Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maana ya Kumpenda Jirani Yetu

Maana ya Kumpenda Jirani Yetu

Maana ya Kumpenda Jirani Yetu

“Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.”—MATHAYO 22:39.

1. Tunaonyesha jinsi gani kwamba tunampenda Mungu?

YEHOVA anataka wale wanaomwabudu wafanye nini? Yesu alijibu swali hilo kwa maneno machache ambayo ni mazito sana. Alisema kwamba amri iliyo kuu ni kumpenda Yehova kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zetu zote. (Mathayo 22:37; Marko 12:30) Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu kama anavyotupenda kwa kumtii na kufuata amri zake. Wale wanaompenda Mungu hawaoni kufanya mapenzi yake kuwa mzigo mzito; wanafurahia kufanya mapenzi yake.—Zaburi 40:8; 1 Yohana 5:2, 3.

2, 3. Kwa nini tunapaswa kukazia uangalifu amri ya kumpenda jirani yetu, na ni maswali gani yanayotokea?

2 Yesu alisema kwamba amri ya pili iliyo kuu inahusiana na ya kwanza: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mathayo 22:39) Sasa tutazungumzia amri hiyo, na tuna sababu nzuri ya kufanya hivyo. Katika nyakati hizi zetu, watu wanaonyesha upendo wa kichoyo na uliopotoka. Katika maelezo yake yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu kuhusu “siku za mwisho,” mtume Paulo aliandika kwamba watu wangejipenda wenyewe badala ya kuwapenda wengine, wangependa pesa, na raha. Wengi ‘hawangekuwa na upendo wa asili’ au kama tafsiri moja ya Biblia inavyosema, “hawangekuwa na upendo wa kawaida kwa familia zao.” (2 Timotheo 3:1-4) Yesu Kristo alitabiri hivi: ‘Watu wengi watasalitiana na kuchukiana. Upendo wa walio wengi zaidi utapoa.’—Mathayo 24:10, 12.

3 Hata hivyo, ona kwamba Yesu hakusema kuwa upendo wa kila mtu ungepoa. Sikuzote kumekuwa na kutakuwa na watu wanaoonyesha upendo ambao Yehova anataka na anastahili. Wale wanaompenda Yehova kikweli watajitahidi kuwaona wengine kama Yehova anavyowaona. Lakini ni nani jirani yetu ambaye tunapaswa kumpenda? Tutaonyesha namna gani kwamba tunampenda jirani yetu? Maandiko yanaweza kutusaidia kujibu maswali hayo muhimu.

Jirani Yangu Ni Nani?

4. Kulingana na Mambo ya Walawi sura ya 19, Wayahudi walipaswa kuwapenda nani?

4 Alipomwambia Farisayo kwamba amri ya pili iliyo kuu ni kumpenda jirani kama unavyojipenda mwenyewe, Yesu alikuwa akizungumzia sheria hususa ambayo Waisraeli walipewa. Inapatikana katika Mambo ya Walawi 19:18. Katika sura hiyohiyo, Wayahudi waliambiwa kwamba walipaswa kuwaona wengine zaidi ya Waisraeli wenzao kuwa majirani wao. Mstari wa 34 unasema: “Mkaaji mgeni anayekaa akiwa mgeni pamoja nanyi atakuwa kwenu kama mwenyeji wenu; nawe utampenda kama wewe mwenyewe, kwa maana mlikuwa wakaaji wageni katika nchi ya Misri.” Kwa hiyo, hata watu wasio Wayahudi, hasa wale waliogeuzwa imani, walipaswa kutendewa kwa upendo.

5. Wayahudi walikuwa na maoni gani kuhusu kumpenda jirani?

5 Hata hivyo, viongozi wa Kiyahudi wa siku za Yesu, walikuwa na maoni tofauti kuhusu jambo hilo. Wengine kati yao walifundisha kwamba maneno “rafiki” na “jirani” yanawahusu Wayahudi tu. Watu wasio Wayahudi walipaswa kuchukiwa. Walimu hao walifundisha kwamba wale waliomwabudu Mungu walipaswa kuwadharau watu wasiomwabudu Mungu. Kitabu kimoja kinasema kwamba “katika hali kama hizo, chuki ilienea sana. Maoni hayo yalichochea chuki.”

6. Ni mambo gani mawili ambayo Yesu alikazia alipozungumza kuhusu kumpenda jirani?

6 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alizungumza kuhusu jambo hilo, akionyesha ni nani anayepaswa kutendewa kwa upendo. Alisema hivi: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Mpende jirani yako na kumchukia adui yako.’ Hata hivyo, mimi ninawaambia ninyi: Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni, kwa kuwa yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:43-45) Katika andiko hilo, Yesu alikazia mambo mawili. Kwanza, Yehova ni mkarimu na mwenye fadhili kwa watu wema na wabaya pia. Pili, tunapaswa kufuata mfano wake.

7. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Msamaria mwema?

7 Wakati mwingine, Myahudi fulani aliyejua sana Sheria alimuuliza Yesu hivi: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alimjibu kwa kumsimulia mfano wa Msamaria aliyempata mtu fulani Myahudi akiwa ameshambuliwa na wanyang’anyi na kuibiwa mali yake yote. Hata ingawa Wayahudi kwa ujumla waliwadharau Wasamaria, Msamaria huyo alifunga majeraha ya mtu huyo na kumpeleka kwenye nyumba ya wageni ili apate nafuu. Tunajifunza nini? Upendo wetu kwa jirani unapaswa kuelekezwa kwa watu wengine ambao si wa jamii, taifa, au dini yetu.—Luka 10:25, 29, 30, 33-37.

Maana ya Kumpenda Jirani Yetu

8. Kulingana na Mambo ya Walawi sura ya 19, upendo ulipaswa kuonyeshwa jinsi gani?

8 Kumpenda jirani, kama vile kumpenda Mungu, si hisia tu; ni jambo linaloonyeshwa kwa matendo. Inafaa kuchunguza mistari mingine inayozunguka amri iliyoandikwa katika Mambo ya Walawi sura ya 19 ambayo inawahimiza watu wa Mungu wampende jirani yao kama wanavyojipenda wenyewe. Tunasoma kwamba Waisraeli waliamriwa wawaruhusu watu wenye kuteseka na wakaaji wageni washiriki katika mavuno. Hawakupaswa kuwaibia, kuwadanganya, au kuwatendea isivyo haki. Waisraeli hawakupaswa kuonyesha ubaguzi katika mambo ya kihukumu. Ingawa walipaswa kukaripia wakosaji ilipohitajiwa, waliagizwa hivi waziwazi: “Usimchukie ndugu yako moyoni mwako.” Amri hiyo na nyingine nyingi zilijumlishwa kwa maneno haya: “Mpende mwenzako kama wewe mwenyewe.”—Mambo ya Walawi 19:9-11, 15, 17, 18.

9. Kwa nini Yehova aliwaamuru Waisraeli wajitenge na mataifa mengine?

9 Ingawa Waisraeli walipaswa kuwapenda wengine, walipaswa pia kujitenga na watu ambao waliabudu miungu ya uwongo. Yehova aliwaonya kuhusu hatari na matokeo ya kuwa na mashirika mabaya. Kwa mfano, Yehova aliamuru hivi kuhusu mataifa ambayo Waisraeli wangemiliki nchi zao: “Usifanye mapatano yoyote ya ndoa pamoja nao. Binti yako usimpe mwana wake, wala binti yake usimchukue kwa ajili ya mwana wako. Kwa maana atamgeuza mwana wako aache kunifuata, nao watatumikia miungu mingine; na hasira ya Yehova itawaka kwelikweli juu yenu.”—Kumbukumbu la Torati 7:3, 4.

10. Tunapaswa kujilinda na nini?

10 Vivyo hivyo, Wakristo wanapaswa kujilinda wasiwe na mahusiano na watu ambao wanaweza kudhoofisha imani yao. (1 Wakorintho 15:33) Tunaonywa hivi: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini,” wale ambao si sehemu ya kutaniko la Kikristo. (2 Wakorintho 6:14) Kwa kuongezea, Wakristo wanashauriwa waoe “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Lakini, hatupaswi kamwe kuwadharau wale ambao hawamwamini Yehova kama sisi. Kristo alikufa kwa ajili ya watenda-dhambi, na wengi waliozoea kutenda mambo maovu walibadili njia zao na kupatanishwa na Mungu.—Waroma 5:8; 1 Wakorintho 6:9-11.

11. Ni njia gani bora zaidi ya kuwaonyesha upendo wale wasiomtumikia Yehova, na kwa nini?

11 Njia bora zaidi ya kuwaonyesha upendo wale wasiomtumikia Mungu ni kumwiga Yehova mwenyewe. Hata ingawa hapendi uovu, Mungu anawaonyesha wote fadhili zenye upendo kwa kuwapa nafasi ya kuacha njia zao mbaya na kupata uzima wa milele. (Ezekieli 18:23) Yehova “hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Ni mapenzi yake kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Ndiyo sababu Yesu aliwatuma wafuasi wake wahubiri na kufundisha na ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 28:19, 20) Tunaposhiriki katika kazi hiyo, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu na jirani, ndiyo, hata maadui wetu!

