Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Isaya—I

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Isaya—I

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Isaya—I

“NITAMTUMA nani, na ni nani atakayeenda kwa ajili yetu?” Yehova Mungu alipotoa mwaliko huo, Isaya mwana wa Amozi alijibu hivi: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isaya 1:1; 6:8) Baada ya kusema hivyo, anapokea mgawo wa kuwa nabii. Shughuli za Isaya akiwa nabii zimeandikwa katika kitabu cha Biblia kinachoitwa kwa jina lake.

Kitabu cha Isaya, ambacho kiliandikwa na nabii huyo kinazungumzia matukio ya miaka 46, kuanzia mwaka wa 778 K.W.K. hivi mpaka muda mfupi baada ya mwaka wa 732 K.W.K. Ingawa kitabu hicho kina matangazo ya hukumu juu ya Yuda, Israeli, na mataifa jirani, jambo kuu la kitabu hicho si hukumu. Badala yake, ni ‘wokovu wa Yehova Mungu.’ (Isaya 25:9) Kwa kweli, jina Isaya linamaanisha “Wokovu wa Yehova.” Makala hii itazungumzia mambo makuu katika Isaya 1:1–35:10.

“MABAKI WACHACHE WATARUDI”

(Isaya 1:1–12:6)

Biblia haisemi ikiwa ujumbe wa unabii ulio katika sura tano za kwanza za kitabu cha Isaya ulitolewa kabla au baada ya Isaya kuwekwa rasmi kuwa nabii. (Isaya 6:6-9) Hata hivyo, ni wazi kwamba Yuda na Yerusalemu yana ugonjwa wa kiroho “kuanzia wayo wa mguu mpaka kwenye kichwa.” (Isaya 1:6) Ibada ya sanamu imeenea. Viongozi ni wafisadi. Wanawake wamejaa kiburi. Watu hawamtumikii Mungu wa kweli kwa njia inayokubalika. Isaya anaagizwa aende na kuwaambia “tena na tena” watu ambao hawaelewi wala hawataki ujuzi wowote.

Majeshi ya muungano kutoka Israeli na Siria yanatisha kuvamia Yuda. Akimtumia Isaya na watoto wake “kama ishara na kama miujiza,” Yehova anahakikishia Yuda kwamba muungano wa Israeli na Siria hautafanikiwa. (Isaya 8:18) Hata hivyo, amani ya kudumu italetwa tu na utawala wa “Mkuu wa Amani.” (Isaya 9:6, 7) Pia Yehova atatoza hesabu Ashuru, taifa ambalo anatumia kama “fimbo ya hasira [yake].” Hatimaye, Yuda itapelekwa utekwani, lakini “mabaki wachache watarudi.” (Isaya 10:5, 21, 22) Kutakuwa na haki ya kweli chini ya utawala wa “tawi [la mfano ambalo] litatoka katika shina la Yese.”—Isaya 11:1.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:8, 9—Ni katika njia gani binti Sayuni “ameachwa akiwa amebaki kama kibanda katika shamba la mizabibu, kama kijumba cha mlinzi ndani ya shamba la matango”? Hilo linamaanisha kwamba wakati wa uvamizi wa Ashuru, Yerusalemu litaonekana kuwa dhaifu sana kama kibanda katika shamba la mizabibu au kijumba kinachoweza kuanguka kwa urahisi kilicho katika shamba la matango. Lakini Yehova analisaidia na hivyo haliruhusu liwe kama Sodoma na Gomora.

1:18—Ni nini maana ya maneno: “Sasa, njooni, nasi tunyooshe mambo kati yetu”? Huu si mwaliko wa kuwa na mazungumzo ya masikilizano. Badala yake, mstari huo unahusu kikao cha hukumu ambapo Hakimu mwadilifu, Yehova, anawapa Waisraeli nafasi ya kubadilika na kujitakasa wenyewe.

6:8a—Kwa nini maneno “nitamtuma” na “yetu” yanatumiwa katika mstari huu? Neno “nitamtuma” linamhusu Yehova Mungu. Neno “yetu” linaonyesha kwamba kuna mtu mwingine aliye pamoja na Yehova. Bila shaka, huyo ni ‘Mwana wake mzaliwa-pekee.’—Yohana 1:14; 3:16.

