Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mpende Mungu Anayekupenda

Mpende Mungu Anayekupenda

Mpende Mungu Anayekupenda

“Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.”—MATHAYO 22:37.

1, 2. Inaelekea ni nini kilichowachochea watu waulize swali kuhusu amri iliyo kuu?

INAELEKEA swali lililoulizwa lilisababisha ubishi mkali kati ya Mafarisayo wa siku za Yesu. Kati ya sheria zaidi ya 600 ambazo zilifanyiza Sheria ya Musa, ni sheria gani iliyokuwa muhimu zaidi? Je, ilikuwa sheria iliyohusu dhabihu? Kwa kweli, dhabihu zilitolewa ili kupata msamaha wa dhambi na kumshukuru Mungu. Au je, sheria iliyokuwa muhimu zaidi ilikuwa sheria ya kutahiriwa? Sheria hiyo pia ilikuwa muhimu kwa sababu kutahiriwa kulikuwa ni ishara ya agano ambalo Yehova alifanya pamoja na Abrahamu.—Mwanzo 17:9-13.

2 Kwa upande mwingine, inaelekea watu wasiopenda mabadiliko walidai kwamba lingekuwa kosa kuinua sheria moja juu ya nyingine kwa kuwa kila sheria ambayo Mungu alitoa ilikuwa muhimu, hata ingawa sheria nyingine hazikuonekana kuwa muhimu sana. Mafarisayo waliamua kumuuliza Yesu swali hilo la ubishi. Huenda angesema jambo fulani ambalo lingeharibu sifa yake. Mmoja wao alimfikia Yesu na kumuuliza: “Amri iliyo kuu katika ile Sheria ni gani?”—Mathayo 22:34-36.

3. Yesu alisema ni amri gani iliyo kuu zaidi?

3 Jibu ambalo Yesu alitoa ni la maana sana kwetu leo. Katika jibu lake, alizungumzia kwa ufupi jambo ambalo daima lilikuwa muhimu zaidi katika ibada ya kweli wakati huo na hata leo. Akitaja maneno ya Kumbukumbu la Torati 6:5, Yesu alisema: “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza.” Ingawa Farisayo huyo aliuliza kuhusu amri moja tu, Yesu alimtajia amri nyingine. Akitaja maneno ya Mambo ya Walawi 19:18, Yesu alisema hivi: “Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’” Kisha, Yesu akaonyesha kwamba amri hizo mbili ndizo zilizokuwa muhimu zaidi katika ibada safi. Ili kuwazuia wasimwambie ataje zile sheria nyingine kulingana na umuhimu wake, Yesu alimalizia hivi: “Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.” (Mathayo 22:37-40) Katika makala hii, tutazungumzia amri kuu zaidi kati ya hizo mbili. Kwa nini ni lazima tumpende Mungu? Tunaonyesha jinsi gani kwamba tunampenda Mungu? Na tunaweza kusitawisha upendo huo kwa njia gani? Ni muhimu kujua majibu ya maswali hayo kwa sababu ili tumpendeze Yehova, ni lazima tumpende kwa moyo, nafsi, na akili yetu yote.

Umuhimu wa Upendo

4, 5. (a) Kwa nini Farisayo hakushangazwa na maneno ya Yesu? (b) Ni nini kilicho na thamani zaidi kwa Mungu kuliko dhabihu na matoleo?

4 Inaonekana kwamba yule Farisayo aliyemuuliza Yesu swali hakushtuka wala kushangazwa na jibu alilopewa. Alijua kwamba kumpenda Mungu ni jambo muhimu katika ibada ya kweli, ingawa wengi hawakuonyesha upendo huo. Katika masinagogi, kulikuwa na desturi ya kurudia-rudia kwa sauti sala ya Shema, au ungamo la imani, ambalo lilitia ndani maneno ya Kumbukumbu la Torati 6:4-9, andiko ambalo Yesu alizungumzia. Kulingana na simulizi la Marko, Farisayo huyo alimwambia Yesu hivi: “Mwalimu, umesema vema kupatana na kweli, ‘Yeye ni Mmoja, na hakuna mwingine ila Yeye’; na jambo hili la mtu kumpenda yeye kwa moyo wote na kwa uelewaji wote na kwa nguvu zote na mtu kumpenda jirani kama yeye mwenyewe ni bora zaidi kuliko matoleo yote mazima ya kuteketezwa na dhabihu zote.”—Marko 12:32, 33.

