Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mpinga-Kristo Anafunuliwa

Mpinga-Kristo Anafunuliwa

Mpinga-Kristo Anafunuliwa

UNGEJILINDA kwa njia gani kama ungejua kwamba ugonjwa hatari wa kuambukiza unaenea katika eneo lenu? Inaelekea kwamba ungejilinda kwa kuimarisha mfumo wako wa kinga ya mwili na kuwaepuka watu wenye ugonjwa huo. Tunapaswa kufanya vivyo hivyo kwa njia ya kiroho. Maandiko yanatuambia kwamba mpinga-Kristo ‘tayari yumo ulimwenguni.’ (1 Yohana 4:3) Ili “tusiambukizwe,” ni lazima tuwatambue watu “wenye ugonjwa” na kuwaepuka. Tunathamini kwamba Biblia inazungumzia sana habari hiyo.

Neno “mpinga-Kristo” linamaanisha “yule aliye kinyume cha (au badala ya) Kristo.” Hivyo, katika maana iliyo pana, neno hilo linawahusu wote wanaompinga Kristo au wanaodai kwa uwongo kuwa Kristo au wawakilishi wake. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Yule ambaye hayuko upande wangu ananipinga [au ni mpinga-Kristo], na yule ambaye hakusanyi pamoja nami anatawanya.”—Luka 11:23.

Bila shaka, Yohana aliandika kuhusu mpinga-Kristo miaka zaidi ya 60 baada ya Yesu kufa na kufufuliwa kwenda mbinguni. Kwa hiyo, utendaji wa mpinga-Kristo unapaswa kueleweka kwa kuchunguza matokeo yake kwa wafuasi washikamanifu wa Yesu duniani.—Mathayo 25:40, 45.

Mpinga-Kristo Anapinga Wakristo

Yesu aliwaonya wafuasi wake kwamba ulimwengu kwa ujumla ungewachukia. Alisema: ‘Watu watawatia ninyi katika dhiki na kuwaua ninyi, nanyi mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu. Na manabii wengi wa uwongo watatokea na kuwapotosha wengi.’—Mathayo 24:9, 11.

Kwa kuwa wanafunzi wa Yesu wanateswa “kwa sababu ya jina la [Yesu],” ni wazi kwamba watu wanaowatesa ni wapinga-Kristo, ambao wako kinyume cha Kristo. “Manabii wa uwongo,” ambao wengine wao walikuwa Wakristo wamo katika kikundi hichohicho. (2 Yohana 7) Hao “wapinga-Kristo wengi,” akaandika Yohana, “waliondoka kwetu, lakini hawakuwa wa namna yetu; kwa maana ikiwa wangekuwa wa namna yetu, wangebaki pamoja na sisi.”—1 Yohana 2:18, 19.

Maneno ya Yesu na ya Yohana yanaonyesha wazi kwamba mpinga-Kristo si mtu mmoja tu bali ni jamii ya watu mmoja-mmoja ambao ni wapinga-Kristo. Zaidi ya hayo, kwa sababu ni manabii wa uwongo, moja ya makusudi yao makuu ni kueneza uwongo wa kidini. Ni mbinu kama gani wanazotumia?

Kueneza Uwongo wa Kidini

Mtume Paulo alimwonya mfanyakazi mwenzake Timotheo ajihadhari na mafundisho ya waasi-imani, kama vile Himenayo na Fileto, ambao “neno lao litaenea kama kidonda chenye kuoza.” Paulo aliongeza hivi: “Watu hao wamegeuka kutoka kwenye kweli, wakisema kwamba ufufuo tayari umetukia; nao wanaipindua imani ya wengine.” (2 Timotheo 2:16-18) Kwa wazi, Himenayo na Fileto walifundisha kwamba ufufuo ulikuwa wa mfano na kwamba Wakristo walikuwa tayari wamefufuliwa katika njia ya kiroho. Ni kweli kwamba kuwa mwanafunzi wa kweli wa Yesu kunamfanya mtu awe hai machoni pa Mungu, kama Paulo mwenyewe alivyosema waziwazi. (Waefeso 2:1-5) Hata hivyo, mafundisho ya Himenayo na Fileto hayakupatana na ahadi ya Yesu ya ufufuo halisi wa wafu chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.—Yohana 5:28, 29.

Mafundisho kuhusu ufufuo wa mfano yaliendelezwa baadaye na kikundi ambacho kinaitwa Waagnosti. Wakiamini kwamba ujuzi (gnoʹsis katika Kigiriki) ungeweza kupatikana kwa njia za mafumbo, Waagnosti walichanganya Ukristo wa waasi-imani, falsafa za Kigiriki, na mambo ya mafumbo kutoka Mashariki. Kwa mfano, waliamini kwamba vitu vyote vya kimwili ni uovu, na kwa sababu hiyo, Yesu hakuja katika mwili bali alionekana tu kuwa na mwili wa kibinadamu. Kama tulivyoona, mtume Yohana alikuwa ameonya kuhusu jambo hilohilo.—1 Yohana 4:2, 3; 2 Yohana 7.

