Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtu Ambaye Alipenda Uhai na Watu

Mtu Ambaye Alipenda Uhai na Watu

Mtu Ambaye Alipenda Uhai na Watu

DANIEL SYDLIK, mshiriki wa muda mrefu wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alikufa mnamo Jumanne (Siku ya 2), Aprili 18, 2006 (18/4/2006) akiwa na tumaini la kwenda mbinguni. Alikuwa na umri wa miaka 87, naye alikuwa ametumikia akiwa mshiriki wa familia ya Betheli huko Brooklyn, New York, kwa miaka karibu 60.

Ndugu Dan, kama alivyoitwa na marafiki wake wa karibu, aliingia Betheli mwaka wa 1946. Kabla ya hapo, alitumika akiwa painia wa pekee huko California na pia alifungwa gerezani kwa muda fulani wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu kwa sababu ya msimamo wake wa Kikristo wa kutokuwamo. Mambo aliyojionea wakati huo yalielezwa waziwazi katika simulizi la maisha yake kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1985 (1/6/1985), chini ya kichwa “Urafiki Wako Ni Wenye Thamani Sana, Ee, Mungu!” katika Kiingereza na Kifaransa.

Ndugu Sydlik alijulikana kuwa mtu mnyenyekevu sana na mwenye urafiki. Alipoongoza ibada ya asubuhi ya familia ya Betheli, mtazamo wake mzuri na wa kupenda uhai ulionekana katika maneno yake ya utangulizi aliyozoea kusema: “Ni vizuri kuwa hai ili kumtumikia Mungu wa kweli na aliye hai.” Alipotoa hotuba za watu wote, aliwatia wengine moyo wawe na mtazamo huo. Alitoa hotuba kama vile “Wenye Furaha Ni Watu Ambao Mungu Wao Ni Yehova,” “Kuonyesha Shangwe ya Yehova,” “Usizime Moto wa Roho ya Mungu,” na “Mambo Bora Zaidi Bado Hayajafika.”

Mnamo 1970, Ndugu Sydlik alimwoa Marina Hodson, kutoka Uingereza, naye alisema kuwa Marina ni “zawadi kutoka kwa Mungu.” Walimtumikia Yehova pamoja kwa miaka zaidi ya 35.

Katika miaka aliyokuwa Betheli, Ndugu Sydlik alitumika katika idara mbalimbali, kutia ndani kiwanda cha uchapishaji na Idara ya Uandikaji. Pia, alitumika katika kituo cha redio cha WBBR. Kisha, mnamo Novemba (Mwezi wa 11) 1974, aliwekwa rasmi kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza na mwishowe alifanya kazi katika Halmashauri ya Wafanyakazi na ya Uandikaji.

Kwa miaka zaidi ya 30, Ndugu Sydlik alipofanya kazi katika Halmashauri ya Wafanyakazi alionyesha kwamba aliwapenda watu sana. Aliwatia wengi moyo kwa sauti yake nzito, sikuzote akikazia pendeleo lenye thamani tulilo nalo la kumtumikia Yehova. Kwa kawaida, alikazia kwamba furaha ya kweli haitegemei mambo ya nje, bali inategemea uhusiano wetu pamoja na Yehova na mtazamo wetu kuhusu uhai.

Ingawa familia ya Betheli inamkosa sana Ndugu Sydlik, mfano wake akiwa mtu ambaye kwa kweli alipenda uhai na watu utaendelea kukumbukwa. Tuna hakika kwamba yuko kati ya wale wanaosemwa katika Ufunuo 14:13: “Wenye furaha ni wafu wanaokufa katika muungano na Bwana tangu wakati huu na kuendelea. Ndiyo, roho inasema, acheni wapumzike kutokana na kazi zao za jasho, kwa maana mambo waliyotenda yanaambatana nao moja kwa moja.”