5 Kwa kweli, ingawa watu waliamriwa na Sheria kutoa matoleo na dhabihu za kuteketezwa, Mungu anathamini zaidi watumishi wake wanapochochewa na upendo kutoka moyoni. Shomoro mmoja aliyetolewa kwa Mungu kwa upendo na kwa ujitoaji alikuwa mwenye thamani zaidi kwake kuliko maelfu ya kondoo-dume waliotolewa kwa nia mbaya. (Mika 6:6-8) Kumbuka simulizi la yule mjane maskini ambaye Yesu alimwona katika hekalu la Yerusalemu. Sarafu mbili ndogo alizotumbukiza ndani ya sanduku la hazina hazingeweza kununua hata shomoro mmoja. Hata hivyo, mchango huo uliotolewa kwa moyo uliochochewa na upendo kwa Yehova, ulikuwa wenye thamani zaidi kuliko michango mikubwa iliyotolewa na matajiri kutokana na ziada yao. (Marko 12:41-44) Inatia moyo kama nini kujua kwamba Yehova anathamini zaidi jambo ambalo sote tunaweza kufanya, yaani, kumpenda, haidhuru hali zetu!

6. Paulo aliandika nini kuhusu umuhimu wa upendo?

6 Akikazia umuhimu wa upendo katika ibada ya kweli, mtume Paulo aliandika hivi: “Nikisema kwa lugha za wanadamu na za malaika lakini sina upendo, nimekuwa chombo cha shaba nyeupe kinachovuma au toazi linalolia. Na ikiwa nina zawadi ya kutoa unabii nami nazijua siri takatifu zote na ujuzi wote, na ikiwa nina imani yote kuweza kuhamisha milima, lakini sina upendo, mimi si kitu. Nami nikitoa mali zangu zote ili kuwalisha wengine, nami nikiutoa mwili wangu, ili nijisifu, lakini sina upendo, sipati faida hata kidogo.” (1 Wakorintho 13:1-3) Ni wazi kwamba ili ibada yetu impendeze Mungu ni lazima tuwe na upendo. Lakini tunaonyesha kwa njia gani kwamba tunampenda Yehova?

Jinsi Tunavyoonyesha Tunampenda Yehova

7, 8. Tunaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tunampenda Yehova?

7 Watu wengi wanaamini kwamba upendo ni hisia ambayo hatuwezi kuizuia; wanasema kuhusu upendo wa kimahaba. Hata hivyo, upendo wa kweli si hisia tu. Upendo huo unaonyeshwa kwa matendo wala si kwa hisia. Biblia inasema upendo ni “njia iliyo bora zaidi” na ni sifa tunayopaswa ‘kufuatia.’ (1 Wakorintho 12:31; 14:1) Wakristo wanatiwa moyo wapende, “si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”—1 Yohana 3:18.

8 Kumpenda Mungu kunatuchochea kufanya mambo yanayompendeza na kutetea na kutegemeza enzi yake kuu, kwa maneno na kwa matendo. Kunatusukuma tuepuke kuupenda ulimwengu na njia zake ambazo hazimpendezi Mungu. (1 Yohana 2:15, 16) Wale ambao wanampenda Mungu wanachukia yaliyo mabaya. (Zaburi 97:10) Kumpenda Mungu kunatia ndani pia kumpenda jirani, jambo ambalo tutazungumzia katika makala inayofuata. Zaidi ya hayo, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu kwa kumtii. Biblia inasema hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.”—1 Yohana 5:3.

