Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mhubiri

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mhubiri

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Mhubiri

“MWANADAMU, aliyezaliwa na mwanamke, ana maisha mafupi na yenye kujaa msukosuko,” akasema mzee wa ukoo Ayubu. (Ayubu 14:1) Ni muhimu sana kutoharibu maisha yetu mafupi tukifuatilia mambo na miradi isiyo na maana! Tunapaswa kutumia wakati wetu, nguvu, na mali zetu kufuatilia mambo gani? Ni mambo gani tunayopaswa kuepuka? Maneno yenye hekima yaliyoandikwa katika kitabu cha Biblia cha Mhubiri yanatoa mwongozo mzuri kuhusu jambo hilo. Ujumbe wa maneno hayo ‘unaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo’ na kutusaidia kuwa na maisha yenye kusudi.—Waebrania 4:12.

Kitabu cha Mhubiri ambacho kiliandikwa na mtu aliyejulikana sana kwa sababu ya hekima yake, yaani, Mfalme Sulemani wa Israeli la kale, kina mashauri kuhusu mambo muhimu na yasiyo muhimu maishani. Kwa kuwa Sulemani anazungumzia baadhi ya miradi yake ya ujenzi, inaonekana aliandika kitabu cha Mhubiri baada ya kukamilisha miradi hiyo ya ujenzi na kabla ya kuacha ibada ya kweli. (Nehemia 13:26) Hivyo, yaelekea kitabu hicho kiliandikwa kabla ya mwaka wa 1000 K.W.K., kuelekea mwisho wa utawala wa miaka 40 wa Sulemani.

NI JAMBO GANI AMBALO SI UBATILI?

(Mhubiri 1:1–6:12)

“Kila kitu ni ubatili!” asema mkutanishaji, naye anauliza hivi: “Mwanadamu anapata faida gani katika kazi yake yote iliyo ngumu anayoifanya kwa bidii chini ya jua?” (Mhubiri 1:2, 3) Maneno “ubatili” na “chini ya jua” yanarudiwa-rudiwa katika kitabu cha Mhubiri. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “ubatili” kihalisi linamaanisha “pumzi” au “mvuke,” nalo linamaanisha kitu kisicho muhimu, kisichodumu, au chenye thamani ndogo. Maneno “chini ya jua” yanamaanisha, “katika dunia hii” au “katika ulimwengu huu.” Hivyo, kila kitu, yaani, jitihada zote za wanadamu ambao wanapuuza mapenzi ya Mungu ni ubatili.

“Linda miguu yako wakati wowote unapoenda kwenye nyumba ya Mungu wa kweli,” asema Sulemani, “na usogee karibu usikie.” (Mhubiri 5:1) Kushiriki katika ibada ya kweli ya Yehova Mungu si ubatili. Kwa kweli, kutilia maanani uhusiano wetu pamoja naye ndilo jambo muhimu ili kuwa na maisha yenye kusudi.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:4-10—Ni mambo gani ‘yanayochosha’ kuhusiana na mizunguko ya asili? Mkutanishaji anataja mambo matatu tu ya msingi ambayo yanaendeleza uhai duniani, yaani, jua, upepo, na mzunguko wa maji. Kwa kweli, mizunguko ya asili ni mingi nayo haieleweki kwa urahisi. Mtu anaweza kutumia maisha yake yote akiichunguza na bado asiweze kuielewa kabisa. Hilo linaweza kuwa jambo lenye ‘kuchosha’ kwelikweli. Inavunja moyo pia, kulinganisha maisha yetu mafupi na mizunguko hiyo inayoendelea daima. Hata jitihada za kuvumbua vitu vipya zinachosha, kwa sababu vitu hivyo vipya vinategemea tu kanuni ambazo Mungu wa kweli tayari ameweka na tayari amezitumia katika uumbaji.

2:1, 2—Kwa nini kicheko “ni wazimu”? Huenda kicheko kikatusaidia kusahau matatizo yetu kwa muda, na shangwe inaweza kutufanya tusiyaone matatizo yetu kuwa mazito. Hata hivyo, kicheko hakituondolei matatizo. Hivyo, kutafuta furaha kwa kucheka kunasemekana kuwa “ni wazimu.”

