Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maamuzi Mazuri Yalileta Baraka za Kudumu

Maamuzi Mazuri Yalileta Baraka za Kudumu

Simulizi la Maisha

Maamuzi Mazuri Yalileta Baraka za Kudumu

Limesimuliwa na Paul Kushnir

MWAKA wa 1897 babu na nyanya yangu walitoka Ukrainia na kuhamia Kanada, nao waliishi karibu na mji wa Yorkton, Saskatchewan. Walikuja na watoto wanne, wavulana watatu na msichana mmoja. Mwaka wa 1923, msichana huyo aliyeitwa Marinka, akawa mama yangu. Nilikuwa mtoto wake wa saba. Wakati huo maisha yalikuwa rahisi na yenye utulivu. Tulikuwa na chakula kizuri na mavazi ya joto, na serikali ilitoa huduma za msingi. Majirani wenye urafiki walikuwa tayari kusaidiana kufanya kazi kubwa. Mwaka wa 1925, wakati wa baridi kali, Mwanafunzi mmoja wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, alitutembelea. Ziara hiyo ilituchochea kufanya maamuzi ambayo ninathamini mpaka leo.

Familia Yetu Inapata Kweli ya Biblia

Mama alikubali vijitabu fulani kutoka kwa Mwanafunzi huyo wa Biblia, na baada ya muda akatambua amepata kweli. Alifanya maendeleo ya haraka ya kiroho na kubatizwa mwaka wa 1926. Mama alipokuwa Mwanafunzi wa Biblia, familia yetu ilipata mtazamo mpya kabisa kuhusu maisha. Tuliwakaribisha watu wengi nyumbani kwetu. Mara nyingi, waangalizi wanaosafiri na Wanafunzi wengine wa Biblia walikaa pamoja nasi. Mwaka wa 1928, mwangalizi anayesafiri alituonyesha sinema iliyoitwa “Eureka Drama,” ambayo ilikuwa sinema ya “Photo-Drama of Creation” iliyofupishwa. Mwangalizi huyo alituomba sisi watoto tumpe chura wa bandia ambaye alikuwa akitoa mlio. Chura huyo alipolia, mwangalizi alibadili picha ya sinema. Tulifurahia sana kumpa chura huyo.

Mara nyingi, mwangalizi anayesafiri anayeitwa Emil Zarysky alitutembelea akiwa na gari lake lenye nyumba. Nyakati nyingine, alikuja na mwanaye mkubwa, ambaye alitutia moyo sisi watoto tufikirie kuwa wahudumu wa wakati wote au mapainia. Mapainia wengi pia walikaa nyumbani kwetu. Siku moja, mama alimwazima painia fulani shati huku akimshonea shati lake lililopasuka. Painia huyo alisahau na kwenda na shati hilo. Muda mrefu baadaye, alituma shati hilo na kuomba msamaha kwa sababu ya kuchelewa kulirudisha. “Sikuwa na senti kumi za kulipia gharama ya posta,” akaandika. Tulisema afadhali angebaki na shati hilo! Nilitumaini kwamba siku moja ningeweza kuwaiga mapainia hao wenye kujidhabihu. Ninamshukuru Mama kwa sababu ya roho yake ya kuwakaribisha wageni ambayo iliboresha maisha yetu na kutusaidia tuwapende zaidi ndugu zetu.—1 Petro 4:8, 9.

Baba hakupata kuwa Mwanafunzi wa Biblia, lakini hakutupinga. Mwaka wa 1930, baba hata aliwaruhusu akina ndugu watumie banda lake kubwa kwa ajili ya kusanyiko la siku moja. Ingawa nilikuwa na umri wa miaka saba tu, shangwe na heshima ya pindi hiyo ilinivutia sana. Baba alikufa mwaka wa 1933. Mama, ambaye wakati huo alikuwa mjane mwenye watoto wanane, hakuacha hata kidogo azimio lake la kutulea katika ibada ya kweli. Alihakikisha kwamba nilihudhuria mikutano pamoja naye. Wakati huo, mikutano ilionekana mirefu, nami nilitamani kujiunga na watoto wengine ambao waliruhusiwa kucheza nje. Hata hivyo, kwa kuwa nilimheshimu mama sikutoka nje. Mama alipokuwa akipika, mara nyingi alitaja andiko na kisha kuniuliza linapatikana wapi katika Biblia. Tulipata mavuno mengi mwaka wa 1933. Mama alitumia pesa za ziada alizopata kununua gari. Majirani fulani walimlaumu kuwa alitumia pesa vibaya, lakini alitumaini kwamba gari hilo lingetusaidia katika utendaji wetu wa kiroho. Hakuwa amekosea.

