Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Utakuwa na Shangwe Kwelikweli”

“Utakuwa na Shangwe Kwelikweli”

“Utakuwa na Shangwe Kwelikweli”

‘Utamfanyia Yehova sherehe, nawe utakuwa na shangwe kwelikweli.’—KUMBUKUMBU LA TORATI 16:15.

1. (a) Shetani alitokeza masuala gani? (b) Yehova alitabiri nini baada ya Adamu na Hawa kuasi?

SHETANI alipowaongoza Adamu na Hawa wamwasi Muumba wao, alitokeza masuala mawili muhimu sana. Kwanza, alitilia shaka ukweli wa Yehova na kufaa kwa njia yake ya kutawala. Pili, Shetani alidai kwamba wanadamu wanamtumikia Mungu kwa sababu tu za kichoyo. Suala hilo la pili lilitokezwa waziwazi wakati wa Ayubu. (Mwanzo 3:1-6; Ayubu 1:9, 10; 2:4, 5) Hata hivyo, Yehova alishughulikia hali hiyo haraka. Hata kabla Adamu na Hawa hawajafukuzwa kutoka katika bustani ya Edeni, Yehova alitabiri jinsi ambavyo angetatua masuala hayo. Alitabiri kuja kwa “uzao” ambao baada ya kutiwa jeraha kwenye kisigino, ungemponda Shetani kichwa na kumuua.—Mwanzo 3:15.

2. Yehova alifunua nini kuhusu njia ambayo angetumia kutimiza unabii ulio katika Mwanzo 3:15?

2 Kadiri wakati ulivyopita, Yehova alifunua habari zaidi kuhusu unabii huo, na hivyo kuonyesha kwamba mwishowe unabii huo ungetimia hakika. Kwa mfano, Mungu alimwambia Abrahamu kwamba “uzao” huo ungetokea kati ya wazao wake. (Mwanzo 22:15-18) Yakobo mjukuu wa Abrahamu akawa baba ya makabila 12 ya Israeli. Katika mwaka wa 1513 K.W.K., makabila hayo yalipokuwa taifa, Yehova aliwapa sheria ambazo zilitia ndani sherehe mbalimbali za kila mwaka. Mtume Paulo alisema kwamba sherehe hizo zilikuwa “kivuli cha mambo yanayokuja.” (Wakolosai 2:16, 17; Waebrania 10:1) Zilionyesha kimbele jinsi ambavyo Yehova angetimiza kusudi lake kuhusiana na Uzao huo. Kusherehekea sherehe hizo kuliwaletea Waisraeli shangwe kubwa. Kuchunguza sheria hizo kwa ufupi kutatia nguvu imani yetu kwamba ahadi za Yehova ni zenye kutegemeka.

Uzao Unatokea

3. Ni nani Uzao ulioahidiwa, naye alitiwa jeraha kwenye kisigino jinsi gani?

3 Miaka zaidi ya 4,000 baada ya unabii wa kwanza wa Yehova kutolewa, Uzao ulioahidiwa ulitokea. Uzao huo ni Yesu. (Wagalatia 3:16) Akiwa mwanadamu, Yesu alidumisha utimilifu wake hadi kifo na hivyo akathibitisha kwamba madai ya Shetani ni ya uwongo. Zaidi ya hayo, kwa kuwa Yesu hakuwa na dhambi, kifo chake kilikuwa dhabihu yenye thamani kubwa. Kupitia dhabihu hiyo, Yesu aliwaandalia wazao waaminifu wa Adamu na Hawa ukombozi kutoka katika dhambi na kifo. Yesu alipokufa kwenye mti wa mateso, Uzao ulioahidiwa ‘ulitiwa jeraha kwenye kisigino.’—Waebrania 9:11-14.

