Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Wimbo wa Sulemani

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Wimbo wa Sulemani

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Wimbo wa Sulemani

“KAMA yungiyungi katikati ya magugu yenye miiba, ndivyo alivyo msichana mwenzi wangu katikati ya mabinti.” “Kama mtofaa katikati ya miti ya msituni, ndivyo alivyo mpenzi wangu katikati ya wana.” “Mwanamke huyu ni nani, anayetazama chini kama mapambazuko, mrembo kama mwezi mpevu, mwenye kutakata kama jua linaloangaza?” (Wimbo wa Sulemani 2:2, 3; 6:10) Jinsi ilivyo bora mistari hiyo ya kitabu cha Biblia cha Wimbo wa Sulemani! Kitabu hicho chote ni shairi lenye maana na uzuri hivi kwamba kinaitwa “wimbo ulio bora.”—Wimbo wa Sulemani 1:1.

Wimbo huo uliotungwa na Mfalme Sulemani wa Israeli la kale yaelekea karibu mwaka wa 1020 K.W.K., mwanzoni mwa utawala wake wa miaka 40, ni simulizi la mapenzi kati ya mvulana na msichana Mshulami wa mashambani. Shairi hilo pia linawataja mama na ndugu za msichana huyo, “binti za Yerusalemu [wanawake wa makao ya mfalme],” na “binti za Sayuni [wanawake wa Yerusalemu].” (Wimbo wa Sulemani 1:5; 3:11) Si rahisi kwa msomaji wa Biblia kuwatambua wasemaji wote katika Wimbo wa Sulemani, lakini anaweza kuwatambua kwa kuchunguza yale wanayosema au yale wanayoambiwa.

Kitabu cha Wimbo wa Sulemani ni sehemu ya Neno la Mungu, na ujumbe wake ni wenye thamani sana kwa sababu mbili. (Waebrania 4:12) Kwanza, unatufundisha upendo wa kweli kati ya mwanamke na mwanamume unahusisha nini. Pili, wimbo huo ni kielelezo cha upendo kati ya Yesu Kristo na kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta.—2 Wakorintho 11:2; Waefeso 5:25-31.

MSIJARIBU “KUAMSHA UPENDO NDANI YANGU”

(Wimbo wa Sulemani 1:1–3:5)

“Na anibusu kwa busu za kinywa chake, maana maonyesho yako ya mapenzi ni bora kuliko divai.” (Wimbo wa Sulemani 1:2) Mazungumzo ya Wimbo wa Sulemani yanaanza kwa maneno ya msichana mnyenyekevu wa mashambani ambaye analetwa ndani ya hema la kifalme la Sulemani. Alifikaje humo?

“Wana wa mama yangu mwenyewe walinikasirikia,” anasema. “Waliniweka kuwa mtunzaji wa mashamba ya mizabibu.” Ndugu zake wamemkasirikia kwa sababu mvulana mchungaji ambaye anampenda amemwomba aende pamoja naye matembezini siku moja nzuri ya masika. Ili kumzuia asiende, wanampa kazi ya kuchunga “mbweha wadogo wanaoharibu mashamba ya mizabibu.” Kazi hiyo inamfanya aje karibu na kambi ya Sulemani. Urembo wake unaonekana anaposhuka kwenye “bustani ya milozi,” naye analetwa kambini.—Wimbo wa Sulemani 1:6; 2:10-15; 6:11.

Mwanamwali huyo anapoeleza jinsi anavyomtamani mchungaji wake mpendwa, wanawake wa makao ya mfalme wanamwambia ‘aende mwenyewe katika nyayo za kundi’ akamtafute. Lakini Sulemani hamruhusu aende. Akieleza jinsi anavyovutiwa na urembo wake, Sulemani anaahidi kumpa “vitaji vya dhahabu pamoja na vifungo vya fedha.” Hata hivyo, msichana huyo havutiwi naye. Mvulana mchungaji anaingia katika kambi ya Sulemani, anampata, na kusema hivi: “Tazama! Wewe ni mrembo, ewe msichana mwenzi wangu. Tazama! Wewe ni mrembo.” Mwanamwali huyo mchanga anawaapisha hivi wanawake wa makao ya mfalme: “Msijaribu kuamsha au kuwasha upendo ndani yangu mpaka wenyewe utake.”—Wimbo wa Sulemani 1:8-11, 15; 2:7; 3:5.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:2, 3—kwa nini kumbukumbu za maonyesho ya mapenzi ya mvulana mchungaji ni kama divai na jina lake kama mafuta? Kama vile divai inavyofanya moyo wa mtu ushangilie na kumiminwa kwa mafuta kichwani kunavyotuliza, ndivyo kumbukumbu za upendo wa mvulana huyo na jina lake lilivyomwimarisha na kumfariji mwanamwali huyo. (Zaburi 23:5; 104:15) Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli, hasa watiwa-mafuta, huimarishwa na kutiwa moyo wanapotafakari kuhusu upendo wa Yesu Kristo kuwaelekea.

