Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Faida ya Kuwa Mnyoofu

Kuna Faida ya Kuwa Mnyoofu

Kuna Faida ya Kuwa Mnyoofu

UKOSEFU wa unyoofu umekuwapo tangu bustani ya Edeni. Hata hivyo, tamaduni na jamii nyingi zinathamini unyoofu na zinaona uwongo na udanganyifu kuwa mambo yasiyopendeza na yenye kuchukiza. Watu wanajivunia kuwa wenye kutumainika. Ingawa hivyo, ukosefu wa unyoofu unazidi kuonwa kuwa jambo la lazima ili kufanikiwa maishani. Una maoni gani kuhusu jambo hilo? Je, kuna faida ya kuwa mnyoofu? Wewe unaamuaje mazoea yaliyo manyoofu na yasiyo manyoofu?

Ili kumpendeza Mungu, ni lazima tuwe wanyoofu katika usemi wetu na maisha yetu. Paulo aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake.” (Waefeso 4:25) Paulo aliandika hivi pia: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Nia yetu ya kuwa wanyoofu si kusifiwa na wanadamu wenzetu. Sisi ni wanyoofu kwa sababu tunamheshimu Muumba wetu na tunataka kumpendeza.

Usifiche Jinsi Ulivyo

Katika nchi nyingi, watu wana zoea la kuficha jinsi walivyo ili wapate faida maishani. Wanapata hati, diploma, na vitambulisho kwa njia ya uwongo ili waingie katika nchi kwa njia isiyo halali au ili wapate kazi au cheo ambacho hawastahili. Wazazi fulani wanaandika habari za uwongo kwenye vyeti vya kuzaliwa vya watoto wao ili watoto hao waendelee na masomo.

Hata hivyo, ili tumpendeze Mungu hatupaswi kuwa wadanganyifu. Biblia inasema kwamba Yehova ni “Mungu wa kweli” na kwamba anatarajia wale walio na uhusiano wa karibu pamoja naye waseme kweli. (Zaburi 31:5) Ikiwa tunataka kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, hatupaswi kuwaiga ‘watu wasiosema kweli,’ na wale ‘wanaoficha jinsi walivyo.’—Zaburi 26:4.

Ni kawaida pia kwa watu kuficha ukweli wanapojua kwamba watatiwa nidhamu kwa sababu ya kosa. Hata katika kutaniko la Kikristo, huenda mtu akashawishiwa kufanya hivyo. Kwa mfano, katika kutaniko moja, kijana mmoja aliwaambia wazee kwamba alitenda dhambi fulani. Hata hivyo, hakukubali kwamba aliiba hata ingawa kulikuwa na uthibitisho wa kwamba aliiba. Mwishowe, ukweli ulifunuliwa na hivyo akatengwa na ushirika wa kutaniko. Je, halingekuwa jambo la hekima kwake kuwa mnyoofu kabisa na kupokea msaada ili kurudisha uhusiano wake wenye thamani pamoja na Yehova? Kwa kweli, Biblia inasema: “Usiipuuze nidhamu kutoka kwa Yehova, wala usizimie wakati anapokurekebisha; kwa maana yeye ambaye Yehova anampenda, humtia nidhamu.”—Waebrania 12:5, 6.

Nyakati nyingine, huenda ndugu anayejaribu kufikia mapendeleo kutanikoni, akaficha matatizo ya kibinafsi au mwenendo mbaya wa zamani. Kwa mfano, anapojaza ombi la mapendeleo ya pekee ya utumishi, huenda asijibu kwa usahihi maswali yanayohusu afya na maadili huku akifikiri kwamba akisema ukweli kuhusu mambo hayo hatastahili. Huenda akafikiri, ‘Kwa kweli sikusema uwongo,’ lakini je, alisema kweli na kuwa mnyoofu kwa wengine? Fikiria hoja ya Methali 3:32: “Mtu mwenye hila ni chukizo kwa Yehova, lakini urafiki Wake uko pamoja na watu wanyoofu.”

Kwanza kabisa, kuwa mnyoofu kunamaanisha kutojidanganya mwenyewe. Mara nyingi, tunaamini yale tunayotaka kuamini badala ya yale yaliyo sawa au ya kweli. Jinsi ilivyo rahisi kwetu kuwalaumu wengine! Kwa mfano, Mfalme Sauli aliwalaumu wengine alipokuwa akijaribu kujitetea kwa kukosa kutii. Kwa sababu hiyo, Yehova alimkataa asiwe mfalme. (1 Samweli 15:20-23) Alikuwa tofauti sana na Mfalme Daudi aliyesali hivi kwa Yehova: “Mwishowe niliungama dhambi yangu kwako, wala sikufunika kosa langu. Nilisema: ‘Nitaungama makosa yangu kwa Yehova.’ Nawe mwenyewe ukanisamehe kosa la dhambi zangu.”—Zaburi 32:5.