Wengine Walinisaidia Kufanya Maamuzi Mazuri

Wakati fulani maishani, kijana anahitaji kufanya maamuzi ambayo yataongoza maisha yake ya wakati ujao. Wakati ulipofika, dada zangu wakubwa, Helen na Kay, walianza upainia. Painia mmoja ambaye tulimkaribisha nyumbani mwetu ni John Jazewsky ambaye alikuwa kijana mzuri. Mama alimwomba akae nasi kwa muda fulani ili atusaidie kufanya kazi ya shamba. Baadaye, John alimwoa Kay, na wakatumikia wakiwa mapainia karibu na nyumbani kwetu. Nilipokuwa na umri wa miaka 12, walinialika nishiriki nao katika utumishi wa shambani wakati wa likizo ya shule. Hilo lilinipa nafasi ya kuonja maisha ya upainia.

Muda si muda, mimi na ndugu yangu John tuliweza kusimamia shamba letu kwa kadiri fulani. Kwa sababu hiyo, wakati wa miezi ya kiangazi, Mama aliweza kufanya utumishi ambao sasa unaitwa upainia-msaidizi. Alitumia gari lenye magurudumu mawili ambalo lilikokotwa na farasi aliyezeeka. Baba alikuwa akimwita farasi huyo mtundu Saul, lakini Mama alimwona kuwa kiumbe mpole ambaye angeweza kuongozwa. Mimi na John tulipenda kazi ya kutunza shamba, lakini kila mara Mama aliporudi nyumbani kutoka katika mahubiri na kutusimulia mambo aliyoona, tulianza kupenda zaidi na zaidi utumishi wa upainia kuliko kazi ya kutunza shamba. Mnamo mwaka wa 1938, niliongeza bidii yangu katika kazi ya kuhubiri, na nikabatizwa mnamo Februari 9, 1940 (9/2/1940).

Muda mfupi baadaye, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa kutaniko. Nilitunza rekodi za kutaniko na nilifurahi sana kila mara kulipokuwa na ongezeko. Nilikuwa na eneo langu la kuhubiri katika mji uliokuwa umbali wa kilomita 16 hivi kutoka kwetu. Wakati wa baridi kali, nilienda huko kwa miguu kila juma na kulala siku moja au mbili katika dari ya nyumba ya familia fulani ambayo ilipendezwa na Biblia. Wakati huo nilihubiri bila busara. Pindi moja, baada ya kuzungumza na mhubiri Mlutheri, alinitisha kwamba angewatuma polisi wanikamate iwapo singewaacha kondoo zake. Hilo lilinichochea tu kuendelea kuhubiri.

Mnamo mwaka wa 1942, dada yangu Kay na mume wake, John, walipanga kuhudhuria kusanyiko huko Cleveland, Ohio, Marekani. Nilifurahi waliponialika nisafiri pamoja nao. Kusanyiko hilo ni moja ya matukio bora zaidi maishani mwangu. Liliniimarisha ili kufuatia miradi yangu ya wakati ujao. Ndugu Nathan Knorr, aliyekuwa akisimamia kazi ulimwenguni pote, alipotoa mwaliko wenye kugusa moyo wa kuomba mapainia 10,000, papo hapo nilifanya uamuzi wangu wa kuwa painia!

Mnamo Januari (Mwezi wa 1) 1943, Henry, mhudumu anayesafiri alitembelea kutaniko letu. Alitoa hotuba yenye kuchochea iliyotusisimua. Siku iliyofuata, baridi ilikuwa kali sana, na upepo mkali kutoka kaskazini-magharibi uliongeza baridi hata zaidi. Kwa kawaida, hatukutoka nyumbani wakati kama huo wa baridi, lakini Henry alitaka kwenda katika utumishi. Yeye na wengine walienda kwenye kijiji kilichokuwa umbali wa kilomita 11 wakitumia gari lililokokotwa na farasi kwenye barafu. Gari hilo lilikuwa na jiko la kuni. Nilienda peke yangu kutembelea familia yenye wavulana watano. Walikubali nijifunze Biblia pamoja nao, na baada ya muda wakawa Mashahidi.

