Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tumtambue Mpinga-Kristo?

Kwa Nini Tumtambue Mpinga-Kristo?

Kwa Nini Tumtambue Mpinga-Kristo?

“Mmesikia kwamba mpinga-Kristo anakuja,” aliandika mtume Yohana ambaye aliongozwa kwa roho ya Mungu zamani za kale. (1 Yohana 2:18) Maneno hayo ni yenye kushangaza kama nini! Kwa karne nyingi, watu wamefikiria maana yake. Mpinga-Kristo ni nani? Atakuja wakati gani? Atafanya nini atakapokuja?

KWA miaka mingi wale ambao wameshutumiwa kuwa mpinga-Kristo ni wengi. Hapo zamani, wale walioitwa “mpinga-Kristo” walitia ndani Wayahudi, mapapa Wakatoliki, na watawala wa Roma. Kwa mfano, Maliki Frederick wa Pili (1194-1250) alipoamua kutojiunga na vita vya dini vya kutetea kanisa, Papa Gregory wa Tisa alimwita mpinga-Kristo na kumtenga na kanisa. Alitengwa pia na Innocent wa Nne, ambaye alichukua mahali pa Gregory. Naye Frederick akasema kwamba Innocent ndiye mpinga-Kristo.

Mtume Yohana ndiye mwandikaji pekee wa Biblia ambaye anatumia neno “mpinga-Kristo.” Katika barua mbili zinazoitwa kwa jina lake, neno hilo linaonekana mara tano likiwa kwa umoja au kwa wingi. Mistari yenye neno hilo inaonyeshwa katika sanduku kwenye ukurasa unaofuata. Kutokana na mistari hiyo, tunaweza kuona kwamba mpinga-Kristo ni mwongo na mdanganyifu, ambaye ameazimia kuharibu uhusiano wa mtu pamoja na Kristo na Mungu. Hivyo, mtume huyo aliwahimiza hivi Wakristo wenzake: “Wapendwa, msiamini kila neno lililoongozwa na roho, lakini yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu, kwa sababu manabii wengi wa uwongo wameingia ulimwenguni.”—1 Yohana 4:1.

Yesu pia alitoa onyo kuhusu wadanganyifu au manabii wa uwongo, aliposema hivi: “Wanakuja kwenu katika mavazi ya kondoo, lakini ndani wao ni mbwa-mwitu wenye kunyafua. Kwa matunda [au, matendo] yao mtawatambua.” (Mathayo 7:15, 16) Je, Yesu alikuwa akiwapa pia wafuasi wake onyo kuhusu mpinga-Kristo wa mfano? Acheni tuone jinsi tunavyoweza kumtambua mdanganyifu huyo mwovu.