Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mashauri Yenye Kutegemeka Kuhusu Kulea Watoto

Mashauri Yenye Kutegemeka Kuhusu Kulea Watoto

Mashauri Yenye Kutegemeka Kuhusu Kulea Watoto

“NILIKUWA na umri wa miaka 19, nilikuwa nikiishi mbali na watu wetu wa ukoo, na sikuwa tayari kabisa,” anasema Ruth kuhusu mimba yake ya kwanza. Akiwa bila ndugu wala dada, Ruth hakuwa amefikiria sana kuhusu kuwa mzazi. Angepata wapi mashauri yenye kutegemeka?

Kwa upande mwingine, Jan, ambaye ni baba mwenye watoto watatu wakubwa, anakumbuka hivi: “Mwanzoni, nilikuwa na uhakika sana. Lakini, punde si punde, nilitambua kwamba sikuwa na ujuzi.” Iwe mwanzoni wazazi wanahisi kwamba hawako tayari kulea watoto au baadaye wanakuwa na shaka kuhusu njia yao ya kuwalea watoto, wanaweza kupata wapi msaada wa kulea watoto wao?

Leo, wazazi wengi hutafuta mashauri kwenye Intaneti. Hata hivyo, huenda ukajiuliza, mashauri hayo yanategemeka kadiri gani? Kuna sababu nzuri ya kuwa mwangalifu sana. Je, kweli unajua ni nani wanaoandaa mashauri hayo kwenye Intaneti? Wamefaulu kadiri gani kuwalea watoto wao wenyewe? Bila shaka, unahitaji kuwa mwangalifu inapohusu mambo ya familia yako. Nyakati nyingine, kama makala iliyotangulia ilivyoonyesha, hata mashauri ya wataalamu huvunja moyo. Basi unaweza kumwendea nani?

Yehova Mungu, Mwanzilishi wa familia, ndiye Chanzo kikuu cha mashauri kuhusu kulea watoto. (Waefeso 3:15) Yeye tu ndiye mtalaamu wa kweli. Katika Neno lake Biblia, anaandaa maagizo yenye kutegemeka ambayo kwa kweli yana matokeo mazuri. (Zaburi 32:8; Isaya 48:17, 18) Hata hivyo, ni juu yetu kuyafuata.

Wazazi fulani waliombwa watoe maoni yao kuhusu mambo ambayo walijifunza walipokuwa wakiwalea watoto wao ili wawe watu wazima wenye usawaziko na wanaomwogopa Mungu. Walisema kuwa walifanikiwa hasa kwa sababu walifuata kanuni za Biblia. Walitambua kwamba mashauri ya Biblia ni yenye kutegemeka leo kama yalivyokuwa Biblia ilipoandikwa.

Tumia Wakati Pamoja na Watoto Wako

Catherine, ambaye ni mama ya watoto wawili, alipoulizwa ni shauri gani lililomsaidia zaidi, mara moja alitaja andiko la Kumbukumbu la Torati 6:7. Mstari huo unasema hivi: “Nawe uyakazie [kanuni za Biblia] kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.” Catherine alitambua kwamba ili afuate shauri hilo, alipaswa kutumia wakati pamoja na watoto wake.

Huenda ukafikiri kwamba ‘ni rahisi kusema hivyo kuliko kutenda.’ Kwa kuwa katika familia nyingi wazazi wote wanahitaji kufanya kazi ili kuandaa riziki, wazazi walio na shughuli nyingi wanawezaje kutumia wakati zaidi pamoja na watoto wao? Torlief, ambaye ana mwana aliye na familia yake sasa, anasema kwamba jambo muhimu ni kufuata shauri lililo katika Kumbukumbu la Torati. Nenda na watoto wako popote uendapo, na nafasi za kuzungumza nao zitajitokeza. Torlief anasema hivi: “Mimi na mwana wangu tulifanya kazi za nyumbani pamoja. Tulisafiri pamoja kama familia. Nasi tulikula chakula pamoja.” Kwa sababu hiyo, anasema, “sikuzote mwana wetu alihisi kwamba anaweza kujieleza kwa uhuru.”