9. Yesu alionyesha kwa njia gani upendo wake kwa Mungu?

9 Yesu alionyesha kwa njia kamilifu maana ya kumpenda Mungu. Upendo ulimsukuma aache makao yake ya mbinguni na kuishi duniani akiwa mwanadamu. Ulimchochea amtukuze Baba yake kwa mambo aliyotenda na kufundisha. Upendo ulimsukuma awe “mtiifu mpaka kifo.” (Wafilipi 2:8) Utii huo ambao ulionyesha upendo wake, uliwafungulia watu waaminifu njia ya kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu. Paulo aliandika hivi: “Kupitia kutotii kwa mtu mmoja [Adamu] wengi walifanywa watenda-dhambi, vivyo hivyo pia kupitia kutii kwa mtu mmoja [Kristo Yesu] wengi watafanywa kuwa waadilifu.”—Waroma 5:19.

10. Kwa nini kumpenda Mungu kunatia ndani kumtii?

10 Kama Yesu, tunaonyesha upendo wetu kwa kumtii Mungu. Mtume Yohana aliyependwa sana na Yesu aliandika hivi: “Upendo unamaanisha hivi, kwamba tuendelee kutembea kulingana na amri zake.” (2 Yohana 6) Wale ambao wanampenda Yehova kikweli wanatamani kufuata mwongozo wake. Wakitambua kwamba hawawezi kuongoza hatua zao wenyewe kwa mafanikio, wanategemea hekima ya Mungu na wanajitiisha chini ya mwongozo wake wenye upendo. (Yeremia 10:23) Wao ni kama Waberoya wa kale waliokuwa wasikivu ambao walikubali ujumbe wa Mungu kwa “hamu kubwa zaidi ya akili,” wakitamani sana kufanya mapenzi ya Mungu. (Matendo 17:11) Walichunguza Maandiko kwa uangalifu ili waelewe mapenzi ya Mungu kwa ukamili zaidi, jambo ambalo liliwasaidia kuonyesha upendo wao kwa matendo zaidi ya utii.

11. Ni nini maana ya kumpenda Mungu kwa moyo, akili, nafsi, na nguvu zetu zote?

11 Kama Yesu alivyosema, tunapaswa kumpenda Mungu kwa moyo, akili, nafsi, na nguvu zetu zote. (Marko 12:30) Upendo kama huo unatoka moyoni, unahusisha hisia, tamaa, na mawazo yetu ya ndani, nasi tunatamani sana kumpendeza Yehova. Pia, tunampenda kwa akili yetu. Ujitoaji wetu unategemea ujuzi; tumemjua Yehova, yaani, sifa zake, viwango vyake, na makusudi yake. Tunatumia nafsi yetu, mwili wetu wote na uhai tulio nao, kumtumikia na kumsifu. Vilevile, tunatumia nguvu zetu kufanya hivyo.

Kwa Nini Tunapaswa Kumpenda Yehova?

12. Kwa nini Mungu anataka tumpende?

12 Sababu moja ya kumpenda Yehova ni kwamba yeye anataka tuonyeshe sifa zake. Mungu ndiye chanzo na mfano bora zaidi wa upendo. Mtume Yohana aliandika hivi akiongozwa kwa roho: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Wanadamu waliumbwa kwa mfano wa Mungu; tuliumbwa tukiwa na uwezo wa kuonyesha upendo. Kwa kweli, enzi kuu ya Yehova inategemea upendo. Anataka kutumikiwa na watu ambao wanapenda na wanatamani utawala wake wa uadilifu. Kwa hakika, upendo ni muhimu ili kuwe na amani na upatano katika uumbaji wote.