6:11—Isaya alimaanisha nini alipouliza: “Ni mpaka wakati gani, Ee Yehova?” Isaya hakuwa akiuliza angewatangazia kwa muda gani watu wasioitikia ujumbe wa Yehova. Badala yake, alitaka kujua ni kwa muda gani hali ya ugonjwa wa kiroho ya watu ingeendelea kufanya jina la Mungu lisiheshimiwe.

7:3, 4—Kwa nini Yehova alimwokoa Mfalme Ahazi mwovu? Wafalme wa Siria na Israeli walipanga kumwondoa Mfalme Ahazi wa Yuda kutoka kwenye kiti cha ufalme na badala yake kumweka mwana wa Tabeeli, ambaye hakuwa mzao wa Daudi, awe mfalme-kibaraka. Njama hiyo ya kishetani ingekatisha agano la Ufalme pamoja na Daudi. Yehova alimwokoa Ahazi ili kulinda uzao ambao kupitia huo “Mkuu wa Amani” aliyeahidiwa angetokea.—Isaya 9:6.

7:8—Efraimu ‘lilivunjwa jinsi gani vipande-vipande’ katika kipindi cha miaka 65? Kuhamishwa kwa watu wa ufalme wa makabila kumi, na nchi yao kukaliwa na wageni kulianza “katika siku za Peka mfalme wa Israeli,” punde tu baada ya Isaya kutoa unabii huo. (2 Wafalme 15:29) Kuliendelea kwa muda mrefu hadi siku za mfalme wa Ashuru Esar-hadoni, mwana wa Senakeribu ambaye alitawala baada yake. (2 Wafalme 17:6; Ezra 4:1, 2; Isaya 37:37, 38) Inaelekea kwamba hali hiyo ya Waashuru kuwahamisha watu kwenda na kutoka Samaria ilichukua miaka 65 inayotajwa kwenye Isaya 7:8.

11:1, 10—Yesu Kristo anaweza kuwa ‘tawi kutoka katika kisiki cha Yese’ na pia “mzizi wa Yese” kwa njia gani? (Waroma 15:12) Yesu alitoka “katika kisiki cha Yese” kwa njia ya kimwili. Alikuwa mzao wa Yese kupitia Daudi mwana wa Yese. (Mathayo 1:1-6; Luka 3:23-32) Hata hivyo, mamlaka ya kifalme ambayo Yesu anapokea inabadili uhusiano wake na mababu zake wa kale. Kwa kuwa amepewa nguvu na mamlaka ya kuwapa wanadamu watiifu uzima wa milele hapa duniani, Yesu anakuwa ‘Baba yao wa Milele.’ (Isaya 9:6) Hivyo, yeye pia ni “mzizi” wa mababu zake, kutia ndani Yese.

Mambo Tunayojifunza:

1:3. Kukataa kuishi kulingana na matakwa ya Muumba wetu ni kuwa na ujuzi mdogo kuliko wa ng’ombe-dume au punda. Kwa upande mwingine, kusitawisha uthamini kwa mambo yote ambayo Yehova ametufanyia kutatuzuia tusijiendeshe bila uelewaji na kumwacha.

1:11-13. Sherehe za kinafiki za kidini na sala za kidesturi zinamchosha Yehova. Matendo na sala zetu zinapaswa kuchochewa na nia nzuri ya moyoni.

1:25-27; 2:2; 4:2, 3Utumwa na ukiwa wa Yuda ulipaswa kukoma baada ya mabaki wenye kutubu kurudi Yerusalemu na kurudisha ibada ya kweli. Yehova anawarehemu wakosaji wenye kutubu.

2:2-4. Tunaposhiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi tunawasaidia watu mmoja-mmoja kutoka katika mataifa mengi kujifunza njia za amani na kufuatia amani mtu na mwenzake.

4:4. Yehova ataondoa, au kusafisha, uchafu wa kiadili na hatia ya damu.

