Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ubatizo Ulitokana na Zoea la Wayahudi la Kuoga Kidesturi?

Je, Ubatizo Ulitokana na Zoea la Wayahudi la Kuoga Kidesturi?

Je, Ubatizo Ulitokana na Zoea la Wayahudi la Kuoga Kidesturi?

YOHANA MBATIZAJI alihubiri juu ya “ubatizo unaoonyesha toba.” Yesu pia aliwaamuru wafuasi wake wafanye wanafunzi na kuwabatiza.—Marko 1:4; Mathayo 28:19.

Biblia inaonyesha kwamba ubatizo wa Kikristo unahusisha kuzamishwa kabisa katika maji. Kitabu kimoja (Jesus and His World) kinadai kwamba “desturi kama hizo, zinafuatwa katika dini nyingi za kale na za sasa, katika nchi na tamaduni mbalimbali.” Kitabu hicho kinadai kwamba “ubatizo wa Kikristo . . . ulitokana na dini ya Kiyahudi.” Je, dai hilo ni la kweli?

Vidimbwi vya Wayahudi vya Kuoga Kidesturi

Wataalamu wa vitu vya kale waliokuwa wakichimba karibu na Hekalu la Mlimani la Yerusalemu waligundua vidimbwi 100 hivi vya kuoga kidesturi, vilivyojengwa katika karne ya kwanza K.W.K., na karne ya kwanza W.K. Maandishi kwenye sinagogi la karne ya pili au ya tatu W.K., yanaonyesha kwamba vidimbwi hivyo vilijengwa kwa ajili ya “wageni waliovihitaji.” Vidimbwi vingine vimegunduliwa katika eneo la Yerusalemu lililokaliwa na matajiri na familia za kikuhani. Karibu kila nyumba ilikuwa na kidimbwi chake cha kuoga kidesturi.

Vidimbwi hivyo vilikuwa matangi yenye umbo la pembe nne yaliyochongwa kwenye miamba au kuchimbwa ardhini kisha yakatandazwa kwa matofali au mawe. Matangi hayo yalipigwa lipu au plasta ili kuyazuia yasivuje. Matangi mengi yalikuwa na upana wa meta 1.8 na urefu wa meta 2.7 hivi. Mabomba yaliingiza maji ya mvua kwenye matangi hayo. Kina cha maji kilikuwa angalau meta 1.2 ili mtu aliyeinama afunikwe kabisa na maji. Katika vidimbwi fulani ngazi za kushuka kwenye kidimbwi ziligawanywa kwa ukuta mfupi. Inasemekana kwamba ngazi za upande mmoja zilitumiwa kuingia kwenye kidimbwi cha kujitakasa mtu alipokuwa najisi, huku ngazi za upande wa pili zikitumiwa kutoka kwenye kidimbwi ili kuepuka kuchafuliwa kwa njia yoyote ile.

Vidimbwi hivyo vilitumiwa kuwatakasa Wayahudi kidesturi. Hilo lilihusisha nini?

Sheria na Desturi za Kuoga

Sheria ya Musa ilikazia uhitaji wa watu wa Mungu kuwa safi kiroho na kimwili. Mambo mbalimbali yaliwafanya Waisraeli wasiwe safi na hivyo walihitaji kujitakasa kwa kuoga na kufua nguo zao.—Mambo ya Walawi 11:28; 14:1-9; 15:1-31; Kumbukumbu la Torati 23:10, 11.

Yehova Mungu ni safi na mtakatifu kabisa. Kwa hiyo, makuhani na Walawi walipaswa kunawa mikono na miguu kabla ya kukaribia madhabahu ili wasife.—Kutoka 30:17-21.