Uwongo mwingine uliotungwa baada ya karne kadhaa, ni lile fundisho linaloitwa eti Utatu mtakatifu, ambalo linadai kwamba Yesu ni Mungu Mweza-Yote na vilevile Mwana wa Mungu. Katika kitabu chake (The Church of the First Three Centuries), Dakt. Alvan Lamson anasema kwamba fundisho la Utatu “halikutokana kamwe na Maandiko ya Kiyahudi wala ya Kikristo; lakini lilisitawi, na kuingizwa katika Ukristo na Mababa wa Kiplato.” “Mababa wa Kiplato” walikuwa akina nani? Walikuwa viongozi wa kidini waasi-imani ambao walivutiwa na mafundisho ya kipagani ya mwanafalsafa Mgiriki, Plato.

Kuingizwa kwa fundisho la Utatu kulikuwa hatua kubwa sana ya mpinga-Kristo, kwa kuwa fundisho hilo lilimfanya Mungu aonekane kuwa fumbo na lilificha uhusiano kati ya Mungu na Mwana wake. (Yohana 14:28; 15:10; Wakolosai 1:15) Hebu wazia, ikiwa Mungu ni fumbo, mtu anaweza jinsi gani ‘kumkaribia Mungu,’ kama Maandiko yanavyohimiza?—Yakobo 4:8.

Kuongezea mvurugo huo, watafsiri wengi wa Biblia wameliondoa jina la Mungu, Yehova, katika tafsiri zao, hata ingawa jina hilo linapatikana mara zaidi ya 7,000 katika maandishi ya awali! Kwa wazi, kujaribu kumfanya Mweza-yote awe fumbo na hata fumbo lisilo na jina ni tendo la kukosa sana heshima kwa Muumba na kwa Neno lake lililoongozwa kwa roho. (Ufunuo 22:18, 19) Zaidi ya hayo, kuliondoa jina la Mungu na badala yake kutumia majina ya cheo kama vile Bwana na Mungu hakupatani na sala ya kielelezo ya Yesu, ambayo inasema hivi kwa sehemu: “Jina lako na litakaswe [lifanywe kuwa takatifu].”—Mathayo 6:9.

Wapinga-Kristo Wanakataa Ufalme wa Mungu

Wapinga-Kristo wamekuwa na shughuli nyingi hasa katika ‘siku hizi za mwisho.’ (2 Timotheo 3:1) Lengo kuu la wadanganyifu hao wa leo ni kuwadanganya watu kuhusu daraka la Yesu akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, ambao ni serikali ya mbinguni itakayoitawala dunia yote hivi karibuni.—Danieli 7:13, 14; Ufunuo 11:15.

Kwa mfano, viongozi fulani wa kidini wanahubiri kwamba Ufalme wa Mungu ni hali iliyo katika moyo wa wanadamu, maoni ambayo hayategemei Maandiko. (Danieli 2:44) Wengine wanadai kwamba Kristo anatumia serikali na mashirika ya wanadamu. Lakini, Yesu alisema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Bila shaka, Shetani ndiye “mtawala wa ulimwengu” na “mungu wa mfumo huu wa mambo,” wala si Kristo. (Yohana 14:30; 2 Wakorintho 4:4) Hilo linaonyesha kwa nini Yesu atazikomesha hivi karibuni serikali zote za wanadamu na kuwa Mtawala pekee wa dunia. (Zaburi 2:2, 6-9; Ufunuo 19:11-21) Watu wanasali juu ya jambo hilo wanaporudia-rudia Sala ya Bwana, inayosema: “Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatimizwe hapa duniani.”—Mathayo 6:10, Union Version.

Kwa sababu wanaunga mkono mifumo ya kisiasa ya ulimwengu, viongozi wengi wa kidini wamewapinga, na hata kuwatesa, wale wanaotangaza ukweli kuhusu Ufalme wa Mungu. Jambo la kupendeza ni kwamba kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinamtaja kahaba wa mfano, yaani, “Babiloni Mkubwa,” ambaye “amelewa damu ya watakatifu na damu ya mashahidi wa Yesu.” (Ufunuo 17:4-6) Kahaba huyo pia anafanya ukahaba wa kiroho kwa kuwaunga mkono “wafalme” wa dunia, au watawala wa kisiasa, na hivyo kupata kibali chao. Mwanamke huyo wa mfano si mwingine ila ni dini za uwongo za ulimwengu huu. Yeye ni sehemu kuu ya mpinga-Kristo.—Ufunuo 18:2, 3; Yakobo 4:4.

Mpinga-Kristo ‘Anafurahisha Masikio’

Zaidi ya kukataa kweli ya Biblia, watu wengi wanaojiita Wakristo wamekataa viwango vya Biblia vya mwenendo na kupendelea viwango vya mwenendo vinavyopendwa na watu wengi. Neno la Mungu lilitabiri jambo hilo kwa kusema hivi: “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo [watu wanaodai kwamba wanamtumikia Mungu] hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe.” (2 Timotheo 4:3) Wadanganyifu hao wa kidini wanasemwa pia kuwa ‘mitume wa uwongo, wafanyakazi wadanganyifu, wanaojigeuza wenyewe kuwa mitume wa Kristo.’ Biblia inaendelea kusema: “Mwisho wao utakuwa kulingana na matendo yao.”—2 Wakorintho 11:13-15.

