Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Suala Linalokuhusu Wewe

Suala Linalokuhusu Wewe

Suala Linalokuhusu Wewe

JE, UNA rafiki au mshiriki wa familia ambaye mna uhusiano wa karibu sana? Ingekuwaje ikiwa mtu fulani angekushutumu kwamba una uhusiano na mtu huyo kwa sababu tu za ubinafsi? Je, hungeumia moyoni au hata kukasirika? Hivyo hasa ndivyo Shetani Ibilisi amewashutumu wote walio na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu.

Fikiria yale yaliyotukia Shetani alipofanikiwa kuwashawishi wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, wavunje sheria ya Mungu na kujiunga naye kumwasi Mungu. Je, yale yaliyotukia yalimaanisha kwamba watu wangemtii Yehova ikiwa tu wangepata faida kwa kufanya hivyo? (Mwanzo 3:1-6) Miaka 2,500 baada ya Adamu kuasi, Shetani alizusha suala hilohilo, lakini wakati huu lilihusiana na mtu aliyeitwa Ayubu. Kwa kuwa shtaka la Ibilisi lilifunua waziwazi suala linalohusika, acheni tuchunguze kwa uangalifu simulizi hilo la Biblia.

“Sitajiondolea Utimilifu Wangu”

Ayubu ni “mtu asiye na lawama na mnyoofu, mwenye kumwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.” Hata hivyo, Shetani anadai kwamba unyoofu wa Ayubu ni wa ubinafsi. “Je, Ayubu amemwogopa Mungu bure?” Shetani anamuuliza Yehova. Kisha, Ibilisi anamchongea Mungu na Ayubu kwa kudai kwamba Yehova amemhonga Ayubu kwa kumlinda na kumbariki ili awe mshikamanifu kwake. “Ili kuwe na badiliko,” Shetani anadai, “tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kila kitu alicho nacho, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.”—Ayubu 1:8-11.

Ili kujibu madai hayo, Yehova anamruhusu Shetani amjaribu Ayubu. Ibilisi anajaribu kumshawishi mwanamume huyo mwaminifu aache kumtumikia Mungu kwa kumletea msiba mmoja baada ya mwingine. Mifugo yote ya Ayubu inaibiwa au kuuawa, na watumishi na wana wa Ayubu wanauawa. (Ayubu 1:12-19) Lakini je, Shetani anafaulu? Bila shaka hapana! Ingawa hajui kwamba Ibilisi ndiye anayemjaribu, Ayubu anasema: “Yehova ametoa, na Yehova amechukua. Jina la Yehova na liendelee kubarikiwa.”—Ayubu 1:21.

Baadaye, Shetani anakuja mbele za Yehova, naye Yehova anamwambia hivi: “[Ayubu] anashikilia sana utimilifu wake, ingawa wewe unanichochea juu yake nimmeze bila sababu.” (Ayubu 2:1-3) Suala muhimu linahusu utimilifu wa Ayubu. Mtu mtimilifu ni yule aliye na ushikamanifu usioyumba-yumba kumwelekea Mungu na anayeshikamana kabisa na uadilifu. Kufikia sasa, Ayubu amekuwa mshindi katika suala hilo la utimilifu. Hata hivyo, Ibilisi hachoki.

Kisha, Shetani anatoa dai linalowahusu wanadamu wote. “Ngozi kwa ngozi,” anamwambia Yehova, “na kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake. Ili kuwe na badiliko, tafadhali nyoosha mkono wako, uguse kufikia mfupa wake na nyama yake, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.” (Ayubu 2:4, 5) Kwa kutumia neno la ujumla “mtu” badala ya kusema Ayubu, Ibilisi anatilia shaka utimilifu wa kila mwanadamu. Ni kana kwamba Ibilisi anadai: ‘Mtu atafanya jambo lolote ili kuokoa uhai wake. Nikipewa nafasi, ninaweza kumgeuza mtu yeyote amwache Mungu.’ Je, hakuna mwanadamu yeyote atakayebaki mshikamanifu kwa Mungu chini ya hali na nyakati zote?

