Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuheshimu Makusanyiko Yetu Matakatifu

Kuheshimu Makusanyiko Yetu Matakatifu

Kuheshimu Makusanyiko Yetu Matakatifu

“Mimi pia nitawaleta katika mlima wangu mtakatifu na kuwafanya washangilie ndani ya nyumba yangu ya sala.”—ISAYA 56:7.

1. Tuna sababu gani za Kimaandiko za kuheshimu inavyofaa mikutano yetu?

YEHOVA amewakusanya watu wake, Wakristo watiwa-mafuta na wenzao wa umati mkubwa, ili wamwabudu katika ‘mlima wake mtakatifu.’ Anawafanya washangilie ndani ya ‘nyumba yake ya sala,’ hekalu lake la kiroho, ambalo ni “nyumba ya sala kwa ajili ya mataifa yote.” (Isaya 56:7; Marko 11:17) Matukio hayo yanaonyesha kwamba ibada ya Yehova ni takatifu, safi, na imeinuliwa. Tunapoheshimu inavyofaa mikutano yetu ya kujifunza na kuabudu, tunathibitisha kwamba tunayaona mambo matakatifu kama Yehova anavyoyaona.

2. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova aliona mahali alipochagua kwa ajili ya ibada yake kuwa patakatifu, na Yesu alionyesha jinsi gani kwamba alikuwa na maoni kama hayo?

2 Katika Israeli la kale, mahali ambapo Yehova alichagua kwa ajili ya ibada yake palipaswa kuonwa kuwa patakatifu. Maskani na vyombo vyake vilipaswa kutiwa mafuta na kutakaswa “ili kwa kweli viwe vitakatifu zaidi.” (Kutoka 30:26-29) Vyumba viwili vya patakatifu viliitwa “Mahali Patakatifu” na “Patakatifu Zaidi.” (Waebrania 9:2, 3) Baadaye, hekalu la Yerusalemu lilichukua mahali pa maskani. Yerusalemu liliitwa “jiji takatifu” kwa sababu lilikuwa kitovu cha ibada ya Yehova. (Nehemia 11:1; Mathayo 27:53) Wakati wa huduma yake duniani, Yesu mwenyewe aliheshimu inavyofaa hekalu. Aliwakasirikia watu kwa sababu ya kutumia kwa njia isiyo ya heshima eneo la hekalu kwa makusudi ya kibiashara na kama njia fupi ya kupitishia vitu kwenda sehemu nyingine za Yerusalemu.—Marko 11:15, 16.

3. Ni nini kinachoonyesha kwamba makusanyiko ya Waisraeli yalikuwa matakatifu?

3 Waisraeli walikusanyika kwa ukawaida ili kumwabudu Yehova na kusikiliza Sheria yake ikisomwa. Siku fulani za sherehe zao ziliitwa mikusanyiko mitakatifu, kuonyesha kwamba makusanyiko hayo yalikuwa matakatifu. (Mambo ya Walawi 23:2, 3, 36, 37) Katika kusanyiko la watu wote siku za Ezra na Nehemia, Walawi “walikuwa wakiwafafanulia watu sheria.” Kwa kuwa “watu wote walikuwa wakilia walipokuwa wakisikiliza maneno ya sheria,” Walawi “walikuwa wanawaamuru watu wote wanyamaze, wakisema: ‘Nyamazeni! kwa maana leo ni siku takatifu.’” Kisha, Waisraeli wakafanya Sherehe ya Vibanda ya siku saba kwa “shangwe kubwa sana.” Zaidi ya hilo, “kitabu cha sheria ya Mungu wa kweli kikasomwa kwa sauti kubwa siku baada ya siku, tangu siku ya kwanza mpaka siku ya mwisho; nao wakaendelea kufanya sherehe hiyo siku saba; na katika siku ya nane kukawa na kusanyiko kuu, kulingana na ile kanuni.” (Nehemia 8:7-11, 17, 18) Kwa kweli, hizo zilikuwa pindi takatifu na wahudhuriaji walipaswa kusikiliza kwa heshima.