Hata hivyo, namna gani mawasiliano yakivunjika na iwe vigumu kuzungumza? Nyakati nyingine inakuwa hivyo watoto wanapokuwa wakubwa. Bado kutumia wakati pamoja nao kunaweza kusaidia. Ken, mume wa Catherine anakumbuka kuwa binti yao alipokuwa tineja alilalamika kwamba hakuwa akimsikiliza. Matineja wengi hulalamika hivyo. Ken angefanya nini? Anakumbuka: “Niliamua kutumia wakati zaidi pamoja naye, tukizungumzia maoni yake, hisia zake, na mambo yaliyomsumbua. Hilo lilisaidia sana.” (Methali 20:5) Hata hivyo, Ken anaamini kwamba alifaulu kwa sababu familia yao ilizoea kuwasiliana. Anasema hivi: “Sikuzote mimi na binti yangu tulikuwa na uhusiano mzuri. Hivyo, alihisi anaweza kuzungumza nami kwa uhuru.”

Kwa kushangaza, uchunguzi fulani uliofanywa hivi karibuni ulionyesha kuwa vijana wako tayari zaidi kuliko wazazi wao kulalamika kwamba wazazi na watoto hawatumii wakati wa kutosha pamoja. Mbona basi usifuate shauri la Biblia? Tumia wakati mwingi iwezekanavyo pamoja na watoto wako, unapopumzika na unapofanya kazi, unapokuwa nyumbani na safarini, unapoamka na kabla hujalala. Ikiwezekana, nenda nao popote uendapo. Kama Kumbukumbu la Torati 6:7 linavyoonyesha, ni lazima utumie wakati pamoja na watoto wako.

Wafundishe Kanuni Zinazofaa

Mario ambaye ni baba ya watoto wawili, anapendekeza hivi pia: “Wapende sana watoto, na uwasomee vitabu.” Hata hivyo, hilo halimaanishi tu kuchochea uwezo wa watoto wa kufikiri. Unahitaji kuwafundisha jinsi ya kutofautisha mema na mabaya. Mario anaongezea: “Jifunze nao Biblia.”

Ili wafaulu, Biblia inawahimiza hivi wazazi: “Msiwachukize watoto wenu ila waleeni katika nidhamu na mafundisho ya Kikristo.” (Waefeso 6:4, Biblia Habari Njema) Watoto katika familia nyingi leo hawafundishwi maadili. Watu fulani wanaamini kwamba watoto watakapokuwa watu wazima wataweza kujiamulia wenyewe kanuni ambazo watafuata. Je, unahisi jambo hilo linapatana na akili? Kama vile miili ya watoto inavyohitaji chakula kinachofaa ili iwe na nguvu na afya, ndivyo akili na mioyo yao inavyohitaji maagizo. Usipowafunza watoto wako kanuni za maadili nyumbani, inaelekea watafuata maoni ya wanafunzi wenzao, walimu, au vyombo vya habari.

Biblia inaweza kuwasaidia wazazi kuwafundisha watoto jinsi ya kutofautisha mema na mabaya. (2 Timotheo 3:16, 17) Jeff, mzee Mkristo mwenye uzoefu ambaye amelea watoto wawili, anapendekeza kutumia Biblia kuwafundisha watoto kanuni zinazofaa. Anasema hivi: “Kuitumia Biblia huwasaidia watoto kutambua maoni ya Muumba kuhusu jambo fulani, wala si maoni ya Mama na Baba tu. Tuligundua uwezo wa pekee wa Biblia wa kuchochea akili na moyo. Ili kurekebisha mwenendo au fikira zisizofaa, tulitumia wakati kutafuta andiko linalofaa. Kisha, faraghani, tulimwomba mtoto asome andiko hilo. Mara nyingi mtoto alianza kulia machozi. Tulistaajabu! Biblia ilikuwa na uvutano mkubwa kuliko kitu chochote ambacho tungesema au kufanya.”

Andiko la Waebrania 4:12 linaeleza hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu . . . nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” Kwa hiyo, ujumbe wa Biblia si maoni tu ya watu au mambo ambayo yaliwapata wale waliotumiwa na Mungu kuandika Biblia. Badala yake, ujumbe huo ni maoni ya Mungu kuhusu maadili. Hivyo, ujumbe wa Biblia ni tofauti kabisa na mashauri mengine yote. Ukitumia Biblia kuwafundisha watoto wako, unawasaidia kuona mambo kama Mungu anavyoyaona. Mazoezi unayowapa yanakuwa na uzito zaidi, na una nafasi nzuri zaidi ya kugusa moyo wa mtoto wako.

