Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Thibitisha Imani Yako Kupitia Maisha Yako

Thibitisha Imani Yako Kupitia Maisha Yako

Thibitisha Imani Yako Kupitia Maisha Yako

“Imani, ikiwa haina matendo, imekufa yenyewe.”—YAKOBO 2:17.

1. Kwa nini Wakristo wa karne ya kwanza walitilia maanani imani na matendo?

KWA ujumla, Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha imani yao kupitia maisha yao. Mwanafunzi Yakobo aliwahimiza hivi Wakristo wote: “Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu.” Naye akaongeza hivi: “Kama vile ambavyo mwili bila roho umekufa, vivyo hivyo pia imani bila matendo imekufa.” (Yakobo 1:22; 2:26) Miaka 35 hivi baada ya kuandika maneno hayo, bado Wakristo wengi walikuwa wakithibitisha imani yao kwa matendo yanayofaa. Lakini inasikitisha kwamba wengine hawakuwa wakifanya hivyo. Yesu alilipongeza kutaniko la Smirna; lakini aliwaambia hivi washiriki wengi wa kutaniko la Sardi: “Mimi nayajua matendo yako, kwamba una jina kuwa uko hai, lakini umekufa.”—Ufunuo 2:8-11; 3:1.

2. Wakristo wanapaswa kujiuliza maswali gani kuhusu imani yao?

2 Hivyo, Yesu aliwahimiza Wakristo huko Sardi na wengine ambao baadaye wangesoma maneno yake wathibitishe upendo wao wa kwanza kuelekea kweli ya Kikristo na kuwa macho kiroho. (Ufunuo 3:2, 3) Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza hivi: ‘Matendo yangu yakoje? Je, matendo yangu yanaonyesha waziwazi kwamba ninafanya yote niwezayo kuthibitisha imani yangu katika shughuli zangu zote, hata katika mambo yasiyohusiana moja kwa moja na kazi ya kuhubiri au mikutano ya kutaniko?’ (Luka 16:10) Kuna mambo mengi maishani yanayohusika, lakini acheni tuzungumzie jambo moja tu: tafrija, kutia ndani zile zinazofanywa katika arusi za Kikristo.

Tafrija Ndogo

3. Biblia inasema nini kuhusu kushiriki katika tafrija?

3 Wengi wetu hufurahia kualikwa kwenye tafrija ya Wakristo wenye furaha. Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” ambaye hutaka watumishi wake wawe wenye furaha. (1 Timotheo 1:11) Mungu alimwongoza Sulemani kuandika jambo hili la hakika katika Biblia: “Nikapongeza kushangilia, kwa sababu wanadamu hawana jambo bora chini ya jua kuliko kula na kunywa na kushangilia, na kwamba hilo liambatane nao katika kazi yao ngumu muda wa siku za maisha yao.” (Mhubiri 3:1, 4, 13; 8:15) Shangwe hiyo inaweza kuonekana familia inapokula pamoja au katika tafrija nyingine ndogo ya waabudu wa kweli.—Ayubu 1:4, 5, 18; Luka 10:38-42; 14:12-14.

4. Mtu anayepanga tafrija anapaswa kufikiria nini?

4 Ikiwa unapanga na kusimamia tafrija kama hiyo, unapaswa kufikiria kwa uangalifu mambo yatakayohusika, hata ikiwa unawaalika waamini wachache tu kwa ajili ya chakula na mazungumzo ya kirafiki. (Waroma 12:13) Ni vizuri uhakikishe kwamba ‘mambo yote yanatendeka kwa adabu,’ yakiongozwa na “hekima inayotoka juu.” (1 Wakorintho 14:40; Yakobo 3:17) Mtume Paulo aliandika hivi: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu. Epukeni kuwa vikwazo.” (1 Wakorintho 10:31, 32) Ni baadhi ya mambo gani yanayohitaji kufikiriwa kwa uangalifu sana? Kufikiria mambo hayo mapema kunaweza kukusaidia kuhakikisha kwamba mambo ambayo wewe na wageni wako mtafanya yataonyesha imani yenu kupitia matendo.—Waroma 12:2.

Mtafanya Tafrija ya Aina Gani?

