Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pigano Letu la Kubaki Wenye Nguvu Kiroho

Pigano Letu la Kubaki Wenye Nguvu Kiroho

Simulizi la Maisha

Pigano Letu la Kubaki Wenye Nguvu Kiroho

Limesimuliwa na Rolf Brüggemeier

Barua ya kwanza niliyopokea nikiwa gerezani ilitoka kwa rafiki fulani. Alinijulisha kwamba mama yangu na ndugu zangu wadogo, Peter, Jochen, na Manfred walikuwa pia wamekamatwa. Hivyo, dada zetu wawili wadogo wakabaki bila wazazi wala ndugu na dada. Kwa nini wenye mamlaka wa Ujerumani Mashariki waliitesa familia yetu? Ni nini kilichotusaidia kubaki wenye nguvu kiroho?

VITA VYA PILI VYA ULIMWENGU vilikomesha utulivu wetu tulipokuwa wachanga; tulijionea wenyewe ukatili wa vita. Baba alijiunga na jeshi la Ujerumani naye akafa akiwa mfungwa wa vita. Kwa hiyo, Mama yangu anayeitwa Berta, alilazimika kulea watoto sita wenye umri wa kuanzia mwaka mmoja mpaka miaka 16.

Kanisa ambalo Mama alishirikiana nalo lilimfanya asipendezwe tena na mambo ya dini, na hivyo hakutaka kusikia jambo lolote kumhusu Mungu. Lakini siku moja, mwaka wa 1949, Ilse Fuchs, mwanamke mwenye busara na mwenye umbo dogo, alikuja mlangoni petu kuzungumza kuhusu Ufalme wa Mungu. Maswali na hoja zake ziliamsha upendezi wa Mama. Funzo la Biblia lilimfanya Mama awe na tumaini.

Hata hivyo, sisi wavulana tulikuwa na shaka mwanzoni. Wanazi na kisha Wakomunisti walikuwa wametoa ahadi nyingi kubwa, lakini walitukatisha tamaa. Ingawa tulikuwa na shaka kuelekea ahadi zozote mpya, tulivutiwa tulipokutana na Mashahidi fulani ambao walikuwa katika kambi za mateso kwa sababu ya kukataa kuunga mkono vita. Mimi, Mama, na Peter, tulibatizwa mwaka uliofuata.

Ndugu yetu mdogo Manfred alibatizwa pia, lakini inaonekana kweli ya Biblia haikuwa imetia mizizi moyoni mwake. Wakomunisti walipopiga marufuku kazi yetu katika mwaka wa 1950, alishinikizwa na polisi wa siri wenye sifa mbaya walioitwa Stasi, naye akafichua mahali tulipofanyia mikutano. Kwa sababu hiyo hatimaye mama na ndugu zangu walikamatwa.

Kutumikia Chini ya Marufuku

Kwa sababu ya marufuku, tulilazimika kuingiza kisiri vichapo vya Biblia Ujerumani Mashariki. Nilisafirisha vichapo kutoka magharibi mwa Berlin, ambako vichapo vyetu havikuwa vimepigwa marufuku na kuviingiza nchini. Nilihepa polisi mara kadhaa, lakini Novemba (Mwezi wa 11) 1950, nilikamatwa.

Stasi walinitia katika chumba cha chini ya ardhi ambacho hakikuwa na dirisha. Sikuruhusiwa kulala mchana, na usiku nilihojiwa, na nyakati nyingine nilipigwa. Sikuweza kupashana habari na mtu yeyote wa familia yetu hadi Machi (Mwezi wa 3) 1951, wakati Mama, Peter, na Jochen walipokuja kusikiza kesi yangu. Nilihukumiwa kifungo cha miaka sita.

Peter, Jochen, na Mama walikamatwa siku sita baada ya kusikizwa kwa kesi yangu. Baadaye, mwamini mwenzetu alimtunza dada yangu Hannelore, aliyekuwa na miaka 11, na shangazi yetu akamchukua Sabine, aliyekuwa na miaka 7. Walinzi wa Stasi waliwatendea Mama na ndugu zangu kama wahalifu hatari, na hata waliwanyang’anya kamba zao za viatu. Walilazimika kusimama muda wote walipokuwa wakihojiwa. Wao pia walihukumiwa kifungo cha miaka sita kila mmoja.