5:11-13. Mtu anayekosa kiasi na kujizuia katika kuchagua tafrija anakataa kutenda kupatana na ujuzi.—Waroma 13:13.

5:21-23. Ni lazima wazee Wakristo, au waangalizi waepuke kuwa “wenye hekima machoni pao wenyewe.” Wanahitaji pia kuwa na kiasi katika “kunywa divai” na wanapaswa kuepuka kuonyesha upendeleo.

11:3a. Mfano na mafundisho ya Yesu yanaonyesha kwamba kumwogopa Yehova kunaleta shangwe.

“YEHOVA ATAMWONYESHA YAKOBO REHEMA”

(Isaya 13:1–35:10)

Sura ya 13 hadi 23 ni matangazo ya hukumu juu ya mataifa. Hata hivyo, “Yehova atamwonyesha Yakobo rehema” kwa kuruhusu makabila yote ya Israeli yarudi nyumbani. (Isaya 14:1) Ujumbe wa kuharibiwa kwa Yuda ambao unapatikana katika sura ya 24 hadi 27 unaambatana na ahadi ya kurudishwa. Yehova anatangaza hasira yake juu ya “walevi wa Efraimu [Israeli]” kwa kufanya mapatano na Siria na juu ya “makuhani na manabii” wa Yuda kwa kutafuta kufanya mapatano pamoja na Ashuru. (Isaya 28:1, 7) Ole inatangazwa juu ya “Arieli [Yerusalemu]” kwa ‘kujitayarisha kushuka kwenda Misri’ ili kupata ulinzi. (Isaya 29:1; 30:1, 2) Hata hivyo, ukombozi unatabiriwa kwa watu mmoja-mmoja wanaomwamini Yehova.

Kama ‘mwana-simba mwenye manyoya shingoni anavyonguruma juu ya mawindo yake,’ Yehova atalinda “Mlima Sayuni.” (Isaya 31:4) Pia kuna ahadi hii: “Tazama! Mfalme atatawala kwa ajili ya uadilifu.” (Isaya 32:1) Huku tisho la Ashuru juu ya Yuda likiwafanya “wajumbe wa amani” walie kwa uchungu, Yehova anaahidi kwamba watu wake wataponywa, ‘watasamehewa kosa lao.’ (Isaya 33:7, 22-24) “Yehova ana hasira juu ya mataifa yote, na ghadhabu juu ya jeshi lao lote.” (Isaya 34:2) Yuda halitaachwa ukiwa. “Nyika na nchi isiyo na maji itafurahi; na nchi tambarare ya jangwani itakuwa na shangwe na kuchanua maua kama zafarani.”—Isaya 35:1.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

13:17—Ni kwa njia gani Wamedi waliona fedha kuwa si kitu na hawakupendezwa na dhahabu? Wamedi na Waajemi waliona utukufu wa kushinda kuwa muhimu zaidi kuliko nyara za vita. Ilikuwa hivyo kwa Koreshi, ambaye aliwapa wahamishwa waliokuwa wakirudi, vyombo vya dhahabu na fedha ambavyo Nebukadneza alipora katika hekalu la Yehova.

14:1, 2—Watu wa Yehova ‘waliwateka jinsi gani wale waliowashika mateka,’ na ‘kuwatiisha wale waliokuwa wakiwalazimisha kwenda kazini’? Hilo lilitimia kuhusiana na watu kama vile Danieli, ambao walikuwa na cheo cha juu huko Babiloni chini ya Wamedi na Waajemi; Esta, ambaye aliwekwa kuwa malkia wa Uajemi; na Mordekai, ambaye aliwekwa kuwa waziri mkuu wa Milki ya Uajemi.

20:2-5—Je, kweli Isaya alitembea akiwa uchi kabisa kwa miaka mitatu? Huenda Isaya alivua vazi lake la nje tu na kutembea akiwa “amejifunika kidogo.” Neno la Kiebrania lililotafsiriwa “uchi” laweza pia kumaanisha kutovaa kikamili au kuvaa nguo chache.—1 Samweli 19:24, maelezo ya chini katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

21:1—Ni eneo gani linaloitwa “nyika ya bahari”? Babiloni linaitwa hivyo hata ingawa halikuwa karibu na bahari halisi. Linaitwa hivyo kwa sababu maji ya mito Efrati na Tigri yalifurika katika eneo hilo kila mwaka na kutokeza “bahari” yenye matope.

