Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Unavyoweza Kufanikiwa

Jinsi Unavyoweza Kufanikiwa

Jinsi Unavyoweza Kufanikiwa

KAMA vile wazazi wanavyowajali watoto wao na kutaka wafanikiwe, ndivyo Baba yetu wa mbinguni anavyotujali na kutaka tufanikiwe. Anaonyesha kwamba anatujali na anatupenda kwa kutufundisha mengi kuhusu kufanikiwa na kutofanikiwa. Kwa kweli, Biblia inasema hivi kwa uhakika kuhusu mtu anayesikiliza yale ambayo Mungu anasema: “Kila jambo analofanya litafanikiwa.”—Zaburi 1:3.

Hata hivyo, ikiwa ndivyo ilivyo, kwa nini watu wengi hawafanikiwi, hawana furaha, na hawana kusudi maishani? Tukichunguza kwa makini zaburi hiyo tutapata jibu na kujua jinsi sisi pia tunavyoweza kufanikiwa.

“Shauri la Waovu”

Mtunga-zaburi anaonya kuhusu hatari ya kutembea katika “shauri la waovu.” (Zaburi 1:1) Shetani Ibilisi ndiye ‘mwovu’ mkuu. (Mathayo 6:13) Maandiko yanatuambia kwamba yeye ndiye “mtawala wa ulimwengu” huu na kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (Yohana 16:11; 1 Yohana 5:19) Hivyo, haishangazi kwamba mashauri mengi yanayotolewa katika ulimwengu yanaonyesha mawazo ya mwovu huyo.

Waovu wanatoa mashauri ya aina gani? Kwa kawaida, waovu hawamheshimu Mungu. (Zaburi 10:13) Mashauri ya waovu ambayo yanampuuza na kutomheshimu Mungu yameenea sana. Jamii ya leo inaendeleza “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani.” (1 Yohana 2:16) Vyombo vya habari vinatumwagia mawazo ya kupenda vitu vya kimwili na kwamba ‘tunapaswa kukusanya kila kitu tunachoweza maishani.’ Ulimwenguni pote, kila mwaka makampuni yanatumia zaidi ya dola bilioni 500 za Marekani kwa ajili ya matangazo ya kibiashara ili kuwashawishi watu wanunue vitu, iwe wanavihitaji au hawavihitaji. Matangazo hayo ya kibiashara yamefanya mengi zaidi ya kubadili mazoea ya watu ya kununua vitu. Yamepotosha maoni ya watu ulimwenguni kuhusu mafanikio.

Matokeo ni kwamba hata ingawa watu wengi wana vitu ambavyo miaka kadhaa iliyopita hawakufikiri kwamba wangepata, bado wanatamani kwa pupa kupata vitu zaidi. Wana maoni ya kwamba usipopata vitu hivyo, huwezi kuwa mwenye furaha au kufanikiwa. Maoni hayo ni ya uwongo na ‘hayatokani na Baba, bali yanatokana na ulimwengu.’—1 Yohana 2:16.

Muumba wetu anajua kile ambacho kitatuletea mafanikio ya kweli. Mashauri yake yanatofautiana na “shauri la waovu.” Kwa hiyo, kujaribu kupata baraka za Mungu huku ukiendelea kutembea katika njia ya ulimwengu ya kupata mafanikio ni kama kujaribu kutembea kwenye barabara mbili tofauti wakati uleule. Hilo haliwezekani kamwe. Kwa sababu hiyo, Biblia inaonya hivi: “Msiige mitindo ya ulimwengu huu”!—Waroma 12:2, Biblia Habari Njema.

Usiache Ulimwengu Ukufinyange

Ulimwengu ulio chini ya uvutano wa Shetani unajaribu kujifanya kana kwamba unapendezwa na hali yetu njema. Hata hivyo, tunahitaji kuwa waangalifu. Kumbuka kwamba Shetani alimdanganya kwa uchoyo mwanamke wa kwanza Hawa ili ajifaidi mwenyewe. Kisha, akamtumia kumwongoza Adamu atumbukie katika dhambi. Leo pia, Shetani anatumia wanadamu kutoa mashauri yake maovu.