5. Kwa nini yule anayepanga tafrija anapaswa kufikiria kwa uangalifu ikiwa ataandaa vileo na kuwa na muziki?

5 Watu wengi wanaopanga tafrija huhitaji kuamua iwapo wataandaa vileo. Si lazima kuwe na vileo ili tafrija iwe yenye kujenga. Kumbuka kwamba Yesu aliandaa chakula kwa ajili ya kundi kubwa la watu waliomjia. Aliwaandalia mikate na samaki wengi. Simulizi hilo halisemi kwamba aliandaa divai kimuujiza ingawa tunajua kwamba angeweza kufanya hivyo. (Mathayo 14:14-21) Ukiamua kuandaa vileo kwenye tafrija, uwe mwenye kiasi na uhakikishe kwamba kuna vinywaji vingine kwa ajili ya wale wasiokunywa vileo. (1 Timotheo 3:2, 3, 8; 5:23; 1 Petro 4:3) Usimlazimishe kamwe mtu yeyote anywe kinywaji ambacho kinaweza kumuuma “kama nyoka.” (Methali 23:29-32) Namna gani muziki au kuimba? Ikiwa tafrija yenu itakuwa na muziki, bila shaka utachagua muziki huo kwa uangalifu ukifikiria mdundo na maneno ya nyimbo. (Wakolosai 3:8; Yakobo 1:21) Wakristo wengi wameona kwamba kucheza nyimbo za Ufalme (Kingdom Melodies au Mélodies du Royaume) au hata kuimba nyimbo hizo pamoja hufanya tafrija iwe yenye furaha. (Waefeso 5:19, 20) Na nyakati zote hakikisha kwamba muziki hauchezwi kwa sauti ya juu hivi kwamba unavuruga mazungumzo mazuri au kuwasumbua majirani.—Mathayo 7:12.

6. Mwenye kupanga tafrija anaweza kuonyeshaje kwamba ana imani iliyo hai katika mazungumzo au shughuli nyinginezo?

6 Kwenye tafrija, Wakristo wanaweza kuzungumzia mambo mbalimbali, kusoma habari fulani kwa sauti, au kusimulia mambo yaliyoonwa yenye kupendeza. Ikiwa mazungumzo yanaenda kombo, yule mwenye kupanga tafrija anaweza kuyanyoosha kwa busara. Pia, anapaswa kuwa mwangalifu ili yeyote asitawale mazungumzo. Ikiwa mtu fulani anatawala mazungumzo, mwenye kupanga tafrija anaweza kuingilia mazungumzo kwa busara na kuwahusisha wengine, labda kwa kuwaomba wachanga wajieleze au kwa kuzungumzia jambo tofauti litakalowachochea wengine watoe maoni yao. Vijana kwa wazee watafurahia jambo hilo katika tafrija. Ikiwa wewe unayesimamia utaelekeza mambo kwa hekima na busara, ‘usawaziko wako utajulikana’ kwa wahudhuriaji wote. (Wafilipi 4:5) Wataona wazi kwamba una imani iliyo hai, na unaionyesha katika sehemu zote za maisha yako.

Arusi na Karamu za Arusi

7. Kwa nini kupanga arusi na tafrija za arusi kunahitaji uangalifu wa pekee?

7 Arusi ya Kikristo ni mojawapo ya matukio yenye kuleta shangwe. Watumishi wa kale wa Mungu, kutia ndani Yesu na wanafunzi wake, walikubali kushiriki katika matukio hayo yenye furaha, kutia ndani karamu. (Mwanzo 29:21, 22; Yohana 2:1, 2) Hata hivyo, hivi karibuni, imeonekana wazi kwamba kupanga tafrija za arusi kunahitaji jitihada za pekee ili tafrija hizo ziendeshwe kwa busara na usawaziko wa Kikristo. Lakini, tafrija ni mambo ya kawaida katika maisha yanayompa Mkristo nafasi ya kuonyesha imani yake.

8, 9. Desturi za arusi nyingi zinapatanaje na maneno tunayosoma kwenye 1 Yohana 2:16, 17?