24:13-16—Ni jinsi gani Wayahudi walipata kuwa “katikati ya vikundi vya watu, kama kupigwa kwa mzeituni, kama masalio wakati ukusanyaji wa zabibu umemalizika”? Kama vile matunda yanavyobaki kwenye mti au mzeituni baada ya mavuno, ni watu wachache tu ambao wangeokoka uharibifu wa Yerusalemu na Yuda. Popote ambapo waokokaji walihamishiwa, iwe ni katika “eneo la nuru [Babiloni upande wa Mashariki]” au “visiwa vya bahari [ya Mediterania],” wangemtukuza Yehova.

24:21—Ni nani “jeshi lililo juu” na “wafalme wa nchi”? “Jeshi lililo juu” linaweza kumaanisha jeshi la roho waovu. Hivyo, “wafalme wa nchi” ni watawala wa dunia ambao wanaongozwa na roho waovu walio na uvutano wenye nguvu.—1 Yohana 5:19.

25:7—“Kifuniko kinachovifunika vikundi vyote vya watu, na mfumo uliofumwa kwa kusokotana juu ya mataifa yote” ni nini? Ulinganifu huo unakazia maadui wawili wakubwa wa wanadamu, yaani, dhambi na kifo.

Mambo Tunayojifunza:

13:20-22; 14:22, 23; 21:1-9. Sikuzote, neno la Yehova la kinabii linatimia kama ilivyokuwa kuhusiana na Babiloni.

17:7, 8Ingawa wengi katika Israeli hawakusikiliza, watu mmoja-mmoja walimtafuta Yehova. Vivyo hivyo, watu fulani katika dini zinazodai kuwa za Kikristo wanakubali ujumbe wa Ufalme.

28:1-6. Israeli litashindwa na Ashuru, lakini Mungu atahakikisha kwamba watu waaminifu wataokoka. Hukumu za Yehova haziwaachi waadilifu bila tumaini.

28:23-29. Yehova anawarekebisha wanyoofu kulingana na mahitaji na hali zao hususa.

30:15. Ili tuokolewe na Yehova, tunapaswa kuonyesha imani kwa “kupumzika,” yaani, kuepuka kutafuta ukombozi kupitia mipango ya wanadamu. Kwa “kukaa bila usumbufu,” yaani, kutokuwa na woga, tunaonyesha kwamba tunategemea uwezo wa Yehova wa kutulinda.

30:20, 21. ‘Tunamwona’ Yehova na ‘kuisikia’ sauti yake ya wokovu kwa kutii yale anayosema kupitia Biblia, Neno lake ambalo limeongozwa kwa roho, na kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mathayo 24:45.

Unabii wa Isaya Unaimarisha Uhakika Wetu Katika Neno la Mungu

Tunashukuru kama nini kwa sababu ya ujumbe wa Mungu ulio katika kitabu cha Isaya! Unabii ambao tayari umetimia unaimarisha uhakika wetu kwamba ‘neno linalotoka katika kinywa cha Yehova halitarudi kwake bila matokeo.’—Isaya 55:11.

Namna gani unabii kumhusu Masihi kama ule ulio katika Isaya 9:7 na 11:1-5, 10? Je, hauimarishi imani yetu katika maandalizi ya Yehova ya kutuokoa? Pia, kitabu hicho kina unabii ambao unatimizwa hasa katika siku zetu au utatimizwa wakati ujao. (Isaya 2:2-4; 11:6-9; 25:6-8; 32:1, 2) Kwa kweli, kitabu cha Isaya kinathibitisha hata zaidi kwamba “neno la Mungu liko hai”!—Waebrania 4:12.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Isaya na watoto wake walikuwa “kama ishara na kama miujiza katika Israeli”

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Yerusalemu lingekuwa “kama kibanda katika shamba la mizabibu”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Watu kutoka katika mataifa wanasaidiwaje ‘kufua panga zao ziwe majembe’?