1:5—Kwa nini msichana huyo wa mashambani analinganisha weusi wake na “mahema ya Kedari”? Vitambaa vilivyotengenezwa kwa manyoya ya mbuzi, vilitumiwa kwa kazi mbalimbali. (Hesabu 31:20) Kwa mfano, “nguo za manyoya ya mbuzi” zilitumiwa kutengeneza “hema juu ya maskani.” (Kutoka 26:7) Kama vile mahema ya Wabedui wa leo, huenda mahema ya Kedari yalitengenezwa kwa manyoya meusi ya mbuzi.

1:15—Mvulana mchungaji anamaanisha nini anaposema: “Macho yako ni kama ya njiwa”? Mvulana mchungaji anasema kwamba macho ya msichana mwenzi wake yanaonekana kuwa laini na yenye wororo kama macho ya njiwa.

2:7; 3:5—Kwa nini wanawake wa makao ya mfalme wanaapishwa “kwa swala-jike au kwa paa wa porini”? Swala na paa wanajulikana kwa sababu ya maringo na urembo wao. Kwa hiyo, mwanamwali Mshulami anawaapisha wanawake wa makao ya mfalme kwa kila kitu chenye maringo na uzuri ili kuwazuia wasijaribu kuamsha upendo ndani yake.

Mambo Tunayojifunza:

1:2; 2:6. Huenda maonyesho safi ya upendo yakafaa wakati wa uchumba. Hata hivyo, mwanamume na mwanamke wanapaswa kuwa waangalifu ili maonyesho hayo yawe ya upendo wa kweli wala si tamaa chafu ya ngono, ambayo inaweza kuwatumbukiza katika uasherati.—Wagalatia 5:19.

1:6; 2:10-15. Ndugu za Mshulami hawakumruhusu dada yao aende na mpenzi wake mahali pa mbali mlimani, lakini hawakufanya hivyo kwa sababu alikuwa na maadili mapotovu au hakuwa na nia nzuri. Badala yake, walifanya hivyo ili kumlinda asiingie katika hali ambayo ingeweza kumfanya ashawishike. Somo ambalo watu wanaochumbiana wanapata ni kwamba wanapaswa kuepuka kuwa peke yao mahali palipojitenga.

2:1-3, 8, 9Ijapokuwa alikuwa mrembo, mwanamwali Mshulami alijiona kwa kiasi kuwa kama “zafarani tu [ua la eneo hilo] ya nchi tambarare ya pwani.” Kwa sababu ya urembo wake na uaminifu kwa Yehova, mvulana mchungaji alimwona kuwa kama “yungiyungi katikati ya magugu yenye miiba.” Naye mvulana mchungaji alikuwaje? Kwa sababu alivutia, msichana huyo alimwona kuwa kama “swala.” Pia, lazima awe alikuwa na imani na alikuwa mshikamanifu kwa Yehova. “Kama mtofaa [unaotoa kivuli na matunda] katikati ya miti ya msituni,” msichana huyo anasema, “ndivyo alivyo mpenzi wangu katikati ya wana.” Je, imani na ushikamanifu kwa Mungu si sifa zenye kuvutia ambazo unapaswa kutafuta katika mtu unayetarajia awe mwenzi wako wa ndoa?

2:7; 3:5. Msichana huyo wa mashambani hakuvutiwa kamwe kimapenzi na Sulemani. Pia, aliwaapisha wanawake wa makao ya mfalme wasijaribu kuamsha ndani yake upendo kwa ajili ya mtu yeyote isipokuwa tu yule mvulana mchungaji. Haiwezekani wala haifai kuvutiwa kimapenzi na mtu yeyote tu. Mkristo mseja anayetaka kufunga ndoa anapaswa kumtafuta tu mtumishi mshikamanifu wa Yehova.—1 Wakorintho 7:39.

