Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, Yesu alikosa heshima au fadhili kwa njia aliyozungumza na mama yake kwenye karamu ya arusi huko Kana?—Yohana 2:4.

Muda mfupi baada ya kubatizwa, Yesu na wanafunzi wake walialikwa kwenye karamu ya arusi huko Kana. Mama yake pia alikuwapo. Divai ilipokwisha, Maria alimwambia Yesu hivi: “Hawana divai.” Yesu alimjibu mama yake hivi: “Nina nini nawe, mwanamke? Saa yangu haijafika bado.”—Yohana 2:1-4.

Leo, inaelekea kwamba mtu yeyote anayemwita mama yake “mwanamke” na kumwambia “nina nini nawe?” angeonwa kuwa mtu asiye na heshima au hata mtukanaji. Lakini kumshutumu Yesu kwamba alikosa heshima au alimtukana mama yake kungekuwa kutojua utamaduni na njia ya kawaida ya kuzungumza ya watu wa wakati huo. Kuelewa matumizi ya maneno hayo katika nyakati za Biblia kutatusaidia sana.

Kamusi moja (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words) inasema hivi kuhusu neno “mwanamke”: “Neno hilo linapotumiwa mtu anapozungumza na mwanamke, si neno kali au la kukaripia, lakini ni neno la upendo au heshima.” Vichapo vingine vinaunga mkono wazo hilo. Kwa mfano, Biblia moja (The Anchor Bible) inasema: “Hilo si kemeo wala si neno lisilo na adabu, wala halionyeshi kwamba humpendi mtu huyo . . . Ilikuwa njia ya kawaida na yenye adabu ya Yesu ya kuzungumza na wanawake.” Kamusi nyingine (The New International Dictionary of New Testament Theology) inaeleza kwamba neno hilo “haliwezi kutumiwa kwa njia yoyote isiyo ya adabu.” Nayo kamusi ya Gerhard Kittel (Theological Dictionary of the New Testament) inasema kwamba matumizi hayo “hayakosi kamwe adabu wala heshima.” Hivyo, hatupaswi kukata kauli kwamba Yesu alikosa heshima au fadhili kwa mama yake alipomwita “mwanamke.”—Mathayo 15:28; Luka 13:12; Yohana 4:21; 19:26; 20:13, 15.

Namna gani maneno “nina nini nawe?” Inaonekana huo ni usemi wa mfano uliotumiwa kwa kawaida na Wayahudi na unapatikana mara kadhaa katika Biblia. Kwa mfano, katika 2 Samweli 16:10, Daudi anasema hivi ili kumzuia Abishai asimuue Shimei: “Nina nini nanyi, enyi wana wa Seruya? Mwacheni alaani hivyo, kwa sababu Yehova amemwambia, ‘Mlaani Daudi!’” Vivyo hivyo, katika 1 Wafalme 17:18 tunasoma kwamba mjane wa Sarefathi, alipompata mwana wake amekufa, alimwambia Eliya: “Nina nini nawe, Ee mtu wa Mungu wa kweli? Umekuja kwangu ili kurudisha kumbukumbu la kosa langu na kumuua mwanangu.”

Kutokana na mifano hiyo ya Biblia, tunaweza kuona kwamba mara nyingi maneno “nina nini nawe?” hayatumiwi kuonyesha dharau au kiburi, bali yanatumiwa mtu anapokataa kushiriki katika jambo fulani lililopendekezwa au lisilopatana na maoni yake. Basi tunaweza kusema nini kuhusu maneno ambayo Yesu alimwambia Maria?

Maria alipomwambia Yesu “hawana divai,” inaelekea hakuwa akimjulisha tu Yesu jambo hilo, bali alikuwa anapendekeza Yesu atatue tatizo hilo. Yesu alitumia usemi huo wa kawaida kukataa pendekezo la werevu la Maria, na maneno “Saa yangu haijafika bado,” yanatusaidia kuelewa sababu ya kukataa kufanya hivyo.

Kuanzia wakati alipobatizwa na kutiwa mafuta mwaka wa 29 W.K., Yesu alijua vizuri kwamba mapenzi ya Yehova kumhusu akiwa Masihi aliyeahidiwa yalikuwa kuishi maisha ya utimilifu ambayo yangeongoza kwenye kifo, ufufuo, na kutukuzwa kwake. Alisema hivi: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Wakati wa kifo chake ulipokaribia, Yesu alisema hivi waziwazi: “Saa imekuja.” (Yohana 12:1, 23; 13:1) Kwa hiyo, katika sala aliyotoa usiku uliotangulia kifo chake, Yesu alisema: “Baba, saa imefika; mtukuze mwana wako, ili mwana wako apate kukutukuza wewe.” (Yohana 17:1) Na mwishowe, umati ulipofika ili kumkamata katika bustani ya Gethsemane, Yesu aliwaamsha mitume wake kutoka usingizini na kusema: “Saa imekuja! Tazama! Mwana wa binadamu anasalitiwa na kutiwa katika mikono ya watenda-dhambi.”—Marko 14:41.

Hata hivyo, wakati wa arusi huko Kana, Yesu alikuwa ameanza tu huduma yake akiwa Masihi na “saa” yake ilikuwa bado haijafika. Kusudi lake kuu lilikuwa kufanya mapenzi ya Baba yake kwa njia na kwa wakati ambao Baba yake alielekeza, na hakuna mtu yeyote ambaye angezuia azimio lake. Yesu alimwonyesha mama yake jambo hilo kwa uthabiti, lakini bila shaka, hakukosa heshima wala fadhili. Maria hakuhisi kwamba ameaibishwa au kutukanwa na mwana wake. Kwa kweli, akiwa ameelewa jibu la Yesu, Maria aliwaambia hivi wale waliokuwa wakihudumu kwenye arusi hiyo: “Lolote atakalowaambia, fanyeni.” Badala ya kumpuuza mama yake, Yesu alifanya muujiza wake wa kwanza akiwa Masihi kwa kugeuza maji kuwa divai bora, na hivyo akaonyesha usawaziko mzuri kwa kufanya mapenzi ya Baba yake na kufanya yale ambayo mama yake alitaka.—Yohana 2:5-11.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Yesu alizungumza na mama yake kwa fadhili lakini kwa uthabiti