Kwa mfano, David aliyetajwa mapema, alitarajiwa kufanya kazi kwa saa nyingi zaidi na kufunga safari nyingi za kibiashara. David anasema: “Nilikuwa nikiondoka asubuhi sana siku ya Jumatatu (Siku ya 1) na kurudi Alhamisi (Siku ya 4) jioni.” Wakijua kwamba mtu anahitaji kujidhabihu hivyo, marafiki, washiriki wa familia, na wafanyakazi wanyoofu walimhimiza David hivi: “Fanya hivyo kwa ajili ya familia yako.” Walimwambia angefanya hivyo kwa miaka michache tu mpaka ajiimarishe. David anaeleza hivi: “Walinisadikisha kwamba familia yangu ingefaidika kwa sababu ningeleta pesa zaidi nyumbani na ningefanikiwa zaidi. Ingawa sikuwa pamoja na familia yangu, marafiki wangu walinisadikisha kwamba kwa kweli nilikuwa nikiisaidia.” Kama David, watu wengi wanafanya kazi kwa bidii ili kuipa familia yao kila kitu ambacho wanafikiri wapendwa wao wanahitaji. Lakini je, kufuata mashauri ya aina hiyo kunaleta mafanikio? Familia inahitaji nini hasa?

David aligundua kile ambacho familia yake ilihitaji alipokuwa mbali katika safari ya kibiashara. “Nilipokuwa nikizungumza na binti yangu Angelica kwenye simu, aliniambia hivi: ‘Baba, kwa nini hutaki kukaa nyumbani pamoja nasi?’ Maneno hayo yaliniumiza sana moyoni,” akasema David. Maneno hayo ya binti yake yalimchochea kupeleka ombi lake la kujiuzulu. David aliamua kuipa familia yake kile ambacho walihitaji hasa, yaani, yeye.

Kutumia Mashauri ya Mungu Kunaleta Mafanikio

Unaweza kushinda jinsi gani maoni yasiyofaa ambayo yameenea katika ulimwengu huu? Mtunga-zaburi anatuambia kwamba mtu ambaye amefanikiwa na kupata furaha ni yule ambaye “mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku.”—Zaburi 1:2.

Mungu alipomchagua Yoshua awe kiongozi wa taifa la Israeli, Yoshua aliambiwa hivi: ‘Nawe usome Neno la Mungu kwa sauti ya chini mchana na usiku.’ Ndiyo, kusoma na kutafakari Neno la Mungu yalikuwa mambo muhimu, lakini Yoshua alihitaji pia “kuangalia kufanya kulingana na yote ambayo [yalikuwa] yameandikwa ndani yake.” Bila shaka, kusoma tu Biblia hakutafanya ufanikiwe kimuujiza. Ni lazima ufuate yale unayosoma. Yoshua aliambiwa hivi: “Ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima.”—Yoshua 1:8.

Wazia mtoto anayetabasamu akiwa ameketi kwenye miguu ya mzazi wake anayempenda huku wakisoma hadithi ambayo anapenda. Haidhuru wamesoma hadithi hiyo mara ngapi, wanafurahia sana pindi hizo zenye thamani. Vivyo hivyo, mtu anayempenda Mungu anafurahia sana kusoma Biblia kila siku. Ni nafasi yenye kufurahisha ya kuwa pamoja na Baba yake wa mbinguni. Mtu huyo anapofuata mashauri na mwongozo wa Yehova, anakuwa “kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.”—Zaburi 1:3.

Mti unaotajwa na mtunga-zaburi haukui tu kimuujiza. Mkulima ameupanda kwa uangalifu karibu na chanzo cha maji naye anautunza. Vivyo hivyo, kupitia mashauri yaliyo katika Maandiko, Baba yetu wa mbinguni anarekebisha na kunyoosha njia yetu ya kufikiri. Kwa sababu hiyo, tunasitawi na kuzaa matunda yanayomletea sifa.

Lakini “waovu hawako hivyo.” Ni kweli kwamba huenda wakaonekana wanafanikiwa kwa muda, lakini, mwishowe wanapata matokeo mabaya. “Hawatasimama katika hukumu.” Badala yake, “njia ya waovu itaangamia.”—Zaburi 1:4-6.

Kwa hivyo, usiache ulimwengu uongoze miradi na viwango vyako. Ingawa huenda ukawa na vipawa na uwezo wa kufanikiwa katika ulimwengu huu, uwe mwangalifu kuhusu jinsi unavyotumia vipawa vyako au jinsi unavyoruhusu ulimwengu uvitumie. Kufuatia mambo ya kimwili yasiyo na maana kunaweza kumfanya mtu ‘anyauke.’ Kwa upande mwingine, kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu kunaleta furaha na mafanikio ya kweli.

