Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Alithawabisha Sana Tamaa Yangu ya Kuwa Mmishonari

Yehova Alithawabisha Sana Tamaa Yangu ya Kuwa Mmishonari

Simulizi la Maisha

Yehova Alithawabisha Sana Tamaa Yangu ya Kuwa Mmishonari

LIMESIMULIWA NA SHEILA WINFIELD DA CONCEIÇÃO

Mmishonari mmoja kutoka Afrika alituambia wakati mmoja kwamba katika mgawo wake kila mtu humkaribisha na kusikiliza kwa makini habari njema ya Ufalme wa Mungu. ‘Ningependa sana kuhubiri katika eneo kama hilo!’ niliwaza. Wakati huo, nilikuwa na umri wa miaka 13, na mazungumzo hayo yalinifanya nitamani kuwa mmishonari.

HATA hivyo, familia yetu ilianza kujifunza kumhusu Yehova mapema sana. Asubuhi moja mnamo mwaka wa 1939, vijana wawili waliovalia vizuri sana walipiga hodi nyumbani kwetu katika mji wa Hemel Hempstead, nje ya jiji la London, Uingereza. Walikuwa Mashahidi wa Yehova. Nilizaliwa mwaka uliotangulia, kwa hivyo sikumbuki ziara hiyo. Ili kuwazuia wasiingie, Mama aliwaambia kwamba huenda Baba akapendezwa lakini atarudi nyumbani baada ya saa tatu usiku. Mama alishangaa sana waliporudi usiku huohuo! Baada ya kujua msimamo wao kuhusu masuala ya kisiasa na ya kitaifa, baba yangu, Henry Winfield, aliwakaribisha na kukubali funzo la Biblia. Alifanya maendeleo haraka naye akabatizwa. Miaka kadhaa baadaye, mama yangu, Kathleen, alianza kujifunza pia. Alibatizwa mwaka wa 1946.

Mnamo mwaka wa 1948, nilianza kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Niliona kwamba nilihitaji saa ya mkononi ili niweze kutoa ripoti sahihi ya muda ninaotumia katika mahubiri. Kila Jumamosi (Siku ya Posho), sisi watoto tungepewa sarafu moja ya senti sita ikiwa tungejiendesha vizuri. Niliweka akiba senti zangu sita kwa karibu miaka miwili ili ninunue saa yenye bei ya chini zaidi wakati huo. Hata hivyo, Ray, ndugu yangu mdogo, sikuzote alimwomba Baba sarafu mbili za senti tatu, wala si sarafu moja ya senti sita. Siku moja alisisitiza sana apewe sarafu mbili mpaka akamkasirisha Baba. Ray alianza kulia na kusema kwamba alihitaji sarafu mbili za senti tatu kwa sababu ya siri fulani kati yake na Yehova. Mwishowe, Ray alieleza hivi: “Sarafu moja ya senti tatu nitaiweka katika sanduku la michango, na sarafu nyingine ya senti tatu ni yangu.” Mama alilia kwa furaha, mara moja Baba akatafuta sarafu mbili, nami nikajifunza umuhimu wa kutegemeza kazi ya Ufalme kifedha.

Karibu wakati huo, Baba alifanya mipango ili kuhamia mahali penye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Katika mwaka wa 1949, aliuza shamba lake na uwanja wake wa kuchimba mchanga na changarawe, naye akaanza upainia, akiwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Nilibatizwa Septemba 24, 1950 (24/9/1950), ili kuonyesha kwamba nilikuwa nimejiweka wakfu kwa Yehova. Tangu hapo na kuendelea, wakati wa likizo ya shule, nilifanya upainia wa likizo (ambao sasa ni upainia msaidizi), na kutumia saa 100 kwa mwezi katika huduma. Lakini huo ulikuwa mwanzo tu. Punde si punde, tamaa kubwa ya kufanya mengi zaidi katika kuendeleza ibada safi ilisitawi moyoni mwangu.