Mikutano Yetu Ni Makusanyiko Matakatifu

4, 5. Ni mambo gani kuhusu mikutano yetu yanayothibitisha kwamba ni makusanyiko matakatifu?

4 Kwa kweli, leo Yehova hana jiji halisi takatifu duniani, lenye hekalu la pekee lililowekwa wakfu kwa ajili ya ibada yake. Hata hivyo, hatupaswi kusahau kwamba mikutano ya kumwabudu Yehova ni makusanyiko matakatifu. Tunakutana mara tatu kwa juma ili kusoma na kujifunza Maandiko. Neno la Yehova ‘linafafanuliwa,’ na kama ilivyokuwa wakati wa Nehemia, ‘maana yake inaelezwa.’ (Nehemia 8:8) Mikutano yetu yote inaanza na kumalizika kwa sala, na katika mikutano mingi, tunaimba nyimbo za kumsifu Yehova. (Zaburi 26:12) Kwa kweli, mikutano ya kutaniko ni sehemu ya ibada yetu na tunahitaji kusikiliza kwa heshima na kusali kwa ajili ya mikutano hiyo.

5 Yehova anawabariki watu wake wanapokutana pamoja ili kumwabudu, kujifunza Neno lake, na kufurahia ushirika mzuri wa Kikristo. Wakati wa mikutano unapofika, tunaweza kuwa na hakika kwamba hapo ndipo mahali ambapo ‘Yehova ameamuru baraka iwepo.’ (Zaburi 133:1, 3) Tunapokea baraka hiyo tunapohudhuria na kusikiliza kwa makini programu ya kiroho. Kwa kuongezea, Yesu alisema hivi: “Palipo na wawili au watatu wakiwa wamekusanyika pamoja katika jina langu, hapo mimi nipo katikati yao.” Mistari inayozunguka andiko hilo inaonyesha kwamba maneno hayo yanahusu hasa wazee Wakristo wanaokutana ili kushughulikia matatizo mazito kati ya watu, lakini kanuni hiyo inaweza pia kuhusu mikutano yetu. (Mathayo 18:20) Ikiwa Kristo, kupitia roho takatifu, yupo pamoja na Wakristo wanapokutana pamoja katika jina lake, je, mikutano hiyo haipaswi kuonwa kuwa mitakatifu?

6. Tunaweza kusema nini kuhusu mahali petu pa ibada, pawe pakubwa au padogo?

6 Ni kweli kwamba Yehova hakai katika mahekalu yaliyojengwa na wanadamu. Hata hivyo, Majumba yetu ya Ufalme ni mahali pa ibada ya kweli. (Matendo 7:48; 17:24) Tunakutana humo ili kujifunza Neno la Yehova, kusali kwake, na kuimba sifa zake. Ndivyo ilivyo pia kuhusu Majumba yetu ya Makusanyiko. Sehemu kubwa kama vile, kumbi, majumba ya maonyesho, au viwanja vya michezo zinapokodiwa kwa ajili ya makusanyiko yetu matakatifu zinakuwa mahali pa ibada. Pindi hizo za ibada, ziwe kubwa au ndogo, zinastahili kuheshimiwa, na tunapaswa kuonyesha heshima hiyo kwa mtazamo na mwenendo wetu.

Njia za Kuonyesha Tunaheshimu Makusanyiko Yetu

7. Ni njia gani iliyo wazi ya kuonyesha kwamba tunaheshimu makusanyiko yetu?

7 Kuna njia zilizo wazi za kuonyesha kwamba tunaheshimu makusanyiko yetu. Njia moja ni kuwapo ili kuimba nyimbo za Ufalme. Nyimbo nyingi zimetungwa kama sala na hivyo zinapaswa kuimbwa kwa heshima. Akitaja Zaburi ya 22, mtume Paulo aliandika hivi kumhusu Yesu: “Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya kutaniko nitakusifu wewe kwa wimbo.” (Waebrania 2:12) Hivyo, tunapaswa kuwa na zoea la kuketi kabla mwenyekiti hajaanzisha wimbo na tunapaswa kuimba huku tukikazia akilini maana ya maneno ya wimbo. Acheni kuimba kwetu kuonyeshe hisia za mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Nitamsifu Yehova kwa moyo wangu wote katika kikundi cha rafiki za karibu walio wanyoofu na katika kusanyiko.” (Zaburi 111:1) Ndiyo, kumwimbia Yehova sifa ni sababu moja nzuri sana ya kufika mapema kwenye mikutano yetu na kuwapo hadi inapomalizika.

