Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni nini maana ya kutiwa muhuri kunakotajwa katika Ufunuo 7:3?

Andiko la Ufunuo 7:1-3 linasema hivi: “Nikaona malaika wanne wamesimama juu ya pembe nne za dunia, wakizishika sana zile pepo nne za dunia, ili upepo wowote usivume juu ya dunia au juu ya bahari au juu ya mti wowote. Nami nikamwona malaika mwingine akipanda kutoka mashariki, akiwa na muhuri wa Mungu aliye hai; naye akapaaza sauti kubwa kwa wale malaika wanne waliopewa ruhusa kuidhuru dunia na bahari, akisema: ‘Msiidhuru dunia au bahari au miti, mpaka baada ya sisi kuwatia muhuri watumwa wa Mungu wetu katika mapaji ya nyuso zao.’”

Wakati “zile pepo nne” zitakapoachiliwa, “dhiki kuu” itatokea, dini ya uwongo na ulimwengu huu mbovu unaobaki wa Shetani utaharibiwa. (Ufunuo 7:14) “Watumwa wa Mungu wetu” ni ndugu watiwa-mafuta wa Kristo walio duniani. (1 Petro 2:9, 16) Hivyo, unabii huu unaonyesha kwamba kuwatia muhuri ndugu za Kristo kutakuwa kumekamilishwa wakati dhiki kuu itakapoanza. Hata hivyo, mistari mingine ya Biblia inaonyesha kwamba kuna kutiwa muhuri kwa watiwa-mafuta kunakofanywa mapema. Kwa hiyo, nyakati nyingine, tunazungumza kuhusu kutiwa muhuri mara ya kwanza na kutiwa muhuri mara ya mwisho. Kuna tofauti gani kati ya aina hizo mbili za kutiwa muhuri?

Acheni tufikirie maana ya maneno ‘kutia muhuri.’ Katika nyakati za kale, muhuri ulitumiwa kutia alama kwenye hati fulani. Maneno hayo yanaweza pia kumaanisha alama yenyewe. Siku hizo, ilikuwa kawaida kuambatanisha muhuri na hati au vitu vingine ili kuonyesha uhalali wa muhuri au umiliki wa kitu.—1 Wafalme 21:8; Ayubu 14:17.

Paulo alilinganisha roho takatifu na muhuri aliposema hivi: “Yeye ambaye hutoa uhakikisho kwamba ninyi na sisi ni wa Kristo na yeye ambaye ametutia mafuta ni Mungu. Yeye pia ametia muhuri wake juu yetu naye ametupa sisi rehani ya kitakachokuja, yaani, roho, katika mioyo yetu.” (2 Wakorintho 1:21, 22) Hivyo, Yehova anawatia mafuta Wakristo hao kwa roho yake takatifu ili kuonyesha kwamba wao ni mali yake.

Hata hivyo, kuna hatua mbili za kuwatia muhuri watiwa-mafuta. Kutiwa muhuri mara ya kwanza kunatofautiana na kutiwa muhuri mara ya mwisho (1) kuhusiana na kusudi na (2) kuhusiana na wakati. Kutiwa muhuri mara ya kwanza kunafanywa ili kuchagua mshiriki mpya anayeongezwa kwenye idadi ya Wakristo watiwa-mafuta. Kutiwa muhuri mara ya mwisho kunafanywa ili kuthibitisha kwamba yule aliyechaguliwa na kutiwa muhuri ameonyesha kabisa ushikamanifu wake. Ni wakati huo tu wa kutiwa muhuri mara ya mwisho, ndipo mtiwa-mafuta atakapotiwa muhuri kwa njia ya kudumu ‘katika paji la uso wake’ na hivyo kutambulishwa kabisa kuwa ‘mtumwa wa Mungu wetu’ ambaye amejaribiwa na kuonekana kuwa mwaminifu. Ufunuo sura ya 7 inazungumzia kutiwa muhuri mara ya mwisho.—Ufunuo 7:3.

Kuhusu wakati wa kutiwa muhuri mara ya kwanza, mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo watiwa-mafuta: “Ninyi pia mlimtumaini yeye baada ya kulisikia neno la kweli, habari njema juu ya wokovu wenu. Kupitia yeye pia, baada ya ninyi kuamini, mlitiwa muhuri kwa roho takatifu iliyoahidiwa.” (Waefeso 1:13, 14) Mara nyingi, Biblia inaonyesha kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa wanatiwa muhuri muda mfupi baada ya kusikia habari njema na kumwamini Kristo. (Matendo 8:15-17; 10:44) Kutiwa muhuri huko kulionyesha kwamba Mungu aliwakubali. Hata hivyo, hilo halikumaanisha kwamba mtu amepata kibali cha mwisho cha Mungu. Kwa nini?

Paulo alisema kwamba Wakristo watiwa-mafuta ‘wametiwa muhuri kwa ajili ya siku ya kuachiliwa huru.’ (Waefeso 4:30) Hilo linaonyesha kwamba baada ya kutiwa muhuri mara ya kwanza muda mrefu ungepita na kwa kawaida muda huo ungechukua miaka mingi. Watiwa-mafuta wanahitaji kuendelea kuwa waaminifu tangu siku wanapotiwa mafuta kwa roho takatifu mpaka ‘siku ya wao kuachiliwa huru’ kutoka katika miili yao ya nyama, yaani, mpaka watakapokufa. (Waroma 8:23; Wafilipi 1:23; 2 Petro 1:10) Hivyo, Paulo angeweza kusema hivi mwishoni kabisa mwa maisha yake: “Nimekimbia mwendo mpaka mwisho, nimeishika imani. Tangu wakati huu na kuendelea nimewekewa akiba ya taji la uadilifu.” (2 Timotheo 4:6-8) Zaidi ya hayo, Yesu aliliambia hivi kutaniko fulani la Wakristo watiwa-mafuta: “Uwe mwaminifu hata kufikia kifo, nami nitakupa taji la uzima.”—Ufunuo 2:10; 17:14.

Neno “taji” linatoa uthibitisho zaidi kwamba wakati fulani unapita kati ya kutiwa muhuri mara ya kwanza na kutiwa muhuri mara ya mwisho. Kwa nini? Nyakati za zamani, kulikuwa na desturi ya kumpa taji mkimbiaji aliyeshinda katika mashindano ya mbio. Ili apewe taji hilo, mkimbiaji huyo alipaswa kufanya mengi zaidi ya kuingia katika mashindano ya mbio. Alipaswa kukimbia mpaka mwisho. Vivyo hivyo, Wakristo watiwa-mafuta watapewa taji la uhai usioweza kufa mbinguni ikiwa watavumilia mpaka mwisho wa mwendo wao, yaani, tangu kutiwa muhuri mara ya kwanza mpaka kutiwa muhuri mara ya mwisho.—Mathayo 10:22; Yakobo 1:12.

Mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta ambao tayari wametiwa muhuri mara ya kwanza watatiwa muhuri mara ya mwisho wakati gani? Yeyote kati yao ambaye bado yuko hai duniani atatiwa muhuri katika ‘paji la uso wake’ kabla ya dhiki kuu kuanza. Pepo nne za dhiki zitakapoachiliwa, Waisraeli wote wa kiroho watakuwa wametiwa muhuri mara ya mwisho, ingawa wachache kati yao watakuwa bado hai katika mwili na lazima wamalize mwendo wao wa kidunia.