Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wahitimu wa Gileadi Wapokea Mafundisho Yanayogusa Moyo

Wahitimu wa Gileadi Wapokea Mafundisho Yanayogusa Moyo

Wahitimu wa Gileadi Wapokea Mafundisho Yanayogusa Moyo

MNAMO Septemba 9, 2006 (9/9/2006), programu ya kuhitimu ya darasa la 121 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) ilifanywa katika Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York. Ilikuwa programu yenye kutia moyo.

Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alianzisha programu hiyo kwa kuwakaribisha wahitimu 56 na wahudhuriaji 6,366 kutoka mataifa mbalimbali. Alizungumzia andiko la Zaburi 86:11, linalosema: “Unifundishe, Ee Yehova, juu ya njia yako. Nitatembea katika kweli yako. Unganisha moyo wangu ili kuliogopa jina lako.” Ndugu Jackson alitaja mambo matatu yanayokaziwa katika mstari huo. Alisema: “Katika sentensi ya kwanza, ni mafundisho; katika sentensi ya pili, ni matumizi; na katika sentensi ya tatu, ni kichocheo. Mambo hayo matatu ni muhimu hasa kwenu ninyi wamishonari mnapoondoka kwenda kwenye migawo yenu.” Kisha, akawakaribisha wasemaji ambao walikazia mambo hayo matatu katika hotuba na mahojiano yao.

Mafundisho Yenye Kutia Moyo

William Malenfant, anayetumika katika makao makuu, alitoa hotuba yenye kichwa “Maisha Bora Kabisa.” Alizungumza kuhusu mfano wa Maria, dada ya Martha. Pindi moja Yesu alipowatembelea nyumbani kwao, Maria alichagua kuketi miguuni pa Yesu na kumsikiliza naye alitanguliza jambo hilo. Yesu alimwambia Martha hivi: “Maria alichagua fungu jema, nalo halitaondolewa kwake.” (Luka 10:38-42) “Wazia hilo,” msemaji akasema. “Maria atakumbuka milele na milele kwamba aliketi miguuni pa Yesu na kusikiliza uso kwa uso kweli za ajabu za kiroho, kwa sababu tu alichagua fungu jema.” