, Yehova angetangaza kwamba wanastahili kuishi “mpaka wakati usio na kipimo” katika makao ambayo alikuwa amewatayarishia, yaani, bustani ya Edeni.—Mwanzo 2:8; 3:22.

Uzima wa Milele Wapotea

Biblia inaonyesha kwamba Mungu alipanda katika bustani “mti wa ujuzi wa mema na mabaya,” naye akawakataza Adamu na Hawa wasile matunda ya mti huo, la sivyo, wangekufa. (Mwanzo 2:9, 17) Ikiwa Adamu na Hawa hawangekula matunda ya mti huo, hilo lingemwonyesha Mungu kwamba wanatambua mamlaka yake. Kwa upande mwingine, kula matunda ya mti huo, kungeonyesha kwamba wanakataa mamlaka ya Mungu. Adamu na Hawa walikataa kutii maagizo ya Yehova na kumuunga mkono Shetani, kiumbe wa roho ambaye aliasi mamlaka ya Mungu. Kwa hiyo, Mungu aliamua kwa haki kwamba Adamu na Hawa hawakustahili kuishi milele.—Mwanzo 3:1-6.

Mungu alikuwa ameweka mbele yao uzima au kifo, kuwapo au kutokuwapo. Kutotii kwao kulisababisha kifo na mwisho wa kuwapo kwao. Haingewezekana kwa Adamu na Hawa au wazao wao kuendelea kuishi kwa kutumia dawa fulani ya kimuujiza au kwa kuwa na nafsi isiyoweza kufa. *

Wazao wote wa Adamu waliteseka kwa sababu ya uasi wake. Mtume Paulo alieleza matokeo ya uasi huo. Aliandika hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

Uzima wa Milele Wapatikana Tena

Mtume Paulo alionyesha hali ya wazao wa Adamu kwa kuilinganisha na hali ya mtumwa katika karne ya kwanza. Kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa, watoto wa Adamu na Hawa hawangeepuka kuzaliwa wakiwa “watumwa wa dhambi,” na hatimaye kufa. (Waroma 5:12; 6:16, 17) Hawangeweza kuepuka jambo hilo ikiwa Yehova hangewakomboa na kuwaweka huru kutoka katika utumwa huo. Paulo alieleza hivi: “Kupitia kosa moja [la Adamu] matokeo kwa watu wa namna zote yalikuwa kuhukumiwa hatia, vivyo hivyo pia kupitia tendo moja la kutetewa kuwa haki matokeo kwa watu wa namna zote ni wao kutangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.” ‘Tendo hilo la kutetewa kuwa haki’ lilimfanya Yesu adhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu “kuwa fidia inayolingana kwa ajili ya wote.” Yehova alitambua nguvu za kisheria za fidia za kuwakomboa wanadamu kutokana na “hukumu” ya kwamba wana “hatia.”—Waroma 5:16, 18, 19; 1 Timotheo 2:5, 6.

Hiyo ndiyo sababu wanasayansi hawatapata kamwe suluhisho la kifo katika chembe za urithi za mwanadamu. Suluhisho linapatikana kwingineko. Kulingana na Biblia, chanzo cha kifo cha mwanadamu ni cha kiadili na kisheria, bali si cha kibiolojia. Njia ya kurudisha uzima wa milele, yaani, dhabihu ya fidia ya Yesu, ni ya kisheria pia. Fidia pia inaonyesha uadilifu na fadhili zenye upendo za Mungu. Basi, ni nani watakaofaidika na fidia hiyo na kupata uzima wa milele?

