Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafundishe Watoto Wako Kutoa Maelezo

Wafundishe Watoto Wako Kutoa Maelezo

Wafundishe Watoto Wako Kutoa Maelezo

PERLA kutoka Mexico anakumbuka kwamba alipokuwa msichana mdogo, mama yake alimsaidia kutayarisha maelezo mafupi ya kutoa katika Funzo la Mnara wa Mlinzi. Sasa Perla ana mtoto mvulana mwenye umri wa miaka mitano. Yeye humsaidiaje? “Kwanza ni lazima nitayarishe. Ninapofanya hivyo, ninatafuta fungu ambalo mtoto wangu anaweza kuelewa,yaani, lile ambalo anaweza kuelezea kwa maneno yake mwenyewe. Kisha, tunakazia fikira fungu hilo ambalo yeye huliita ‘fungu langu.’ Mimi humwomba atoe maelezo kuhusiana na fungu hilo akitumia mifano ya kawaida maishani. Halafu, tunafanya mazoezi ya kutoa maelezo hayo mara kadhaa. Tunatumia kitu kinachofanana na kikuza-sauti ili ajue jinsi ya kushika kikuza-sauti anapotoa maelezo. Ninafurahi sana kwa sababu yeye huinua mkono wake au kutoa maelezo katika kila mkutano. Mara nyingi, kabla ya mkutano kuanza, yeye humfikia yule atakayeongoza na kumwambia fungu ambalo angependa kutoa maelezo.”

Jens, mzee anayeshirikiana na kikundi cha lugha ya Kihindi, ana watoto wawili wavulana, mmoja ana umri wa miaka miwili na yule mwingine miaka minne. Wakati Jens na mke wake wanapotayarisha mikutano pamoja na watoto wao, wanatumia njia ambayo Jens alijifunza kutoka kwa wazazi wake. Anasema hivi: “Tunachagua sehemu ambazo watoto wanaweza kuelewa. Kisha, tunajaribu kuwaeleza kwa ufupi habari inayozungumziwa au jambo kuu la makala hiyo. Halafu, tunawauliza maswali ambayo tunataka wajibu mikutanoni. Mara nyingi, tunashangaa tunaposikia majibu wanayotoa kwa maneno yao wenyewe. Maelezo yao yanaonyesha kikweli mambo ambayo wanaelewa. Kwa njia hiyo, maelezo yao yanamletea Yehova sifa na yanaonyesha imani yao.”