Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kubali Sikuzote Nidhamu ya Yehova

Kubali Sikuzote Nidhamu ya Yehova

‘Nidhamu ya Yehova, usiichukie.’—METHALI 3:11.

1. Kwa nini tunapaswa kukubali nidhamu kutoka kwa Mungu?

MFALME SULEMANI wa Israeli la kale anampa kila mmoja wetu sababu nzuri ya kukubali nidhamu kutoka kwa Mungu. Sulemani anasema hivi: “Ewe mwanangu, usikatae nidhamu ya Yehova; wala usichukie karipio lake, kwa sababu yeye ambaye Yehova anampenda, humkaripia, kama vile baba anavyomkaripia mwana anayemfurahia.” (Methali 3:11, 12) Naam, Baba yako wa mbinguni anakutia nidhamu kwa sababu anakupenda.

2. ‘Nidhamu’ inamaanisha nini, na mtu anaweza kutiwaje nidhamu?

2 “Nidhamu” humaanisha kupigwa, kurekebishwa, kuagizwa, na kuelimishwa. Mtume Paulo aliandika hivi: “Hakuna nidhamu inayoonekana kwa sasa kuwa yenye shangwe, bali ni yenye kuhuzunisha; lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo huzaa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Waebrania 12:11) Kukubali na kufuata nidhamu ya Mungu kunaweza kukusaidia kufuata mwenendo wa uadilifu na hivyo kumkaribia zaidi Mungu mtakatifu, Yehova. (Zaburi 99:5) Unaweza kurekebishwa na waamini wenzako, kupitia mambo unayojifunza kwenye mikutano ya Kikristo, funzo lako la Neno la Mungu, na vichapo vya “msimamizi-nyumba mwaminifu.” (Luka 12:42-44) Unapaswa kushukuru kama nini unapojulishwa jambo fulani unalohitaji kurekebisha! Lakini ni nidhamu gani ambayo huenda ikahitajiwa mtu akitenda dhambi nzito?

Kwa Nini Wengine Hutengwa na Ushirika

3. Mtu hutengwa na ushirika iwapo ametenda nini?

3 Watumishi wa Mungu hujifunza Biblia na vichapo vya Kikristo. Viwango vya Yehova huzungumziwa kwenye mikutano na makusanyiko yao. Kwa hivyo, Wakristo wanaweza kuelewa vizuri mambo ambayo Yehova anataka wafanye. Mshiriki wa kutaniko hutengwa na ushirika iwapo tu ametenda dhambi nzito bila kutubu.

4, 5. Tunapewa mfano gani wa Kimaandiko wa mtu aliyetengwa na ushirika, na kwa nini kutaniko lilihimizwa limrudishe mtu huyo?

4 Fikiria mfano mmoja katika Maandiko wa mtu ambaye alitengwa na ushirika. Kutaniko la Korintho liliachilia “uasherati wa namna ambayo hata [haikuwa] kati ya mataifa, kwamba mwanamume fulani [alikuwa na] mke wa baba yake.” Paulo aliwahimiza Wakristo wa Korintho ‘wamkabidhi mtu wa namna hiyo kwa Shetani kwa ajili ya kuangamizwa kwa mwili, ili roho iweze kuokolewa.’ (1 Wakorintho 5:1-5) Mtenda-dhambi huyo alipotengwa na ushirika na hivyo kukabidhiwa kwa Shetani, mtu huyo alirudi katika ulimwengu wa Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Kutengwa kwake na ushirika kuliondoa uvutano mwovu wa kimwili kutanikoni na kudumisha “roho” ya Mungu ili kutaniko liendelee kuonyesha sifa za Mungu.—2 Timotheo 4:22; 1 Wakorintho 5:11-13.