Zawadi ya Kutoweza Kufa

Yehova Mungu ni wa “tangu wakati usio na kipimo mpaka wakati usio na kipimo.” Hawezi kufa. (Zaburi 90:2) Yesu Kristo ndiye mtu wa kwanza aliyepewa na Yehova zawadi ya kutoweza kufa. Mtume Paulo anaeleza hivi: “Kristo hafi tena, kwa kuwa sasa amekwisha kufufuliwa kutoka kwa wafu; kifo si bwana juu yake tena.” (Waroma 6:9) Kwa kweli, akionyesha tofauti kati ya watawala wa dunia na Yesu aliyefufuliwa, Paulo anasema kwamba ni Yesu peke yake asiyeweza kufa. Yesu ataendelea “kuwa hai milele.” Uhai wake ‘hauwezi kuharibika.’—Waebrania 7:15-17, 23-25; 1 Timotheo 6:15, 16.

Si Yesu peke yake anayepewa zawadi hiyo. Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho ambao wamechaguliwa kutawala wakiwa wafalme katika utukufu mbinguni wanapata ufufuo kama wa Yesu. (Waroma 6:5) Mtume Yohana anaonyesha kwamba watu 144,000 wanapewa pendeleo hilo. (Ufunuo 14:1) Wao pia wanapewa zawadi ya kutoweza kufa. Paulo anasema hivi kuhusu ufufuo wao: “Nyama na damu haviwezi kuurithi ufalme wa Mungu . . . Tarumbeta italia, na wafu watafufuliwa wakiwa wasioweza kuharibika, nasi tutabadilishwa. Kwa maana huu ulio wa kuharibika lazima uvae kutoweza kuharibika, na huu unaoweza kufa lazima uvae kutoweza kufa.” Kifo hakina nguvu juu ya wale wanaopokea ufufuo huo.—1 Wakorintho 15:50-53; Ufunuo 20:6.

Ufunuo huo kutoka kwa Mungu ni wa ajabu sana. Hata malaika ambao ni viumbe wa roho, hawakuumbwa wakiwa na hali ya kutoweza kufa. Tunajua hilo kwa sababu viumbe wa roho waliounga mkono uasi wa Shetani wataangamizwa. (Mathayo 25:41) Kwa upande mwingine, wale watakaotawala pamoja na Yesu, wanapewa zawadi ya kutoweza kufa, na hilo linaonyesha kuwa Yehova anasadiki kabisa kwamba wao ni waaminifu.

Je, hilo linamaanisha kwamba watu 144,000 tu—ambayo ni idadi ndogo ikilinganishwa na mabilioni ya wanadamu ambao wamewahi kuishi—ndio watakaoishi milele? Hapana. Acheni tuone sababu.

Uzima wa Milele Katika Paradiso Duniani

Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinaonyesha hali yenye kupendeza sana ya umati wa watu usioweza kuhesabiwa ambao unapewa uzima wa milele katika paradiso duniani. Miongoni mwao kuna wale waliokufa na kufufuliwa na kurudishiwa afya na nguvu za ujana. (Ufunuo 7:9; 20:12, 13; 21:3, 4) Wanaelekezwa kwenye “mto wa maji ya uzima, mwangavu kama fuwele, ukitiririka kutoka katika kiti cha ufalme cha Mungu.” Kwenye kingo za mto huo kuna “miti ya uzima . . . , na majani ya miti ile yalikuwa ya kuponya mataifa.” Yehova Mungu anatoa mwaliko huu kwa fadhili: “Yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.”—Ufunuo 22:1, 2, 17.

Miti hiyo na maji hayo si chemchemi ya ujana wala dawa za kimuujiza kama zile zilizotafutwa na wataalamu wa dawa na wavumbuzi karne nyingi zilizopita. Badala yake, zinawakilisha mambo ambayo Mungu ameandaa kupitia Yesu Kristo ili kuwawezesha wanadamu kurudia hali kamilifu kama ilivyokuwa mwanzoni.