Tamaa Yangu ya Kuwa Mmishonari

Mwaka wa 1951, Baba alipewa mgawo wa kwenda Bideford, Devon Kaskazini. Baada tu ya kufika, yule mmishonari aliyetumika Afrika alitembelea kutaniko letu, kama ilivyotajwa mwanzoni. Baada ya hapo, tamaa yangu ya kuwa mmishonari iliongoza maamuzi yangu yote. Shuleni walimu walijua mradi wangu nao walijitahidi wawezavyo kunivunja moyo, wakitumaini kwamba ningefuatilia kazi ya kimwili. Hata hivyo, siku yangu ya mwisho shuleni, nilipoenda kwenye chumba cha walimu ili kuwashukuru na kuwaaga, mmoja wao alisema hivi: “Pongezi! Wewe ndiye mwanafunzi pekee ambaye anajua kwa kweli kile anachotaka maishani. Tunatumaini kwamba utafikia mradi wako.”

Bila kukawia, nilipata kazi ya muda, na Desemba 1, 1955 (1/12/1955), nikawa painia wa kawaida. Baadaye, Mama na ndugu zangu wakawa mapainia pia. Kwa hivyo, kwa miaka kadhaa, familia yetu yote ilikuwa katika utumishi wa wakati wote.

Naenda Ireland

Mwaka mmoja baadaye, niliombwa nikatumikie huko Ireland. Hilo lilinisaidia kupiga hatua ya kufikia mradi wangu wa kuwa mmishonari. Mnamo Februari (Mwezi wa Pili) 1957, mimi pamoja na mapainia wengine wawili vijana, June Napier na Beryl Barker, tulifika Cork, kusini mwa Ireland.

Kazi ya kuhubiri huko Ireland ilikuwa ngumu. Kulikuwa na upinzani mkali kutoka kwa Kanisa Katoliki. Tulijifunza kutafuta njia ya kuondoka kwenye jengo au mtaa, iwapo tungehitaji kukimbia. Tulikuwa tukificha baiskeli zetu mbali kidogo, lakini mara nyingi mtu fulani angezipata na kukatakata magurudumu yake au kuondoa hewa kwenye magurudumu hayo.

Siku moja, mimi na Beryl tulipokuwa tukitembelea mtaa fulani mkubwa, kikundi cha watoto kilianza kututukana na kuturushia mawe. Kwa hiyo, tuliingia katika duka moja ambamo maziwa yaliuzwa. Duka hilo lilipakana na nyumba ya mtu fulani. Umati ulianza kukusanyika nje. Kwa kuwa Beryl alipenda maziwa, alikunywa glasi mbili au tatu polepole sana, akitumaini kwamba umati huo ungetawanyika. Lakini haukutawanyika. Kisha, kasisi mmoja kijana akaingia dukani. Alidhani sisi ni watalii, kwa hiyo akajitolea kututembeza. Hata hivyo, kwanza alituingiza katika chumba kingine nyumbani humo, na tukiwa tumeketi kimya, akafanya desturi za mwisho za dini kwa ajili ya mzee fulani aliyekaribia kufa. Kisha, tukaondoka na kasisi huyo. Umati huo ulitawanyika ulipotuona tukiongea na kasisi huyo.

Naenda Gileadi

Mnamo mwaka wa 1958, Kusanyiko la Kimataifa la Mapenzi ya Kimungu lingefanyika huko New York. Baba angeenda huko, nami pia nilitaka kwenda lakini sikuwa na pesa. Kisha nyanya yangu akafa ghafula naye akaniachia pauni 100 (Dola 280 za Marekani). Nauli ya kwenda na kurudi ilikuwa pauni 96. Kwa hiyo, mara moja nikakata tikiti ya ndege.