Jinsi Unavyoweza Kufanikiwa

Kwa nini wakati mtu anapofuata mashauri ya Mungu, kila kitu anachofanya kitafanikiwa? Mtunga-zaburi hakuwa akizungumza kuhusu mafanikio katika ulimwengu huu. Mafanikio ya mtu anayemwogopa Mungu yanahusiana na kufanya mapenzi ya Mungu, na nyakati zote mapenzi ya Mungu yanafanikiwa. Acha tuone jinsi kufuata kanuni za Biblia kunavyoweza kukuletea mafanikio.

Familia: Maandiko yanawashauri waume ‘wawe wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe,’ na mke Mkristo anaagizwa ‘amheshimu sana mume wake.’ (Waefeso 5:28, 33) Wazazi wanatiwa moyo watumie wakati pamoja na watoto wao, wacheke nao, na kuwafundisha mambo muhimu maishani. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Mhubiri 3:4) Pia, Neno la Mungu linawashauri hivi wazazi: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu.” Shauri hilo likifuatwa itakuwa rahisi kwa watoto ‘kuwatii wazazi wao’ na ‘kumheshimu baba yao na mama yao.’ (Waefeso 6:1-4) Wale wanaofuata shauri hilo la Mungu wanaweza kufanikiwa katika maisha yao ya familia.

Marafiki: Watu wengi wanataka kuwa na marafiki. Tumeumbwa tukiwa na uwezo wa kiakili na wa kihisia wa kupendwa na kuwapenda wengine. Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba wanapaswa ‘kupendana.’ (Yohana 13:34, 35) Kati yao, tunapata marafiki ambao tunaweza kuwapenda na kuwatumaini, na hata kuwafunulia hisia na mawazo yetu ya ndani. (Methali 18:24) Jambo bora zaidi ni kwamba tukifuata kanuni za Biblia, tunaweza ‘kumkaribia Mungu’ na tunaweza kuitwa “rafiki ya Yehova” kama Abrahamu.—Yakobo 2:23; 4:8.

Kusudi Maishani: Badala ya kuwa na maisha yasiyo na kusudi, wale ambao wamefanikiwa kikweli wanapata kusudi maishani. Maisha yao hayategemei hali zisizotegemeka za ulimwengu huu. Miradi yao inawawezesha kutosheka sikuzote kwa kuwa inakazia kusudi la kweli la maisha. Ni nini kinachomfanya mtu awe na kusudi maishani? “Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhubiri 12:13.

Tumaini: Mungu anapokuwa Rafiki yetu, tunakuwa pia na tumaini la wakati ujao. Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo “waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu.” Kwa kufanya hivyo, wangekuwa “wakijiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.” (1 Timotheo 6:17-19) Uzima huo ulio wa kweli utapatikana hivi karibuni wakati Ufalme wa kimbingu wa Mungu utakaporudisha Paradiso duniani.—Luka 23:43.

Ukifuata kanuni za Biblia, haimaanishi hutapatwa na matatizo, lakini utaepuka maumivu ya moyoni na huzuni nyingi ambayo waovu wanajiletea. David ambaye alitajwa mwanzoni, na mamilioni walio kama yeye wamejifunza faida za kufuata kanuni za Biblia maishani mwao. Baada ya kupata kazi yenye ratiba nzuri, David alisema: “Ninashukuru kwa sababu nina uhusiano mzuri pamoja na mke na watoto wangu, na pia pendeleo la kumtumikia Yehova Mungu nikiwa mzee wa kutaniko.” Haishangazi kwamba zaburi inasema hivi kumhusu mtu anayesikiliza mashauri ya Mungu: “Kila jambo analofanya litafanikiwa”!

[Chati katika ukurasa wa 6]

HATUA TANO ZA KUPATA MAFANIKIO

1 Kataa kufinyangwa na viwango vya ulimwengu.

Zaburi 1:1; Waroma 12:2

2 Soma na kutafakari Neno la Mungu kila siku.

Zaburi 1:2, 3

3 Fuata mashauri ya Biblia maishani mwako.

Yoshua 1:7-9

4 Mfanye Mungu awe rafiki yako.

Yakobo 2:23; 4:8

5 Mwogope Mungu wa kweli, na ushike amri zake.

Mhubiri 12:13

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, unafuata hatua za kupata mafanikio?