Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitunze Katika Upendo wa Mungu!

Jitunze Katika Upendo wa Mungu!

Jitunze Katika Upendo wa Mungu!

“Wapendwa, . . . jitunzeni katika upendo wa Mungu, . . . kwa kutazamia uzima wa milele.”—YUDA 20, 21.

1, 2. Unawezaje kubaki katika upendo wa Mungu?

YEHOVA anaupenda sana ulimwengu wa wanadamu hivi kwamba alimtoa Mwana wake mzaliwa-pekee ili wale wanaomwamini wawe na uzima wa milele. (Yohana 3:16) Ni jambo kubwa kama nini kuonyeshwa upendo kama huo! Ikiwa wewe ni mtumishi wa Yehova, bila shaka unataka kufurahia upendo huo milele.

2 Mwanafunzi Yuda alifunua jinsi unavyoweza kubaki katika upendo wa Mungu. Aliandika hivi: “Kwa kujijenga wenyewe juu ya imani yenu iliyo takatifu zaidi, na kusali mkiwa na roho takatifu, jitunzeni katika upendo wa Mungu, huku mkiingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa kutazamia uzima wa milele.” (Yuda 20, 21) Kujifunza Neno la Mungu na kuhubiri habari njema hukusaidia kujijenga juu ya ‘imani iliyo takatifu zaidi,’ yaani, mafundisho ya Kikristo. Ili kubaki katika upendo wa Mungu, ni lazima usali ‘ukiwa na roho takatifu,’ au ukiongozwa nayo. Ili upate baraka za uzima wa milele, ni lazima pia uwe na imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo.—1 Yohana 4:10.

3. Kwa nini watu fulani si Mashahidi wa Yehova tena?

3 Watu fulani ambao walikuwa na imani hawajabaki katika upendo wa Mungu. Kwa sababu wameamua kufuata mwenendo wa dhambi, wao si Mashahidi wa Yehova tena. Unaweza kuepukaje hali hiyo? Kutafakari mambo yafuatayo kunaweza kukusaidia kuepuka dhambi na kukuwezesha ujitunze katika upendo wa Mungu.

Onyesha Upendo Wako kwa Mungu

4. Kumtii Mungu ni muhimu kadiri gani?

4 Onyesha upendo wako kwa Mungu kwa kumtii. (Mathayo 22:37) Mtume Yohana aliandika hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Kuzoea kumtii Mungu kunaweza kukuimarisha ushinde vishawishi na kunaweza kukuletea shangwe. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la waovu, . . . bali mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova.”—Zaburi 1:1, 2.

5. Upendo kwa Yehova utakuchochea utendeje?

5 Upendo wako kwa Yehova utakuchochea uepuke kutenda dhambi nzito inayoweza kuleta suto juu ya jina lake. Aguri alisali hivi: “Usinipe umaskini wala utajiri. Acha nile chakula nilichoamriwa, nisije nikashiba nikakukana, nikasema: ‘Yehova ni nani?’ wala nisiwe maskini, nikaiba na kulishambulia jina la Mungu wangu.” (Methali 30:1, 8, 9) Azimia ‘kutolishambulia jina la Mungu’ kwa kumletea suto. Badala yake, sikuzote jitahidi kufanya mambo yaliyo sawa ambayo yanamletea utukufu.—Zaburi 86:12.

6. Matokeo yanaweza kuwa nini tukitenda dhambi kimakusudi?

6 Sali kwa ukawaida kwa Baba yako wa mbinguni mwenye upendo ili akusaidie kushinda vishawishi vya kutenda dhambi. (Mathayo 6:13; Waroma 12:12) Endelea kufuata mashauri ya Mungu ili sala zako zisizuiwe. (1 Petro 3:7) Ukitenda dhambi kimakusudi, matokeo yanaweza kuwa mabaya sana kwa sababu ni kana kwamba Yehova anaweka kizuizi cha wingu kubwa ili sala za wale wanaoasi zisipenye na kumfikia. (Maombolezo 3:42-44) Kwa hiyo, onyesha roho ya unyenyekevu na usali ili usifanye jambo lolote linaloweza kumfanya Mungu asisikilize sala zako.—2 Wakorintho 13:7.

Onyesha Upendo kwa Mwana wa Mungu

7, 8. Kutii shauri la Yesu kunaweza kumsaidiaje mtu akatae mwenendo wa dhambi?

7 Onyesha upendo kwa Yesu Kristo kwa kuzitii amri zake, kwa kuwa kufanya hivyo kutakusaidia ukatae mwenendo wa dhambi. Yesu alisema hivi: “Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu, kama vile mimi nilivyoshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake.” (Yohana 15:10) Kuishi kupatana na maneno ya Yesu kutakusaidiaje ubaki katika upendo wa Mungu?