Yehova anamruhusu Ibilisi ampige Ayubu kwa ugonjwa wenye kuua. Ayubu anateseka sana hivi kwamba anaomba afe. (Ayubu 2:7; 14:13) Hata hivyo, Ayubu anasema: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!” (Ayubu 27:5) Ayubu anasema hivyo kwa sababu anampenda Mungu, na hakuna chochote kinachoweza kubadili jambo hilo. Ayubu anajithibitisha mwenyewe kuwa mtu mtimilifu. Biblia inasema hivi: “Naye Yehova akaubariki mwisho wa Ayubu baadaye kuliko mwanzo wake.” (Ayubu 42:10-17) Je, kumekuwa na watu wengine kama Ayubu? Kupita kwa wakati kumeonyesha nini?

Jinsi Ambavyo Suala Hilo Limejibiwa

Katika sura ya 11 ya kitabu cha Biblia cha Waebrania, mtume Paulo anataja majina ya wanaume na wanawake waaminifu wa kabla ya Ukristo, kutia ndani Noa, Abrahamu, Sara, na Musa. Kisha, mtume huyo anasema hivi: “Kwa maana nitakosa wakati nikiendelea kusimulia juu ya [wengine].” (Waebrania 11:32) Watumishi hao waaminifu wa Mungu walikuwa wengi sana hivi kwamba Paulo anawataja kuwa ‘wingu kubwa la Mashahidi,’ akiwalinganisha na wingu kubwa ambalo linatanda angani. (Waebrania 12:1) Naam, kwa karne nyingi idadi kubwa sana ya watu wametumia uhuru wao wa kuchagua na kuamua kuwa upande wa Yehova Mungu.—Yoshua 24:15.

Jibu bora kabisa kwa dai la Shetani la kwamba anaweza kugeuza watu wamwache Yehova lilitolewa na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. Hata maumivu makali ya kifo kwenye mti wa mateso hayakuvunja utimilifu wake kwa Mungu. Alipokuwa akikata pumzi, Yesu alisema hivi kwa sauti: “Baba, ninaikabidhi roho yangu mikononi mwako.”—Luka 23:46.

Kadiri ambavyo wakati umepita, imeonekana wazi kwamba Ibilisi hajafaulu kumgeuza kila mtu aache kumtumikia Mungu wa kweli. Wanadamu wengi sana wamemjua Yehova na ‘kumpenda kwa moyo wao wote na kwa nafsi yao yote na kwa akili yao yote.’ (Mathayo 22:37) Ushikamanifu wao usioyumba-yumba kwa Yehova umethibitisha kwamba Shetani alisema uwongo kuhusu suala la utimilifu wa wanadamu. Wewe pia unaweza kumthibitisha Ibilisi kuwa mwongo ukiwa mwanamume au mwanamke mtimilifu.

Unapaswa Kufanya Nini?

Ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Unaweza kufanyaje hivyo? Tenga wakati wa kujifunza Biblia na ‘kupata ujuzi juu ya Mungu wa pekee wa kweli na juu ya yule aliyemtuma, Yesu Kristo.’—Yohana 17:3.

Shetani alizusha suala la utimilifu wa mwanadamu kwa kutilia shaka nia ya mwanadamu ya kumtumikia Mungu. Ili ujuzi uongoze nia yako, ni lazima ujuzi huo uguse moyo wako. Na ili hilo litukie, unahitaji kufanya mengi zaidi ya kutafuta tu habari katika Biblia. Sitawisha zoea la kutafakari yale unayojifunza. (Zaburi 143:5) Unaposoma Biblia au vichapo vya Biblia, hakikisha kwamba unachukua wakati ili kutafakari kuhusu maswali kama haya: ‘Habari hii inanifundisha nini kumhusu Yehova? Inafunua sifa gani za Mungu? Ninahitaji kuonyesha sifa hizo katika sehemu gani za maisha yangu? Ni mambo gani ambayo Mungu anakubali au anakataa? Hilo linafanya niwe na maoni gani kumhusu Mungu?’ Kutafakari kwa njia hiyo kutajaza moyoni mwako upendo na uthamini kumwelekea Muumba.