8. Ni mfano gani katika Biblia unaoonyesha kwamba tunapaswa kusikiliza kwa heshima sala zinazotolewa katika mikutano yetu?

8 Jambo lingine linalofanya mikutano yetu yote iwe yenye thamani zaidi kiroho ni sala zinazotoka moyoni ambazo zinatolewa kwa ajili ya wote wanaohudhuria. Wakati fulani, Wakristo wa karne ya kwanza huko Yerusalemu walikutana pamoja na “wakampaazia Mungu sauti zao kwa umoja” katika sala ambayo walitoa kwa moyo wote. Basi, ijapokuwa waliteswa, waliendelea ‘kusema neno la Mungu kwa ujasiri.’ (Matendo 4:24-31) Je, tunaweza kuwazia yeyote kati ya waliohudhuria akiruhusu akili zake zitangetange sala hiyo ilipokuwa ikitolewa? Hapana, walisali “kwa umoja.” Sala zinazotolewa katika mikutano yetu zinaonyesha hisia za wote wanaohudhuria. Tunapaswa kuzisikiliza kwa heshima.

9. Tunaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tunaheshimu makusanyiko yetu matakatifu kupitia mavazi na mwenendo wetu?

9 Zaidi ya hayo, tunaweza kuonyesha jinsi tunavyoheshimu sana utakatifu wa makusanyiko yetu kwa njia tunayovalia. Mavazi yetu na mitindo yetu ya nywele inaweza kufanya mikutano yetu iheshimiwe zaidi. Mtume Paulo alishauri hivi: “Natamani kwamba kila mahali wanaume waendelee kutoa sala, wakiinua mikono yenye ushikamanifu, bila ghadhabu na mabishano. Vivyo hivyo natamani wanawake wajipambe kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, si kwa mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mavazi yaliyo ghali sana, bali kwa njia inayowafaa wanawake wanaodai kumheshimu Mungu.” (1 Timotheo 2:8-10) Tunapohudhuria makusanyiko makubwa katika viwanja vya michezo, tunaweza kuvaa mavazi yanayopatana na hali ya hewa na bado yawe yenye kuheshimika. Kwa kuongezea, tukiheshimu tukio hilo hatutakula au kutafuna chingamu (au bazooka) wakati wa programu. Kuvalia na kujiendesha inavyofaa kwenye makusanyiko yetu, humletea heshima Yehova Mungu, ibada yake, na waabudu wenzetu.

Mwenendo Unaostahili Katika Nyumba ya Mungu

10. Mtume Paulo alionyesha jinsi gani kwamba tunapaswa kujiendesha kwa njia inayostahili katika mikutano yetu ya Kikristo?

10 Katika 1 Wakorintho, sura ya 14, tunapata mashauri yenye hekima ya mtume Paulo yanayoonyesha jinsi mikutano ya Kikristo inavyopaswa kuendeshwa. Alimalizia kwa kusema hivi: “Mambo yote na yatendeke kwa adabu na kwa mpango.” (1 Wakorintho 14:40) Mikutano yetu ni sehemu muhimu ya utendaji wa kutaniko la Kikristo, na tunapokuwa kwenye mikutano hiyo tunapaswa kujiendesha kwa njia inayostahili nyumba ya Yehova.

11, 12. (a) Ni nini kinachopaswa kukaziwa akilini mwa watoto wanaohudhuria mikutano yetu? (b) Watoto wanaweza kutangaza jinsi gani imani yao kwa njia inayofaa kwenye mikutano yetu?