Muda mfupi baadaye, mwakilishi wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Uingereza alitutembelea naye akawaalika mapainia wote wa pekee ambao wangesafiri kwenda kwenye kusanyiko wajaze fomu ya ombi la mazoezi ya umishonari katika Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Sikuamini masikio yangu! Alimpa kila mmoja fomu isipokuwa mimi tu. Nilikuwa na umri mdogo sana. Mimi pia niliomba nipewe fomu na kueleza kwamba nilikuwa tayari nimeondoka nchi yangu na kwenda katika mgawo wa umishonari. Alipoona azimio langu akanipa fomu. Nilisali sana ili ombi langu likubaliwe! Jibu lilikuja haraka nami nikaalikwa kuhudhuria Shule ya Gileadi.

Nilifurahi sana kuwa katika darasa la 33 la Gileadi pamoja na mapainia wengine 81 kutoka katika nchi 14. Miezi mitano ya shule hiyo ilipita haraka. Ilipokaribia mwisho, Ndugu Nathan H. Knorr alitutolea hotuba yenye kuchochea kwa muda wa saa nne. Aliwatia moyo wote ambao wangeweza kubaki waseja wafanye hivyo. (1 Wakorintho 7:37, 38) Lakini kwetu sisi ambao tulitamani kufunga ndoa wakati fulani, alipendekeza kwamba tuorodheshe sifa tunazotaka mwenzi mzuri wa ndoa awe nazo. Kisha, mtu fulani akipendezwa nasi, tungeweza kumchunguza kupatana na matakwa hayo.

Orodha yangu ya matakwa ya yule angekuwa mume wangu ilitia ndani mambo yafuatayo: Angepaswa kuwa mmishonari kama mimi na ampende Yehova, ajue kweli za Biblia zaidi yangu, awe tayari kutokuwa na watoto kabla ya Har-magedoni ili kuendelea na utumishi wa wakati wote, aongee Kiingereza kwa ufasaha, na awe na umri mkubwa kuliko wangu. Orodha hiyo ilinisaidia sana, nikiwa na umri wa miaka 20 na tayari kupokea mgawo katika nchi ya mbali.

Naenda Brazili

Jumapili (Siku ya Yenga), Agosti 2, 1959 (2/8/1959), tulihitimu na kupewa migawo yetu. Mimi pamoja na Vehanouch Yazedjian, Sarah Greco, Ray na Inger Hatfield, Sonia Springate, na Doreen Hines, tulitumwa Brazili. Tulisisimuka sana. Niliwazia Brazili ni nchi yenye misitu, nyoka, miti ya mpira, na Wenyeji wa Asili wa Amerika. Hata hivyo, nilipofika nilishangaa sana! Badala ya msitu wa mvua wa Amazoni, nilikuta Rio de Janeiro, jiji la kisasa lenye jua ambalo wakati huo lilikuwa jiji kuu la nchi hiyo.

Tatizo la kwanza tulilokabili ni kujifunza Kireno. Mwezi wa kwanza, tulijifunza kwa saa 11 kila siku. Baada ya kuhubiri katika jiji la Rio na kuishi kwa muda kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, nilitumwa kwenye makao ya wamishonari huko Piracicaba, katika Jimbo la São Paulo, na baadaye nikatumwa kwenye makao ya wamishonari huko Porto Alegre, katika Jimbo la Rio Grande do Sul.

Kisha, mwanzoni mwa mwaka wa 1963, niliombwa kutumikia katika Idara ya Tafsiri kwenye ofisi ya tawi. Floriano Ignez da Conceição, ambaye alitufunza Kireno tulipofika, ndiye aliyekuwa msimamizi wa idara hiyo. Alijifunza kweli mwaka wa 1944, nchi ya Brazili ilipokuwa na Mashahidi karibu 300, naye alihudhuria darasa la 22 la Shule ya Gileadi. Siku moja, miezi kadhaa baadaye, Ndugu Conceição aliniomba nibaki baada ya kengele ya chakula cha mchana ili azungumze nami. Kwanza, nilikuwa na wasiwasi. Je, nilikuwa nimefanya kosa fulani? Baada ya kengele kulia, nilimuuliza alichotaka kuniambia. Akanijibu hivi: “Ningependa kukuoa.” Nilipigwa na bumbuazi. Nilimwomba anipe wakati wa kufikiria jambo hilo nami nikaenda haraka kula chakula cha mchana.