Wasomi wanaamini kwamba kufikia karne ya kwanza W.K., dini ya Kiyahudi iliwataka watu wengine wasio Walawi wafuate matakwa hayo ya usafi wa makuhani. Waesene na Mafarisayo walikuwa na mazoea ya kunawa kidesturi. Kichapo kimoja kinasema hivi kuhusu siku za Yesu: “Myahudi alihitajiwa kujitakasa kidesturi kabla ya kuingia katika Hekalu la Mlimani, kabla ya kutoa dhabihu, kabla ya kuhudumiwa na kuhani, na kwa sababu nyingine kama hizo.” Maandishi ya Talmud yanasema kwamba watu waliokuja kuoga walipaswa kujizamisha kabisa majini.

Yesu aliwashutumu Mafarisayo kwa sababu ya kusisitiza watu wajitakase kidesturi. Ni wazi kwamba walikuwa na “mabatizo mbalimbali,” kutia ndani “ubatizo wa vikombe na mitungi na vyombo vya shaba.” Yesu alisema kwamba Mafarisayo walivunja amri za Mungu ili kuwalazimisha watu wafuate mapokeo yao. (Waebrania 9:10; Marko 7:1-9; Mambo ya Walawi 11:32, 33; Luka 11:38-42) Sheria ya Musa haikuwataka watu wajizamishe kabisa majini.

Je, ubatizo wa Kikristo ulitokana na zoea hilo la Wayahudi la kuoga kidesturi? Hapana!

Kuoga Kidesturi na Ubatizo wa Kikristo

Wayahudi walijitakasa kidesturi. Hata hivyo, ubatizo wa Yohana haukuwa zoea fulani la kuoga kidesturi ambalo lilijulikana kwa Wayahudi. Kwa kuwa Yohana aliitwa Mbatizaji, ni wazi kwamba uzamisho aliofanya ulikuwa tofauti. Hata viongozi wa dini ya Kiyahudi walituma watu wakamuulize hivi: “Kwa nini . . . unabatiza?”—Yohana 1:25.

Utakaso chini ya Sheria ya Musa ulihitaji kurudiwa kila mara mwabudu alipokuwa najisi. Haikuwa hivyo kuhusu ubatizo wa Yohana wala ubatizo uliofanywa na Wakristo. Ubatizo wa Yohana ulionyesha kwamba mtu ametubu na kuacha mwenendo wake wa zamani. Ubatizo wa Kikristo ulionyesha kwamba mtu alikuwa amejiweka wakfu kwa Mungu. Mkristo alifanya hivyo mara moja tu, wala si tena na tena.

Zoea la kuoga kidesturi lililofanywa katika nyumba za makuhani Wayahudi na katika vidimbwi vya watu wote vilivyokuwa karibu na Hekalu la Mlimani lilifanana kijuujuu tu na ubatizo wa Kikristo. Hata hivyo, maana ya mabatizo hayo mawili ilitofautiana kabisa. Kamusi moja (The Anchor Bible Dictionary) inasema hivi: “Wasomi wanakubaliana kwamba Yohana [Mbatizaji] hakuendeleza wala kuiga ubatizo fulani hususa katika jamii yake,” yaani, katika dini ya Kiyahudi. Ndivyo ilivyo na ubatizo unaofanywa katika kutaniko la Kikristo.

Ubatizo wa Kikristo unamaanisha “ombi linalotolewa kwa Mungu ili kupata dhamiri njema.” (1 Petro 3:21) Unaonyesha kwamba mtu amejiweka wakfu kabisa kwa Yehova ili kumtumikia akiwa mwanafunzi wa Mwana Wake. Kuzamishwa kabisa katika maji ni ishara inayofaa ya wakfu huo. Kuzamishwa huko kunaonyesha kwamba mtu amekufa kuhusiana na mwenendo wake wa zamani. Kuinuliwa kutoka katika maji kunaonyesha kwamba amefufuliwa ili afanye mapenzi ya Mungu.

Yehova Mungu huwapa dhamiri njema wale wanaojiweka wakfu na kubatizwa. Ndiyo sababu mtume Petro aliyeongozwa kwa roho ya Mungu aliwaambia hivi waamini wenzake: ‘Ubatizo unawaokoa ninyi sasa pia.’ Zoea la Wayahudi la kuoga kidesturi halingeweza kamwe kutimiza hilo.