8 Kutii maneno ya Yesu kunaweza kukusaidia udumishe utimilifu wa maadili. Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilisema hivi: “Usifanye uzinzi.” (Kutoka 20:14) Lakini Yesu alifunua kanuni ambayo ndiyo msingi wa amri hiyo aliposema: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:27, 28) Mtume Petro alisema kwamba watu fulani katika kutaniko la karne ya kwanza walikuwa na “macho yenye kujaa uzinzi” nao ‘walizishawishi nafsi zisizo imara.’ (2 Petro 2:14) Hata hivyo, tofauti na watu wengine, unaweza kuepuka dhambi zinazohusiana na ngono ikiwa utampenda na kumtii Mungu na Kristo na ukiazimia kulinda uhusiano wako pamoja nao.

Iruhusu Roho ya Mungu Ikuongoze

9. Kuhusiana na roho takatifu, ni nini kinachoweza kutukia mtu akizoea kutenda dhambi?

9 Sali ili upate roho takatifu ya Mungu, na uiruhusu ikuongoze. (Luka 11:13; Wagalatia 5:19-25) Ukizoea kutenda dhambi, Mungu anaweza kuondoa roho yake isikuongoze. Baada ya kutenda dhambi na Bath-sheba, Daudi alimsihi Mungu hivi: “Usinitupilie mbali na uso wako; wala usiniondolee roho yako takatifu.” (Zaburi 51:11) Kwa sababu alikuwa mtenda-dhambi asiyetubu, Mfalme Sauli alipoteza roho ya Mungu. Sauli alitenda dhambi kwa kutoa dhabihu ya kuteketezwa na kwa kutoangamiza mbuzi, kondoo, na ng’ombe wote, na pia mfalme wa Amaleki. Baada ya hapo, Yehova aliiondoa roho yake takatifu juu ya Sauli.—1 Samweli 13:1-14; 15:1-35; 16:14-23.

10. Kwa nini tunapaswa kukataa kabisa wazo la kuzoea kutenda dhambi?

10 Kataa kabisa wazo la kuzoea kutenda dhambi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Tukizoea kutenda dhambi kimakusudi baada ya kupokea ujuzi sahihi juu ya kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi.” (Waebrania 10:26-31) Litakuwa jambo lenye msiba kama nini ikiwa utazoea kutenda dhambi kimakusudi!

Onyesha Upendo wa Kweli kwa Wengine

11, 12. Ni katika njia gani upendo na heshima inaweza kumzuia mtu asijihusishe na mwenendo mpotovu kingono?

11 Upendo kwa wanadamu wenzako utakuzuia usijihusishe katika mwenendo mpotovu kingono. (Mathayo 22:39) Upendo huo utakuchochea kuulinda moyo wako ili usikushawishi kuiba upendo wa mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine. Kufanya hivyo kunaweza kuongoza katika dhambi ya uzinzi. (Methali 4:23; Yeremia 4:14; 17:9, 10) Mwige Ayubu aliyekuwa mnyoofu, ambaye hakujiruhusu kumkazia fikira mwanamke mwingine ambaye hakuwa mke wake.—Ayubu 31:1.

12 Kuheshimu utakatifu wa ndoa kunaweza kukusaidia uepuke dhambi nzito. Mungu alikusudia kwamba ndoa na mahusiano ya ngono yenye kuheshimika yatumiwe kupitisha uhai. (Mwanzo 1:26-28) Kumbuka kwamba viungo vya uzazi vimekusudiwa kupitisha uhai, ambao ni mtakatifu. Waasherati na wazinzi hawamtii Mungu, wanafanya tendo la ngono lidharauliwe, hawaheshimu utakatifu wa ndoa, na wanaitendea dhambi miili yao wenyewe. (1 Wakorintho 6:18) Lakini kumpenda Mungu na jirani na pia kumtii Mungu, kutamzuia mtu asijihusishe katika mwenendo unaoweza kumfanya atengwe na ushirika wa kutaniko la Kikristo.

13. Ni kwa njia gani mzinzi “huharibu vitu vyenye thamani”?

13 Tunahitaji kudhibiti mawazo ya dhambi ili tusiwaumize wapendwa wetu. Andiko la Methali 29:3 linasema hivi: “Yeye anayeshirikiana na makahaba huharibu vitu vyenye thamani.” Mzinzi asiyetubu huharibu uhusiano wake pamoja na Mungu na mahusiano ya familia. Mke wake ana msingi wa kumpa talaka. (Mathayo 19:9) Iwe mume au mke ndiye aliyekosea, ndoa inapovunjika mwenzi asiye na hatia, watoto, na wengine huumia sana. Je, hukubali kwamba kujua madhara ya mwenendo mpotovu kiadili kunapaswa kutuchochea tushinde vishawishi vya kujihusisha katika mwenendo huo?