Catherine, ambaye alitajwa mwanzoni anakubaliana na jambo hilo. Anasema hivi: “Kadiri hali ilivyozidi kuwa ngumu, ndivyo tulivyotafuta zaidi mwongozo katika Neno la Mungu, nasi tulifanikiwa!” Je, unaweza kuitumia zaidi Biblia kuwafundisha watoto wako kutofautisha mema na mabaya?

Uwe Mwenye Usawaziko

Mtume Paulo anataja kanuni nyingine muhimu ambayo inasaidia katika kulea mtoto. Aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Bila shaka, hilo linatia ndani kuwaacha watoto wetu waone usawaziko wetu. Pia kumbuka, usawaziko huonyesha kwamba mtu ana “hekima inayotoka juu.”—Yakobo 3:17.

Hata hivyo, usawaziko unahusikaje katika kuwalea watoto wetu? Ingawa tunawapa msaada wowote wanaohitaji, hatuwaongozi katika kila jambo wanalofanya. Kwa mfano, Mario, aliyetajwa mapema, ni Shahidi wa Yehova, naye anakumbuka hivi: “Sikuzote tuliwawekea watoto wetu miradi ya kiroho, kama vile ubatizo na utumishi wa wakati wote. Lakini tuliwaambia waziwazi kwamba walipaswa kufanya uamuzi wao wenyewe kwa wakati unaofaa.” Ikawaje? Sasa watoto wao wawili ni wahubiri wa Injili wa wakati wote.

Katika andiko la Wakolosai 3:21 Biblia inawaonya hivi akina baba: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.” Catherine anathamini sana andiko hilo. Mzazi anapokosa subira, ni rahisi kukasirika au kudai mengi. Lakini, Catherine anasema, “usimtarajie mtoto wako afanye mambo kama yale unayoweza kufanya.” Catherine pia ni Shahidi wa Yehova, naye anaongeza hivi: “Fanya kumtumikia Yehova kuwe jambo la kufurahisha.”

Jeff, aliyetajwa mapema, anatoa pendekezo hili zuri: “Watoto wetu walipoendelea kukua, rafiki mmoja mzuri alituambia aligundua kwamba mara nyingi hakuwaruhusu watoto wake wafanye walichotaka. Hilo liliwafanya waudhike na kuhisi wamekandamizwa. Ili kuepuka hilo, alipendekeza tutafute mambo tunayoweza kuwaruhusu wafanye.

Jeff anasema hivi: “Hilo lilikuwa shauri zuri. Tuliwatafutia watoto wetu nafasi ya kufanya mambo pamoja na wengine chini ya mwongozo wetu. Hivyo, tuliwauliza: ‘Je, mlijua kwamba fulani na fulani wanafanya hili au lile? Mbona msijiunge nao?’ Au watoto walipotuomba ruhusa ya kwenda mahali fulani, tulijilazimisha kwenda nao hata tulipokuwa tumechoka. Tulifanya hivyo ili tusiwanyime ruhusa.” Hiyo ndiyo maana ya kuwa mwenye usawaziko, yaani, kutopendelea, kuwa mwenye ufikirio, na kukubali maoni ya wengine bila kuvunja kanuni za Biblia.

Faidika na Mashauri Yenye Kutegemeka

Leo, wazazi wengi kati ya hao wana wajukuu. Wanafurahia kuona kanuni hizohizo za Biblia zikiwasaidia watoto wao kufaulu wakiwa wazazi. Je, wewe unaweza kufaidika kutokana na mashauri ya Biblia?

Ruth, aliyetajwa mwanzoni, alipokuwa mzazi, nyakati nyingine yeye na mume wake walihisi hawana mwongozo wowote. Lakini walikuwa nao. Walikuwa na mashauri bora ya Neno la Mungu, Biblia. Mashahidi wa Yehova wamechapisha vichapo vingi vizuri sana vya kujifunzia Biblia ambavyo vinaweza kuwasaidia wazazi. Vinatia ndani kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, na Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi. Torlief, mume wa Ruth anasema hivi: “Leo wazazi wanaweza kupata kwa urahisi mashauri mengi sana yanayotegemea Biblia. Wakiyatumia vizuri, yanaweza kuwasaidia kumfundisha mtoto mambo mbalimbali maishani kadiri anavyokua.”