3:11—Ni nini ambacho Mungu amefanya kuwa “chenye kupendeza kwa wakati wake”? Baadhi ya vitu ambavyo Yehova Mungu amefanya kuwa ‘vyenye kupendeza,’ au vyenye kufaa na vizuri kwa wakati wake ni kuumbwa kwa Adamu na Hawa, agano la upinde wa mvua, agano pamoja na Abrahamu, agano pamoja na Daudi, kuja kwa Masihi, na kutawazwa kwa Yesu Kristo kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Lakini, kuna kitu kingine ambacho Yehova atakifanya kuwa “chenye kupendeza” hivi karibuni. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba ulimwengu mpya wenye uadilifu utakuwa halisi kwa wakati unaofaa.—2 Petro 3:13.

3:15b—‘Mungu wa kweli anatafutaje kile kinachofuatiliwa’? Huenda “kile kinachofuatiliwa” kikamaanisha yale ambayo Mungu anakusudia kufanya. Ingawa mambo yanayojirudia-rudia kwa ukawaida kama vile kuzaliwa, kufa, vita na amani, huenda yakamfanya mwanadamu kujihisi hoi na kufikiri kwamba historia hujirudia-rudia, Mungu wa kweli anaweza kutafuta na kutimiza yote ambayo Anataka. (Mhubiri 3:1-10, 15a) “Kile kinachofuatiliwa” kinaweza pia kumaanisha waadilifu, ambao mara nyingi hufuatiliwa na waovu. Katika kisa hiki, Yehova huendelea kuwatafuta waadilifu ili “aonyeshe nguvu zake” kwa ajili yao.—2 Mambo ya Nyakati 16:9.

5:9—“Faida ya dunia iko kati yao wote” jinsi gani? Wakaaji wote wa dunia, kutia na mfalme, wanategemea “faida ya dunia,” yaani, mazao ya nchi. Ili apate mazao ya shamba lake, mfalme anahitaji watumishi wake wafanye kazi ngumu ya kulima shamba lake.

Mambo Tunayojifunza:

1:15. Ni ubatili kutumia wakati na nguvu zetu kujaribu kukomesha ukandamizaji na ukosefu wa haki ambao tunaona leo. Ufalme wa Mungu tu ndio unaoweza kukomesha uovu.—Danieli 2:44.

2:4-11. Mambo ya kitamaduni, kama vile ujenzi, kutunza mabustani, na muziki, na pia maisha ya starehe, yote hayo ni “kufuatilia upepo” kwa sababu hayafanyi maisha yawe yenye kusudi kikweli wala hayaleti furaha ya kudumu.

2:12-16. Hekima ina faida kuliko upumbavu kwa sababu inaweza kumsaidia mtu kutatua matatizo fulani. Hata hivyo, kuhusu kifo, hekima ya wanadamu haina faida yoyote. Na hata ikiwa huenda mtu alipata umaarufu kwa sababu ya kuwa na hekima hiyo, muda si muda anasahaulika.

2:24; 3:12, 13, 22. Si kosa kufurahia matunda ya kazi yetu ngumu.

2:26. ‘Mtu aliye mwema mbele za Mungu wa kweli,’ ndiye anayepewa hekima ya kimungu, ambayo huleta shangwe. Haiwezekani kamwe kupata hekima hiyo bila kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu.

3:16, 17. Si jambo linalopatana na akili kutarajia haki itekelezwe katika hali zote. Badala ya kuhangaishwa na mambo yanayotukia ulimwenguni leo, tunapaswa kumngojea Yehova anyooshe mambo.

4:4. Kazi ngumu inayofanywa kwa ustadi inaweza kuleta uradhi. Hata hivyo, kazi ngumu inayofanywa ili kujionyesha kuwa bora kuliko wengine huchochea mashindano na inaweza kusababisha hisia mbaya na wivu. Kazi yetu ngumu katika huduma ya Kikristo inapaswa kuchochewa na nia nzuri.

4:7-12. Uhusiano wa kibinadamu ni muhimu zaidi kuliko mali na haupaswi kupuuzwa kwa sababu ya kutafuta mali.

4:13. Cheo na umri havimfanyi mtu aheshimiwe sikuzote. Watu walio na madaraka wanapaswa kutenda kwa hekima.

4:15, 16. Huenda mwanzoni “mtoto wa pili,” anayechukua mahali pa mfalme, akaungwa mkono na ‘watu wote ambao aliwatangulia,’ lakini “baadaye hawatamshangilia.” Kwa kweli, umashuhuri haudumu.