Kuhubiri Wakati wa Marufuku

Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, kazi ya Ufalme ilipigwa marufuku nchini Kanada. Tulilazimika kuficha vitabu vyetu vya kujifunzia Biblia, na shamba letu lilikuwa na sehemu nyingi za kuficha vitabu hivyo. Polisi walikuja kwetu mara nyingi, lakini hawakupata chochote. Tulihubiri kwa kutumia Biblia tu. Tulikutana katika vikundi vidogo-vidogo, na mimi na ndugu yangu John tulipewa kazi ya kusafirisha vitabu kisiri.

Wakati wa vita, kutaniko letu lilishiriki katika kazi ya kusambaza nchini kote kijitabu Mwisho wa Wanazi (End of Nazism). Tulienda kufanya kazi hiyo katikati ya usiku. Nilikuwa na wasiwasi mwingi tulipokuwa tukikaribia kila nyumba tukiwa chonjo na kuacha kijitabu mlangoni. Sijawahi kamwe kufanya kazi yenye kuogopesha kama hiyo. Tulifurahi kama nini tulipoacha kijitabu cha mwisho! Kisha, tulirudi haraka kwenye gari lililoegeshwa, na kuangalia kama kila mmoja alikuwepo, halafu tukaondoka haraka kwa gari na kutoweka gizani.

Upainia, Magereza, na Makusanyiko

Mnamo Mei 1, 1943 (1/5/1943), nilimuaga Mama. Nikiwa na dola 20 mfukoni na sanduku dogo, nilifunga safari kwenda kwenye mgawo wangu wa kwanza wa upainia. Ndugu Tom Troop na familia yake yenye upendo huko Quill Lake, Saskatchewan, walinikaribisha. Mwaka uliofuata, nilienda kwenye eneo la mbali huko Weyburn, Saskatchewan. Nilikamatwa nilipokuwa nikihubiri barabarani mnamo Desemba 24, 1944 (24/12/1944). Baada ya kukaa kwa muda fulani katika gereza la eneo hilo, nilipelekwa kwenye kambi moja huko Jasper, Alberta. Nilikuwa huko pamoja na Mashahidi wengine, nasi tulizungukwa na uumbaji mtukufu wa Yehova, yaani, Milima ya Roki ya Kanada. Mwanzoni mwa mwaka wa 1945, maofisa wa kambi walituruhusu tuhudhurie mkutano huko Edmonton, Alberta. Ndugu Knorr alitoa ripoti yenye kusisimua kuhusu maendeleo ya kazi ya ulimwenguni pote. Tulitamani sana wakati ambapo tungeachiliwa huru na kupata tena nafasi ya kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri.

Nilipoachiliwa huru, nilianza tena upainia. Muda mfupi baadaye, ilitangazwa kwamba Kusanyiko la “Mpanuko wa Mataifa Yote” lingefanywa huko Los Angeles, California. Ndugu fulani katika mgawo wangu mpya wa upainia aliweka viti ambavyo vilitoshea watu 20 ndani ya gari lake. Mnamo Agosti 1, 1947 (1/8/1947), tulifunga safari ambayo hatuwezi kusahau. Tulisafiri umbali wa kilomita 7,200 kupitia majangwa, maeneo yenye nyasi, na maeneo yenye kuvutia sana, kama vile mbuga ya kitaifa ya Yellowstone na ya Yosemite. Safari yote ilichukua siku 27 nayo ilikuwa nzuri ajabu!

Kusanyiko lenyewe pia lilikuwa tukio zuri sana ambalo hatuwezi kusahau. Ili kushiriki kikamili katika kusanyiko hilo, nilijitolea kuwa mkaribishaji wakati wa mchana na mlinzi wakati wa usiku. Baada ya kuhudhuria mkutano wa wale wanaopendezwa na utumishi wa umishonari, nilijaza ombi langu lakini sikutarajia kuitwa. Mwaka wa 1948, nilijitolea kuwa painia na kutumika katika jimbo la Quebec huko Kanada.—Isaya 6:8.