Utimilifu kwa Mungu hauhusu tu imani ya kidini. (1 Wafalme 9:4) Ili udumishe utimilifu wako kwa Yehova Mungu unahitaji kuwa na maadili mazuri katika sehemu zote za maisha yako. Hata hivyo, ukidumisha utimilifu hutapungukiwa kwa vyovyote. Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” naye anataka ufurahie maisha. (1 Timotheo 1:11) Sasa tuchunguze mazoea fulani unayohitaji kuepuka ili ubaki safi kiadili na hivyo uwe na maisha yenye furaha zaidi na kupata kibali cha Mungu.

Epuka Mwenendo Mpotovu Kingono

Yehova mwenyewe aliweka viwango vya ndoa katika Neno lake Biblia, ambayo inasema: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:21-24) Kwa kuwa wamekuwa “mwili mmoja,” wenzi wa ndoa huheshimu mpango wa Mungu wa ndoa kwa kuwa na uhusiano wa ngono na mwenzi wao wa ndoa tu. Mtume Paulo alisema hivi: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Maneno “kitanda cha ndoa” hurejelea ngono kati ya mwanamume na mwanamke waliofunga ndoa kihalali. Mmoja wao akifanya ngono nje ya ndoa anafanya uzinzi na anaweza kuhukumiwa vikali na Mungu.—Malaki 3:5.

Namna gani kufanya ngono kabla ya kufunga ndoa? Tendo hilo pia ni kinyume cha viwango vya maadili vilivyowekwa na Yehova. Biblia inasema hivi: “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu . . . kwamba mjiepushe na uasherati.” (1 Wathesalonike 4:3) Pia, ngono kati ya watu wa jinsia moja, watu wa ukoo, na ngono pamoja na wanyama ni dhambi dhidi ya Mungu. (Mambo ya Walawi 18:6, 23; Waroma 1:26, 27) Yeyote anayetaka kumpendeza Mungu na kuwa na maisha yenye furaha kikweli anapaswa kuepuka mazoea yaliyo mapotovu kiadili.

Namna gani tabia ya kuamsha tamaa ya ngono kabla ya kufunga ndoa? Zoea hilo linamchukiza Yehova. (Wagalatia 5:19) Ni lazima pia mtu aepuke kufikiria mambo mapotovu kiadili. Yesu alisema: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Maneno hayo yanahusu kutazama picha za ngono katika vichapo, sinema, au Intaneti; kusoma vitabu vinavyoeleza vitendo vichafu vya ngono; na kusikiliza nyimbo zenye maneno ambayo yanapendekeza mambo machafu. Kuepuka mambo kama hayo humpendeza Mungu na huwa na uvutano mzuri katika maisha ya mtu.

Namna gani kuchezeana kimapenzi? Kuchezeana kimapenzi ni tabia ya kumshawishi mtu kimahaba au kingono. Mwanamume aliyeoa au mwanamke aliyeolewa anayemchezea kimapenzi mtu mwingine asiye mwenzi wake wa ndoa anavunja kanuni za Biblia, na hilo linaonyesha kwamba hamheshimu Yehova. (Waefeso 5:28-33) Ni jambo lisilofaa kama nini kwa waseja kuonyeshana ishara za kimapenzi ili kujifurahisha tu! Namna gani mmoja wao akichukua kwa uzito ishara hizo? Wazia maumivu ya kihisia ambayo yanaweza kusababishwa. Jambo zito zaidi ni kwamba kuchezeana kimapenzi kunaweza kumwongoza mtu afanye uzinzi au uasherati. Kwa upande mwingine, kuwatendea watu wa jinsia tofauti kwa usafi wa kiadili huongeza heshima ya mtu.—1 Timotheo 5:1, 2.