4. Dhabihu ya Yesu ilionyeshwa kimbele kwa njia gani?

4 Yesu alikufa Nisani 14, 33 W.K. * Katika Israeli, Nisani 14 ilikuwa siku yenye shangwe ya kusherehekea Pasaka. Kila mwaka katika Nisani 14, familia zilikula pamoja chakula kilichotia ndani mwana-kondoo asiye na kasoro. Kwa kufanya hivyo, walikumbuka umuhimu wa damu ya mwana-kondoo katika kuwakomboa wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli, wakati malaika alipoua wazaliwa wa kwanza wa Wamisri mnamo Nisani 14, mwaka wa 1513 K.W.K. (Kutoka 12:1-14) Mwana-kondoo wa Pasaka alifananisha Yesu, ambaye mtume Paulo alisema hivi kumhusu: “Kristo pasaka yetu ametolewa dhabihu.” (1 Wakorintho 5:7) Kama damu ya mwana-kondoo wa Pasaka, damu ya Yesu iliyomwagwa inatoa wokovu kwa ajili ya wengi.—Yohana 3:16, 36.

‘Matunda ya Kwanza ya Wale Waliokufa’

5, 6. (a) Yesu alifufuliwa wakati gani, na tukio hilo lilionyeshwa kimbele katika Sheria jinsi gani? (b) Ufufuo wa Yesu uliwezesha jinsi gani utimizo wa Mwanzo 3:15?

5 Katika siku ya tatu, Yesu alifufuliwa ili atoe thamani ya dhabihu yake kwa Baba yake. (Waebrania 9:24) Ufufuo wake ulionyeshwa kimbele katika sherehe nyingine. Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu ilianza Nisani 15. Siku iliyofuata, yaani, Nisani 16, Waisraeli walileta mganda wa matunda ya kwanza ya mavuno ya shayiri, ambayo yalikuwa mavuno ya kwanza kabisa katika Israeli, ili kuhani ayatikise mbele za Yehova. (Mambo ya Walawi 23:6-14) Inafaa kama nini kwamba siku hiyohiyo mwaka wa 33 W.K., Yehova alikomesha jitihada mbovu za Shetani za kumnyamazisha milele “shahidi [wake] mwaminifu na wa kweli”! Mnamo Nisani 16, 33 W.K., Yehova alimfufua Yesu kutoka kwa wafu na kumpa uhai wa roho usioweza kufa.—Ufunuo 3:14; 1 Petro 3:18.

6 Yesu akawa “matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala usingizi katika kifo.” (1 Wakorintho 15:20) Tofauti na wale waliokuwa wamefufuliwa mapema, Yesu hakufa tena. Badala yake, alipanda mbinguni na kuketi kwenye mkono wa kuume wa Yehova, ambako alingoja mpaka awekwe kuwa Mfalme wa Ufalme wa kimbingu wa Yehova. (Zaburi 110:1; Matendo 2:32, 33; Waebrania 10:12, 13) Kwa kuwa amewekwa kuwa Mfalme, Yesu anaweza sasa kumponda kichwa milele yule adui mkuu, Shetani, na kuuharibu uzao wake.—Ufunuo 11:15, 18; 20:1-3, 10.

Washiriki Zaidi wa Uzao wa Abrahamu

7. Sherehe ya Majuma ilikuwa nini?

7 Yesu ndiye Uzao ulioahidiwa huko Edeni na Yehova atamtumia ‘kuzivunja kazi za Ibilisi.’ (1 Yohana 3:8) Lakini, Yehova aliposema na Abrahamu, alionyesha kwamba “uzao” wa Abrahamu ungekuwa zaidi ya mtu mmoja tu. Ungekuwa “kama nyota za mbinguni na kama chembe za mchanga zilizo kando ya bahari.” (Mwanzo 22:17) Kutokea kwa washiriki wengine wa “uzao” huo kulionyeshwa kimbele na sherehe nyingine yenye shangwe. Siku 50 kuanzia Nisani 16, Waisraeli walisherehekea Sherehe ya Majuma. Sheria kuhusu sherehe hiyo inasema: “Mpaka siku inayofuata sabato ya 7 mtahesabu, siku 50, nanyi mtamtolea Yehova toleo jipya la nafaka. Kutoka katika makao yenu mtaleta mikate miwili iwe toleo la kutikisa. Itakuwa ya sehemu mbili za kumi za efa ya unga laini. Itaokwa ikiwa imetiwa chachu, kama matunda ya kwanza yaliyoiva kwa Yehova.” *Mambo ya Walawi 23:16, 17, 20.