“MNAONA NINI KWA MSHULAMI?”

(Wimbo wa Sulemani 3:6–8:4)

Kuna kitu kinachokuja “kutoka nyikani kama nguzo za moshi.” (Wimbo wa Sulemani 3:6) Wanawake wa Yerusalemu wanaona nini wanapotoka nje ili kutazama? Tazama, Sulemani na watumishi wake wanarudi jijini! Na mfalme amemleta mwanamwali Mshulami.

Mvulana mchungaji anamfuata mwanamwali na punde si punde anapata njia ya kumwona. Anapomhakikishia upendo wake, msichana huyo anaeleza jinsi anavyotamani kuondoka jijini kwa kusema hivi: “Mpaka mchana uvume upepo mtulivu na vivuli viwe vimekimbia, nitakwenda zangu kwenye mlima wa manemane na kwenye kilima cha ubani.” Anamwomba mchungaji huyo “aje katika bustani yake, ale matunda yake yaliyo bora kabisa.” Mchungaji anajibu: “Nimeingia katika bustani yangu, ewe dada yangu, bibi-arusi wangu.” Wanawake wa Yerusalemu wanawaambia hivi: “Kuleni, enyi wapenzi! Kunyweni, mlewe maonyesho ya mapenzi!”—Wimbo wa Sulemani 4:6, 16; 5:1.

Baada ya kuwasimulia wanawake wa makao ya mfalme kuhusu ndoto yake, mwanamwali Mshulami anawaambia: “Nimelewa mapenzi.” Wanamuuliza: “Jinsi gani mpenzi wako ni bora kuliko mpenzi mwingine yeyote?” Anajibu: “Mpenzi wangu anametameta na ni mwekundu, mwenye kuvutia zaidi kati ya elfu kumi.” (Wimbo wa Sulemani 5:2-10) Sulemani anapomsifu-sifu sana, Mshulami anamjibu hivi kwa unyenyekevu: “Mnaona nini kwa Mshulami?” (Wimbo wa Sulemani 6:4-13) Akifikiri kwamba hiyo ndiyo nafasi ya kumpata, mfalme anamsifu hata zaidi. Hata hivyo, msichana huyo anabaki imara katika upendo wake kwa mvulana mchungaji. Mwishowe, Sulemani anamwacha aende nyumbani.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

4:1; 6:5—Kwa nini nywele za mwanamwali huyo zinalinganishwa na “kundi la mbuzi”? Inaelekea ulinganisho huo unaonyesha kwamba nywele zake ziling’aa na zilisitawi kama manyoya meusi ya mbuzi.

4:11—Maneno midomo ya Mshulami “inadondosha asali ya sega” na ‘asali na maziwa viko chini ya ulimi wake’ yanakazia nini? Asali ya sega ina ladha zaidi na ni tamu kuliko asali iliyopigwa na upepo. Ulinganisho huo, na pia wazo la kwamba asali na maziwa yalikuwa chini ya ulimi wa mwanamwali huyo, unakazia kwamba maneno ya Mshulami yalikuwa mazuri na yenye kupendeza.

5:12—Ni nini maana ya maneno “macho yake ni kama njiwa kando ya mifereji ya maji, ambao wanaoga katika maziwa”? Mwanamwali huyo anazungumzia macho mazuri ya mpenzi wake. Labda analinganisha kishairi mboni nyeusi zilizozungukwa na sehemu nyeupe za macho yake na njiwa wa rangi ya bluu-kijivu ambao wanaoga katika maziwa.

5:14, 15—Kwa nini mikono na miguu ya mchungaji inafafanuliwa kwa njia hii? Yaelekea mwanamwali anasema kwamba vidole vya mchungaji ni kama mianzi ya dhahabu na kucha zake kama krisolito. Analinganisha miguu yake na “nguzo za marumaru” kwa sababu ina nguvu na inavutia.

