Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujenga kwa Umoja Ili Kumsifu Mungu

Kujenga kwa Umoja Ili Kumsifu Mungu

Kujenga kwa Umoja Ili Kumsifu Mungu

WATU katika mojawapo ya Visiwa vya Solomon waliona Jumba la Ufalme jipya la Mashahidi wa Yehova. Mwanamke mmoja alisema hivi: “Katika kanisa letu watu wengi huchanga pesa. Sisi huwaomba waumini wetu watoe pesa, lakini bado hatuna pesa za kutosha kujenga kanisa jipya. Ninyi Mashahidi mnapataje pesa?” Shahidi huyo akamjibu hivi: “Tunamwabudu Yehova tukiwa familia ya ulimwenguni pote. Kutaniko letu na ndugu zetu ulimwenguni pote walitoa michango tuliyohitaji ili kujenga Jumba hili jipya la Ufalme. Yehova ametufundisha kuwa na umoja katika mambo yote.”

Unaweza kuona umoja miongoni mwa Mashahidi wa Yehova katika shughuli zao zote, kutia ndani ujenzi wa maelfu ya Majumba ya Ufalme. Umoja katika kutimiza miradi hiyo si jambo jipya. Watu wa Mungu wamekuwa na umoja huo kwa maelfu ya miaka. Jinsi gani?

Kujenga Maskani na Hekalu

Yehova alikuwa akifikiria taifa la Israeli alipomwambia Musa maneno haya miaka zaidi ya 3,500 iliyopita: “Nao watanifanyia patakatifu.” (Kutoka 25:8) Kuhusu muundo wa mradi huo wa ujenzi, Yehova aliendelea kusema: “Kulingana na yote ninayokuonyesha wewe [mtu mmoja, yaani, Musa] kuwa mfano wa maskani na mfano wa vyombo vyake vyote, hivyo ndivyo mtakavyoifanya [watu wengi, yaani, taifa lote].” (Kutoka 25:9) Kisha, Yehova akatoa maelezo kamili kuhusu muundo wa patakatifu, na vyombo vyake vyote. (Kutoka 25:10–27:19) “Maskani” hiyo au hema, ingekuwa kitovu cha ibada ya kweli kwa Waisraeli wote.

Hatujui ni watu wangapi walioshiriki katika mradi huo, lakini Waisraeli wote waliombwa wauunge mkono. Musa aliwaambia: “Kutoka katikati yenu toeni mchango kwa ajili ya Yehova. Kila mtu mwenye moyo wenye nia na aulete ukiwa mchango wa Yehova.” (Kutoka 35:4-9) Waisraeli walitendaje? Andiko la Kutoka 36:3 linasema hivi: “Wakachukua toka mbele ya Musa michango yote ambayo wana wa Israeli walikuwa wameleta kwa ajili ya kazi ya utumishi mtakatifu ili kuifanya, na, hao wa mwisho, bado walimletea matoleo ya hiari asubuhi kwa asubuhi.”

Mara moja kulikuwa na rundo kubwa la vitu vilivyochangwa, na watu waliendelea kuleta vitu zaidi. Hatimaye, mafundi waliokuwa wakifanya kazi wakamwambia Musa: “Watu wanaleta vitu vingi zaidi kuliko vinavyohitajiwa kwa utumishi kwa ajili ya kazi ambayo Yehova ameamuru ifanywe.” Basi, Musa akaamuru: “Wanaume na wanawake, msitoe vitu zaidi kwa ajili ya mchango mtakatifu.” Nayo matokeo yakawaje? “Vitu hivyo vikawa vya kutosha kwa ajili ya kazi yote iliyopasa kufanywa, na kuzidi.”—Kutoka 36:4-7.