8. Ni jambo gani la maana lililotukia katika Pentekoste ya 33 W.K.?

8 Yesu alipokuwa duniani, Sherehe ya Majuma ilikuwa ikiitwa Pentekoste (kutokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “-a 50”). Katika Pentekoste ya 33 W.K., Kuhani Mkuu zaidi, Yesu Kristo aliyefufuliwa, alimwaga roho takatifu juu ya kikundi kidogo cha wanafunzi 120 waliokusanyika Yerusalemu. Hivyo, wanafunzi hao wakawa wana wa Mungu waliotiwa mafuta na pia wakawa ndugu za Yesu Kristo. (Waroma 8:15-17) Wakawa pia taifa jipya, “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16) Kuanzia hapo, taifa hilo dogo lingeongezeka na kuwa na washiriki 144,000.—Ufunuo 7:1-4.

9, 10. Kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lilionyeshwa kimbele siku ya Pentekoste jinsi gani?

9 Kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lilionyeshwa kimbele na ile mikate miwili iliyotiwa chachu ambayo ilitikiswa mbele za Yehova kila siku ya Pentekoste. Kutiwa chachu kwa mikate hiyo kulionyesha kwamba Wakristo watiwa-mafuta bado wangekuwa na chachu ya dhambi waliyorithi. Hata hivyo, wangeweza kumkaribia Yehova kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu. (Waroma 5:1, 2) Kwa nini mikate miwili ilitumiwa? Huenda hilo lilionyesha uhakika wa kwamba wana hao wa Mungu waliotiwa mafuta wangetoka katika vikundi viwili, kwanza kutoka kwa Wayahudi wa asili, na baadaye kutoka kwa Watu wa Mataifa.—Wagalatia 3:26-29; Waefeso 2:13-18.

10 Mikate miwili iliyotolewa siku ya Pentekoste ilitokana na matunda ya kwanza ya mavuno ya ngano. Kwa njia inayolingana, Wakristo waliozaliwa kwa roho wanaitwa “sehemu fulani ya matunda ya kwanza ya viumbe vyake.” (Yakobo 1:18) Wao ndio wa kwanza kusamehewa dhambi kwa msingi wa damu iliyomwagwa ya Yesu, na hilo linawawezesha kupewa uhai usioweza kufa huko mbinguni ambako watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme wake. (1 Wakorintho 15:53; Wafilipi 3:20, 21; Ufunuo 20:6) Wakiwa wana wa kimbingu, hivi karibuni ‘watachunga mataifa kwa fimbo ya chuma’ na kuona ‘Shetani akipondwa chini ya miguu yao.’ (Ufunuo 2:26, 27; Waroma 16:20) Mtume Yohana alisema: “Hao ndio wale wanaoendelea kumfuata Mwana-Kondoo popote anapoenda. Hao walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.”—Ufunuo 14:4.

Siku Iliyokazia Ukombozi

11, 12. (a) Ni nini kilichotukia Siku ya Upatanisho? (b) Waisraeli walipata faida gani kutokana na dhabihu za ng’ombe-dume na mbuzi?

11 Katika siku ya kumi ya mwezi wa Ethanimu (baadaye uliitwa Tishri), * Waisraeli walifanya sherehe ambayo ilionyesha kimbele jinsi ambavyo thamani ya dhabihu ya fidia ya Yesu ingetumiwa. Siku hiyo, taifa lote lilikusanyika pamoja kwa ajili ya Siku ya Upatanisho ili dhabihu zitolewe kwa ajili yao kwa kusudi kufunika dhambi zao.—Mambo ya Walawi 16:29, 30.