Mnamo 1953, mimi pamoja na wafungwa wengine Mashahidi tulipewa kazi ya kujenga uwanja mdogo wa ndege za kijeshi. Tulikataa kazi hiyo. Wenye mamlaka walituadhibu kwa kututenga na wengine kwa siku 21, bila kazi, barua, na chakula cha kutosha. Dada fulani Wakristo walibakisha mkate kutokana na posho yao ndogo na kutuletea kisiri. Hilo liliniwezesha kumfahamu Anni, mmoja wa dada hao, na kisha kumuoa baada ya kutoka gerezani mwaka wa 1956, na yeye mwaka wa 1957. Mwaka mmoja baada ya kuoana, binti yetu Ruth, alizaliwa. Peter, Jochen, na pia Hannelore walifunga ndoa karibu wakati huohuo.

Miaka mitatu hivi baada ya kutoka gerezani, nilikamatwa tena. Ofisa wa Stasi alijaribu kunishawishi niwe mpelelezi. Alisema: “Bwana mpendwa Brüggemeier, tafadhali tumia akili. Unajua jinsi maisha yalivyo gerezani, na hatutaki uteseke tena. Unaweza kubaki ukiwa Shahidi, kuendelea kujifunza, na kuzungumza kuhusu Biblia kama upendavyo. Tunataka tu utujulishe mambo mapya. Fikiria mke wako na binti yako mdogo.” Maneno hayo ya mwisho yaliniumiza sana. Hata hivyo, nilijua kwamba nikiwa gerezani, Yehova angetunza familia yangu vizuri zaidi kuliko jinsi ambavyo ningeitunza, naye alifanya hivyo!

Wenye mamlaka walijaribu kumlazimisha Anni afanye kazi wakati wote na kuwacha watu wengine wamtunze Ruth katikati ya juma. Anni alikataa, naye alifanya kazi usiku ili amtunze Ruth mchana. Ndugu zetu walitujali sana na walimpa mke wangu vitu vingi hivi kwamba aliweza kuwagawia wengine. Wakati huo, nilikaa gerezani karibu miaka sita zaidi.

Jinsi Tulivyodumisha Imani Tulipokuwa Gerezani

Baada tu ya kurudi gerezani, Mashahidi tuliofungwa nao walitaka sana kujua habari mpya ambazo zilikuwa zimechapishwa karibuni. Nilifurahi sana kwamba nilikuwa nimejifunza kwa makini gazeti la Mnara wa Mlinzi na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida ili niweze kuwatia moyo kiroho!

Tulipowaomba walinzi Biblia, walijibu hivi: “Kuwapa Mashahidi wa Yehova Biblia ni hatari kama tu kumpa mhalifu aliye gerezani vifaa vya kuvunja gereza ili atoroke.” Kila siku, ndugu walioongoza walichagua andiko la Biblia ambalo tungezungumzia. Kila siku tuliporuhusiwa kutembea kwa dakika 30 kwenye uwanja wa gereza, tulipendezwa zaidi kuchunguza andiko la Biblia la siku kuliko kufanya mazoezi ya mwili ama kupunga hewa. Ingawa kila mmoja alipaswa kuwa umbali wa meta 5 hivi kutoka kwa mwenzake na ingawa hatukuruhusiwa kuzungumza, bado tulipata njia za kujulisha wengine andiko la siku. Tuliporudi katika vyumba vyetu gerezani, kila mmoja alisema yale ambayo aliweza kusikia, na kisha tukawa na mazungumzo yetu ya kila siku ya Biblia.

Hatimaye, mpelelezi fulani alitusaliti, nami nikawekwa katika kifungo cha upweke. Ilikuwa baraka kama nini kwamba kufikia wakati huo nilikuwa nimetia akilini mamia kadhaa ya maandiko! Nilitumia siku hizo za upweke kutafakari kuhusu habari mbalimbali za Biblia. Kisha, nilihamishiwa kwenye gereza lingine ambako mlinzi aliniweka katika chumba ambamo mlikuwa na Mashahidi wengine wawili, na jambo lenye kufurahisha zaidi ni kwamba alitupa Biblia. Baada ya kukaa kwa miezi sita katika kifungo cha upweke, nilithamini sana kuweza tena kuzungumzia habari za Biblia pamoja na waamini wenzangu.

Ndugu yangu Peter anaeleza jambo ambalo lilimsaidia kuvumilia alipokuwa katika gereza lingine: “Nilifikiria maisha katika ulimwengu mpya na kutafakari kuhusu habari za Biblia. Sisi Mashahidi tuliimarishana kwa kuulizana maswali ya Biblia au mitihani mingine ya Kimaandiko. Maisha hayakuwa rahisi. Wakati mwingine tuliwekwa watu 11 katika chumba kidogo chenye ukubwa wa meta 12 za mraba. Tulilazimika kufanya kila kitu humo—kula, kulala, kuoga, hata kwenda choo. Tulikuwa wenye wasiwasi na hasira.”