Kuwapenda Ndugu Zetu Wakristo

12. Mtume Yohana aliandika nini kuhusu kumpenda ndugu yetu?

12 Mtume Paulo aliandika hivi: “Tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Tukiwa Wakristo, tuna wajibu wa kuwapenda waamini wenzetu, ndugu na dada zetu wa kiroho. Upendo huo ni muhimu kadiri gani? Akikazia jambo hilo muhimu, mtume Yohana aliandika hivi: “Kila mtu anayemchukia ndugu yake ni muuaji . . . Yeyote akisema: ‘Mimi nampenda Mungu,’ na bado anamchukia ndugu yake, yeye ni mwongo. Kwa maana yeye ambaye hampendi ndugu yake, ambaye amemwona, hawezi kuwa anampenda Mungu, ambaye hajamwona.” (1 Yohana 3:15; 4:20) Hayo ni maneno mazito. Yesu Kristo alisema kwamba Shetani Ibilisi ni “muuaji” na “mwongo.” (Yohana 8:44) Hatungependa kamwe tuitwe hivyo!

13. Ni katika njia gani tunaweza kuwaonyesha waamini wenzetu upendo?

13 Wakristo wa kweli ‘wanafundishwa na Mungu kupendana.’ (1 Wathesalonike 4:9) Tunapaswa kupendana “si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yohana 3:18) Upendo wetu unapaswa kuwa “bila unafiki.” (Waroma 12:9) Upendo unatuchochea kuwa wenye fadhili, huruma, wenye kusamehe, na wastahimilivu, lakini si wenye wivu, wenye kujigamba, wenye kiburi, au wenye ubinafsi. (1 Wakorintho 13:4, 5; Waefeso 4:32) Upendo unatuchochea ‘kutumikiana.’ (Wagalatia 5:13) Yesu aliwaambia wanafunzi wake wapendane kama alivyowapenda. (Yohana 13:34) Kwa hiyo, Mkristo anapaswa kuwa tayari hata kufa kwa ajili ya waamini wenzake, ikiwa ni lazima.

14. Tunaweza kuonyesha upendo katika familia kwa njia gani?

14 Upendo unapaswa kuonyeshwa hasa katika familia ya Kikristo na kati ya mume na mke. Kifungo cha ndoa ni cha karibu sana hivi kwamba Paulo alisema hivi: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” Akaongezea hivi: “Yeye anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe.” (Waefeso 5:28) Paulo anarudia himizo hilo mistari mitano baadaye. Mume anayempenda mke wake hatakuwa kama Waisraeli wa siku za Malaki ambao waliwatendea wake zao kwa hila. (Malaki 2:14) Atamthamini sana. Atampenda kama Kristo alivyolipenda kutaniko. Pia, upendo utamchochea mke amheshimu mume wake.—Waefeso 5:25, 29-33.

15. Watu fulani walisema na kufanya nini walipoona upendo wa kindugu ukionyeshwa kwa matendo?

15 Ni wazi kwamba upendo wa aina hiyo unawatambulisha Wakristo wa kweli. Yesu alisema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Tunapopendana, tunavuta watu kwa Mungu ambaye tunampenda na kumwakilisha. Kwa mfano, ona ripoti hii kuhusu familia moja ya Mashahidi kutoka Msumbiji. “Hatujawahi kamwe kuona jambo kama hili. Wakati wa mchana, upepo wenye nguvu ulianza kuvuma ukifuatana na mvua nzito ya mawe. Upepo huo wenye nguvu uliharibu nyumba yetu iliyojengwa kwa matete, kisha ukang’oa mabati ya paa. Ndugu zetu kutoka makutaniko jirani walipokuja na kutusaidia kujenga upya nyumba yetu, jirani yetu aliyeshangaa alisema hivi: ‘Dini yenu ni nzuri sana. Hatujawahi kamwe kusaidiwa hivi na kanisa letu.’ Tulifungua Biblia na kuwaonyesha Yohana 13:34, 35. Sasa majirani wetu wengi wanajifunza Biblia.”

Kumpenda Mtu Mmoja-Mmoja

16. Kuna tofauti gani kati ya kupenda kikundi cha watu na kumpenda mtu mmoja-mmoja?

16 Si vigumu kuwapenda majirani wetu kwa ujumla, wakiwa kikundi. Hata hivyo, ni vigumu zaidi kumpenda mtu mmoja-mmoja. Kwa mfano, watu fulani wanaonyesha upendo wao kwa jirani kwa kutoa tu michango kwa mashirika ya misaada. Kwa wazi, ni rahisi zaidi kusema kwamba tunampenda jirani yetu kuliko kumpenda mfanyakazi mwenzetu ambaye anaonekana hatujali, au mtu mwenye kusumbua anayeishi karibu nasi, au rafiki anayetuvunja moyo.