Kwenda Gileadi na Maisha ya Baadaye

Mnamo 1949, nilifurahia kupokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 14 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Mazoezi hayo yaliimarisha imani yangu na kunivuta karibu zaidi na Yehova. Tayari John na Kay walikuwa wamehitimu katika darasa la 11 na walikuwa wakitumika wakiwa wamishonari huko Rhodesia Kaskazini (leo inaitwa Zambia). Ndugu yangu John alihitimu Gileadi mwaka wa 1956. Akiwa pamoja na mke wake, Frieda, alitumika huko Brazili kwa miaka 32 hadi alipokufa.

Siku yangu ya kuhitimu mnamo Februari (Mwezi wa 2) 1950, nilitiwa moyo sana kupokea telegramu mbili, moja kutoka kwa Mama na nyingine kutoka kwa familia ya Troop huko Quill Lake. Telegramu ya Troop, yenye kichwa, “Mashauri kwa Mhitimu,” ilisema hivi: “Hii ni siku ya pekee sana kwako. Ni siku ambayo utaithamini daima; tunakutakia furaha na mafanikio maishani mwako.”

Nilipewa mgawo wa kutumika katika jiji la Quebec, lakini kwa muda nilibaki kwenye Shamba la Ufalme, katika Jimbo la New York, ambako Shule ya Gileadi ilikuwa. Siku moja, Ndugu Knorr aliniuliza ikiwa ningekubali kwenda nchini Ubelgiji. Hata hivyo, baada ya siku kadhaa, aliniuliza ikiwa ningekubali mgawo wa kwenda Uholanzi. Nilipopokea barua ya mgawo, ilisema kwamba nimepewa “mgawo wa kuwa mtumishi wa ofisi ya tawi.” Sikuamini macho yangu.

Mnamo Agosti 24, 1950 (24/8/1950), nilifunga safari ya siku 11 kwa meli kuelekea Uholanzi. Ulikuwa wakati wa kutosha kusoma Biblia mpya ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Nilifika Rotterdam Septemba 5, 1950 (5/9/1950), ambako nilikaribishwa kwa uchangamfu na familia ya Betheli. Ingawa Vita vya Pili vya Ulimwengu vilisababisha uharibifu mkubwa, akina ndugu walijitahidi sana kuanzisha tena utendaji wa Kikristo. Nilipokuwa nikiwasikiliza wakisimulia jinsi walivyodumisha utimilifu wakati wa mateso makali, niliwazia kwamba ingekuwa vigumu kwao kufanya kazi chini ya mtumishi wa ofisi ya tawi asiye na uzoefu. Hata hivyo, baada ya muda ilionekana wazi kwamba sikuwa na sababu yoyote ya kuwa na wasiwasi.

Bila shaka, mambo fulani yalihitaji kushughulikiwa. Nilifika kabla tu ya kusanyiko, nami nilivutiwa kuona jinsi maelfu ya wajumbe walivyotayarishiwa mahali pa kulala kwenye uwanja wa kusanyiko. Nilipendekeza kwamba katika kusanyiko litakalofuata wajumbe wakaribishwe katika nyumba za watu. Akina ndugu waliona pendekezo hilo kuwa zuri, lakini lisilofaa katika nchi yao. Baada ya kujadiliana kuhusu jambo hilo, tulikubaliana kwamba nusu ya wajumbe walale kwenye uwanja wa kusanyiko na nusu wakaribishwe kwenye nyumba za watu ambao hawakuwa Mashahidi. Nikiwa mwenye shangwe, nilimweleza Ndugu Knorr matokeo ya mpango wetu alipohudhuria kusanyiko hilo. Hata hivyo, baadaye shangwe yangu ilipotea mara tu niliposoma ripoti kuhusu kusanyiko hilo katika Mnara wa Mlinzi. Ripoti hiyo ilisema: “Tuna hakika kwamba wakati ujao ndugu watakuwa na imani na hivyo kuwatafutia wajumbe mahali ambapo wataweza kutoa ushahidi kwa matokeo zaidi, yaani, katika nyumba za watu.” Hivyo ndivyo hasa tulivyofanya “wakati ujao” ulipofika!

Mnamo Julai (Mwezi wa 7) 1961, wawakilishi wawili wa ofisi yetu ya tawi walialikwa kuhudhuria mkutano huko London pamoja na wawakilishi wa ofisi nyingine. Ndugu Knorr alitangaza kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko Matakatifu ingepatikana katika lugha zaidi, kutia ndani Kiholanzi. Habari hizo zilitusisimua kama nini! Hatukujua mradi huo ulihusisha nini. Miaka miwili baadaye, mnamo 1963, nilifurahi kushiriki katika programu ya kusanyiko huko New York ambako Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kiholanzi ilitolewa.

