Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuinuka na Kuanguka kwa “Wataalamu”

Kuinuka na Kuanguka kwa “Wataalamu”

Kuinuka na Kuanguka kwa “Wataalamu”

KATIKA ulimwengu wa leo, watu wanaotumia kompyuta wanaweza kutafuta kwenye Intaneti mashauri kuhusu wazazi na kupata mara moja marejeo zaidi ya milioni 26. Ukitumia dakika moja kutazama na kusoma kila moja ya marejeo hayo, mtoto wako atakuwa mtu mzima na kuondoka nyumbani kabla hujamaliza kuyasoma.

Kabla ya madaktari wa watoto, wanasaikolojia wa watoto, na Intaneti kutokea, wazazi waliwaendea nani ili kupata mashauri? Kwa kawaida, waliwaendea watu wao wa ukoo. Akina mama, baba, shangazi, na wajomba, walikuwa tayari na waliweza kutoa mwongozo, msaada wa kifedha, na kuwatunza watoto wachanga. Lakini katika nchi nyingi, watu hawana mahusiano ya karibu ya familia kwa sababu watu wengi wametoka mashambani na kuhamia mijini. Leo, kwa kawaida akina mama na baba hulazimika kufanya kazi ngumu ya kuwalea watoto bila msaada wowote.

Bila shaka, hiyo ni mojawapo ya sababu ambazo zimefanya kazi ya kuwatunza watoto iwe biashara ambayo imesitawi haraka. Sababu nyingine ni kwamba watu wanaamini kuwa sayansi inaweza kutoa mashauri mazuri. Kufikia mwishoni mwa miaka ya 1800, tayari Wamarekani walikuwa wakisadiki kwamba sayansi inaweza kuboresha kila sehemu ya maisha ya wanadamu. Pia, walisadiki kwamba sayansi ingeboresha njia ya kulea watoto. Hivyo, mnamo 1899, Chama cha Kitaifa cha Akina Mama cha Marekani kilipolalamika waziwazi kuhusu “kushindwa kwa wazazi” kuwalea watoto, wataalamu wengi wa “kisayansi” walijitokeza haraka ili kutoa msaada. Waliahidi kuwasaidia akina mama na baba waliohitaji msaada wa kuwalea watoto wao.

Kutegemea Vitabu Vyenye Mashauri ya Kulea Watoto

Hata hivyo, wataalamu hao wametimiza nini? Je, leo wazazi wana mahangaiko machache na wanaweza kuwalea vizuri zaidi watoto wao kuliko wazazi wa miaka iliyopita? Uchunguzi uliofanywa hivi majuzi nchini Uingereza unaonyesha kwamba sivyo ilivyo. Uchunguzi huo ulionyesha kwamba karibu asilimia 35 ya wazazi bado wanatafuta mashauri yenye kutegemeka. Wazazi wengine hawana la kufanya ila kufuata fikira zao wenyewe.

Katika kitabu chake (Raising America: Experts, Parents, and a Century of Advice About Children), Ann Hulbert anachanganua vitabu vya kitaalamu kuhusu kulea watoto. Hulbert, ambaye ni mama mwenye watoto wawili, anasema kwamba kauli chache za wataalamu zilitegemea sayansi iliyothibitishwa. Kwa kweli, yaelekea kwamba mashauri yao yanategemea mambo waliyojionea maishani mwao badala ya mambo yaliyothibitishwa. Leo, tunapofikiria mashauri ambayo yaliandikwa zamani, mara nyingi mashauri hayo huonekana kuwa yenye kubadilika-badilika, kupingana, na nyakati nyingine ya kiajabu-ajabu.

Basi, wazazi wa leo watafanya nini? Kwa wazi, wengi wamechanganyikiwa, kwa sababu kuna mashauri, maoni, na ubishi mwingi kuliko wakati mwingine wowote. Hata hivyo, si wazazi wote ambao wanahisi kuwa hawana mwongozo. Wazazi ulimwenguni pote wanafaidika kutokana na chanzo cha zamani cha hekima ambacho bado kinatoa mashauri yenye kutegemeka kama makala inayofuata itakavyoonyesha.