13. (a) Kwa nini Waisraeli waliambiwa: “Umpende Yehova Mungu wako”? (b) Kwa nini ni jambo linalopatana na akili kwamba Yehova anatutazamia tumpende?

13 Sababu nyingine ya kumpenda Yehova ni kwamba tunathamini yale ambayo ametufanyia. Kumbuka kwamba Yesu aliwaambia hivi Wayahudi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako.” Hawakutazamiwa wampende mungu fulani aliye mbali na asiyejulikana. Walipaswa kumpenda Mungu ambaye alikuwa amefunua upendo wake kwao. Yehova alikuwa Mungu wao. Yeye Ndiye aliyewatoa Misri na kuwaingiza Nchi ya Ahadi, Ndiye aliyewalinda, kuwategemeza, na kuwapenda, naye Ndiye aliyewatia nidhamu kwa upendo. Leo pia, Yehova ni Mungu wetu, yeye ndiye aliyemtoa Mwana wake awe fidia ili tupate uzima wa milele. Ni jambo linalopatana na akili kwamba Yehova anatutazamia tumpende kama anavyotupenda! Upendo wake unatuchochea tumpende; tunatakiwa kumpenda Mungu anayetupenda. Tunampenda Yule ambaye “alitupenda sisi kwanza.”—1 Yohana 4:19.

14. Upendo wa Yehova ni kama upendo wa mzazi katika njia gani?

14 Yehova anawapenda wanadamu kama mzazi mwenye upendo anavyowapenda watoto wake. Ingawa si wakamilifu, wazazi wenye upendo wanafanya kazi kwa bidii kwa miaka mingi ili kuwatunza watoto wao, na wanajitoa sana kimwili na kwa njia nyinginezo. Wazazi wanawafundisha, wanawatia moyo, na kuwatia nidhamu watoto wao kwa sababu wanataka wapate furaha na mafanikio. Nao wazazi wanataka watoto wafanye nini? Wanataka watoto wao wawapende na kutia moyoni yale ambayo wamewafundisha ili wafaidike. Je, si jambo linalopatana na akili kwamba Baba yetu wa mbinguni aliye mkamilifu anatazamia tuonyeshe upendo na tuthamini yote ambayo ametufanyia?

Kukuza Upendo Kuelekea Mungu

15. Ili kusitawisha upendo kwa Mungu ni lazima kwanza tufanye nini?

15 Hatujamwona Mungu wala kusikia sauti yake wakati wowote. (Yohana 1:18) Hata hivyo, anatukaribisha tuwe na uhusiano wenye upendo pamoja naye. (Yakobo 4:8) Tunaweza kufanya hivyo kwa njia gani? Ili kumpenda mtu yeyote ni lazima kwanza umjue; ni vigumu kumpenda kabisa mtu ambaye hatumjui. Yehova ametupa Neno lake, Biblia, ili tujifunze kumhusu. Ndiyo sababu Yehova, kupitia tengenezo lake, anatutia moyo tusome Biblia kwa ukawaida. Biblia ndiyo inayotufundisha kumhusu Mungu, sifa zake, utu wake, na pia matendo yake kuhusiana na wanadamu kwa maelfu ya miaka. Tunapotafakari juu ya masimulizi hayo, tunamthamini na kumpenda zaidi.—Waroma 15:4.