Matendo yao yanatia ndani “mwenendo mpotovu.” Watu wenye mwenendo mpotovu wanadharau bila aibu kanuni bora za maadili. (2 Petro 2:1-3, 12-14) Je, hatuoni idadi inayoongezeka ya viongozi wa kidini na wafuasi wao wakifuata au kuruhusu mazoea yasiyo ya Kikristo, kama vile ngono kati ya watu wa jinsia moja na ngono nje ya ndoa? Tafadhali, linganisha maoni na mitindo hiyo ya maisha inayokubaliwa na watu wengi na yale ambayo Biblia inasema kwenye Mambo ya Walawi 18:22; Waroma 1:26, 27; 1 Wakorintho 6:9, 10; Waebrania 13:4; na Yuda 7.

“Yajaribuni Maneno Yaliyoongozwa na Roho”

Kwa sababu ya mambo ambayo tumezungumzia, tunapaswa kutii maneno ya mtume Yohana kwa kutopuuza imani yetu ya kidini. “Msiamini kila neno lililoongozwa na roho,” anaonya, “lakini yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu, kwa sababu manabii wengi wa uwongo wameingia ulimwenguni.”—1 Yohana 4:1.

Fikiria mfano mzuri wa watu fulani “wasikivu” walioishi katika jiji la Beroya katika karne ya kwanza. “Walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo [yaliyosemwa na Paulo na Sila] ndivyo yalivyo.” (Matendo 17:10, 11) Ndiyo, ingawa walikuwa na hamu kubwa sana ya kujifunza, Waberoya walihakikisha kwamba mambo waliyosikia na kukubali yalitegemea kabisa Maandiko.

Leo pia, Wakristo wa kweli hawashawishiwi na maoni ya watu wengi ambayo yanabadilika-badilika, lakini wanashikamana kabisa na kweli ya Biblia. Mtume Paulo aliandika hivi: “Hili ndilo ninaloendelea kusali, kwamba upendo wenu uwe mwingi hata zaidi na zaidi pamoja na ujuzi sahihi na utambuzi kamili.”Wafilipi 1:9.

Ikiwa bado hujafanya hivyo, jiwekee mradi wa kupata “ujuzi sahihi na utambuzi kamili” kwa kujifunza mambo ambayo Biblia inafundisha hasa. Wale wanaowaiga Waberoya hawadanganywi na “maneno yasiyo ya kweli” ya wapinga-Kristo. (2 Petro 2:3) Badala yake, wanawekwa huru na kweli ya kiroho kuhusu Kristo wa kweli na wafuasi wake wa kweli.—Yohana 8:32, 36.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]

KILE AMBACHO BIBLIA INASEMA KUHUSU MPINGA-KRISTO

“Watoto wachanga, ni saa ya mwisho [kwa wazi, mwisho wa siku za mitume], na, kama vile ambavyo mmesikia kwamba mpinga-Kristo anakuja, hata sasa kumekuwa na wapinga-Kristo wengi.” 1 Yohana 2:18.

“Ni nani aliye mwongo kama si yule anayekana kwamba Yesu ndiye Kristo? Huyo ndiye mpinga-Kristo, yeye anayemkana Baba na Mwana.”1 Yohana 2:22.

“Kila neno lililoongozwa na roho ambalo halimkiri Yesu halitokani na Mungu. Zaidi ya hayo, hili ndilo neno lililoongozwa na roho la yule mpinga-Kristo ambalo mmesikia kwamba linakuja, na sasa tayari limo ulimwenguni.” 1 Yohana 4:3.

“Kwa maana wadanganyifu wengi wametokea katika ulimwengu, watu ambao hawamkiri Yesu Kristo kuwa alikuja katika mwili. Hao ndio yule mdanganyifu na mpinga-Kristo.”2 Yohana 7.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

MDANGANYIFU MWENYE SURA NYINGI

Neno “mpinga-Kristo” linawahusu wote ambao wanakana yale ambayo Biblia inasema kumhusu Yesu Kristo, wote wanaopinga Ufalme wake, na wote wanaowatesa wafuasi wake. Pia, neno hilo linahusu mtu mmoja-mmoja, mashirika, na mataifa yanayodai kwa uwongo kumwakilisha Kristo au ambayo yanajitwika isivyofaa daraka la Masihi kwa kuahidi kwa kimbelembele kutimiza yale ambayo ni Kristo peke yake anaweza kufanya, yaani, kuleta amani na usalama wa kweli.

[Hisani]

Augustine: ©SuperStock/age fotostock

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kama Waberoya, tunapaswa ‘kuchunguza Maandiko kila siku’