Kusudi la Mungu la kuwapa wanadamu watiifu uzima wa milele duniani, halijabadilika. Kusudi hilo litatimia kwa sababu Yehova ni mshikamanifu. Andiko la Zaburi 37:29 linasema hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” Ahadi hiyo inatuchochea sisi pamoja na wanadamu wanaopewa hali ya kutoweza kufa mbinguni, kusema hivi: “Matendo yako ni makuu na ya ajabu, Yehova Mungu, Mweza-Yote. Njia zako ni za uadilifu na za kweli, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kwa kweli hatakuogopa wewe, Yehova, na kulitukuza jina lako, kwa sababu wewe peke yako ni mshikamanifu?”—Ufunuo 15:3, 4.

Je, unatamani zawadi yenye thamani ya uzima wa milele? Ikiwa ndivyo, ni lazima uwe mshikamanifu na mtiifu kwa “Mfalme wa umilele.” Unahitaji kujifunza kumhusu Yehova na yule ambaye kupitia kwake uhai huo unawezekana, yaani, Yesu Kristo. Wale wote wanaokubali kwa hiari kanuni za Mungu kuhusu mema na mabaya watapewa zawadi ya “uzima wa milele.”—Yohana 17:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kwa habari kamili kuhusu fundisho la kutokufa kwa nafsi, tafadhali ona broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

Tamaa ya Muda Mrefu

Inasemekana kwamba Hadithi ya Gilgamesh, ambalo ni simulizi la huko Mesopotamia, iliandikwa katika milenia ya pili K.W.K. Hadithi hiyo inaeleza jitihada za shujaa fulani za kutafuta njia ya kuwa kijana milele. Wamisri wa kale walihifadhi maiti wakifikiri kwamba nafsi ambazo waliamini hazifi, zingeweza kutumia tena miili yao. Hivyo, makaburi fulani ya Wamisri yalijazwa vitu vyote ambavyo wafu wangehitaji katika maisha hayo ya baadaye.

Inaonekana kwamba tangu karne ya nane K.W.K. hivi, wataalamu wa dawa wa Kichina waliamini kwamba mwili hauwezi kufa, na katika karne ya nne K.W.K., walianza kuamini kwamba inawezekana kuzuia mwili usife kwa kutumia dawa za kimuujiza. Wataalamu wa dawa wa Ulaya na Arabia katika enzi za kati walitafuta na kujaribu kutengeneza dawa zao za kurefusha maisha. Baadhi ya dawa hizo zilikuwa na kemikali za aseniki, zebaki, na salfa. Haikosi watu walikufa walipotumia dawa hizo!

Pia, wakati fulani kulikuwa na hadithi nyingi kuhusu Chemchemi ya Ujana, ambayo ilisemekana ingewawezesha wote wanaokunywa kutokana nayo kupata nguvu tena.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Je, Uzima wa Milele Utachosha?

Watu fulani husema kwamba uzima wa milele utachosha. Wanasema ni sawa na kupoteza wakati milele kwa kufanya mambo yasiyo na maana kwa kuyarudia-rudia. Huenda wanawazia kwamba wataishi milele huku wakikabili hali na maisha ya sasa, ambayo watu wengi huyaona kuwa yanachosha na hayana maana. Lakini, katika Paradiso ambayo Mungu atarudisha, anaahidi wanadamu ‘furaha tele katika wingi wa amani.’ (Zaburi 37:11) Maisha hayo yatawapa wanadamu nafasi ya kupata ujuzi kuhusu uumbaji wa Yehova na wakati wa kusitawisha ustadi fulani au ustadi wa aina zote, kujifunza, na kufanya kazi ambazo tunatamani kuzifanya lakini hatuwezi kwa sasa.

Dakt. Aubrey de Grey, mtaalamu wa chembe za mwili kwenye Chuo Kikuu cha Cambridge, ambaye anafanya utafiti kuhusu kurefusha uhai, anasema hivi: “Leo, watu walio na elimu na wakati wa kuitumia hawachoshwi nayo na hawawezi kuwazia wakikosa mambo mapya ya kufanya.” Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake linasema kwamba “mwanadamu [hataweza] kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.”—Mhubiri 3:11.