Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ufufuo wa Kwanza”—Unaendelea Sasa!

“Ufufuo wa Kwanza”—Unaendelea Sasa!

“Ufufuo wa Kwanza”—Unaendelea Sasa!

“Wale walio wafu katika muungano na Kristo watafufuliwa kwanza.”—1 WATHESALONIKE 4:16.

1, 2. (a) Kuna tumaini gani kwa wale ambao wamekufa? (b) Kwa nini unaamini ufufuo? (Ona maelezo ya chini.)

“WALIO hai wanajua kwamba watakufa.” Imekuwa hivyo tangu Adamu alipofanya dhambi. Katika historia yote, kila mtu anayezaliwa anajua kwamba mwishowe atakufa, na watu wengi wamejiuliza hivi: ‘Ni nini kinachotukia baada ya kufa? Wafu wako katika hali gani?’ Biblia inajibu hivi: “Wafu, hawajui lolote kamwe.”—Mhubiri 9:5.

2 Je, kuna tumaini lolote kwa wafu? Ndiyo. Ni lazima kuwe na tumaini kwa ajili ya wafu ili kusudi la kwanza la Mungu litimie. Kwa karne nyingi, watumishi washikamanifu wa Mungu wameamini ahadi ya Yehova kuhusu Uzao ambao utamharibu Shetani na kuondoa madhara ambayo alisababisha. (Mwanzo 3:15) Wengi wao wamekufa. Ili waone utimizo wa ahadi hiyo na ahadi nyingine ambazo Yehova ametoa, wanahitaji kufufuliwa. (Waebrania 11:13) Je, hilo linawezekana? Ndiyo, linawezekana. Mtume Paulo alisema hivi: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Wakati mmoja Paulo alimfufua kijana aliyeitwa Eutiko, ambaye alianguka chini kutoka kwenye dirisha la ghorofa ya tatu na ‘kuokotwa akiwa amekufa.’ Huo ndio ufufuo wa mwisho kati ya masimulizi tisa ya Biblia kuhusu ufufuo.—Matendo 20:7-12. *

3. Wewe binafsi umefarijiwa kwa njia gani na maneno ya Yesu yaliyo katika Yohana 5:28, 29, na kwa nini?

3 Matukio hayo tisa ya ufufuo yanatupa msingi wa kuamini maneno ya Paulo. Yanaimarisha uhakika wetu katika uhakikisho huu wa Yesu: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Hayo ni maneno yenye kugusa moyo kama nini! Nayo yanawafariji kama nini mamilioni ya watu ambao wapendwa wao wamelala usingizi katika kifo!

4, 5. Biblia inataja ufufuo gani mbalimbali, na tutazungumzia ufufuo gani?

4 Wengi kati ya wale ambao watafufuliwa wataishi katika dunia yenye amani chini ya Ufalme wa Mungu. (Zaburi 37:10, 11, 29; Isaya 11:6-9; 35:5, 6; 65:21-23) Hata hivyo, ufufuo mwingine ungetukia kabla ya huo. Kwanza, Yesu Kristo angefufuliwa ili atoe thamani ya dhabihu yake mbele za Mungu kwa ajili yetu. Yesu alikufa na kufufuliwa katika mwaka wa 33 W.K.

5 Kisha, ni lazima washiriki watiwa-mafuta wa “Israeli wa Mungu” waungane na Bwana Yesu Kristo katika utukufu wa mbinguni, ambako ‘watakuwa pamoja na Bwana sikuzote.’ (Wagalatia 6:16; 1 Wathesalonike 4:17) Tukio hilo linaitwa “ufufuo wa mapema” au “ufufuo wa kwanza.” (Wafilipi 3:10, 11; Ufunuo 20:6) Ufufuo huo utakapokamilika, wakati utakuwa umefika kwa mamilioni kufufuliwa duniani wakiwa na tumaini la kupata uzima wa milele katika Paradiso. Hivyo, iwe tuna tumaini la kuishi mbinguni au duniani, tungependa kuelewa vizuri “ufufuo wa kwanza.” Huo ni ufufuo wa aina gani? Unatukia wakati gani?

“Wakiwa na Mwili wa Namna Gani?”