14. Andiko la Methali 6:30-35 linatufunza nini kuhusu kutenda dhambi?

14 Kujua kwamba hatuwezi kulipia uzinzi kwa njia yoyote ile, kunapaswa kumchochea mtu aepuke tendo hilo ambalo kwa kweli ni la ubinafsi. Andiko la Methali 6:30-35 linaonyesha kwamba watu wanaweza kumhurumia mwizi anayeiba kwa sababu ana njaa, lakini wanamdharau mzinzi kwa sababu ana nia mbaya. “Anaiangamiza nafsi yake [au, uhai wake] mwenyewe.” Chini ya Sheria ya Musa, mzinzi aliuawa. (Mambo ya Walawi 20:10) Mtu anayefanya uzinzi anawaumiza wengine ili atosheleze tu tamaa yake, na mzinzi asiyetubu habaki katika upendo wa Mungu, anatengwa na ushirika wa kutaniko safi la Kikristo.

Dumisha Dhamiri Njema

15. Dhamiri iliyotiwa alama “kama kwa chuma cha kutilia alama” ikoje?

15 Ili kubaki katika upendo wa Mungu, hatuwezi kuacha dhamiri zetu zife ganzi kuhusiana na dhambi. Kwa kweli, hatupaswi kuvikubali viwango vya chini vya maadili vya ulimwengu, na tunahitaji kuwa waangalifu katika mambo kama vile kuchagua watu tunaoshirikiana nao, vichapo tunavyosoma, na burudani. Paulo alionya hivi: “Katika vipindi vya nyakati za mwisho wengine wataanguka kutoka kwenye imani, wakisikiliza maneno yaliyoongozwa kwa roho yenye kupotosha na mafundisho ya roho waovu, kwa unafiki wa watu wanaosema uwongo, waliotiwa alama katika dhamiri zao kama kwa chuma cha kutilia alama.” (1 Timotheo 4:1, 2) Dhamiri iliyotiwa alama “kama kwa chuma cha kutilia alama” ni kama ngozi ngumu yenye makovu iliyokufa ganzi. Dhamiri kama hiyo haiwezi tena kutuonya tuwaepuke waasi-imani na hali zinazoweza kutufanya tuiache imani.

16. Kwa nini ni muhimu sana kuwa na dhamiri njema?

16 Wokovu wetu unategemea kuwa na dhamiri njema. (1 Petro 3:21) Kupitia imani katika damu iliyomwagwa ya Yesu, dhamiri zetu zimesafishwa kutoka katika matendo yaliyokufa, “ili tutoe utumishi mtakatifu kwa Mungu aliye hai.” (Waebrania 9:13, 14) Tukitenda dhambi kimakusudi, dhamiri zetu zitachafuka na hatutakuwa tena watu safi ambao wanastahili kumtumikia Mungu. (Tito 1:15) Lakini Yehova anaweza kutusaidia kuwa na dhamiri njema.

Njia Nyingine za Kuepuka Mwenendo Mbaya

17. ‘Kumfuata Yehova kikamili’ kuna faida gani?

17 ‘Mfuate Yehova kikamili’ kama alivyofanya Kalebu wa Israeli la kale. (Kumbukumbu la Torati 1:34-36) Fanya yale ambayo Mungu anataka ufanye, na usijaribu kamwe kula kwenye “meza ya roho waovu.” (1 Wakorintho 10:21) Kataa uasi-imani. Kwa shukrani, kula chakula cha kiroho kinachopatikana tu kwenye meza ya Yehova. Ukifanya hivyo, hutapotoshwa na walimu wa uwongo au majeshi ya roho waovu. (Waefeso 6:12; Yuda 3, 4) Kazia fikira mambo ya kiroho, kama vile kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano, na huduma ya shambani. Bila shaka, utapata furaha ukimfuata Yehova kikamili na kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.—1 Wakorintho 15:58.

18. Kumwogopa Yehova kutaongozaje mwenendo wako?

18 Azimia ‘kumtolea Mungu utumishi mtakatifu kwa woga wa kimungu na heshima.’ (Waebrania 12:28) Kumwogopa Yehova kutakuchochea ukatae njia yoyote iliyopotoka. Kutakusaidia ujiendeshe kupatana na shauri hili ambalo Petro aliwatolea watiwa-mafuta wenzake: “Ikiwa mnamwitia Baba ambaye huhukumu bila ubaguzi kulingana na matendo ya kila mmoja, jiendesheni kwa kuogopa katika wakati wa kukaa kwenu ugenini.”—1 Petro 1:17.