Floriano hakuwa ndugu wa kwanza kupendezwa nami. Lakini kufikia wakati huo hakuna yeyote aliyekuwa ametimiza matakwa yangu ya mwenzi wa ndoa anayefaa. Ninaamini kwamba orodha yangu ilinisaidia kutofanya uamuzi mbaya. Mara hii mambo yalikuwa tofauti. Floriano alitimiza matakwa yangu yote! Kwa hiyo, tukafunga ndoa Mei 15, 1965 (15/5/1965).

Kukabili Tatizo la Ugonjwa

Mimi na Floriano tumefurahia maisha ya ndoa licha ya kwamba tumekabili matatizo. Mojawapo ya matatizo hayo ni afya ya Floriano ambayo ilizorota muda mfupi kabla ya arusi yetu. Miaka iliyotangulia, pafu lake la kushoto liliharibika na hilo likamfanya ateseke sana. Kwa hiyo, tuliacha utumishi wa Betheli na tukapewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee katika jiji la Teresópolis katika eneo lenye milima la Jimbo la Rio de Janeiro. Tulitumaini kwamba hali ya hewa ya huko ingemsaidia kupona.

Zaidi ya hayo, mnamo Desemba (Mwezi wa 12) 1965, nilipokea habari kwamba mama yangu alikuwa mgonjwa sana kwa sababu ya kansa. Kwa kawaida, tuliandikiana barua lakini sikuwa nimemwona kwa miaka saba. Kwa hiyo, alitulipia nauli ya kwenda Uingereza ili kumwona. Mama alifanyiwa upasuaji, lakini madaktari hawakufaulu kuondoa kansa hiyo. Ingawa alikuwa mgonjwa sana na hangetoka kitandani, alidumisha tamaa yake ya kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Alikuwa na mashini ya kupiga chapa katika chumba chake cha kulala. Alisema mambo aliyotaka yaandikwe kwa kutumia mashini hiyo. Alikuwa pia akiwahubiria kwa ufupi watu waliomtembelea. Alikufa Novemba 27, 1966 (27/11/1966). Mwezi huohuo aliripoti saa kumi katika utumishi wa shambani! Baba aliendelea kuwa mwaminifu katika utumishi wa upainia hadi kifo chake mwaka wa 1979.

Baada ya kifo cha Mama, mimi na Floriano tulirudi Brazili ambako tunaendelea kutumika katika Jimbo la Rio de Janeiro. Kwanza, tulipewa mgawo kuzungukia makutaniko ya jiji kuu, lakini shangwe hiyo ilikuwa ya muda mfupi kwa kuwa Floriano alikuwa tena mgonjwa sana. Kwa hiyo, tukarudi Teresópolis kuwa mapainia wa pekee.

Mwaka wa 1974, baada ya matibabu yenye maumivu, madaktari waliondoa pafu la kushoto la Floriano. Wakati huo, hangeweza kutumika akiwa mwangalizi-msimamizi au painia wa pekee, lakini aliongoza mafunzo ya Biblia wageni walipomtembelea hospitalini. Mmoja aliyejifunza naye katika Kiingereza ni Bob, mzee Mmarekani aliyestaafu. Bob alikubali kweli na baadaye akabatizwa. Hatua kwa hatua Floriano alipata nafuu na tangu hapo amekuwa painia wa kawaida.

Yehova Amebariki Huduma Yangu

Kwa miaka mingi, nimeendelea kutumika nikiwa painia wa pekee, na Yehova amebariki huduma yangu. Huko Teresópolis, nilikuwa na pendeleo la pekee la kuwasaidia watu zaidi ya 60 kuweka maisha yao wakfu kwa Yehova. Mmoja wao ni mwanamke anayeitwa Jupira, ambaye nilimfunza pia kusoma. Baadaye, nilijifunza na watoto wake wanane ambao walikuwa watu wazima. Leo, Jupira na washiriki zaidi ya 20 wa familia yake na watu wake wa ukoo wanamtumikia Yehova kwa bidii. Mmoja ni mzee wa kutaniko, watatu ni watumishi wa huduma, na wawili ni mapainia.

Nimejifunza kudumisha mtazamo mzuri kuhusu uwezekano wa watu kujifunza kweli. Pindi moja, nilikuwa nikijifunza Biblia na mwanamke kijana anayeitwa Alzemira wakati mume wake Antônio, alipotisha kwamba angewaachilia mbwa wake wawili wakubwa wanishambulie endapo singeondoka nyumbani mwake mara moja. Tangu hapo nilikutana na Alzemira pindi kwa pindi tu. Baada ya miaka saba kupita, Antônio aliniruhusu nijifunze tena na Alzemira. Hata hivyo, Antônio alinikataza nisimwambie chochote kuhusu Biblia. Lakini, siku moja yenye mvua nilimwomba Antônio ahudhurie funzo. Ndipo nilipogundua kwamba hakujua kusoma wala kuandika. Tangu wakati huo na kuendelea, Floriano na wengine walijifunza na Antônio nao wakamfundisha kusoma. Leo, Alzemira na Antônio wamebatizwa. Antônio ni msaada mkubwa kutanikoni, naye huandamana na vijana wengi katika huduma.

Hayo ni machache tu kati ya mambo mengi tuliyojionea katika muda wa zaidi ya miaka 20 ambayo tumetumika Teresópolis. Mwanzoni mwa mwaka wa 1988, tulipokea mgawo mpya kwenda jiji la Niterói, ambako tulitumika kwa miaka mitano iliyofuata kabla ya kuhamia Santo Aleixo. Kisha, tulihamishwa hadi Kutaniko la Japuíba katikati ya Jimbo la Rio. Tukiwa huko tulikuwa na pendeleo la kuanzisha Kutaniko la Ribeira.

Maisha Rahisi Lakini Yenye Kuthawabisha

Kwa miaka mingi, mimi na Floriano tumekuwa na pendeleo la kuwasaidia watu zaidi ya 300 kuweka maisha yao wakfu kwa Yehova. Hivi sasa, baadhi yao wanatumika kwenye ofisi ya tawi, na wengine ni mapainia, wazee, na watumishi wa huduma. Ninamshukuru Mungu kama nini kwamba kupitia roho yake takatifu ametutumia kuwasaidia watu wengi sana!—Marko 10:29, 30.

Ni kweli kwamba Floriano amekuwa akikabiliana na matatizo mazito ya kiafya. Licha ya hali hiyo, amebaki imara, mwenye shangwe, na mwenye kumtumaini Yehova. Mara nyingi yeye husema hivi: “Leo furaha haitegemei kuishi bila matatizo. Inategemea kuwa na msaada wa Yehova ili kukabiliana na matatizo yetu.”—Zaburi 34:19.

Katika mwaka wa 2003, iligunduliwa kwamba nilikuwa na kansa katika jicho langu la kushoto. Nilifanyiwa upasuaji na kuwekwa jicho bandia, ambalo linahitaji kusafishwa mara nyingi kila siku. Licha ya hayo, Yehova amenibariki kwa kunipa nguvu ya kuendelea kumtumikia nikiwa painia wa pekee.

Kuhusu vitu vya kimwili, nimeishi maisha rahisi. Hata hivyo, Yehova amenibariki katika mgawo wangu naye amenifanya tajiri kiroho. Maelezo ya yule dada mmishonari kuhusu kazi ya kuhubiri huko Afrika yanaeleza vizuri mgawo wetu nchini Brazili. Kwa kweli, Yehova amethawabisha sana tamaa yangu ya kuwa mmishonari!

[Picha katika ukurasa wa 9]

Nikiwa na familia yetu, 1953

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kutoa ushahidi huko Ireland, 1957

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nikiwa na wamishonari wengine huko Brazili, 1959. Kutoka kushoto hadi kulia: Mimi, Inger Hatfield, Doreen Hines, na Sonia Springate

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nikiwa na mume wangu