Jochen, mmoja wa ndugu zangu, anasema hivi kuhusu hali yake gerezani: “Niliimba nyimbo za kitabu chetu cha nyimbo ambazo niliweza kukumbuka. Kila siku nilitafakari kuhusu moja ya maandiko ambayo nilikumbuka. Baada ya kuachiliwa huru, niliendelea na zoea zuri la kujielimisha kiroho. Kila siku nilisoma andiko la Biblia la siku pamoja na familia yangu. Pia, tulitayarisha mikutano yote.”

Mama Atoka Gerezani

Baada ya kukaa gerezani kwa miaka miwili hivi, Mama aliachiliwa huru. Alitumia uhuru wake kujifunza Biblia pamoja na Hannelore na Sabine akiwasaidia kujiwekea msingi mzuri wa imani. Aliwafundisha pia kushughulikia masuala au mambo mbalimbali yaliyotokea shuleni kwa sababu ya imani yao katika Mungu. Hannelore anasema: “Hatukujali sana hali ingekuwaje kwa sababu tulihimizana nyumbani. Uhusiano wa karibu wa familia yetu ulitusaidia kukabiliana na tatizo lolote.”

Hannelore anaendelea kusema: “Pia, tuliwapelekea chakula cha kiroho ndugu zetu waliokuwa gerezani. Kwa kutumia maandishi madogo, tuliandika kwa mkono nakala ndogo ya gazeti zima la Mnara wa Mlinzi kwenye karatasi yenye nta.” Kisha, tukafunika kurasa hizo kwa karatasi isiyolowa maji na kuificha katika furushi lenye matunda makavu tulilotuma kila mwezi. Tulifurahi kwelikweli walipotuambia kwamba matunda tuliyotuma yalikuwa ‘matamu sana.’ Tulikazia sana fikira kazi yetu hivi kwamba sina budi kusema kuwa huo ulikuwa wakati mzuri ajabu!”

Maisha Wakati wa Marufuku

Peter anaeleza jinsi maisha yalivyokuwa kwa makumi ya miaka wakati wa marufuku nchini Ujerumani Mashariki: “Tulikutana vikundi vidogo-vidogo katika nyumba za akina ndugu, nasi tulifika na kuondoka wakati tofauti-tofauti. Katika kila mkutano, tulifanya mipango kwa ajili ya mkutano ambao ungefuata. Tulifanya hivyo kwa kutumia ishara na vikaratasi vyenye maandishi kwa kuwa tuliogopa kwamba tungesikiwa na Stasi.”

Hannelore anaeleza: “Nyakati nyingine, tulipokea kaseti za programu ya kusanyiko. Kwa kawaida, hiyo ilifanya mikutano iwe yenye kufurahisha. Kikundi chetu kidogo kilikutana ili kusikiliza mafundisho ya Biblia kwa saa kadhaa. Ingawa hatungeweza kuwaona wasemaji, tulisikiliza programu hiyo kwa makini na kuandika mambo makuu.”

Peter anasema: “Ndugu zetu Wakristo katika nchi nyingine walijitolea sana ili kutuandalia vichapo vya Biblia. Miaka kumi hivi ya mwisho kabla ya ukuta wa Berlin kuangushwa mnamo 1989, walituchapishia vitabu vidogo. Ndugu fulani walihatarisha magari yao, pesa zao, na hata uhuru wao ili kusafirisha chakula cha kiroho hadi Ujerumani Mashariki. Usiku mmoja wenzi fulani wa ndoa tuliokuwa tukiwangoja hawakufika. Polisi walipata vichapo walivyokuwa navyo na wakachukua gari lao. Ingawa tulikabili hatari hizo, hatukufikiria kamwe kuacha kazi hiyo ili kuishi maisha ya utulivu.”

Manfred, ndugu yangu mdogo ambaye alitusaliti mnamo 1950, anaeleza kilichomsaidia kuwa tena na imani na kuidumisha: “Baada ya kufungwa kwa miezi michache, nilihamia Ujerumani Magharibi na kuacha kweli ya Biblia. Nilirudi Ujerumani Mashariki mwaka wa 1954 na kuoa mwaka uliofuata. Punde si punde, mke wangu alikubali kweli ya Biblia, naye akabatizwa mwaka wa 1957. Baada ya muda dhamiri yangu ilianza kunisumbua, na kwa msaada wa mke wangu, nikarudi kutanikoni.