Kwa sababu ya ukarimu wa Waisraeli, ujenzi wa maskani ulikamilishwa kwa muda wa mwaka mmoja. (Kutoka 19:1; 40:1, 2) Kwa kutegemeza ibada ya kweli, watu wa Mungu walimheshimu Yehova. (Methali 3:9) Baadaye, wangeshiriki katika mradi mkubwa zaidi wa ujenzi. Na mara nyingine tena, wote waliopenda wangeweza kusaidia katika mradi huo, iwe walikuwa na ustadi wa kujenga au hapana.

Karibu karne tano baada ya kujenga maskani, Waisraeli walianza kujenga hekalu huko Yerusalemu. (1 Wafalme 6:1) Lingekuwa jengo la kudumu na lenye utukufu, lililojengwa kwa mawe na mbao. (1 Wafalme 5:17, 18) Yehova alimpa Daudi ramani za ujenzi wa hekalu ‘kwa kumwongoza kwa roho.’ (1 Mambo ya Nyakati 28:11-19) Hata hivyo, alimchagua Sulemani mwana wa Daudi aongoze kazi hiyo ya ujenzi. (1 Mambo ya Nyakati 22:6-10) Daudi alitegemeza mradi huo kwa moyo wake wote. Alikusanya mawe, nguzo, na vifaa vingine, naye akachanga kiasi kikubwa cha dhahabu na fedha yake. Pia, aliwatia moyo Waisraeli wenzake wawe wakarimu kwa kuwauliza hivi: “Ni nani anayejitolea kuujaza mkono wake leo kwa zawadi kwa ajili ya Yehova?” Watu walitendaje?—1 Mambo ya Nyakati 29:1-5.

Sulemani alipoanza kujenga hekalu, alikuwa na maelfu ya tani za dhahabu na fedha. Kulikuwa na shaba na chuma nyingi sana hivi kwamba hazingeweza kupimwa. (1 Mambo ya Nyakati 22:14-16) Kwa msaada wa Yehova na utegemezo wa Waisraeli wote, mradi huo ulikamilika katika muda wa miaka saba na nusu.—1 Wafalme 6:1, 37, 38.

“Nyumba ya Mungu wa Kweli”

Maskani na pia hekalu liliitwa “nyumba ya Mungu wa kweli.” (Waamuzi 18:31; 2 Mambo ya Nyakati 24:7) Yehova hahitaji kamwe nyumba ya kuishi. (Isaya 66:1) Aliagiza majengo hayo yajengwe ili kuwafaidi wanadamu. Kwa kweli, wakati wa kuzindua hekalu, Sulemani aliuliza hivi: “Je, kweli Mungu atakaa duniani? Tazama! Mbingu, ndiyo, mbingu za mbingu, haziwezi kukutosha; jinsi gani basi, nyumba hii ambayo nimeijenga!”—1 Wafalme 8:27.

Yehova alisema hivi kupitia nabii wake Isaya: “Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa ajili ya vikundi vyote vya watu.” (Isaya 56:7) Dhabihu na sala zilizotolewa hekaluni, na vilevile sherehe zilizofanywa huko, ziliwawezesha watu wanaomwogopa Mungu, yaani, Wayahudi na wasio Wayahudi, wamkaribie Mungu wa kweli. Walipata kuwa marafiki wa Yehova na kulindwa naye kwa sababu ya kuabudu katika nyumba yake. Sala ambayo Sulemani alitoa wakati wa kuweka wakfu hekalu inakazia ukweli huo. Unaweza kusoma maneno yake yenye kugusa moyo aliyomwambia Mungu kwenye 1 Wafalme 8:22-53 na 2 Mambo ya Nyakati 6:12-42.

Nyumba hiyo ya zamani ya Mungu wa kweli ilitoweka zamani za kale, lakini Neno la Mungu lilionyesha kwamba kuna wakati ambapo watu kutoka mataifa yote wangekusanywa ili kumwabudu Yehova katika hekalu kubwa zaidi la kiroho. (Isaya 2:2) Dhabihu kamilifu ya Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, iliyowakilishwa na dhabihu za wanyama zilizotolewa hekaluni, ingekuwa njia ya kumkaribia Yehova. (Yohana 14:6; Waebrania 7:27; 9:12) Leo, Mashahidi wa Yehova wanamwabudu Mungu kupitia njia hiyo bora zaidi, nao wanawasaidia wengine wengi wafanye vivyo hivyo.