6, 7. (a) Kabla Wakristo watiwa-mafuta hawajaenda mbinguni, ni lazima nini kitukie? (b) Watafufuliwa wakiwa na mwili wa aina gani?

6 Katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, Paulo anauliza hivi kuhusu ufufuo wa kwanza: “Wafu watafufuliwaje? Ndiyo, watakuja wakiwa na mwili wa namna gani?” Kisha anajibu hivi: “Kile unachopanda hakiwi hai isipokuwa kwanza kife . . . lakini Mungu huipa mwili kama inavyompendeza . . . Utukufu wa miili ya mbinguni ni wa namna moja, na ule wa miili ya duniani ni wa namna nyingine.”—1 Wakorintho 15:35-40.

7 Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho takatifu lazima wafe kabla ya kupokea thawabu yao ya kimbingu. Wanapokufa, miili yao ya kidunia inarudi mavumbini. (Mwanzo 3:19) Wakati wa Mungu unapofika, wanafufuliwa wakiwa na mwili wa aina inayofaana na uhai wa kimbingu. (1 Yohana 3:2) Pia, Mungu anawapa kutoweza kufa. Hawazaliwi wakiwa na kutoweza kufa, kana kwamba walipuliziwa ile inayoitwa eti nafsi isiyoweza kufa. “Huu unaoweza kufa lazima uvae kutoweza kufa,” anasema Paulo. Kutoweza kufa ni zawadi kutoka kwa Mungu, ambayo ‘inavaliwa’ na wale wanaopata ufufuo wa kwanza.—1 Wakorintho 15:50, 53; Mwanzo 2:7; 2 Wakorintho 5:1, 2, 8.

8. Tunajua jinsi gani kwamba Mungu hachagui wale 144,000 kutoka katika dini mbalimbali?

8 Ni watu 144,000 tu wanaopata ufufuo wa kwanza. Yehova alianza kuwachagua katika Pentekoste ya 33 W.K., muda mfupi baada ya kumfufua Yesu. Wote wana “jina la [Yesu] na jina la Baba yake limeandikwa juu ya mapaji ya nyuso zao.” (Ufunuo 14:1, 3) Kwa hiyo, hawachaguliwi kutoka katika dini mbalimbali. Wote ni Wakristo, na wote wanajivunia kuwa na jina la Baba, Yehova. Wanapofufuliwa, wanapewa kazi ya kufanya mbinguni. Tumaini la kumtumikia Mungu katika njia hiyo ya moja kwa moja linawasisimua kwelikweli.

Je, Unaendelea Sasa?

9. Ufunuo 12:7 na 17:14 yanatusaidia jinsi gani kukadiria wakati ambapo ufufuo wa kwanza unaanza?

9 Ufufuo wa kwanza unatukia wakati gani? Kuna uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba unaendelea sasa. Kwa mfano, linganisha sura mbili za kitabu cha Ufunuo. Kwanza, tazama Ufunuo sura ya 12. Katika sura hiyo tunasoma kwamba Yesu Kristo, ambaye ametoka tu kuwekwa kuwa mfalme, pamoja na malaika zake watakatifu, anapigana vita na Shetani na roho wake waovu. (Ufunuo 12:7-9) Kama vile gazeti la Mnara wa Mlinzi limekuwa likionyesha, vita hivyo vilianza mwaka wa 1914. * Hata hivyo, ona kwamba hakuna mfuasi yeyote mtiwa-mafuta wa Kristo anayesemekana kuwa pamoja na Yesu katika vita hivyo vya mbinguni. Sasa, tazama sura ya 17 ya Ufunuo. Tunasoma kwamba baada ya “Babiloni Mkubwa” kuharibiwa, Mwana-Kondoo atayashinda mataifa. Kisha, andiko hilo linaongeza hivi: “Pia, wale walioitwa na waliochaguliwa na walio waaminifu pamoja naye watawashinda.” (Ufunuo 17:5, 14) Ni lazima wale “walioitwa na waliochaguliwa na walio waaminifu” wawe tayari wamefufuliwa ili wawe pamoja na Yesu katika ushindi huo wa mwisho juu ya ulimwengu wa Shetani. Hivyo, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba watiwa-mafuta wanaokufa kabla ya Har–Magedoni wanafufuliwa wakati fulani kati ya mwaka wa 1914 na Har–Magedoni.