5 Muda si muda, Paulo aliwahimiza Wakristo wa Korintho wamrudishe mkosaji huyo kutanikoni. Kwa nini? Mtume huyo alisema kwamba walipaswa kufanya hivyo ili ‘Shetani asiwashinde akili.’ Yaelekea mtenda-dhambi huyo alikuwa ametubu na kusafisha maisha yake. (2 Wakorintho 2:8-11) Ikiwa Wakorintho wangekataa kumrudisha mtu huyo aliyetubu, Shetani angewashinda akili kwa kuwa wangekuwa wagumu na wasiosamehe kama Ibilisi alivyotaka wawe. Yaelekea sana kwamba baada ya muda mfupi ‘walimsamehe na kumfariji’ mtu huyo aliyetubu.—2 Wakorintho 2:5-7.

6. Kutenga na ushirika hutimiza nini?

6 Kutenga na ushirika hutimiza nini? Kunazuia jina takatifu la Yehova lisiletewe suto na kunalinda sifa nzuri ya watu wake. (1 Petro 1:14-16) Kumwondoa mkosaji asiyetubu kutanikoni hutegemeza viwango vya Mungu na kulinda usafi wa kiroho wa kutaniko. Pia, huenda kukamsaidia mtu huyo asiyetubu atambue uzito wa dhambi yake.

Toba ni Muhimu ili Kurudishwa

7. Daudi alipokosa kuungama dhambi zake matokeo yalikuwa nini?

7 Watu wengi wanaotenda dhambi nzito hutubu kikweli na hivyo hawatengwi na ushirika wa kutaniko. Bila shaka, ni vigumu kwa wengine kuonyesha toba ya kweli. Fikiria Mfalme Daudi wa Israeli, ambaye alitunga Zaburi ya 32. Wimbo huo unaonyesha kwamba kwa muda fulani Daudi hakuungama dhambi zake ambazo yaelekea zilihusiana na Bath-sheba. Kwa sababu hiyo, huzuni kuhusu dhambi zake ilifyonza nguvu zake kama vile joto kavu linavyofyonza umajimaji kutoka katika mti. Daudi aliteseka kimwili na kiakili, lakini ‘alipoungama dhambi zake, Yehova alimsamehe.’ (Zaburi 32:3-5) Kisha, Daudi aliimba hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hamhesabii kosa.” (Zaburi 32:1, 2) Lilikuwa jambo zuri kama nini kuonyeshwa rehema na Mungu!

8, 9. Toba inaonyeshwaje, nayo ni muhimu jinsi gani ili mtu aliyetengwa na ushirika arudishwe?

8 Hivyo, ni wazi kwamba ni lazima mtenda-dhambi atubu ikiwa anataka kuonyeshwa rehema. Hata hivyo, kutubu si kuona aibu wala kuogopa kwamba dhambi ya mtu itajulikana. Kutubu kunamaanisha mtu kubadili akili yake kuhusiana na mwenendo mbaya kwa sababu ya kujutia dhambi yake. Mtu mwenye toba ana “moyo uliovunjika na kupondwa” na anataka “kurekebisha kosa” ikiwezekana.—Zaburi 51:17; 2 Wakorintho 7:11.

9 Kutubu ni jambo muhimu sana ili mtu arudishwe katika kutaniko la Kikristo. Mtu aliyetengwa na ushirika harudishwi tu kutanikoni kwa sababu kipindi fulani cha wakati kimepita. Kabla ya kurudishwa, ni lazima moyo wake ubadilike kabisa. Ni lazima atambue uzito wa dhambi yake na kwamba ameleta suto juu ya Yehova na kutaniko. Ni lazima mtenda-dhambi huyo atubu, asali kwa bidii ili asamehewe, na kupatanisha maisha yake na matakwa ya uadilifu ya Mungu. Anapoomba kurudishwa, anapaswa kuonyesha uthibitisho wa kwamba ametubu naye anafanya “matendo yanayostahili toba.”—Matendo 26:20.

Kwa Nini Tuungame Dhambi?

10, 11. Kwa nini hatupaswi kujaribu kuficha dhambi?