Kumpendeza Mungu Katika Sehemu Nyingine za Maisha

Pombe inapatikana kwa urahisi katika nchi nyingi. Je, ni kosa kunywa pombe? Maandiko hayakatazi kunywa kwa kiasi divai, bia, au aina nyingine za pombe. (Zaburi 104:15; 1 Timotheo 5:23) Hata hivyo, kunywa kupita kiasi na kulewa ni makosa machoni pa Mungu. (1 Wakorintho 5:11-13) Ni wazi kwamba hungetaka kunywa kupita kiasi kuathiri afya yako na kuharibu maisha yako ya familia.—Methali 23:20, 21, 29-35.

Yehova ni “Mungu wa ukweli.” (Zaburi 31:5) Biblia inasema kwamba “Mungu hawezi kamwe kusema uwongo.” (Waebrania 6:18) Ikiwa unataka kibali cha Mungu, utaepuka kusema uwongo. (Methali 6:16-19; Wakolosai 3:9, 10) Biblia inawahimiza hivi Wakristo: “Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.”—Waefeso 4:25.

Pia, kuna zoea la kucheza kamari. Ingawa zoea hilo linapendwa na watu wengi, kucheza kamari ni aina fulani ya pupa kwa kuwa ni kujaribu kupata pesa kwa hasara ya wengine. Yehova hawakubali watu “wenye pupa ya pato lisilo la haki.” (1 Timotheo 3:8) Hivyo, ikiwa unataka kumpendeza Yehova, utaepuka aina yoyote ya kamari kutia ndani, bahati nasibu, kamari aina ya bingo, na ya mashindano ya mbio za farasi. Kwa kufanya hivyo, huenda ukawa na pesa zaidi za kutimiza mahitaji ya familia yako.

Kuiba, yaani, kuchukua kitu ambacho si chako ni aina nyingine ya pupa. Biblia inasema hivi: “Usiibe.” (Kutoka 20:15) Ni kosa kununua kitu kilichoibiwa huku ukijua, na pia ni kosa kuchukua vitu bila ruhusa. Biblia inasema: “Mwizi asiibe tena,bali afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema, ili awe na kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.” (Waefeso 4:28) Badala ya kuiba wakati wa matajiri wao, wale wanaompenda Yehova hufanya kazi kwa unyoofu na kwa bidii. Wao ‘hutaka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.’ (Waebrania 13:18) Na bila shaka dhamiri njema humfanya mtu awe na amani ya akili.

Mungu anamwonaje mtu aliye na hasira kali? Biblia inaonya hivi: “Usishirikiane na mtu yeyote mwenye mazoea ya kukasirika; wala usiende pamoja na mtu wa mifoko ya ghadhabu.” (Methali 22:24) Mara nyingi, hasira isiyozuiliwa humfanya mtu atende kwa jeuri. (Mwanzo 4:5-8) Kuhusu kulipiza kisasi, Biblia inasema hivi: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. Fanyeni mambo mema machoni pa watu wote. Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi ghadhabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Waroma 12:17-19) Tukifuata mashauri kama hayo, maisha yetu yatakuwa yenye amani zaidi na furaha yetu itaongezeka.

Unaweza Kufaulu

Je, unaweza kufaulu kudumisha utimilifu wako kwa Mungu licha ya mikazo inayokubana usiwe mtimilifu? Naam, unaweza. Tambua kwamba Mungu anataka ufaulu kuthibitisha kuwa Shetani ni mwongo kuhusiana na suala la utimilifu, kwa sababu Neno Lake linasema hivi: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.”—Methali 27:11.

Unaweza kumwomba Yehova akuimarishe kufanya yaliyo sawa machoni pake. (Wafilipi 4:6, 7, 13) Kwa hiyo, jitahidi kabisa kuongeza ujuzi wako wa Neno la Mungu, Biblia. Kutafakari kwa uthamini kuhusu mambo unayojifunza katika Biblia kutakusaidia uimarishe upendo wako kwa Mungu na kutakuchochea umpendeze. Andiko la 1 Yohana 5:3 linasema: “Kwa maana kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukusaidia kujifunza Biblia. Waombe wakusaidie au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Ayubu alibaki mwaminifu alipojaribiwa

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kuongeza ujuzi wako kuhusu Neno la Mungu kutaimarisha azimio lako la kufanya yaliyo sawa