Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shule Ambayo Wahitimu Wake Wanawafaidi Watu Ulimwenguni Pote

Shule Ambayo Wahitimu Wake Wanawafaidi Watu Ulimwenguni Pote

Shule Ambayo Wahitimu Wake Wanawafaidi Watu Ulimwenguni Pote

KATIKA makutaniko zaidi ya 98,000 ya Mashahidi wa Yehova katika nchi zaidi ya 200, watu wa tabaka zote za maisha wanafundishwa na Mungu. Kitabu kikuu cha mafundisho ni Biblia, na kusudi la elimu hiyo ni kumsaidia mtu mmoja-mmoja afanye maendeleo ya kiroho kwa kujifunza mapenzi ya Mungu na jinsi ya kuishi kupatana nayo. Wale wanaokubali elimu hiyo wanafaidika sana. Kupatana na agizo la Yesu Kristo la kufanya wanafunzi, watu hao huwajulisha wengine mambo wanayojifunza.—Mathayo 28:19, 20.

Mbali na elimu inayoendelea katika makutaniko yao, Mashahidi wa Yehova wameanzisha shule mbalimbali za pekee. Moja ya shule hizo ni Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Shule hiyo ilianzishwa mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) 1987 huko Pittsburgh, Pennsylvania, Marekani. Darasa la kwanza lilikuwa na wanafunzi 24 walioongea Kiingereza. Tangu wakati huo, shule hiyo imefanywa katika lugha 21 na nchi 43. Kufikia sasa, wazee na watumishi wa huduma waseja kutoka nchi zaidi ya 90 wamehudhuria. Baada ya kumaliza masomo ya majuma manane, wahitimu hutumwa kutumikia mahali penye uhitaji katika nchi yao wenyewe au nchi nyingine. Kufikia mwishoni mwa mwaka wa 2005, zaidi ya wahudumu Wakristo 22,000 walikuwa wamepata mazoezi katika shule hiyo. Bidii na unyenyekevu wao katika kuendeleza kazi ya Ufalme na kuwafaidi wengine imebarikiwa sana.—Methali 10:22; 1 Petro 5:5.

Kufanya Mipango Ili Kuhudhuria

Ili kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, wanafunzi wengi wanahitaji kuomba ruhusa kazini. Nyakati nyingine si rahisi kupata ruhusa. Huko Hawaii, wanaume wawili Wakristo ambao walialikwa kwenye shule hiyo walihitaji kuomba ruhusa kazini kwa sababu walikuwa walimu. Kwa imani, walipeleka maombi yao wakieleza kwa nini walitaka kuhudhuria shule hiyo na jinsi ambavyo ingewafaidi. Wote wawili walipewa ruhusa.

Katika visa kadhaa, Mashahidi ambao waliomba ruhusa kazini waliambiwa kwamba wangepoteza kazi zao. Waliamua kwenda kupata mazoezi kutoka kwa tengenezo la Yehova hata kama wangepoteza kazi zao. Baadaye, baadhi ya watu hao waliombwa na matajiri wao warudi kazini baada ya shule. Azimio kama hilo la kuhudhuria shule hiyo linaweza kufafanuliwa hivi kwa ufupi: Omba ruhusa, sali ili Yehova akusaidie, na umwachie mengine yote.—Zaburi 37:5.

‘Kufundishwa na Yehova’

Katika shule hiyo inayochukua majuma manane, wanafunzi wanajifunza Biblia kindani. Wao hujifunza jinsi ambavyo watu wa Yehova wamepangwa wakiwa tengenezo linalofanya mapenzi ya Mungu na jinsi ambavyo wao wenyewe wanaweza kutumia Biblia kwa matokeo zaidi katika huduma yao ya shambani, mikutano ya kutaniko, na katika makusanyiko.

Mhitimu mmoja mwenye uthamini alimwandikia hivi mwanafunzi ambaye bado hakuwa amehudhuria shule hiyo: “Bila shaka, utapokea elimu bora zaidi ambayo hujawahi kupata. Utalithamini zaidi andiko linalosema kuhusu ‘kufundishwa na Yehova.’ Utafinyangwa, na moyo na utu wako utaboreshwa ili upatane zaidi na kielelezo cha Kristo Yesu. Hilo litakuwa jambo bora zaidi maishani mwako.”—Isaya 54:13.

Waeneza-injili, Wachungaji, na Walimu

Leo, wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wanatumika katika nchi 117. Nchi hizo zinatia ndani visiwa vya Atlantiki, Karibea, na Pasifiki na pia nchi ambazo zina ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Ofisi za tawi zinaripoti kwamba mazoezi mazuri ambayo wanafunzi wanapokea yameboresha kazi yao ya kueneza injili, uchungaji, na ufundishaji. Mazoezi hayo yanawasaidia kutumia Biblia vizuri zaidi katika huduma ya shambani. (2 Timotheo 2:15) Wanapojibu maswali ya wenye nyumba, mara nyingi wanatumia kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, * na wanawazoeza wahubiri wengine wa Ufalme kufanya hivyo. Bidii ya wahitimu hao inawachochea wengine, na kazi yao inayaimarisha makutaniko.