Maamuzi na Migawo Mipya

Mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 1961, nilimwoa Leida Wamelink. Familia yao yote ilikuwa imekubali kweli mwaka wa 1942 wakati wa mateso ya Wanazi. Leida alianza kufanya upainia mwaka wa 1950 na kuanza utumishi wa Betheli mwaka wa 1953. Bidii yake Betheli na kutanikoni ilinisadikisha kwamba angekuwa mshiriki mshikamanifu katika huduma yangu.

Mwaka mmoja hivi baada ya kufunga ndoa, nilialikwa Brooklyn kwa ajili ya mazoezi ya ziada ya miezi kumi. Wakati huo, wake hawakwenda pamoja na waume zao. Ingawa Leida alikuwa na afya mbaya, kwa upendo alikubali niitikie mwaliko huo. Baadaye, afya ya Leida ilizidi kuwa mbaya. Tulijaribu kuendelea na utumishi wa Betheli lakini mwishowe tukaamua ingefaa zaidi kuendelea na utumishi wa wakati wote shambani. Hivyo, tukaanza kazi ya mzunguko. Muda mfupi baadaye, mke wangu alifanyiwa upasuaji mkubwa. Marafiki walitutegemeza kwa upendo, hivyo tukafaulu kukabiliana na hali hiyo, na mwaka mmoja baadaye tulikubali kutumika katika kazi ya wilaya.

Kwa muda wa miaka saba, tulifurahia kazi yenye kuchangamsha ya kusafiri. Kisha, tukahitajika kufanya uamuzi mzito nilipopewa mgawo wa kufundisha Shule ya Huduma ya Ufalme iliyofanyiwa Betheli. Tulikubali, ingawa ilikuwa vigumu kufanya mabadiliko kwa kuwa tulipenda kazi ya kusafiri. Madarasa 47 ya shule hiyo, ambayo yalichukua majuma mawili kila moja, yalitupa nafasi ya kushiriki baraka za kiroho pamoja na wazee wa makutaniko.

Wakati huo, nilikuwa nikifanya mipango ya kumtembelea mama yangu mwaka wa 1978. Lakini kwa ghafula, mnamo Aprili 29, 1977 (29/4/1977), tulipokea telegramu iliyotujulisha kwamba Mama amekufa. Nilihuzunika sana kwa sababu singesikia tena sauti yake changamfu wala kumwambia tena jinsi ninavyothamini yote aliyonifanyia.

Mwishoni mwa Shule ya Huduma ya Ufalme, tuliombwa tuwe washiriki wa familia ya Betheli. Miaka iliyofuata, nilitumika kwa miaka kumi nikiwa mratibu wa Halmshauri ya Tawi. Baadaye, Baraza Linaloongoza liliweka rasmi mratibu mpya, ambaye angeweza kushughulikia daraka hilo vizuri zaidi. Ninashukuru sana kwa jambo hilo.

Kutumika Kadiri Umri Unavyoruhusu

Mimi na Leida tuna umri wa miaka 83 sasa. Nimefurahia kutumika katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 60, na kwa miaka 45 iliyopita nimetumika pamoja na mke wangu mshikamanifu. Ameona utegemezo ambao amenipa katika migawo yetu yote kuwa sehemu ya utumishi wake mtakatifu kwa Yehova. Kwa sasa, tukiwa Betheli na pia katika kutaniko, tunafanya kadiri tunavyoweza.—Isaya 46:4.

Mara kwa mara, tunafurahia kukumbuka matukio mazuri maishani mwetu. Hatujuti kamwe kwa sababu ya yale ambayo tumefanya katika utumishi wa Yehova, na tuna hakika kwamba maamuzi tuliyofanya mapema maishani yalikuwa bora kabisa. Tumeazimia kuendelea kumtumikia na kumheshimu Yehova kwa nguvu zetu zote.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nikiwa na Bill, ndugu yangu mkubwa, na farasi wetu aliyeitwa Saul

[Picha katika ukurasa wa 15]

Siku yetu ya arusi, Agosti 1961

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na Leida leo