6:4—Je, “Jiji la Kupendeza” ni Yerusalemu? Hapana. “Jiji la Kupendeza” ni “Tirsa.” Jiji hilo la Wakanaani lilitekwa na Yoshua na baada ya wakati wa Sulemani likawa jiji kuu la kwanza la ufalme wa kaskazini wa Israeli wa makabila kumi. (Yoshua 12:7, 24; 1 Wafalme 16:5, 6, 8, 15) Kitabu kimoja kinasema hivi: “Inaonekana kwamba jiji hilo lilikuwa zuri sana, na ndiyo sababu linatajwa hapa.”

6:13—“Dansi ya kambi mbili” ni nini? Maneno hayo yanaweza pia kutafsiriwa kuwa “dansi ya Mahanaimu.” Jiji lililoitwa kwa jina hilo lilikuwa mashariki ya Mto Yordani karibu na bonde la mto la Yaboki. (Mwanzo 32:2, 22; 2 Samweli 2:29) Huenda “dansi ya kambi mbili” ikarejelea dansi iliyofanywa katika jiji hilo wakati wa sherehe fulani.

7:4—kwa nini Sulemani analinganisha shingo ya mwanamwali Mshulami na “mnara wa pembe ya tembo”? Mwanzoni msichana huyo alisifiwa hivi: “Shingo yako ni kama mnara wa Daudi.” (Wimbo wa Sulemani 4:4) Mnara ni mrefu na mwembamba, na pembe ya tembo ni laini. Sulemani anavutiwa na wembamba na ulaini wa shingo ya msichana huyo.

Mambo Tunayojifunza:

4:1-7. Ijapokuwa Mshulami hakuwa mkamilifu, kwa kukataa kutongozwa na Sulemani, alijithibitisha kuwa mwenye maadili mazuri. Nguvu zake za kiadili zilizidisha urembo wake. Hivyo ndivyo wanawake Wakristo wanavyopaswa kuwa.

4:12. Kama bustani maridadi iliyozingirwa kwa ua au ukuta, ambayo inaweza kuingiwa tu kupitia lango lililofungwa, mwanamwali Mshulami alimwonyesha tu upendo mwororo yule aliyetarajiwa kuwa mume wake. Huo ni mfano mzuri kama nini kwa wanawake na wanaume waseja!

“MWALI WA MOTO WA YAH”

(Wimbo wa Sulemani 8:5-14)

“Mwanamke huyu ni nani, anayepanda kutoka nyikani, akimwegemea mpenzi wake?” wanauliza ndugu za Mshulami wanapomwona akirudi nyumbani. Muda fulani mapema, mmoja wao alikuwa amesema: “Kama akiwa ukuta, tutajenga juu yake mnara wa fedha; lakini akiwa mlango, tutamzuia kwa ubao wa mwerezi.” Kwa kuwa sasa upendo wa Mshulami umejaribiwa na kuthibitika kuwa imara, yeye anasema: “Mimi ni ukuta, na maziwa yangu ni kama minara. Basi nimekuwa machoni pake yeye kama msichana anayepata amani.”—Wimbo wa Sulemani 8:5, 9, 10.

Upendo wa kweli ni “mwali wa moto wa Yah.” Kwa nini? Kwa sababu Yehova ndiye chanzo cha upendo wa aina hiyo. Yeye ndiye ametuumba tukiwa na sifa ya upendo. Ni mwali ambao miwako yake haiwezi kuzimwa. Wimbo wa Sulemani unaonyesha kwa njia nzuri sana kwamba upendo kati ya mwanamume na mwanamke unaweza kuwa na “nguvu [hauwezi kushindwa] kama kifo.”—Wimbo wa Sulemani 8:6.

Pia, wimbo bora wa Sulemani unatuonyesha kifungo kati ya Yesu Kristo na washiriki wa “bibi-arusi” wake wa mbinguni. (Ufunuo 21:2, 9) Upendo wa Yesu kwa Wakristo watiwa-mafuta ni mkubwa kuliko upendo wowote kati ya mwanamume na mwanamke. Washiriki wa jamii ya bibi-arusi hawayumbi-yumbi katika ujitoaji wao. Kwa upendo, Yesu alitoa uhai wake kwa ajili ya “kondoo wengine” pia. (Yohana 10:16) Kwa hiyo, waabudu wote wa kweli wanaweza kuiga kielelezo cha Mshulami cha upendo na ushikamanifu usioyumbayumba.

[Picha katika ukurasa wa 18, 19]

Wimbo wa Sulemani unatufundisha nini kuhusu sifa za kutafuta katika mwenzi wa ndoa?