17, 18. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba alimpenda mtu mmoja-mmoja, na alifanya hivyo akiwa na nia gani?

17 Kuhusu kumpenda mtu mmoja-mmoja, tunajifunza kutoka kwa Yesu, ambaye alionyesha sifa za Mungu kwa ukamilifu. Ingawa alikuja duniani kuondoa dhambi ya ulimwengu, alimpenda mtu mmoja-mmoja, kama vile mwanamke mgonjwa, mtu mwenye ukoma, na mtoto. (Mathayo 9:20-22; Marko 1:40-42; 7:26, 29, 30; Yohana 1:29) Vivyo hivyo, tunaonyesha upendo kwa jirani yetu kwa jinsi tunavyoshughulika na watu mmoja-mmoja tunaokutana nao kila siku.

18 Lakini, hatupaswi kamwe kusahau kwamba kumpenda jirani kunahusiana na kumpenda Mungu. Ingawa Yesu aliwasaidia maskini, aliwaponya wagonjwa, na kuwalisha wenye njaa, nia yake ya kufanya mambo yote hayo na kuufundisha umati ilikuwa kuwasaidia watu wapatanishwe na Yehova. (2 Wakorintho 5:19) Yesu alifanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu, bila kusahau kwamba alimwakilisha na kuonyesha sifa za Mungu ambaye alimpenda. (1 Wakorintho 10:31) Kwa kuiga mfano wa Yesu, sisi pia tunaweza kuonyesha upendo wa kweli kwa jirani na wakati huohuo kuendelea kutokuwa sehemu ya ulimwengu wa wanadamu waovu.

Tunampenda Jirani Yetu Kama Sisi Wenyewe Jinsi Gani?

19, 20. Ni nini maana ya kumpenda jirani yetu kama sisi wenyewe?

19 Yesu alisema: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” Ni jambo la kawaida kujipenda na kujiheshimu kwa kiasi. Kama haingekuwa hivyo, amri hiyo haingekuwa na maana yoyote. Kujipenda kwa njia inayofaa hakupaswi kueleweka kimakosa kuwa ubinafsi kama inavyotajwa na mtume Paulo kwenye 2 Timotheo 3:2. Badala yake, ni kujiheshimu kwa usawaziko. Kuhusu sifa hiyo, msomi mmoja wa Biblia anaeleza kwamba “kujipenda kwa usawaziko si sawa na kujiona kuwa mtu bora kuliko wote au kujidharau na kujiona kuwa mtu asiyefaa kitu.”

20 Kuwapenda wengine kama tunavyojipenda wenyewe kunamaanisha kwamba tunawaona wengine kama tunavyotaka watuone na kuwatendea kama tunavyotaka watutendee. Yesu alisema: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Ona kwamba Yesu hakusema tufikirie sana yale ambayo wengine walitutendea zamani na kulipiza kisasi. Badala yake, tunapaswa kufikiria jinsi ambavyo tungependa watutendee na kisha tuwatendee vivyo hivyo. Ona pia kwamba Yesu hakusema tuwatendee hivyo marafiki na ndugu zetu tu. Alitumia neno “watu,” labda kuonyesha kwamba tunapaswa kuwatendea hivyo watu wote, yaani, kila mtu tunayekutana naye.

21. Tunapowapenda wengine tunaonyesha nini?

21 Kumpenda jirani kutatulinda tusitende maovu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Sheria zinazosema, ‘Usifanye uzinzi, Usiue, Usiibe, Usitamani,’ na amri nyingine yoyote iliyoko, zimejumlishwa katika neno hili, yaani, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Upendo haumfanyii uovu jirani.” (Waroma 13:9, 10) Upendo utatusukuma tutafute njia za kuwatendea wengine mema. Tunapowapenda wanadamu wenzetu, tunaonyesha kwamba tunampenda pia yule aliyemuumba mwanadamu kwa mfano wake, Yehova Mungu.—Mwanzo 1:26.

Ungejibuje?

• Tunapaswa kuwapenda nani, na kwa nini?

• Tunaweza kuwapenda jinsi gani wale wasiomtumikia Yehova?

• Biblia inaeleza nini kuhusu upendo ambao tunapaswa kuwaonyesha ndugu zetu?

• Ni nini maana ya kumpenda jirani yetu kama sisi wenyewe?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Yesu anampenda mtu mmoja-mmoja