10 Huenda watu fulani waliotenda dhambi wakasema hivi: ‘Nikimwambia mtu yeyote dhambi yangu, huenda nikalazimika kujibu maswali yenye kuaibisha na ninaweza kutengwa na ushirika. Lakini nikinyamaza, ninaweza kuepuka aibu hiyo na hakuna yeyote atakayejua kutanikoni.’ Mtu anayefikiri kwa njia hiyo hupuuza mambo fulani muhimu. Ni mambo gani hayo?

11 Yehova ni “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli, anayehifadhi fadhili zenye upendo kwa ajili ya maelfu, anayesamehe kosa na ubaya na dhambi.” Hata hivyo, yeye huwarekebisha watu wake “kwa kiwango kinachofaa.” (Kutoka 34:6, 7; Yeremia 30:11) Ikiwa ungetenda dhambi nzito na kujaribu kuificha, ungewezaje kupata rehema za Mungu? Yehova anajua dhambi hiyo, naye hapuuzi tu dhambi.—Methali 15:3; Habakuki 1:13.

12, 13. Kujaribu kuficha dhambi kunaweza kuwa na matokeo gani?

12 Ikiwa umetenda dhambi nzito, kuungama kunaweza kukusaidia uwe na dhamiri njema tena. (1 Timotheo 1:18-20) Lakini kukosa kuungama kunaweza kuichafua dhamiri na hivyo kukuongoza kwenye dhambi zaidi. Kumbuka kwamba hukutenda dhambi dhidi ya mwanadamu mwingine au kutaniko tu. Ulitenda dhambi dhidi ya Mungu. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Yehova—kiti chake cha ufalme kiko mbinguni. Macho yake yanaangalia, macho yake yanayong’aa yanawachunguza wana wa binadamu. Yehova humchunguza mwadilifu na pia mwovu.”—Zaburi 11:4, 5.

13 Yehova hatambariki mtu yeyote anayeficha dhambi nzito na kujaribu kukaa ndani ya kutaniko safi la Kikristo. (Yakobo 4:6) Kwa hiyo, ikiwa umetenda dhambi na unataka kufanya yaliyo sawa, usisite kuungama kwa unyoofu. Usipofanya hivyo, utakuwa na dhamiri yenye hatia, hasa unaposikia au kusoma mashauri kuhusu mambo mazito kama hayo. Itakuwaje ikiwa Yehova ataiondoa roho yake juu yako kama alivyoiondoa kutoka kwa Mfalme Sauli? (1 Samweli 16:14) Mungu akiondoa roho yake, unaweza kutenda dhambi nzito hata zaidi.

Watumaini Ndugu Zako Waaminifu

14. Kwa nini mkosaji anapaswa kufuata shauri la Yakobo 5:14, 15?

14 Hivyo basi, mkosaji mwenye kutubu anapaswa kufanya nini? “Na awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, nao wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamponya huyo asiyejisikia vizuri, na Yehova atamwinua.” (Yakobo 5:14, 15) Kuwafikia wazee ni njia moja ya mkosaji ‘kuzaa matunda yanayofaa toba.’ (Mathayo 3:8) Wanaume hao waaminifu na wenye fadhili ‘watasali juu yake na kumpaka mafuta katika jina la Yehova.’ Kama mafuta yanayotuliza, mashauri ya Biblia wanayotoa yatamfariji mtu yeyote anayetubu kikweli.—Yeremia 8:22.

15, 16. Wazee Wakristo huigaje mfano wa Yehova unaotajwa kwenye Ezekieli 34:15, 16?