Miradi ya Ujenzi Leo

Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wanamtumikia Mungu wa kweli. Wanafanyiza “taifa lenye nguvu,” linalozidi kupanuka. (Isaya 60:22) Mashahidi wa Yehova hukutana hasa katika Majumba ya Ufalme. * Kuna maelfu ya majengo hayo ambayo yanatumiwa, na bado maelfu zaidi yanahitajiwa.

Mashahidi wa Yehova ‘hujitoa kwa hiari’ kujenga Majumba ya Ufalme yanayohitajiwa. (Zaburi 110:3) Hata hivyo, mara nyingi Mashahidi wa maeneo fulani hawana ustadi unaohitajiwa wa kujenga, na maeneo mengine ambako kuna ongezeko kubwa ni yenye umaskini sana. Katika mwaka wa 1999, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilianzisha mpango wa kujenga Majumba ya Ufalme ili kusaidia maeneo hayo yenye matatizo. Kupitia mpango huo, Mashahidi walio na ustadi wa kujenga wamesafiri kwenda kwenye maeneo ya mbali ili kuwazoeza ndugu na dada zao kujenga Majumba ya Ufalme. Kisha, wafanyakazi hao waliozoezwa wameendelea na kazi ya ujenzi katika maeneo yao. Jitihada hizo za pekee zimekuwa na matokeo gani?

Kufikia Februari (Mwezi wa Pili) 2006, Mashahidi wa Yehova katika nchi maskini wameona Majumba ya Ufalme mapya zaidi ya 13,000 yakijengwa. Soma baadhi ya maneno ya wale wanaotumia Majumba mapya ya Ufalme.

“Hudhurio la wastani la kutaniko lilikuwa 160. Baada ya Jumba jipya la Ufalme kujengwa, mkutano wa kwanza ulikuwa na hudhurio la watu 200. Sasa, miezi sita baadaye, kuna hudhurio la watu 230. Ni wazi kwamba Yehova amebariki ujenzi wa majengo hayo ya kawaida yanayofaa.”—Mwangalizi wa mzunguko nchini Ekuado.

“Kwa miaka mingi watu wametuuliza, ‘Ni wakati gani mtakapokuwa na Jumba la Ufalme kama yale tunayoona katika vichapo vyenu?’ Hatimaye, Yehova ametuwezesha kuwa na mahali pazuri pa ibada. Zamani tulifanyia mikutano katika duka la ndugu fulani, na kwa wastani hudhurio lilikuwa watu 30. Watu 110 walihudhuria mkutano wa kwanza katika Jumba jipya la Ufalme.”—Kutaniko fulani nchini Uganda.

“Dada wawili ambao ni mapainia wa kawaida wanasema kwamba wanafurahia zaidi kuhubiri katika eneo baada ya Jumba la Ufalme kujengwa. Watu wako tayari zaidi kusikiliza katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba na pia katika mahubiri yasiyo rasmi. Sasa dada hao wanaongoza mafunzo 17 ya Biblia, na wengi wa wanafunzi hao wa Biblia wanahudhuria mikutano.”—Ofisi ya tawi ya Visiwa vya Solomon.

“Kasisi mmoja anayeishi karibu na Jumba jipya la Ufalme anasema kwamba Jumba hilo linafanya eneo hilo lote liheshimiwe, nao wakaaji wanajivunia jumba hilo. Watu wengi wanaopita mahali hapo huzungumza kuhusu uzuri wa jumba hilo. Hilo huwapa ndugu nafasi nzuri ya kuhubiri. Watu wengi zaidi wanataka kujua kuhusu undugu wetu wa ulimwenguni pote. Wengi ambao waliacha kuhudhuria mikutano miaka mingi iliyopita wamechochewa kuanza tena kuhudhuria mikutano kwa ukawaida.”—Ofisi ya tawi ya Myanmar.