Wazee wa kutaniko wana pendeleo la ‘kulichunga kundi,’ nao hushughulikia mahitaji ya kiroho ya wengine. (1 Petro 5:2, 3) Mzee mmoja alisema hivi kuhusu shule hiyo: “Tunashukuru kwamba ofisi ya tawi inawatuma ndugu waliozoezwa vizuri ili watusaidie kufanya kazi ya kulichunga kundi la Mungu.” Vivyo hivyo, ofisi moja ya tawi katika Mashariki ya Mbali ilisema hivi: “Wahitimu wa shule hiyo wana huruma sana. Wanafanya kazi kwa bidii na hivyo wanaheshimiwa sana na kutaniko. Unyenyekevu, uchangamfu, na bidii yao zinajulikana na kuthaminiwa sana. Wanajitoa kwa hiari na kuhamia katika makutaniko ambayo yanahitaji wachungaji.” (Wafilipi 2:4) Wanaume kama hao wanawaburudisha waamini wenzao na wanastahili pongezi.—1 Wakorintho 16:18.

Isitoshe, walimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wanawasaidia wanafunzi kuboresha uwezo wao wa kutoa hotuba. Kwa kutumia mapendekezo na mashauri wanayopokea, baada ya muda mfupi, wahitimu wengi wanaweza kutumiwa katika programu za kusanyiko la mzunguko na la wilaya. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema kwamba wahitimu wanatoa “hotuba nzuri sana na kuonyesha faida za habari hiyo kwa njia yenye kusadikisha.”—1 Timotheo 4:13.

Ufundishaji uliboreka sana kwenye mikutano ya kutaniko katika nchi moja barani Afrika baada ya Shule ya Mazoezi ya Kihuduma kufanywa huko na wahitimu kutumwa katika makutaniko mbalimbali. Wazee wanaotumwa kutoka shule hiyo wanasaidia katika kueneza injili, uchungaji, na ufundishaji, na hivyo wanayajenga makutaniko kiroho.—Waefeso 4:8, 11, 12.

Uangalizi wa Makutaniko Umeboreshwa

Katika maeneo mengi, kuna uhitaji zaidi wa wazee na watumishi wa huduma. Makutaniko fulani hayangekuwa na mzee yeyote ikiwa mhitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma hangetumwa huko. Kwa hiyo, wahitimu wengi wanapewa mgawo wa kutumikia katika maeneo yaliyo na uhitaji kama huo.

Ofisi kadhaa za tawi zinaripoti kwamba wanaume hao, “wanafahamu vizuri mipango ya tengenezo,” “wanachukua migawo yao kwa uzito,” “wanawasaidia wengine kuelewa na kuheshimu tengenezo la Yehova,” na “wanachangia uchangamfu na hali ya kiroho ya makutaniko yao.” Hii ni kwa sababu wahitimu wa shule hiyo wanafuata yale yaliyoandikwa katika Neno la Mungu na hawategemei uelewaji wao wenyewe au kuwa wenye hekima machoni pao wenyewe. (Methali 3:5-7) Wanaume kama hao wanakuwa zawadi za kiroho katika makutaniko ambako wametumwa.

Kutumikia Katika Maeneo ya Mbali

Wahitimu fulani waliowekwa rasmi kuwa mapainia wa pekee wanasaidia vikundi vilivyo mbali kuwa makutaniko. Akishukuru kwa msaada wao, mzee katika eneo la mbali huko Guatemala alisema hivi: “Kwa miaka 20 nilikuwa na wasiwasi kuhusu jinsi eneo hili kubwa lingehubiriwa. Mara nyingi, nilisali kuhusu jambo hilo. Ndugu kutoka katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wamezoezwa vizuri kutoa hotuba na pia katika mambo ya kitengenezo, nami ninashukuru sana kuona kwamba eneo hili sasa linashughulikiwa kwa upendo.”

Wahitimu wamejifunza kuwa na matokeo katika maeneo ambako wanahitaji kusafiri sana kwenye sehemu zenye milima ili kufikia vijiji vilivyotawanyika. Bila kukawia, wao huanzisha na kupanga vikundi vidogo, hata katika maeneo ambako wahubiri wengine hawajafaulu kufanya hivyo. Kwa mfano, mzee mmoja huko Niger aliomba msaada wa wahitimu kwa sababu alihisi kwamba wangeweza kufanya kazi nzuri katika eneo ambako anaishi. Inaweza kuwa rahisi zaidi kwa wanaume waseja kutumikia wakiwa mapainia wa pekee na waangalizi wa mizunguko hasa katika maeneo ya mbali. Kama mtume Paulo, ni lazima wakabiliane na ‘hatari za kutokana na mito, hatari za kutokana na wanyang’anyi wa njia kuu, hatari za nyikani,’ matatizo ya kibinafsi, na pia mahangaiko kwa ajili ya makutaniko wanayotumikia.—2 Wakorintho 11:26-28.