8 Watu wengi ambao hawajui wala hawajali kanuni za Kimungu, huona arusi kuwa nafasi ya kufanya mambo kupita kiasi, au mahali ambapo mtu ana uhuru wa kufanya lolote atakalo. Mwanamke mmoja aliyeolewa hivi karibuni aliliambia hivi gazeti moja la Ulaya kuhusu arusi yake ya “kifalme”: ‘Tulibebwa katika msafara wenye magari manne yenye kukokotwa na farasi na kufuatwa na magari mengine 12 yenye kukokotwa na farasi, na gari lingine lenye bendi inayopiga muziki. Kisha, kukawa na chakula kitamu sana na muziki motomoto; ilikuwa sherehe kubwa. Siku hiyo nilikuwa malkia kama nilivyotamani.’

9 Huenda desturi zikatofautiana katika sehemu mbalimbali, lakini maneno hayo yanapatana kabisa na yale ambayo mtume Yohana aliandika: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.” Je, unaweza kuwazia Wakristo wakomavu wakitaka kufanya arusi ya “kifalme” yenye karamu kubwa? Badala ya kufanya hivyo, mtazamo wao unapaswa kuonyesha kwamba wanatambua kuwa “yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:16, 17.

10. (a) Ili kuwa na arusi yenye usawaziko, kwa nini ni muhimu kufanya mipango? (b) Maamuzi kuhusu wageni watakaoalikwa yanapaswa kufanywaje?

10 Wenzi Wakristo wanahitaji kuona mambo kihalisi na kuwa na usawaziko, na Biblia inaweza kuwasaidia. Ingawa siku ya arusi ni muhimu, wanajua kwamba ni mwanzo tu wa ndoa ya Wakristo wawili ambao wanatazamia kuishi milele. Hawahitaji kufanya karamu kubwa ya arusi. Wakiamua kufanya tafrija, wanapaswa kuhesabu gharama yake na kufikiria jinsi itakavyokuwa. (Luka 14:28) Wakiwa pamoja kama Wakristo, mume ndiye kichwa kulingana na Maandiko. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:22, 23) Hivyo, bwana-arusi ndiye aliye na daraka la kusimamia karamu ya arusi. Bila shaka, atawasiliana na bibi-arusi kuhusu mambo kama vile wageni watakaoalikwa au idadi ya wageni watakaohudhuria karamu ya arusi. Huenda isiwezekane au isifae kuwaalika marafiki na watu wote wa ukoo. Kwa hiyo, huenda watahitaji kufanya maamuzi fulani kwa usawaziko. Wenzi hao wanapaswa kuwa na uhakika kwamba hata wasipowaalika baadhi ya Wakristo wenzao, Wakristo hao wataelewa na hawataudhika.—Mhubiri 7:9.

“Msimamizi wa Karamu”

11. “Msimamizi wa karamu” anaweza kutimiza nini katika arusi?

11 Wenzi wakiamua kufanya karamu ya arusi, wanaweza kuhakikishaje kwamba karamu hiyo ni yenye heshima? Kwa miaka mingi sasa, Mashahidi wa Yehova wametambua hekima ya kutilia maanani jambo fulani linalotajwa kuhusiana na kikusanyiko ambacho Yesu alihudhuria huko Kana. Kulikuwa na “msimamizi wa karamu,” ambaye bila shaka alikuwa mwamini mkomavu. (Yohana 2:9, 10) Vivyo hivyo, bwana-arusi mwenye hekima atachagua ndugu Mkristo aliye mkomavu kiroho atimize daraka hilo muhimu. Baada ya kujua mapendezi ya bwana-arusi, msimamizi wa karamu anaweza kutekeleza mapendezi hayo kabla na wakati wa karamu.