11 Watoto hasa, wanahitaji kufundishwa jinsi ya kujiendesha katika mikutano yetu. Wazazi Wakristo wanapaswa kuwaeleza watoto wao kwamba Jumba la Ufalme na mahali pa Funzo la Kitabu la Kutaniko si mahali pa kuchezea. Ni mahali pa kumwabudu Yehova na kujifunzia Neno lake. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Linda miguu yako wakati wowote unapoenda kwenye nyumba ya Mungu wa kweli; na usogee karibu usikie.” (Mhubiri 5:1) Musa aliwafundisha Waisraeli wakusanyike pamoja, watu wazima na “watoto wadogo.” Alisema hivi: “Wakutanishe watu . . . ili wasikilize na ili wajifunze, kwa maana ni lazima wamwogope Yehova Mungu wenu na kuwa waangalifu kuyatimiza maneno yote ya sheria hii. Na wana wao ambao hawakujua wanapaswa kusikiliza, nao lazima wajifunze kumwogopa Yehova.”—Kumbukumbu la Torati 31:12, 13.

12 Vivyo hivyo leo, watoto wetu huhudhuria mikutano pamoja na wazazi ili hasa wasikilize na kujifunza. Mara tu wanapoweza kusikiliza kwa makini na kuelewa kweli za msingi za Biblia, watoto pia wanaweza kufanya “tangazo la hadharani” la imani yao kwa kutoa maelezo mafupi. (Waroma 10:10) Huenda mtoto mdogo akaanza kwa kujibu kwa maneno machache swali ambalo anaelewa. Mwanzoni, huenda akasoma jibu, lakini baada ya muda, atajitahidi kujibu kwa maneno yake mwenyewe. Hilo litamfurahisha mtoto, naye atapata faida, na maelezo kama hayo ya imani yanayotoka moyoni huwafurahisha watu wazima wanaohudhuria. Kwa kawaida, wazazi wanaweka mfano wanapotoa maelezo wao wenyewe. Ikiwezekana, ni vizuri pia watoto wawe na Biblia yao, kitabu cha nyimbo, na kichapo kinachotumiwa mkutanoni. Wanapaswa kujifunza kuheshimu inavyofaa vichapo hivyo. Mambo hayo yote yatakazia akilini mwa watoto kwamba mikutano yetu ni makusanyiko matakatifu.

13. Tunatazamia wale wanaohudhuria mikutano yetu kwa mara ya kwanza wafanye nini?

13 Bila shaka, hatutaki mikutano yetu ifanane na mikutano ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Watu katika mikutano hiyo wanakuwa wenye ubaridi na wanajionyesha kuwa watakatifu. Mikutano mingine ina kelele kama maonyesho ya muziki wa roki. Tunataka mikutano yetu kwenye Jumba la Ufalme iwe michangamfu na yenye urafiki, lakini isiwe kama majumba ya kijamii. Tunakutana ili kumwabudu Yehova, kwa hiyo mikutano yetu inapaswa sikuzote kuwa yenye heshima. Ni tamaa yetu kwamba baada ya kusikiliza mafundisho na kutazama mwenendo wetu na wa watoto wetu, wale wanaohudhuria kwa mara ya kwanza watasema: “Kwa kweli Mungu yupo katikati yenu.”—1 Wakorintho 14:25.

Jambo Linalodumu la Ibada Yetu

14, 15. (a) Tunaweza kuepuka kwa njia gani “kuipuuza nyumba ya Mungu wetu”? (b) Andiko la Isaya 66:23 linatimizwa jinsi gani leo?