Unyoofu Unaleta Baraka

Kuwa au kutokuwa mnyoofu kunawafanya watu wawe na maoni fulani juu yetu. Watu wakijua kwamba umewadanganya hata mara moja, wataacha kukuamini, na si rahisi wakuamini tena. Lakini ikiwa wewe ni mnyoofu na msema-kweli, utajulikana kuwa mtu mtimilifu anayestahili kutegemewa. Mashahidi wa Yehova wamejiletea sifa hiyo. Fikiria mifano fulani.

Mkurugenzi wa kampuni moja aligundua kwamba wafanyakazi wengi walikuwa wakiibia kampuni, hivyo basi, akawaomba polisi wafanye uchunguzi. Alipotambua kwamba mfanyakazi mmoja ambaye ni Shahidi wa Yehova alikuwa kati ya wale ambao walikuwa wamekamatwa, alienda kwenye kituo cha polisi na kuomba aachiliwe mara moja. Kwa nini? Kwa sababu mkurugenzi huyo alijua kwamba mtu huyo alikuwa mfanyakazi mnyoofu naye hakuwa na hatia. Shahidi huyo alirudishwa kazini huku wengine wakifutwa kazi. Mashahidi wenzake walifurahi, kwa sababu walijua kwamba mwenendo wake ulifanya jina la Yehova liheshimiwe.

Watu wanatambua mwenendo mzuri. Katika kijiji kimoja cha Afrika, daraja fulani lilihitaji kurekebishwa kwa sababu mbao kadhaa zilikuwa zimeibiwa. Wenyeji waliamua kukusanya pesa ili kununua mbao nyingine. Lakini, ni nani angeweza kutegemewa ili kutunza pesa hizo? Wote walikubaliana kwamba alipaswa kuwa Shahidi wa Yehova.

Nchi moja ya Afrika ilipokuwa na michafuko ya kisiasa na ya kikabila, Shahidi aliyekuwa akishughulikia hesabu katika kampuni moja ya kimataifa, alihamishwa na kampuni hiyo kwa kuwa maisha yake yalikuwa hatarini. Kampuni hiyo ilimlipia gharama ili afanye kazi kwa miezi mingi katika nchi nyingine hadi hali itulie. Kwa nini? Kwa sababu wakati fulani alikataa kushirikiana na watu ambao walikuwa wakipanga njama ya kuiibia kampuni. Wasimamizi walijua kwamba yeye ni mtu mnyoofu kabisa. Je, wangekubali kumsaidia mfanyakazi huyo ikiwa hakuwa mnyoofu?

Andiko la Methali 20:7 linasema hivi: “Mwadilifu anatembea kwa utimilifu wake.” Mtu mnyoofu ni mtu mtimilifu. Hasemi uwongo wala kuwadanganya wanadamu wenzake. Je, hungependa wengine wakutendee hivyo? Unyoofu ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli. Tunapokuwa wanyoofu tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu na jirani. Pia, tunaonyesha kwamba tunatamani kufuata kanuni hii ya mwenendo iliyotajwa na Yesu: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12; 22:36-39.

Wakati mwingine, kuwa mnyoofu kunaweza kumletea mtu matatizo, lakini ni afadhali kupata matatizo na kubaki ukiwa na dhamiri njema. Mwishowe, tutapata faida kubwa sana kwa kuwa wanyoofu. Ukweli ni kwamba uhusiano pamoja na Yehova ni wenye thamani isiyo na kifani. Kwa nini tuharibu uhusiano huo kwa kutenda jambo lisilo la unyoofu ili tu tusipoteze kibali cha watu au ili tupate faida kwa njia isiyo halali? Hata tukikabili tatizo gani, tunaweza kuwa na uhakika kwamba maneno haya ya mtunga-zaburi yatatimia: “Mwenye furaha ni mwanamume ambaye amemfanya Yehova kuwa tegemeo lake na ambaye hakuelekeza uso wake kwa watu wakaidi, wala kwa wale wanaogeukia uwongo.”—Zaburi 40:4.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wakristo wa kweli hawanunui wala kutumia hati za uwongo