10, 11. (a) Wale wazee 24 ni nani, na mmoja wao anamfunulia Yohana nini? (b) Tunaweza kukata kauli gani kutokana na hilo?

10 Je, tunaweza kusema kwa usahihi zaidi ni wakati gani ufufuo wa kwanza unapoanza? Andiko la Ufunuo 7:9-15 linatoa wazo fulani zuri. Katika andiko hilo, mtume Yohana anaeleza maono aliyopewa kuhusu “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu.” Mmoja wa wale wazee 24 anamweleza Yohana watu hao ni akina nani. Wazee hao 24 wanawakilisha wale 144,000 ambao ni warithi-washirika pamoja na Kristo wakiwa katika utukufu wao wa mbinguni. * (Luka 22:28-30; Ufunuo 4:4) Yohana mwenyewe alikuwa na tumaini la kimbingu. Lakini kwa kuwa alikuwa angali mwanadamu duniani mzee huyo alipozungumza naye katika maono hayo, ni lazima Yohana awe anawakilisha watiwa-mafuta walio duniani ambao bado hawajapokea thawabu yao ya kimbingu.

11 Hivyo basi, tunaweza kukata kauli gani kutokana na uhakika wa kwamba mmoja wa wale wazee 24 anamsaidia Yohana kutambua umati mkubwa ni akina nani? Inaonekana kwamba huenda washiriki waliofufuliwa wa kikundi cha wale wazee 24 wanahusika leo katika kutoa kweli ya Mungu. Kwa nini hilo ni jambo muhimu? Ni kwa sababu utambulisho halisi wa umati mkubwa ulifunuliwa kwa watumishi watiwa-mafuta wa Mungu hapa duniani mwaka wa 1935. Ikiwa mmoja wa wale wazee 24 alitumiwa kupitisha kweli hiyo muhimu, ingekuwa lazima awe amefufuliwa na kwenda mbinguni kufikia mwaka wa 1935. Hilo linaonyesha kwamba ufufuo wa kwanza ulianza muda fulani kati ya 1914 na 1935. Je, tunaweza kusema kwa usahihi hata zaidi ni wakati gani ufufuo wa kwanza ulianza?

12. Eleza kwa nini inawezekana kwamba ufufuo wa kwanza ulianza mwaka wa 1918.

12 Sasa, tutatafaidika tukichunguza simulizi lingine la Biblia ambalo linaweza kuonwa kuwa linahusiana na jambo hilo. Katika Oktoba (Mwezi wa 10) mwaka wa 29 W.K., Yesu Kristo alitiwa mafuta awe Mfalme wa wakati ujao wa Ufalme wa Mungu. Miaka mitatu na nusu baadaye, katika Aprili (Mwezi wa 4) mwaka wa 33 W.K., Yesu alifufuliwa akiwa mtu wa roho mwenye nguvu. Je, tunaweza kusema kwamba kwa kuwa Yesu aliwekwa kuwa mfalme mwaka wa 1914, ufufuo wa wafuasi wake waaminifu watiwa-mafuta ulianza miaka mitatu na nusu baadaye, mnamo mwaka wa 1918? Hilo ni jambo linalowezekana. Ingawa haliwezi kuthibitishwa moja kwa moja katika Biblia, linapatana na maandiko mengine ambayo yanaonyesha kwamba ufufuo wa kwanza ulianza muda mfupi baada ya kuanza kwa kuwapo kwa Kristo.

13. Andiko la 1 Wathesalonike 4:15-17 linatoa wazo gani linaloonyesha kwamba ufufuo wa kwanza ulianza mapema wakati wa kuwapo kwa Kristo?