12 Siku ya Upatanisho, kuhani mkuu alichinja ng’ombe-dume mchanga na kunyunyiza sehemu ya damu yake mara saba mbele ya kifuniko cha Sanduku, akiwa katika Patakatifu Zaidi, na hivyo kwa njia ya mfano akatoa damu mbele za Yehova. Toleo hilo lilikuwa kwa ajili ya dhambi za kuhani mkuu na “nyumba yake,” makuhani wadogo na Walawi. Kisha, kuhani mkuu alichukua mbuzi wawili. Alichinja mbuzi mmoja kama toleo la dhambi “kwa ajili ya watu.” Sehemu ya damu ya mbuzi huyo pia ilinyunyizwa mbele ya kifuniko cha Sanduku lililokuwa katika Patakatifu Zaidi. Baadaye, kuhani mkuu aliweka mikono yake juu ya kichwa cha mbuzi wa pili na kuungama makosa ya wana wa Israeli. Kisha, akaagiza mbuzi huyo apelekwe nyikani. Mbuzi huyo alichukua kwa njia ya mfano dhambi za taifa.—Mambo ya Walawi 16:3-16, 21, 22.

13. Matukio katika Siku ya Upatanisho yalionyesha kimbele daraka la Yesu jinsi gani?

13 Kama matukio hayo yalivyoonyesha kimbele, Kuhani Mkuu zaidi, Yesu, anatumia thamani ya damu yake mwenyewe ili kutoa msamaha wa dhambi. Kwanza, thamani ya damu yake inatumiwa kwa ajili ya “nyumba ya kiroho” ya Wakristo watiwa-mafuta 144,000, ikiwawezesha kutangazwa kuwa waadilifu na kuwa na msimamo safi mbele za Yehova. (1 Petro 2:5; 1 Wakorintho 6:11) Hilo lilionyeshwa kimbele na dhabihu ya ng’ombe-dume. Hivyo, watiwa-mafuta wanapata nafasi ya kupokea urithi wao wa kimbingu. Pili, thamani ya damu ya Yesu inatumiwa kwa ajili ya mamilioni ya wengine wanaomwamini Kristo, kama inavyoonyeshwa na dhabihu ya mbuzi. Watu hao watapata baraka ya uzima wa milele hapa duniani, urithi ambao Adamu na Hawa walipoteza. (Zaburi 37:10, 11) Kwa msingi wa damu hiyo iliyomwagwa, Yesu anachukua na kuondolea mbali dhambi za wanadamu, kama vile tu mbuzi aliye hai alivyochukua kwa njia ya mfano dhambi za Waisraeli mpaka nyikani.—Isaya 53:4, 5.

Kushangilia Mbele za Yehova

14, 15. Ni nini kilichotukia wakati wa Sherehe ya Vibanda, na sherehe hiyo iliwakumbusha Waisraeli nini?

14 Baada ya Siku ya Upatanisho, Waisraeli walisherehekea Sherehe ya Vibanda, sherehe ambayo ilikuwa yenye shangwe zaidi katika mwaka wa Kiyahudi. (Mambo ya Walawi 23:34-43) Sherehe hiyo ilifanywa kuanzia siku ya 15 mpaka siku ya 21 ya mwezi wa Ethanimu, nayo ilimalizika kwa kusanyiko kuu lililofanywa siku ya 22 ya mwezi huo. Sherehe hiyo ilionyesha mwisho wa kipindi cha kukusanya mavuno, na ilikuwa pindi ya kutoa shukrani kwa ajili ya wema mwingi wa Mungu. Kwa sababu hiyo, Yehova aliwaamuru hivi watu waliofanya sherehe: “Yehova Mungu wako atakubariki katika mazao yako yote na katika kila tendo la mkono wako, nawe utakuwa na shangwe kwelikweli.” (Kumbukumbu la Torati 16:15) Ulikuwa wakati wenye furaha kama nini!