15 Ni mfano wenye upendo kama nini uliowekwa na Mchungaji wetu, Yehova, alipowaweka huru Wayahudi waliporudi kutoka utekwani Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., na alipowaweka huru Waisraeli wa kiroho kutoka “Babiloni Mkubwa” mwaka wa 1919 W.K.! (Ufunuo 17:3-5; Wagalatia 6:16) Hivyo, alitimiza ahadi yake: “Mimi mwenyewe nitawalisha kondoo zangu, na mimi mwenyewe nitawalaza . . . Aliyepotea nitamtafuta, na aliyefukuzwa nitamrudisha, na aliyevunjika nitamfunga na anayeugua nitamtia nguvu.”—Ezekieli 34:15, 16.

16 Yehova aliwalisha kondoo wake wa mfano, akawalaza kwa usalama, na kuwatafuta waliopotea. Vivyo hivyo, wachungaji Wakristo huhakikisha kwamba kundi la Mungu linalishwa vizuri kiroho na liko salama. Wazee huwatafuta kondoo wanaopotea kutoka kutanikoni. Kama vile tu Mungu ‘alivyomfunga aliyevunjika,’ ndivyo waangalizi ‘wanavyowafunga’ kondoo waliojeruhiwa na maneno ya mtu mwingine au na matendo yao wenyewe. Na kama vile Mungu ‘alivyomtia nguvu yule anayeugua,’ wazee huwasaidia wale ambao wamekuwa wagonjwa kiroho, labda kwa sababu ya kutenda dhambi.

Jinsi Wachungaji Wanavyoandaa Msaada

17. Kwa nini hatupaswi kusita kuwaomba wazee msaada wa kiroho?

17 Wazee hufuata shauri hili kwa furaha: “Endeleeni kuonyesha . . . rehema, mkifanya hivyo kwa kuogopa.” (Yuda 23) Wakristo fulani wametenda dhambi nzito kwa kujihusisha na mwenendo mpotovu kingono. Lakini wakitubu kikweli, wanaweza kutarajia kuonyeshwa rehema na kutendewa kwa upendo na wazee ambao wanataka sana kuwasaidia kiroho. Akijitia ndani, Paulo alisema hivi kuhusu wanaume hao: “Si kwamba sisi ndio mabwana juu ya imani yenu, bali sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu.” (2 Wakorintho 1:24) Kwa hiyo, usisite kamwe kuwaomba msaada wa kiroho.

18. Wazee hushughulikiaje waamini wenzao wanaotenda dhambi?

18 Ikiwa umetenda dhambi nzito, kwa nini unaweza kuwatumaini wazee? Kwa sababu wao hasa ni wachungaji wa kundi la Mungu. (1 Petro 5:1-4) Hakuna mchungaji mwenye upendo anayempiga mwana-kondoo mpole anayelia kwa uchungu kwa sababu amejiumiza. Hivyo, wazee wanaposhughulika na waamini wenzao waliotenda dhambi, hawafikirii adhabu watakayowapa kwa sababu ya makosa yao, lakini wanafikiria dhambi na jinsi watakavyowasaidia kiroho, inapowezekana. (Yakobo 5:13-20) Wazee wanapaswa kuhukumu kwa uadilifu na ‘kulitendea kundi kwa wororo.’ (Matendo 20:29, 30; Isaya 32:1, 2) Kama Wakristo wengine wote, wazee wanapaswa ‘kutenda haki, kupenda fadhili, na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wao.’ (Mika 6:8) Sifa kama hizo ni muhimu wanapofanya maamuzi yanayohusu uhai na utumishi mtakatifu wa “kondoo wa malisho [ya Yehova].”— Zaburi 100:3.

19. Wazee Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani wanapojaribu kumrekebisha mtu fulani?

19 Wachungaji Wakristo huwekwa rasmi na roho takatifu nao hujitahidi kuongozwa nayo. “Mtu akijikwaa katika kosa fulani kabla ya yeye kulijua,” yaani, bila kutarajia, wanaume wenye sifa za kustahili kiroho hujaribu “kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole.” (Wagalatia 6:1; Matendo 20:28) Kwa upole lakini wakishikamana kwa uthabiti na viwango vya Mungu, wazee hujaribu kurekebisha maoni yake, kama vile tu daktari mwenye kujali anavyonyoosha kwa uangalifu mfupa uliovunjika, ili kushughulikia tatizo hilo bila kumletea maumivu yasiyo ya lazima. (Wakolosai 3:12) Kwa kuwa kuonyesha rehema kunategemea sala na Maandiko, uamuzi wa wazee utaonyesha maoni ya Mungu.—Mathayo 18:18.