12. Bwana-arusi anapaswa kufikiria nini kuhusu matumizi ya vileo?

12 Kupatana na yale tuliyozungumzia kwenye fungu la 5, wenzi fulani huamua kutoandaa vileo katika karamu ili visitumiwe vibaya na hivyo kufanya karamu hiyo isiwe yenye furaha na isifanikiwe. (Waroma 13:13; 1 Wakorintho 5:11) Hata hivyo, ikiwa vileo vitaandaliwa, bwana-arusi anapaswa kuhakikisha kwamba vinaandaliwa kwa kiasi. Kulikuwa na divai kwenye arusi ambayo Yesu alihudhuria huko Kana, naye aliandaa divai nzuri. Inapendeza kwamba msimamizi huyo wa karamu alieleza hivi: “Wengine wote hutoa divai nzuri kwanza, na ile hafifu wakati ambapo watu wameingiwa na kileo. Wewe umehifadhi divai nzuri mpaka sasa.” (Yohana 2:10) Hapana shaka kwamba Yesu hakuwatia moyo watu walewe, kwa kuwa alichukia zoea hilo. (Luka 12:45, 46) Akistaajabia uzuri wa divai hiyo, msimamizi huyo alionyesha wazi kwamba aliwahi kuwaona watu fulani wakilewa katika karamu ya arusi. (Matendo 2:15; 1 Wathesalonike 5:7) Kwa hiyo, bwana-arusi na Mkristo mwenye kutegemeka ambaye amemweka kuwa msimamizi wa karamu wanapaswa kuhakikisha kwamba wahudhuriaji wote wanafuata mwongozo huu ulio wazi: “Msiwe mkilewa divai, ambayo ina upotovu ndani yake.”—Waefeso 5:18; Methali 20:1; Hosea 4:11.

13. Wenzi wanapaswa kufikiria nini wakiamua kuwa na muziki kwenye karamu yao ya arusi, na kwa nini?

13 Kama ilivyo kwenye tafrija nyinginezo, ikiwa kutakuwa na muziki, kiasi cha sauti kinapaswa kutiliwa maanani ili kuwawezesha watu wazungumze bila shida. Mzee mmoja Mkristo alisema hivi: “Kadiri usiku unavyoingia, wakati mazungumzo yanapopamba moto au watu wanapoanza kucheza dansi, ndivyo nyakati nyingine sauti ya muziki inavyoongezeka. Muziki uliokuwa ukichezwa kwa sauti ya chini unaweza kuwa wenye kelele na kuvuruga mazungumzo. Karamu ya arusi ni pindi ya kuwa na ushirika mzuri. Ingesikitisha kama nini ikiwa muziki ungechezwa kwa sauti ya juu na hivyo kuvuruga pindi hiyo!” Katika jambo hilo, bwana-arusi na msimamizi wa karamu wanahitaji kuchukua hatua ya kuamua aina ya na kiasi cha sauti ya muziki, bila kuacha daraka hilo mikononi mwa wanaoshughulikia muziki, iwe wamekodiwa au hapana. Paulo aliandika hivi: “Lolote lile mnalofanya kwa neno au kwa tendo, fanyeni kila jambo katika jina la Bwana Yesu.” (Wakolosai 3:17) Wageni wanaporudi nyumbani baada ya karamu ya arusi, je, watakumbuka kuwa muziki ulionyesha kwamba wenzi hao walifanya kila jambo kwa jina la Yesu? Inapaswa kuwa hivyo.

14. Wakristo wanapaswa kukumbuka nini kwa shangwe kuhusiana na arusi?

14 Naam, arusi iliyopangwa vizuri inaweza kukumbukwa kwa shangwe. Adam na Edyta, ambao walifunga ndoa miaka 30 iliyopita, walisema hivi kuhusu arusi moja: “Ungeweza kwa kweli kuona roho ya Kikristo. Kulikuwa na nyimbo za kumsifu Yehova na vilevile burudani nyingine nzuri. Kucheza dansi na muziki hayakuwa mambo muhimu. Ilikuwa sherehe yenye kupendeza na yenye kujenga, na kila kitu kilifanywa kupatana na kanuni za Biblia.” Ni wazi kwamba kuna mambo mengi ambayo bwana na bibi-arusi wanaweza kufanya ili kuthibitisha imani yao kwa matendo.