15 Wakati wa sherehe hiyo, Waisraeli walikaa katika vibanda kwa siku saba. Hilo liliwakumbusha kwamba wakati fulani walikaa katika vibanda nyikani. Sherehe hiyo iliwapa nafasi ya kutosha ya kutafakari kuhusu jinsi Yehova alivyowatunza kama baba. (Kumbukumbu la Torati 8:15, 16) Na kwa kuwa wote, matajiri kwa maskini, walikaa katika vibanda vilivyofanana, Waisraeli walikumbushwa kwamba kuhusiana na sherehe hiyo, wote walikuwa sawa.—Nehemia 8:14-16.

16. Sherehe ya Vibanda ilionyesha nini kimbele?

16 Sherehe ya Vibanda ilikuwa sherehe ya mavuno, sherehe yenye shangwe ya kukusanya, ambayo ilionyesha kimbele kazi yenye shangwe kukusanya wale wanaomwamini Yesu Kristo. Kazi hiyo ilianza katika Pentekoste ya 33 W.K., wakati wanafunzi 120 wa Yesu walipotiwa mafuta wawe sehemu ya “ukuhani mtakatifu.” Kama vile Waisraeli walikaa katika vibanda kwa siku chache, watiwa-mafuta wanajua kwamba wao ni “wakaaji wa muda” katika ulimwengu huu usiomwogopa Mungu. Wana tumaini la kwenda mbinguni. (1 Petro 2:5, 11) Kazi ya kukusanya Wakristo watiwa-mafuta inafikia mwisho wake katika ‘siku hizi za mwisho,’ wakati washiriki wa mwisho wa wale 144,000 wanapokusanywa.—2 Timotheo 3:1.

17, 18. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba watu wengine ambao si Wakristo watiwa-mafuta wanapata faida kutokana na dhabihu ya Yesu? (b) Ni nani wanaofaidika leo na Sherehe ya Vibanda ya mfano, na sherehe hiyo yenye shangwe itafikia kilele chake wakati gani?

17 Inapendeza kujua kwamba wakati wa sherehe hiyo ya zamani, ng’ombe-dume 70 walitolewa. (Hesabu 29:12-34) Namba 70 ni 7 mara 10. Katika Biblia, namba 7 na 10 zinafananisha ukamilifu wa kimbingu na wa kidunia. Hivyo, dhabihu ya Yesu itafaidi waaminifu kutoka katika familia zote 70 za wanadamu ambazo zilitokana na Noa. (Mwanzo 10:1-29) Kupatana na hilo, katika wakati wetu, kazi ya kukusanya imepanuliwa ili kuwakusanya watu mmoja-mmoja kutoka katika mataifa yote ambao wanamwamini Yesu na wanatumaini kuishi katika paradiso duniani.

18 Mtume Yohana aliona katika maono kazi hiyo ya kukusanya inayofanywa leo. Kwanza, alisikia tangazo kuhusu kutiwa muhuri kwa washiriki wa mwisho wa wale 144,000. Kisha, akaona “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu,” wakiwa wamesimama mbele za Yehova na Yesu, wakiwa na “matawi ya mitende mikononi mwao.” Hao ndio “wanaotoka katika ile dhiki kuu” na kuingia katika ulimwengu mpya. Sasa, wao pia ni wakaaji wa muda katika mfumo huu wa kale, nao wanatazamia kwa uhakika wakati ambapo “Mwana-Kondoo . . . atawachunga, na kuwaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima.” Wakati huo, “Mungu atafuta kila chozi katika macho yao.” (Ufunuo 7:1-10, 14-17) Sherehe ya Vibanda ya mfano itafikia kilele chake baada ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, wakati umati mkubwa pamoja na waaminifu watakaofufuliwa watakapopewa uzima wa milele.—Ufunuo 20:5.