20. Ni wakati gani huenda ikawa lazima kutaniko litangaziwe kwamba mtu fulani amekaripiwa?

20 Ikiwa dhambi inajulikana sana au itajulikana, itafaa tangazo litolewe kutanikoni ili kulinda sifa ya kutaniko. Pia, tangazo litatolewa ikiwa kutaniko linahitaji kujulishwa. Wakati mtu ambaye amekaripiwa kihukumu anaendelea kupona kiroho, anaweza kulinganishwa na mtu anayeendelea kupona jeraha ambalo linamzuia kwa kipindi fulani asifanye mambo mengi. Kwa muda, inaelekea sana kwamba itafaa mtu aliyetubu asikilize badala ya kutoa maelezo mikutanoni. Wazee wanaweza kupanga mtu fulani ajifunze naye Biblia ili amwimarishe na kumsaidia kuwa na “afya katika imani.” (Tito 2:2) Mambo yote hayo yanafanywa kwa upendo wala si kwa kusudi la kumwadhibu mkosaji.

21. Visa fulani vya ukosaji vinaweza kushughulikiwaje?

21 Wazee wanaweza kuandaa msaada wa kiroho kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, tuseme ndugu ambaye zamani alikuwa na tatizo la kunywa pombe anakunywa kupita kiasi mara moja au mbili akiwa nyumbani peke yake. Au labda mtu ambaye zamani aliacha kuvuta sigara anavuta sigara mara moja au mbili faraghani kwa sababu ya udhaifu. Ingawa amesali na kuamini kwamba Mungu amemsamehe, mtu huyo anapaswa kuomba msaada wa mzee ili asizoee kutenda dhambi hiyo. Mzee mmoja au wawili wanaweza kushughulikia hali hiyo. Hata hivyo, mzee au wazee hao watamjulisha mwangalizi-msimamizi, kwa kuwa huenda mambo mengine yanahusika.

Endelea Kukubali Nidhamu ya Mungu

22, 23. Kwa nini uendelee kukubali nidhamu ya Mungu?

22 Ili apate kibali cha Mungu, kila Mkristo anapaswa kukubali nidhamu ya Yehova. (1 Timotheo 5:20) Hivyo, kubali rekebisho lolote unalopata unapojifunza Maandiko na vichapo vya Kikristo au unaposikia mashauri yakitolewa kwenye mikutano na makusanyiko ya watu wa Yehova. Uwe macho kuhusu kufanya mapenzi ya Yehova. Ndipo nidhamu ya Mungu itakapokusaidia kudumisha ngome yako ya kiroho, yaani, ulinzi ulio kama ukuta wenye nguvu dhidi ya dhambi.

23 Kukubali nidhamu ya Mungu kutakuwezesha ubaki katika upendo wa Mungu. Ni kweli kwamba Wakristo fulani wametengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo, lakini unaweza kuepuka hali hiyo ‘ukilinda moyo wako’ na ‘kutembea kama mtu mwenye hekima.’ (Methali 4:23; Waefeso 5:15) Hata hivyo, ikiwa sasa umetengwa na ushirika, kwa nini usichukue hatua ili urudishwe kutanikoni? Mungu anataka wote ambao walijiweka wakfu kwake wamwabudu kwa uaminifu na kwa “shangwe ya moyo.” (Kumbukumbu la Torati 28:47) Unaweza kufanya hivyo milele ukikubali sikuzote nidhamu ya Yehova.—Zaburi 100:2.