“Ndugu Wakristo walionijua kabla sijaiacha kweli, walinikubali kwa upendo kana kwamba sikuwa nimefanya chochote. Kusalimiwa kwa tabasamu changamfu na kukumbatiwa ni jambo zuri sana. Ninafurahi sana kupatanishwa tena na Yehova na ndugu zangu.”

Pigano la Kiroho Laendelea

Kila mshiriki wa familia yetu amelazimika kupigana pigano kali la imani. Ndugu yangu Peter anasema kwamba “leo, kuliko wakati mwingine wowote, tunakabili vikengeusha-fikira na vishawishi vingi vya kimwili. Wakati wa marufuku, tuliridhika na vitu tulivyokuwa navyo. Kwa mfano, hakuna yeyote kati yetu aliyetaka kuhudhuria funzo lingine kwa sababu tu za kibinafsi, na hakuna yeyote aliyelalamika kwamba mikutano ilikuwa mbali au ilichelewa sana. Sote tulifurahi kukutanika hata ikiwa baadhi yetu tungelazimika kungoja hadi saa 5:00 usiku kwa ajili ya zamu yetu ya kutoka mahali pa mikutano.”

Mnamo 1959, Mama aliamua kuhamia Ujerumani Magharibi pamoja na Sabine ambaye alikuwa na umri wa miaka 16. Kwa kuwa walitaka kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme, ofisi ya tawi iliwaomba waende Ellwangen, Baden-Württemberg. Ingawa Mama alikuwa na afya mbaya, bidii yake ilimchochea Sabine kuanza upainia akiwa na umri wa miaka 18. Sabine alipoolewa, Mama alijifunza kuendesha gari ili ashiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri. Wakati huo, alikuwa na umri wa miaka 58. Alifurahia sana utumishi huo hadi kifo chake mwaka wa 1974.

Baada ya kukaa gerezani kwa miaka sita hivi ya kifungo changu cha pili, nilihamishwa hadi Ujerumani Magharibi mwaka wa 1965, bila familia yangu kujua. Hata hivyo, mke wangu Anni, na binti yetu Ruth, walijiunga nami. Niliuliza ofisi ya tawi ikiwa tungeweza kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa wa wahubiri, basi tukatumwa Nördlingen, Bavaria. Ruth na ndugu yake Johannes, walikulia huko. Anni alianza utumishi wa upainia. Mfano mzuri wa Anni ulimchochea Ruth aanze upainia mara tu baada ya shule. Watoto wetu wawili walifunga ndoa na mapainia. Sasa wana familia, na tumebarikiwa kuwa na wajukuu sita wazuri.

Mwaka wa 1987, nilistaafu mapema na kujiunga na Anni katika huduma ya upainia. Miaka mitatu baadaye nilialikwa kwenye ofisi ya tawi ya Selters ili kusaidia kupanua majengo. Kisha, tukasaidia kujenga Jumba la kwanza la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Glauchau, katika ile iliyokuwa Ujerumani Mashariki, na baadaye tukafanya kazi ya kulitunza jumba hilo. Kwa sababu za kiafya, tulirudi ili kuwa na binti yetu katika Kutaniko la Nördlingen ambako tunatumikia tukiwa mapainia.

Ninafurahi sana kwamba ndugu na dada zangu wote na washiriki wengi wa familia yetu wanaendelea kumtumikia Mungu wetu mzuri, Yehova. Kwa miaka yote hiyo, tumejifunza kwamba maadamu tunadumu tukiwa wenye nguvu kiroho, tutaona maneno haya ya Zaburi 126:3 yakitimia maishani mwetu: “Yehova amefanya jambo kuu katika yale ambayo ametufanyia. Tumekuwa na shangwe.”

[Picha katika ukurasa wa 13]

Siku yetu ya arusi, 1957

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nikiwa na familia yetu, 1948: (mbele, kushoto kwenda kulia) Manfred, Berta, Sabine, Hannelore, Peter; (nyuma, kushoto kwenda kulia) mimi na Jochen

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kitabu kidogo kilichotumiwa wakati wa marufuku na vidude vya “Stasi” vya kunasa sauti

[Hisani]

Forschungs- und Gedenkstätte NORMANNENSTRASSE

[Picha katika ukurasa wa 16]

Nikiwa na ndugu zangu: (mbele, kushoto kwenda kulia) Hannelore na Sabine; (nyuma, kushoto kwenda kulia) mimi, Jochen, Peter, na Manfred