19. Ni faida gani tunayopata kwa kuchunguza sherehe zilizofanywa huko Israeli?

19 Sisi pia tunaweza kuwa na “shangwe kwelikweli” tunapotafakari kuhusu maana ya sherehe hizo za zamani za Kiyahudi. Inasisimua kujua kwamba Yehova alionyesha kimbele jinsi ambavyo unabii wake uliotolewa huko Edeni ungetimizwa, na inafurahisha sana kuona ukitimia kihalisi hatua kwa hatua. Leo, tunajua kwamba Uzao umetokea na kwamba umetiwa jeraha kwenye kisigino. Sasa Uzao huo ni Mfalme wa kimbingu. Zaidi ya hayo, wengi wa wale 144,000 tayari wamethibitisha uaminifu wao mpaka kifo. Ni nini kinachobaki? Ni muda gani unaobaki ili unabii huo utimizwe kikamili? Habari hiyo itazungumzwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Mwezi wa Nisani unalingana na Machi/Aprili (Mwezi wa 3/4) katika kalenda tunayotumia leo.

^ fu. 7 Wakati mikate miwili iliyotiwa chachu ilipotolewa kama toleo la kutikisa, mara nyingi kuhani aliibeba mikate hiyo kwenye viganja vyake, kisha akainua mikono yake na kuipeleka mikate hiyo huku na huku. Tendo hilo la kutikisa lilifananisha kutolewa kwa vitu vilivyotolewa dhabihu kwa Yehova.—Ona Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 528 au Étude Perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 850, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 11 Mwezi wa Ethanimu, au Tishri, unalingana na Septemba/Oktoba (Mwezi wa 9 na wa 10) katika kalenda tunayotumia leo.

Je, Unaweza Kueleza?

• Mwana-kondoo wa Pasaka alionyesha nini kimbele?

• Ni kazi gani ya kukusanya iliyoonyeshwa kimbele na Sherehe ya Pentekoste?

• Ni mambo gani yaliyofanywa Siku ya Upatanisho ambayo yalionyesha kimbele jinsi dhabihu ya fidia ya Yesu inavyotumiwa?

• Kukusanywa kwa Wakristo kulionyeshwa kimbele na Sherehe ya Vibanda jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Chati katika ukurasa wa 22, 23]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Pasaka

Nisani 14

Tukio:

Mwana-kondoo wa Pasaka achinjwa

Kimbele:

Yesu atolewa kama dhabihu

Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu (Nisani 15-21)

Nisan 15

Tukio:

Sabato

Nisani 16

Tukio:

Shayiri yatolewa

Kimbele:

Yesu afufuliwa

Siku 50

Sherehe ya Majuma (Pentekoste)

Sivani 6

Tukio:

Mikate miwili yatolewa

Kimbele:

Yesu alimtolea Yehova ndugu zake watiwa-mafuta

Siku ya Upatanisho

Tishri 10

Tukio:

Ng’ombe-dume na mbuzi wawili watolewa

Kimbele:

Yesu atoa thamani ya damu yake kwa ajili ya wanadamu wote

Sherehe ya Vibanda (Kukusanya, Mahema)

Tishri 15-21

Tukio:

Waisraeli washangilia kukaa katika vibanda na kushangilia mavuno, ng’ombe-dume 70 watolewa

Kimbele:

Kukusanywa kwa watiwa-mafuta na “umati mkubwa”

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kama damu ya mwana-kondoo wa Pasaka, damu ya Yesu iliyomwagwa inaandaa wokovu kwa ajili ya wengi

[Picha katika ukurasa wa 22]

Matunda ya kwanza ya mavuno ya shayiri ambayo yalitolewa Nisani 16 yalionyesha kimbele ufufuo wa Yesu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ile mikate miwili iliyotolewa siku ya Pentekoste ilionyesha kimbele kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta

[Picha katika ukurasa wa 24]

Sherehe ya Vibanda ilionyesha kimbele kazi yenye shangwe ya kukusanya watiwa-mafuta na “umati mkubwa” kutoka katika mataifa yote