13 Kwa mfano, Paulo aliandika hivi: “Sisi tulio hai ambao tutabaki mpaka kuwapo kwa Bwana [si, mpaka mwishoni mwa kuwapo kwake] hatutawatangulia kwa vyovyote wale ambao wamelala usingizi katika kifo; kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni akiwa na mwito wenye amri, kwa sauti ya malaika mkuu na kwa tarumbeta ya Mungu, na wale walio wafu katika muungano na Kristo watafufuliwa kwanza. Baadaye sisi tulio hai tuliobaki tutanyakuliwa, pamoja nao, katika mawingu ili kukutana na Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana sikuzote.” (1 Wathesalonike 4:15-17) Hivyo, Wakristo watiwa-mafuta waliokufa kabla ya kuwapo kwa Kristo walifufuliwa na kupata uhai wa kimbingu kabla ya wale ambao bado walikuwa hai wakati wa kuwapo kwa Kristo. Hilo linamaanisha kwamba ni lazima ufufuo wa kwanza uwe ulianza mapema wakati wa kuwapo kwa Kristo, na unaendelea “wakati wa kuwapo kwake.” (1 Wakorintho 15:23) Badala ya kutukia mara moja, ufufuo wa kwanza unatukia hatua kwa hatua kwa muda fulani.

“Kila Mmoja Wao Akapewa Kanzu Nyeupe”

14. (a) Maono yaliyo katika Ufunuo sura ya 6 yanatimizwa wakati gani? (b) Ni nini kinachoonyeshwa katika Ufunuo 6:9?

14 Pia fikiria uthibitisho unaopatikana katika Ufunuo sura ya 6. Katika andiko hilo Yesu anaonekana akiendesha farasi akiwa Mfalme anayeshinda. (Ufunuo 6:2) Mataifa yamo katika vita vikubwa sana. (Ufunuo 6:4) Njaa kali imeenea. (Ufunuo 6:5, 6) Wanadamu wanakumbwa na magonjwa hatari. (Ufunuo 6:8) Matukio yote hayo yaliyotabiriwa yanapatana kabisa na hali za ulimwengu tangu mwaka wa 1914. Lakini jambo lingine linatukia. Tunaonyeshwa madhabahu ya dhabihu. Chini yake kuna “nafsi za wale waliouawa kwa sababu ya neno la Mungu na kwa sababu ya kazi ya ushahidi waliyokuwa nayo.” (Ufunuo 6:9) Kwa kuwa “nafsi [au, uhai] ya mwili iko katika damu,” kile hasa kilicho chini ya madhabahu ni damu ya watumishi waaminifu wa Yesu ambao walichinjwa kwa sababu ya kutoa ushahidi kwa ujasiri na kwa bidii.—Mambo ya Walawi 17:11.

15, 16. Eleza kwa nini maneno ya Ufunuo 6:10, 11 yanahusu ufufuo wa kwanza.

15 Kama vile damu ya Abeli mwadilifu, damu ya Wakristo hao waliouawa kwa sababu ya imani yao inalia ili haki ifanywe. (Mwanzo 4:10) “Wakalia kwa sauti kubwa, wakisema: ‘Utajizuia mpaka wakati gani, Bwana Mwenye Enzi Kuu mtakatifu na wa kweli, kuhukumu na kulipiza kisasi cha damu yetu juu ya wale wanaokaa duniani?’” Ni nini kinachofuata? “Kila mmoja wao akapewa kanzu nyeupe; nao wakaambiwa wapumzike tena muda kidogo, mpaka ijazwe pia hesabu ya watumwa wenzao na ndugu zao waliokuwa karibu kuuawa kama vile wao pia walivyouawa.”—Ufunuo 6:10, 11.

16 Je, damu iliyo chini ya madhabahu ndiyo iliyopewa kanzu hizo nyeupe? Bila shaka, hapana! Watu mmoja-mmoja ambao damu yao ilimwagwa kwa njia ya mfano kwenye madhabahu ndio waliopewa kanzu hizo. Walitoa uhai wao kwa ajili ya jina la Yesu na wakati huo walikuwamefufuliwa wakiwa watu wa roho. Tunajuaje jambo hilo? Mwanzoni mwa kitabu cha Ufunuo tunasoma hivi: “Yeye atakayeshinda atapambwa hivyo mavazi meupe ya nje; nami sitalifuta kwa vyovyote jina lake kutoka katika kitabu cha uzima.” Pia, kumbuka kwamba wale wazee 24 walikuwa ‘wamevikwa mavazi meupe ya nje, na juu ya vichwa vyao kulikuwa na mataji ya dhahabu.’ (Ufunuo 3:5; 4:4) Kwa hiyo, baada ya vita, njaa kali, na magonjwa kuanza kuikumba dunia, washiriki wa wale 144,000 ambao walikuwa wamekufa na ambao wanawakilishwa na damu iliyo chini ya madhabahu, walifufuliwa kwenye uhai wa kimbingu na kuvishwa kanzu nyeupe za mfano.