19. Kwa nini sikuzote unapaswa kutumia yale unayojifunza katika Neno la Mungu?

19 Sikuzote tumia yale unayojifunza katika Neno la Mungu. Hilo litakusaidia kuepuka dhambi nzito kwa sababu utakuwa mmoja wa “wale ambao kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Badala ya kuongea na kujiendesha bila kujali, uwe mwangalifu ili utembee kama mtu mwenye hekima ‘ukijinunulia wakati unaofaa’ katika siku hizi zenye uovu. ‘Endelea kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova,’ na uendelee kuyafanya.—Waefeso 5:15-17; 2 Petro 3:17.

20. Kwa nini tunapaswa kuepuka kutamani?

20 Epuka kabisa tamaa, yaani, kutamani kwa pupa vitu vya wengine. Moja ya zile Amri Kumi inasema hivi: “Usiitamani nyumba ya mwenzako. Usimtamani mke wa mwenzako, wala mtumwa wake wala kijakazi wake wala ng’ombe-dume wake wala punda wake wala chochote cha mwenzako.” (Kutoka 20:17) Sheria hiyo ililinda nyumba ya mtu, mke, watumishi, wanyama, na vitu vingine. Jambo la muhimu hata zaidi ni maneno ya Yesu ya kwamba kutamani humtia mtu unajisi.—Marko 7:20-23.

21, 22. Mkristo anaweza kujihadhari jinsi gani ili kuepuka kutenda dhambi?

21 Jihadhari ili tamaa isikuongoze kwenye dhambi. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.” (Yakobo 1:14, 15) Kwa mfano, ikiwa zamani mtu alikuwa na tatizo la kunywa pombe, huenda akaamua kutokuwa na pombe nyumbani mwake. Ili kuepuka kushawishiwa na mtu wa jinsia tofauti, huenda Mkristo akahitaji kubadili mahali pake pa kazi au kutafuta kazi nyingine.—Methali 6:23-28.

22 Usithubutu kamwe kuchukua hatua ya kwanza kuelekea dhambi. Kuwachezea wengine kimapenzi na kufikiria mambo mapotovu kiadili kunaweza kukuongoza kwenye uasherati au uzinzi. Kusema uwongo katika mambo madogo kunaweza kumpa mtu ujasiri wa kusema uwongo wenye kudhuru na kunaweza kuongoza kwenye zoea la dhambi ya kusema uwongo. Kuiba vitu vidogo-vidogo kunaweza kudhoofisha dhamiri ya mtu hivi kwamba aanze kuiba vitu vikubwa. Hata kukubali kidogo mawazo ya waasi-imani kunaweza mwishowe kumfanya mtu awe mwasi-imani.—Methali 11:9; Ufunuo 21:8.

Namna Gani Ikiwa Umetenda Dhambi?

23, 24. Ni faraja gani tunayopata katika 2 Mambo ya Nyakati 6:29, 30 na Methali 28:13?

23 Wanadamu wote si wakamilifu. (Mhubiri 7:20) Lakini ikiwa umetenda dhambi nzito, unaweza kufarijiwa na sala ambayo Mfalme Sulemani alitoa wakati wa kuzinduliwa kwa hekalu la Yehova. Sulemani alisali hivi kwa Mungu: “Sala yoyote, ombi lolote la kutaka kibali ambalo huenda likatolewa na mwanadamu au na watu wako wote Israeli, kwa sababu wanajua kila mmoja wao pigo lake na maumivu yake mwenyewe; wakati anaponyoosha mikono yake kuelekea nyumba hii, basi na usikie ukiwa mbinguni, makao yako, nawe usamehe na kumpa kila mmoja kulingana na njia zake zote, kwa sababu unaujua moyo wake (kwa maana ni wewe peke yako unayejua vema moyo wa wanadamu).”—2 Mambo ya Nyakati 6:29, 30.

24 Naam, Mungu anajua moyo naye husamehe. Andiko la Methali 28:13 linasema hivi: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” Kwa kuungama, kutubu, na kuacha dhambi, mtu anaweza kupata rehema ya Mungu. Hata hivyo, ikiwa umedhoofika kiroho ni nini kingine unachoweza kufanya ili ubaki katika upendo wa Mungu?

Ungejibuje?

• Tunaweza kujitunzaje wenyewe katika upendo wa Mungu?

• Upendo kwa Mungu na kwa Kristo unatusaidiaje kukataa mwenendo wa dhambi?

• Kwa nini upendo wa kweli kwa wengine hutuzuia kujihusisha na mwenendo mpotovu kingono?

• Taja njia kadhaa za kuepuka mwenendo mbaya.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Yuda anatuonyesha jinsi tunavyoweza kujitunza wenyewe katika upendo wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ndoa inapovunjika, mwenzi asiye na hatia na watoto wanaweza kuumia sana

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, umeazimia ‘kumfuata Yehova kikamili’ kama Kalebu?

[Picha katika ukurasa wa 25]

Sali kwa ukawaida ili upate msaada wa kushinda vishawishi