14 Kama ilivyotajwa mwanzoni, Yehova anawakusanya watu wake na kuwafanya washangilie ndani ya ‘nyumba yake ya sala,’ hekalu lake la kiroho. (Isaya 56:7) Mwanamume mwaminifu Nehemia aliwakumbusha Wayahudi wenzake kwamba walipaswa kuonyesha heshima inayofaa kwa hekalu halisi kwa kulitegemeza kwa mali zao. Alisema hivi: “Hatupaswi kuipuuza nyumba ya Mungu wetu.” (Nehemia 10:39) Zaidi ya hilo, hatupaswi kupuuza mwaliko wa Yehova wa kumwabudu ndani ya ‘nyumba yake ya sala.’

15 Akionyesha uhitaji wa kukutanika pamoja kwa ukawaida kwa ajili ya ibada, Isaya alitabiri hivi: “‘Na hakika itatukia kwamba kutoka mwezi mpya mpaka mwezi mpya na kutoka sabato mpaka sabato wanadamu wote wataingia ili kuinama mbele zangu,’ Yehova amesema.” (Isaya 66:23) Unabii huo unatimizwa leo. Kwa kawaida, kila juma katika kila mwezi, Wakristo waliojiweka wakfu wanakusanyika ili kumwabudu Yehova. Wanafanya hivyo kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kushiriki katika huduma ya hadharani, na pia kwa kufanya mambo mengine. Je, wewe ni mmoja wa wale ambao kwa kawaida ‘wanaingia ili kuinama mbele za Yehova’?

16. Kwa nini kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kunapaswa kuwa jambo la kudumu la maisha yetu sasa?

16 Andiko la Isaya 66:23 litatimizwa kikamili kuhusiana na maisha katika ulimwengu mpya ambao Yehova ameahidi. Wakati huo, kwa njia halisi, “wanadamu wote wataingia” juma baada ya juma na mwezi baada ya mwezi, “ili kuinama mbele,” au kumwabudu Yehova kwa umilele wote. Kwa kuwa kukutana pamoja ili kumwabudu Yehova ni jambo litakalodumu la maisha yetu ya kiroho katika mfumo mpya wa mambo, je, hatupaswi kufanya kuhudhuria kwa ukawaida makusanyiko yetu matakatifu kuwe jambo la kudumu la maisha yetu sasa?

17. Kwa nini tunahitaji mikutano yetu ‘zaidi kwa kadiri tunavyoona siku ile kuwa inakaribia’?

17 Kadiri mwisho unavyokaribia, ndivyo tunavyopaswa kuazimia zaidi kuliko wakati mwingine wowote kuhudhuria makusanyiko yetu ya Kikristo ili kuabudu. Kwa kuwa tunaheshimu utakatifu wa mikutano yetu, haturuhusu kazi ya kimwili, kazi ya shule, au masomo ya jioni yatuzuie tusihudhurie mikutano kwa ukawaida pamoja na waamini wenzetu. Tunahitaji kuimarishwa na ushirika wetu. Mikutano yetu ya kutaniko inatupa nafasi ya kufahamiana, kutiana moyo, na kuchocheana katika “upendo na matendo mazuri.” Tunahitaji kufanya hivyo ‘zaidi kwa kadiri tunavyoona siku ile kuwa inakaribia.’ (Waebrania 10:24, 25) Kwa hivyo, acheni nyakati zote tuheshimu ifaavyo makusanyiko yetu matakatifu kwa kuyahudhuria kwa ukawaida, kuvalia ifaavyo, na kujiendesha kwa njia inayostahili. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunayaona mambo matakatifu kama Yehova anavyoyaona.

Kwa Kupitia

• Ni nini kinachoonyesha kwamba makusanyiko ya watu wa Yehova yanapaswa kuonwa kuwa matakatifu?

• Ni mambo gani kuhusu mikutano yetu ambayo yanathibitisha kwamba ni makusanyiko matakatifu?

• Watoto wanaweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanaheshimu utakatifu wa mikutano yetu?

• Kwa nini kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kunapaswa kuwa jambo la kudumu la maisha yetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Mikutano ya kumwabudu Yehova ni makusanyiko matakatifu haidhuru inafanyiwa wapi

[Picha katika ukurasa wa 31]

Watoto wetu wanahudhuria mikutano ili kusikiliza na kujifunza