Zawadi za Arusi

15. Ni mashauri gani ya Biblia yanayoweza kufuatwa kuhusu zawadi za arusi?

15 Katika nchi nyingi ni jambo la kawaida kwa marafiki na watu wa ukoo kuwapa zawadi wale wanaofanya arusi. Ni vizuri kukumbuka nini ukiamua kutoa zawadi? Kumbuka maneno haya ya mtume Yohana: “Mtu kujionyesha mali yake maishani.” Yohana hakuhusianisha jambo hilo na Wakristo ambao wanaonyesha imani yao kwa matendo, lakini alilihusianisha na ‘ulimwengu ambao unapitilia mbali.’ (1 Yohana 2:16, 17) Tukifikiria maneno ya Yohana yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu, je, wenzi hao wapya wanapaswa kutangaza majina ya wale ambao wametoa zawadi? Wakristo wa Makedonia na Akaya walitoa michango kwa ajili ya akina ndugu huko Yerusalemu, lakini hakuna jambo linaloonyesha kwamba majina yao yalitangazwa. (Waroma 15:26) Wakristo wengi wanaotoa zawadi za arusi wasingetaka wajulikane ili wasijiletee sifa. Kuhusu jambo hilo, fikiria shauri la Yesu kwenye Mathayo 6:1-4.

16. Kuhusiana na zawadi za arusi, wenzi wapya wanaweza kuepukaje kuumiza hisia za wengine?

16 Kutangaza majina ya waliotoa zawadi kunaweza “kuchochea mashindano” kuhusu ni zawadi gani iliyo bora au ghali zaidi. Hivyo, wenzi wapya Wakristo huepuka kutangaza majina ya wenye kutoa zawadi. Kutangaza majina ya watu wanaotoa zawadi kwaweza kuwaaibisha wengine ambao labda hawakuweza kutoa zawadi. (Wagalatia 5:26; 6:10) Kwa kweli si vibaya kwa bwana na bibi-arusi kujua ni nani aliyetoa zawadi fulani. Labda wanaweza kuona jina la yule aliyetoa zawadi kwenye kadi iliyoambatanishwa na zawadi hiyo ingawa haitasomwa mbele ya watu wote. Tunaponunua, kutoa, au kupokea zawadi za arusi, sote tuna nafasi ya kuthibitisha kwamba hata katika jambo la kibinafsi kama hilo, imani yetu inaonyeshwa kwa matendo yetu. *

17. Wakristo wanapaswa kuwa na lengo gani kuhusiana na imani na matendo yao?

17 Kuthibitisha imani yetu kunahusisha mengi zaidi ya kuishi maisha ya adili, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Acheni kila mmoja wetu awe na imani iliyo hai ambayo inamwongoza katika kila jambo analofanya. Naam, tunaweza kuonyesha imani yetu kwa matendo ambayo ‘yanafanywa kwa ukamili,’ kutia ndani yale ambayo tumezungumzia.—Ufunuo 3:2.

18. Maneno ya Yohana 13:17 yanaweza kuthibitikaje kuwa ya kweli kuhusiana na arusi za Kikristo na tafrija?

18 Baada ya Yesu kuwawekea mitume wake waaminifu kielelezo kizuri kwa kujishusha na kuwaosha miguu, alisema hivi: “Ikiwa mnajua mambo haya, wenye furaha ni ninyi ikiwa mnayatenda.” (Yohana 13:4-17) Katika maeneo tunamoishi leo, huenda isiwe lazima au jambo la kawaida kuosha miguu ya mtu mwingine, kama vile mgeni anayetutembelea. Hata hivyo, kama tulivyoona katika makala hii, tunaweza kuonyesha imani yetu kwa kuwatendea wengine kwa upendo na ufikirio katika mambo mengine maishani, kutia ndani yale yanayohusu tafrija na arusi za Kikristo. Tunaweza kufanya hivyo iwe tunafanya arusi au tumealikwa kwenye arusi au tafrija ya arusi ya Wakristo wenye furaha ambao wanataka kuonyesha imani yao kwa matendo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Mambo mengine kuhusu arusi na karamu za arusi yanazungumziwa katika makala inayofuata yenye kichwa, “Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi.”

Ungejibuje?

Unaweza kuthibitishaje imani yako

• unapopanga tafrija?

• unapopanga arusi au karamu ya arusi?

• unapotoa au kupokea zawadi za arusi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Hata unapowaalika watu wachache tu, ongozwa na “hekima inayotoka juu”