16. Kutafakari kuhusu huduma ya Yesu kunaongeza jinsi gani upendo wetu kwa Mungu?

16 Njia nzuri zaidi ya kukuza upendo wetu kwa Yehova ni kutafakari kuhusu maisha na huduma ya Yesu. Kwa kweli, Yesu alimwiga Baba yake kwa ukamili sana hivi kwamba alisema: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Je, si kweli kwamba moyo wako unaguswa na huruma ambayo Yesu alionyesha kwa kumfufua mwana wa pekee wa mjane? (Luka 7:11-15) Je, haipendezi kujua kwamba Mwana wa Mungu, ambaye ndiye mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, aliwaosha wanafunzi wake miguu kwa unyenyekevu? (Yohana 13:3-5) Je, huchochewi kujua kwamba watu wote, kutia ndani watoto waliweza kumfikia Yesu kwa urahisi hata ingawa alikuwa mtu mkuu na mwenye hekima zaidi kuliko mtu mwingine yeyote? (Marko 10:13, 14) Tunapotafakari na kuthamini mambo hayo, tunakuwa kama Wakristo ambao Petro aliandika hivi kuwahusu: “Ninyi mnampenda, ingawa hamkumwona [Yesu] kamwe.” (1 Petro 1:8) Kadiri upendo wetu kwa Yesu unavyoongezeka, ndivyo upendo wetu kwa Yehova utakavyoongezeka.

17, 18. Upendo wetu kwa Yehova unaweza kukua tukitafakari kuhusu mambo gani ambayo ametuandalia kwa upendo?

17 Njia nyingine tunayoweza kukuza upendo wetu kwa Mungu ni kutafakari kuhusu mambo mengi ambayo ametuandalia kwa upendo ili tufurahie maisha, kama vile uzuri wa uumbaji, vyakula vingi sana vitamu, uhusiano mchangamfu wa marafiki wazuri, na pia vitu vingine vingi vizuri ambavyo vinatufurahisha na kuturidhisha. (Matendo 14:17) Jinsi tunavyoendelea kujifunza kuhusu Mungu wetu, ndivyo tunavyothamini zaidi wema na ukarimu wake mwingi sana. Fikiria mambo yote ambayo Yehova amekufanyia wewe binafsi. Je, si kweli kwamba unapaswa kumpenda?

18 Moja ya zawadi nyingi ambazo Mungu ametupa ni pendeleo la kumfikia katika sala wakati wowote huku tukijua kwamba “Msikiaji wa sala” anatusikiliza. (Zaburi 65:2) Yehova amempa Mwana wake mpendwa mamlaka ya kutawala na kuhukumu. Lakini, hajawapa wengine, wala Mwana wake, daraka la kusikiliza sala. Yeye mwenyewe anasikiliza sala zetu. Tunavutwa kumkaribia Yehova kwa sababu anampenda na kumhangaikia kila mmoja wetu.

19. Ni ahadi gani za Yehova ambazo zinatuvuta kwake?

19 Pia, tunavutwa kwa Yehova tunapotafakari kuhusu mambo ambayo anakusudia kuwafanyia wanadamu. Ameahidi kukomesha magonjwa, huzuni, na kifo. (Ufunuo 21:3, 4) Baada tu ya wanadamu kufanywa kuwa wakamilifu, hakuna mtu atakayeshuka moyo, kuvunjika moyo, au kupata msiba. Njaa, umaskini, na vita havitakuwapo tena. (Zaburi 46:9; 72:16) Dunia itageuzwa kuwa paradiso. (Luka 23:43) Yehova ataleta baraka hizo kwa sababu anatupenda, wala si kwa sababu analazimika kufanya hivyo.

20. Musa alisema kuna faida gani ya kumpenda Yehova?

20 Kwa hiyo, kuna sababu nzuri sana zinazotufanya tumpende Mungu wetu na kuukuza upendo huo. Je, utaendelea kuimarisha upendo wako kwa Mungu, na kumruhusu aongoze njia zako? Uamuzi ni wako. Musa alijua faida za kukuza na kudumisha upendo kwa Yehova. Musa aliwaambia hivi Waisraeli wa kale: “Lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye; kwa maana yeye ni uhai wako na urefu wa siku zako.”—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini ni muhimu tumpende Yehova?

• Tunaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tunampenda Mungu?

• Tuna sababu gani za kumpenda Yehova?

• Tunaweza kukuza jinsi gani upendo kwa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Yehova anathamini sana jambo ambalo sote tunaweza kufanya, yaani, kumpenda

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yohana 14:9