17. Wale wanaopokea kanzu nyeupe ‘wanapumzika’ katika njia gani?

17 Ni lazima watu hao waliotoka kufufuliwa “wapumzike.” Ni lazima wangojee kwa uvumilivu siku ya Mungu ya kisasi. “Watumwa wenzao,” yaani, Wakristo watiwa-mafuta ambao wangali duniani, wanapaswa kuthibitisha utimilifu wao chini ya majaribu. Wakati wa hukumu ya Mungu utakapofika, ‘pumziko’ hilo litakwisha. (Ufunuo 7:3) Wakati huo, wale waliofufuliwa watajiunga pamoja na Bwana Yesu Kristo katika kuwaharibu waovu, kutia ndani wale ambao walimwaga damu ya Wakristo wasio na hatia.—2 Wathesalonike 1:7-10.

Jinsi Mambo Haya Yanavyotuhusu

18, 19. (a) Kwa nini unaweza kukata kauli kwamba ufufuo wa kwanza unaendelea sasa? (b) Kuelewa ufufuo wa kwanza kunakufanya uhisi namna gani?

18 Neno la Mungu halionyeshi tarehe hususa ya ufufuo wa kwanza, lakini linafunua kwamba unatukia kwa muda fulani, wakati wa kuwapo kwa Kristo. Wakristo watiwa-mafuta waliokufa kabla ya kuwapo kwa Kristo kuanza ndio wanaofufuliwa kwanza. Kuwapo kwa Kristo kunapoendelea, Wakristo watiwa-mafuta wanaokufa duniani wanabadilishwa, “kufumba na kufumbua jicho,” na kuwa viumbe wa roho wenye nguvu. (1 Wakorintho 15:52) Je, watiwa-mafuta wote watapokea thawabu yao ya kimbingu kabla ya vita vya Har–Magedoni? Hatujui. Hata hivyo, tunajua kwamba, wakati wa Mungu ukifika, wale 144,000 wote watakuwa wamesimama kwenye Mlima Sayuni wa kimbingu.

19 Pia, tunajua kwamba idadi kubwa ya wale 144,000 tayari wameungana na Kristo. Ni wachache tu wanaobaki duniani. Ni uthibitisho wenye nguvu kama nini kwamba wakati wa Mungu wa kutekeleza hukumu yake unakaribia haraka! Hivi karibuni, ulimwengu wote wa Shetani utaharibiwa. Shetani mwenyewe atatupwa katika abiso. Kisha, ufufuo wa wanadamu kwa ujumla utaanza, na wanadamu waaminifu wataweza kuinuliwa kwa msingi wa fidia ya dhabihu ya Yesu na kuwa na ukamilifu kama ule ambao Adamu alipoteza. Unabii wa Yehova katika Mwanzo 3:15 unaendelea kutimizwa kwa njia ya ajabu. Ni pendeleo kubwa kama nini kuishi katika nyakati hizi!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Ili kupata uthibitisho wa Kimaandiko wa kwamba kuwapo kwa Kristo kulianza 1914, ona kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? ukurasa wa 215-218, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 10 Ili ujue kwa nini tunasema kwamba wazee 24 wanawakilisha Wakristo watiwa-mafuta wakiwa mbinguni katika vyeo vyao, ona Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! ukurasa wa 77, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

Maandiko yafuatayo yanatusaidia kwa njia gani kuelewa wakati ambapo “ufufuo wa kwanza” unatukia?

Ufunuo 12:7; 17:14

Ufunuo 7:13, 14

1 Wakorintho 15:23; 1 Wathesalonike 4:15-17

Ufunuo 6:2, 9-11

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ni ufufuo gani unaotukia kabla ya ufufuo wa wanadamu kwa ujumla?

[Picha katika ukurasa wa 29]

Watu fulani ambao walikuwa wamelala usingizi katika kifo wanapewa vazi jeupe jinsi gani?