Kuwasaidia Vijana

Maandiko huwahimiza vijana wamkumbuke Muumba wao. (Mhubiri 12:1) Wahitimu wenye bidii wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wamewawekea vijana Wakristo mfano mzuri. Baada ya wahitimu wawili kufika katika kutaniko moja nchini Marekani, jumla ya saa ambazo ndugu walitumia katika huduma ziliongezeka mara mbili. Zaidi ya hilo, idadi ya mapainia wa kawaida au wahubiri wa Ufalme wa wakati wote, iliongezeka kutoka 2 hadi 11. Na imekuwa hivyo katika makutaniko mengi.

Wahitimu pia wanawatia moyo wanaume vijana wafikirie kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Hilo limewachochea wengine ambao si watumishi wa huduma wafikie pendeleo hilo. Ofisi ya tawi ya Uholanzi inasema kwamba wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ni “vielelezo kwa vijana wanaume ambao wanafikiria jinsi watakavyotumia maisha yao.”

Kutumikia Katika Makutaniko ya Lugha za Kigeni

Katika nchi nyingi, jitihada za kuwahubiria watu habari njema katika lugha zao zinapamba moto. Mara nyingi, wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wanajifunza lugha nyingine na wanatumikia katika maeneo yenye idadi kubwa ya wageni kutoka nchi nyingine. Kwa mfano, nchini Ubelgiji, kuna uhitaji wa wahubiri zaidi wa Ufalme katika maeneo ya Kialbania, Kiajemi, na Kirusi.

Makutaniko na vikundi vya lugha za kigeni nchini Italia, Marekani, Mexico, Uingereza, Ujerumani, na nchi nyingine tayari vinafaidika sana kutokana na waangalizi wanaosafiri, wazee, na watumishi wa huduma ambao ni wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Ofisi ya tawi ya Korea inaripoti kwamba “wahitimu zaidi ya 200 wanatimiza majukumu muhimu sana katika kusaidia makutaniko na vikundi vya lugha za kigeni.”

Kutimiza Migawo Mingine kwa Unyenyekevu

Mbali na kutumikia katika vikundi na makutaniko ya lugha za kigeni, wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wanatumika wakiwa wazee, watumishi wa huduma na waangalizi wanaosafiri. Baadhi yao hukubali migawo ya kwenda nchi nyingine, ambako huenda wakatimiza uhitaji wa haraka katika Idara ya Utumishi kwenye ofisi ya tawi. Wale ambao ni mafundi wa kujenga wanaweza kushiriki katika programu ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme.

Kwa sababu ya ongezeko la ulimwenguni pote la idadi ya makutaniko na mizunguko, kuna uhitaji mkubwa zaidi wa waangalizi wanaosafiri. Ili kutimiza uhitaji huo, wahitimu waliochaguliwa wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma huzoezwa kwa majuma kumi katika kazi ya kusafiri na kisha wanatumikia wakiwa waangalizi wa mzunguko au waangalizi wa mzunguko wa badala. Wahitimu 1,300 hivi wanatumika sasa katika nchi 97 wakiwa waangalizi wanaosafiri. Katika nchi moja ya Afrika, asilimia 55 ya waangalizi wanaosafiri ni wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Katika nchi nyingine ya Afrika, ni asilimia 70.

Huko Australia, Kanada, Marekani, Mashariki ya Mbali, na Ulaya, mamia ya wahitimu wa shule hiyo wametumwa ili kutimiza mahitaji ya pekee katika nchi nyingine. Kwa njia hiyo, faida za shule hiyo zimeenea ulimwenguni pote.

Kupitia Mwana wake, Yesu Kristo, Yehova ametokeza waeneza-injili, wachungaji, walimu, na wengine ambao wanaendeleza kazi ya Ufalme katika siku hizi za mwisho. Je, kuna uwezekano kwamba idadi ya watu wa Mungu itaongezeka zaidi? Bila shaka! Hivyo, kuna uhitaji unaozidi kuongezeka wa wanaume waliojiweka wakfu kujitahidi kufikia mapendeleo makubwa zaidi. (Isaya 60:22; 1 Timotheo 3:1, 13) Shule ya Mazoezi ya Kihuduma inawapa wazee na watumishi wa huduma nafasi ya kuzoezwa ili wapanue huduma yao na kupata faida wao wenyewe, na pia kuwafaidi watu wengine ulimwenguni pote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Shule ya Mazoezi ya Kihuduma inaendeleza kazi ya Ufalme ulimwenguni pote

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, unatarajia kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma na kisha uwafaidi wengine?