“Dada mmoja alimwomba mwanamume mwenye kupendezwa atembelee mahali pa ujenzi katika eneo lao. Baadaye, mwanamume huyo alisema hivi: ‘Nilifikiri kwamba wafanyakazi hawangeniruhusu niingie. Nilishangaa kwamba Mashahidi hao walinisalimu kwa fadhili. Wanaume na wanawake walikuwa wakifanya kazi kwa bidii na hawakupoteza wakati. Kulikuwa na upatano na furaha.’ Mwanamume huyo alikubali funzo la Biblia naye akaanza kuhudhuria mikutano. Baadaye, alisema hivi: ‘Maoni yangu yamebadilika. Nimempata Mungu nami sitamwacha.’”—Ofisi ya tawi ya Kolombia.

Utegemezo Wetu ni Muhimu

Kujenga Majumba ya Ufalme ni sehemu muhimu ya utumishi wetu mtakatifu. Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanastahili kupongezwa sana kwa sababu wametegemeza kazi hiyo kifedha na kwa njia nyinginezo. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba utumishi wetu mtakatifu unahusisha mambo mengine muhimu. Mara kwa mara, Wakristo hukumbwa na misiba ya kiasili nao huhitaji msaada wetu. Uchapishaji wa vichapo vya Biblia ni muhimu sana katika kuendeleza utumishi mtakatifu. Wengi wetu tumeona jinsi gazeti au kitabu kinachotegemea Biblia kilivyo na nguvu ya kumchochea mtu mwenye mwelekeo unaofaa anayekipokea. Isitoshe, ni muhimu sana kuwategemeza wamishonari na wengine walio katika utumishi wa pekee wa wakati wote. Wakristo hao wenye kujidhabihu husaidia sana kupanua kazi ya kuhubiri katika siku hizi za mwisho.

Wale waliotoa michango kwa ajili ya ujenzi wa hekalu walishangilia sana. (1 Mambo ya Nyakati 29:9) Vivyo hivyo leo, kutegemeza ibada ya kweli kwa michango yetu hutuletea furaha. (Matendo 20:35) Tunapata furaha hiyo tunapotumbukiza michango yetu katika sanduku la michango ya Hazina ya Majumba ya Ufalme na tunapotoa michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, na hivyo kutegemeza miradi mingine inayohusiana na kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Leo, kwa njia ya ajabu, Mashahidi wa Yehova wana umoja katika ibada ya kweli. Acheni sote tujawe na furaha inayotokana na kutegemeza ibada hiyo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Kuhusu mwanzo wa jina “Jumba la Ufalme,” ona kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 319, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa way 20]

JINSI AMBAVYO WENGINE HUTOA MICHANGO

MICHANGO KWA AJILI YA KAZI YA ULIMWENGUNI POTE

Wengi hutenga kiasi fulani cha pesa ambacho wao hutia katika masanduku ya michango yaliyoandikwa, “Michango kwa Ajili ya Kazi ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.”

Kila mwezi, makutaniko hutuma pesa hizo kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova inayohudumia nchi yao. Pia, michango ya hiari ya pesa inaweza kutumwa moja kwa moja kwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, c/o Office of the Secretary and Treasurer, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201-2483, au kwenye ofisi ya tawi inayohudumia nchi yenu. Hundi za benki zinapaswa kuonyesha kwamba zitalipwa kwa shirika la “Watch Tower.” Vito au vitu vingine vyenye thamani vinaweza kuchangwa pia. Barua fupi inayoonyesha kwamba vitu hivyo ni zawadi inayotolewa bila masharti inapaswa kuambatanishwa na michango hiyo.

