Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoa Ushahidi Kamili kwa ‘Kujipa Moyo’

Kutoa Ushahidi Kamili kwa ‘Kujipa Moyo’

“Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu”

Kutoa Ushahidi Kamili kwa ‘Kujipa Moyo’

UMATI wenye jeuri unataka kumpiga na kumuua mtumishi mtiifu wa Mungu. Kwa wakati unaofaa kabisa, askari wa Roma wanamnyakua mtu huyo kutoka mikononi mwa wale wanaotaka kumshambulia kisha wanamtia kizuizini. Huo ndio mwanzo wa mfululizo wa matukio yanayoendelea kwa miaka mitano hivi. Matukio hayo yanawawezesha maofisa wengi wa Roma wenye vyeo vikubwa kusikia habari kumhusu Yesu Kristo.

Mtu huyo anayeteswa ni mtume Paulo. Karibu mwaka wa 34 W.K., Yesu alifunua kwamba Paulo (Sauli) angetangaza jina Lake mbele za “wafalme.” (Matendo 9:15) Kufikia mwaka wa 56 W.K., Paulo hakuwa amefanya hivyo. Hata hivyo, hali inabadilika mtume huyo anapokaribia mwisho wa safari yake ya tatu ya umishonari.

Anashambuliwa na Umati Lakini Harudi Nyuma

Paulo anaendelea na safari yake ya kwenda Yerusalemu, na “kupitia roho” Wakristo fulani wanamwonya kwamba atateswa vikali katika jiji hilo. Paulo anasema hivi kwa ujasiri: “Niko tayari si kufungwa tu bali pia kufa Yerusalemu kwa ajili ya jina la Bwana Yesu.” (Matendo 21:4-14) Baada tu ya Paulo kufika katika hekalu la Yerusalemu, Wayahudi kutoka Asia ambao wanajua mafanikio aliyopata mtume huyo alipohubiri Asia, wanauchochea umati ili umuue. Askari wa Roma wanakuja haraka kumsaidia. (Matendo 21:27-32) Wanapomwokoa, Paulo anapata nafasi za pekee sana za kutangaza kweli kumhusu Kristo kwa watu wenye jeuri na watu wa vyeo vikubwa.

Kuwahubiria Watu Wasioweza Kupatikana kwa Urahisi

Paulo anakokotwa na kupelekwa mahali salama juu ya ngazi za ngome inayoitwa Mnara wa Antonia. * Akiwa kwenye ngazi hizo, mtume huyo anatoa ushahidi wenye nguvu kwa umati huo wa wafuasi wa dini. (Matendo 21:33–22:21) Lakini mara tu anapotaja utume wake wa kuwahubiria watu wa Mataifa, jeuri inazuka tena. Kiongozi wa jeshi anayeitwa Lisia anaamuru kwamba Paulo ahojiwe kwa kupigwa mijeledi ili ajue ni kwa nini Wayahudi wanamshtaki. Hata hivyo, Paulo anasema kwamba yeye ni raia Mroma, na hilo linazuia asipigwe mijeledi. Siku inayofuata, Lisia anampeleka Paulo mbele ya Sanhedrini ili ajue ni kwa nini Wayahudi wanamshtaki.—Matendo 22:22-30.

Akiwa amesimama mbele ya mahakama hiyo kuu, Paulo ana nafasi nyingine nzuri ya kuwatolea ushahidi Wayahudi wenzake. Mweneza-injili huyo asiye na woga anatangaza imani yake katika ufufuo. (Matendo 23:1-8) Bado Wayahudi wanamchukia sana na wanataka kumuua, hivyo Paulo anapelekwa katika makao ya askari-jeshi. Usiku unaofuata, Paulo anapokea uhakikisho huu wenye kutia moyo kutoka kwa Bwana: “Jipe moyo! Kwa maana kama vile ambavyo umekuwa ukitoa ushahidi kamili katika Yerusalemu juu ya mambo yanayonihusu, vivyo hivyo utatoa ushahidi katika Roma pia.”—Matendo 23:9-11.

Njama ya kumuua Paulo inazuiwa mtume huyo anapopelekwa haraka na kisiri-siri hadi Kaisaria, makao makuu ya jimbo la Yudea katika milki ya Roma. (Matendo 23:12-24) Huko Kaisaria, Paulo anapata nafasi nyingine nzuri, naye anatoa ushahidi mbele za “wafalme.” Hata hivyo, kwanza mtume huyo anamwonyesha Gavana Feliksi kwamba hakuna ushahidi unaounga mkono mashtaka juu yake. Baadaye, Paulo anamhubiria Feliksi na mke wake Drusila kumhusu Yesu, kuhusu kujizuia, uadilifu, na hukumu inayokuja. Lakini Paulo anazuiliwa gerezani kwa miaka miwili, huku Feliksi akitumaini kwamba Paulo atamhonga, bila mafanikio!—Matendo 23:33–24:27.

Festo anapochukua mahali pa Feliksi, Wayahudi wanaanza tena jitihada zao za kufanya Paulo ahukumiwe na kuuawa. Kesi hiyo inasikilizwa tena huko Kaisaria, na ili kuzuia kesi hiyo isipelekwe Yerusalemu, Paulo anasema hivi: “Mimi nimesimama mbele ya kiti cha hukumu cha Kaisari . . . Ninakata rufani kwa Kaisari.” (Matendo 25:1-11, 20, 21) Siku kadhaa baadaye, baada ya mtume huyo kufikisha kesi yake mbele ya Mfalme Herode Agripa wa Pili, mfalme anasema hivi: “Kwa muda mfupi ungenishawishi niwe Mkristo.” (Matendo 26:1-28) Karibu mwaka wa 58 W.K., Paulo anapelekwa Roma. Akiwa mfungwa huko, mtume huyo mwenye ubunifu anaendelea kwa miaka miwili zaidi kutafuta njia za kuhubiri kuhusu Kristo. (Matendo 28:16-31) Inaonekana kwamba mwishowe Paulo alisimama mbele ya Maliki Nero, lakini hakupatikana na hatia, na hatimaye aliendelea na kazi yake ya umishonari akiwa mtu huru. Hakuna maandishi yoyote yanayoonyesha kwamba mtume mwingine yeyote alipata nafasi za kuwahubiria habari njema watu mashuhuri kama hao.

Kama habari hii inavyoonyesha, mtume Paulo aliishi kupatana na kanuni hii muhimu ambayo ilisemwa na Wakristo wenzake mbele ya mahakama ya Kiyahudi: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Alituwekea mfano mzuri kama nini! Licha ya wanadamu kuendelea kujitahidi kumzuia, mtume huyo alitii kabisa amri ya kutoa ushahidi kamili. Kwa sababu ya kumtii Mungu bila kuyumba-yumba, Paulo alitimiza mgawo wake akiwa “chombo kilichochaguliwa” ili kupeleka jina la Yesu “kwa mataifa na vilevile kwa wafalme na wana wa Israeli.”—Matendo 9:15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ona Kalenda ya Mwaka wa 2006 ya Mashahidi wa Yehova, Novemba/Desemba (mwezi wa 11/12).

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

JE, PAULO ALITAKA TU KUJITETEA?

Akizungumzia swali hilo, mtungaji wa vitabu Ben Witherington wa Tatu, anaandika hivi: ‘Kulingana na maoni ya Paulo, jambo muhimu halikuwa kujitetea, lakini lilikuwa kuwatolea wenye mamlaka ushahidi kuhusu injili, kwa Wayahudi na kwa watu wa Mataifa. Kwa kweli, injili ndiyo iliyokuwa ikishtakiwa.’