[Picha katika ukurasa wa 5]

Maoni ya WATAALAMU . . . Maoni ya BIBLIA

Kuhusu Kuonyesha Upendo:

Katika kitabu kimoja (The Psychological Care of Infant and Child cha mwaka wa 1928), Dakt. John Broadus Watson aliwahimiza hivi wazazi: “Usiwakumbatie wala kuwabusu kamwe” watoto wako. “Usiwapakate kamwe.” Hata hivyo, hivi karibuni, Dakt. Vera Lane na Dakt. Dorothy Molyneaux, walisema hivi katika gazeti moja (Our Children la Machi 1999): “Utafiti unaonyesha kwamba watoto wadogo ambao hawaguswi wala kuonyeshwa upendo mara nyingi hawasitawi.”

Kinyume na hilo, andiko la Isaya 66:12 linasema kwamba Mungu aliwaonyesha watu wake upendo kama mzazi mwenye upendo. Vivyo hivyo, wanafunzi wa Yesu walipojaribu kuwazuia watu wasimletee watoto wachanga, yeye aliwakosoa kwa kusema hivi: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia.” Kisha, “akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki.”—Marko 10:14, 16.

Kuhusu Kuwafundisha Kanuni Zinazofaa:

Katika makala fulani ya mwaka wa 1969 iliyochapishwa katika gazeti moja (New York Times Magazine), Dakt. Bruno Bettelheim alikazia kwamba mtoto “ana haki ya kuwa na maoni yake binafsi, bila kushawishiwa na [maoni] ambayo anasisitiziwa na [wazazi wake], lakini anapaswa tu kufuata mambo anayojionea maishani.” Hata hivyo, miaka 30 hivi baadaye, Dakt. Robert Coles, mtungaji wa kitabu kimoja (The Moral Intelligence of Children cha mwaka wa 1997) alikiri hivi: “Watoto wanahitaji sana kuwa na kusudi na kupewa mwongozo maishani, yaani, kupewa kanuni za maadili” zinazokubaliwa na wazazi wao na watu wengine wazima.

Andiko la Methali 22:6 linawahimiza wazazi hivi: “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.” Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “mlee” linamaanisha pia “anzisha” na hapa linadokeza wazo la kuanza kumfundisha mtoto mchanga mafundisho ya kwanza. Hivyo, wazazi wanatiwa moyo waanze kuwafundisha watoto wao maadili yanayofaa tangu wakiwa wachanga. (2 Timotheo 3:14, 15) Yaelekea hawatasahau mambo waliyojifunza walipokuwa wachanga.

Kuhusu Nidhamu:

Dakt. James Dobson aliandika hivi katika kitabu kimoja (The Strong-Willed Child cha mwaka wa 1978): “Adhabu inayotolewa na mzazi mwenye upendo ni njia ya kufundisha ambayo inazuia tabia zenye madhara zisisitawi.” Kwa upande mwingine, katika makala inayotegemea toleo la saba la kitabu kimoja maarufu (Baby and Child Care cha 1998), Dakt. Benjamin Spock alisema hivi: “Kuwachapa watoto viboko huwafundisha kwamba mtu mwenye umri mkubwa na mwenye nguvu zaidi ana uwezo wa kufanya atakavyo iwe amekosea au hajakosea.”

Kuhusu nidhamu, Biblia inasema hivi: “Fimbo na karipio ndivyo hutia hekima.” (Methali 29:15) Hata hivyo, si watoto wote wanaohitaji kuadhibiwa kwa kutumia kiboko. Andiko la Methali 17:10 linatuambia: “Kemeo huingia ndani zaidi katika mtu mwenye uelewaji kuliko kumpiga mjinga mara mia moja.”

[Picha]

Tumia Biblia kugusa moyo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wazazi wenye hekima hupanga tafrija kwa ajili ya watoto wao