MPANGO WA MICHANGO YENYE MASHARTI

Pesa zinaweza kuwekwa amana kwa Watch Tower ili zitumiwe kwa kazi ya ulimwenguni pote. Hata hivyo, zinaweza kurudishwa iwapo zitaitishwa. Kwa habari zaidi, tafadhali wasiliana na Ofisi ya Katibu na Mweka-Hazina ukitumia anwani iliyoonyeshwa juu.

UTOAJI ULIOPANGWA

Mbali na zawadi za kifedha zinazotolewa bila masharti, kuna njia nyinginezo za kutoa kwa ajili ya kazi ya Ufalme ulimwenguni pote. Zinatia ndani:

Bima: Watch Tower Society linaweza kuandikishwa kuwa shirika ambalo litafaidika kutokana na bima ya maisha, malipo ya kustaafu, au ya uzeeni.

Akiba za Benki: Akaunti za benki, hati za amana, au akiba za pesa za kustaafu za mtu mmoja-mmoja zinaweza kuwekwa amana, au kulipwa wakati wa kifo, kwa Watch Tower, kulingana na matakwa ya benki za kwenu.

Hisa na Dhamana: Hisa na dhamana zinaweza kuchangwa kwa Watch Tower zikiwa zawadi isiyo na masharti.

Ardhi na Nyumba: Ardhi au nyumba zinazoweza kuuzwa zinaweza kutolewa zikiwa zawadi isiyo na masharti au iliyo na masharti, yaani, mtoaji anaweza kuendelea kuishi humo hadi kifo chake. Wasiliana na ofisi ya tawi katika nchi yenu kabla ya kutoa ardhi au nyumba kama mchango.

Malipo-Mwaka: Huo ni mpango wa kutoa pesa, hisa na amana, ziwe mali za Watch Tower. Yule anayetoa mchango huo, au mtu fulani aliyechaguliwa na mtoaji, hupata kiasi fulani cha pesa kila mwaka maishani mwake. Mtoaji hupunguziwa kodi ya serikali mwaka ule ambao mpango huo unaanzishwa.

Wasia na Amana: Watch Tower linaweza kuachiwa urithi wa mali au pesa kwa njia ya wasia halali, au linaweza kuandikishwa kuwa shirika ambalo litafaidika katika mkataba wa amana. Kuwa na amana inayofaidi shirika la kidini kunaweza kupunguza kwa kiasi fulani kiwango cha kodi.

Kama vile usemi “utoaji uliopangwa” unavyodokeza, ili mtu atoe michango ya aina hii anapaswa kufanya mipango hususa. Broshua yenye kichwa Charitable Planning to Benefit Kingdom Service Worldwide imetayarishwa katika Kiingereza na Kihispania ili kuwasaidia watu wanaotamani kuendeleza kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kwa njia ya utoaji uliopangwa. Broshua hiyo ilichapishwa ili kuonyesha njia mbalimbali za kutoa zawadi sasa au kupitia wasia mtu anapokufa. Baada ya kusoma broshua hiyo na kushauriana na washauri wao wa mambo ya sheria au kodi, wengi wameweza kuunga mkono kazi ya kidini na ya kutoa misaada ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, na kupunguziwa kodi wanapofanya hivyo. Unaweza kuomba broshua hiyo moja kwa moja kutoka kwenye Charitable Planning Office.

Ukitaka habari zaidi, unaweza kuwasiliana na Charitable Planning Office, ama kwa kuandika ama kwa kupiga simu, kwenye anwani iliyoonyeshwa chini, au unaweza kuwasiliana na ofisi ya tawi inayohudumia nchi yenu.

Mashahidi wa Yehova

P.O. Box 47788

GPO Nairobi 00100

Kenya

Simu: (020) 3873211

[Picha katika ukurasa wa 18]

Jitihada zetu za pamoja zinatuwezesha kujenga Majumba ya Ufalme maridadi ulimwenguni pote

[Picha katika ukurasa wa 18]

Jumba jipya la Ufalme nchini Ghana