5:2. Sala zetu zinapaswa kufikiriwa kwa uzito na kutolewa kwa heshima, wala hazipaswi kuwa na maneno mengi.

5:3-7. Kuhangaikia sana mambo ya kimwili kunaweza kumfanya mtu aote ndoto za mchana kuhusu tamaa za kibinafsi. Kunaweza pia kumfanya mtu akose utulivu usiku, na hivyo kumzuia asipate usingizi mtamu. Wingi wa maneno unaweza kumfanya mtu aonekane kuwa mpumbavu na kunaweza kumfanya aweke nadhiri haraka mbele za Mungu. ‘Kumwogopa Mungu wa kweli’ hutuzuia tusifanye mambo hayo.

6:1-9. Mambo kama vile utajiri, utukufu, maisha marefu, na hata familia kubwa yana faida gani ikiwa hali hazituruhusu kuyafurahia? “Ni afadhali kuona kwa macho,” au kukabili hali halisi za maisha kuliko “kutembea huku na huku kwa nafsi,” yaani, kujitahidi kutosheleza tamaa ambazo haziwezi kutoshelezwa. Basi, njia bora ya maisha ni kuridhika na “chakula na kitu cha kujifunika” huku tukifurahia mambo mazuri maishani na kudumisha uhusiano mzuri pamoja na Yehova.—1 Timotheo 6:8.

MASHAURI KWA WENYE HEKIMA

(Mhubiri 7:1–12:8)

Tunaweza kulindaje jina au sifa yetu nzuri? Tunapaswa kuwa na maoni gani kuelekea watawala wa kibinadamu na ukosefu wa haki ambao huenda tukauona? Kwa kuwa wafu hawajui jambo lolote, tunapaswa kutumiaje maisha yetu sasa? Vijana wanaweza kutumiaje wakati na nguvu zao kwa hekima? Mashauri mazuri ya mkutanishaji kuhusu mambo hayo na mengineyo, yameandikwa kwa ajili yetu katika sura ya 7 hadi ya 12 ya kitabu cha Mhubiri.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

7:19—Ni katika maana gani hekima ina nguvu zaidi kuliko “watu kumi wenye mamlaka”? Katika Biblia, namba kumi inatumiwa kwa njia ya mfano kuwakilisha ukamili. Sulemani anasema kwamba uwezo wa hekima wa kulinda ni mkubwa kuliko kikosi kamili cha askari wanaolinda jiji.

10:2—Ni nini maana ya maneno moyo wa mtu upo “upande wa mkono wake wa kuume” au “upande wa mkono wake wa kushoto”? Kwa kuwa mara nyingi upande wa mkono wa kuume huonyesha kwamba mtu amependelewa, moyo wa mtu kuwa upande wa mkono wa kuume humaanisha kwamba moyo wake humchochea kufanya mema. Hata hivyo, moyo ukimchochea mtu kutenda mabaya, inasemekana kwamba upo upande wa mkono wake wa kushoto.

10:15—‘Kazi ngumu ya wajinga huwachoshaje’? Mtu akikosa busara, kazi yake ngumu haizai matunda yoyote mazuri. Haimletei uradhi wowote. Jitihada hizo za bure humchosha tu.

11:7, 8—Ni nini maana ya maneno: “Nuru ni tamu pia, na ni vema macho yaone jua”? Nuru na jua huwaletea shangwe walio hai. Hapa Sulemani anasema kwamba ni vizuri kuwa hai na kwamba tunapaswa ‘kushangilia’ kabla siku za giza, au siku za uzee, hazijatupokonya nguvu zetu.

11:10—Kwa nini “ujana na upeo wa maisha” ni ubatili? Mambo hayo yasipotumiwa vizuri, yanakuwa ubatili kwa sababu, siku za nguvu za ujana hutoweka haraka kama mvuke.

Mambo Tunayojifunza:

7:6. Kicheko kwa wakati usiofaa kinaudhi na ni bure kama sauti ya miiba inayoteketea chini ya chungu. Tunapaswa kuepuka kicheko hicho.

7:21, 22. Hatupaswi kuhangaikia sana yale ambayo wengine wanasema.

8:2, 3; 10:4. Tunapochambuliwa au kurekebishwa na msimamizi au mkubwa wa kazi, ni jambo la hekima tubaki tukiwa watulivu. Ni afadhali kufanya hivyo kuliko ‘kufanya haraka kuondoka mbele yake,’ yaani, kujiuzulu haraka.

8:8; 9:5-10, 12. Tunaweza kufa ghafula kama vile samaki anavyonaswa katika wavu au ndege wanavyonaswa katika mtego. Isitoshe, hakuna mtu anayeweza kuzuia nguvu za uhai zisitoke mtu anapokufa, wala hakuna anayeweza kuachiliwa katika vita ambavyo kifo hupiga dhidi ya wanadamu. Kwa hivyo, hatupaswi kupoteza wakati. Yehova anataka tuthamini uhai na kuufurahia kwa njia inayofaa. Ili kufanya hivyo, tunapaswa kutanguliza utumishi wa Yehova maishani mwetu.

8:16, 17. Mwisho wa kila jambo ambalo Mungu amefanya na ambalo ameruhusu litukie miongoni mwa wanadamu hauwezi kueleweka, hata ikiwa tutakosa usingizi ili kujaribu kuuelewa. Kuhangaika kuhusu maovu yote ambayo yametendwa kutatuondolea tu shangwe yetu maishani.

9:16-18. Hekima inapaswa kuonwa kuwa kitu chenye thamani hata ikiwa watu wengi hawaithamini. Maneno yanayosemwa kwa utulivu na mtu mwenye hekima ni bora kuliko kelele za mjinga.

10:1. Tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu usemi na matendo yetu. Tendo moja tu lisilo la busara kama vile kufoka kwa hasira, kutumia kileo vibaya, au tendo linalohusisha mwenendo usio safi kingono, linatosha kuharibu sifa nzuri ya mtu anayeheshimika.

10:5-11. Mtu asiye na uwezo aliye katika cheo cha juu hapaswi kuonewa wivu. Kutofanya vizuri hata kazi iliyo ndogo kunaweza kuwa na matokeo mabaya. Badala yake, kusitawisha uwezo wa “kutumia hekima kwa mafanikio” huleta faida. Ni muhimu kama nini kuwa stadi katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi!

11:1, 2Tunapaswa kuzoea kuonyesha ukarimu kwa moyo wote. Mtu mkarimu huonyeshwa ukarimu.—Luka 6:38.

11:3-6. Mambo yasiyotarajiwa maishani hayapaswi kutufanya tuwe wenye kusitasita.

11:9; 12:1-7. Vijana watatozwa hesabu na Yehova. Kwa hiyo, wanapaswa kutumia wakati na nguvu zao katika utumishi wa Mungu kabla uzee haujawapokonya nguvu zao.

“MANENO YA WENYE HEKIMA” ILI KUTUONGOZA

(Mhubiri 12:9-14)

Tunapaswa kuyaonaje “maneno yenye kupendeza” ambayo mkutanishaji alijitahidi kutafuta na kuandika? Tofauti na “vitabu vingi” vyenye hekima ya kibinadamu, “maneno ya wenye hekima ni kama michokoo ya kuongoza ng’ombe, na kama tu misumari iliyopigiliwa ndani, ndivyo walivyo wale wanaoshughulika mno kukusanya maneno; wametolewa kutoka kwa mchungaji mmoja.” (Mhubiri 12:10-12) Maneno ya hekima yanayotoka kwa “mchungaji mmoja,” Yehova, yanaimarisha maisha yetu.

Bila shaka, kutumia mashauri yenye hekima yaliyo katika kitabu cha Mhubiri kutatusaidia kuwa na maisha yenye kusudi na furaha. Isitoshe, tunahakikishiwa hivi: “Mambo yatawaendea vyema wale wanaomwogopa Mungu wa kweli.” Hivyo basi, acheni tuazimie kwa uthabiti ‘kumwogopa Mungu wa kweli na kushika amri zake.’—Mhubiri 8:12; 12:13.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mojawapo ya kazi nzuri zaidi za mikono ya Mungu itakuwa halisi kwa wakati wake

[Picha katika ukurasa wa 16]

Zawadi za Mungu zinatia ndani, chakula, kinywaji, na kuona mema kwa sababu ya kazi yetu yote iliyo ngumu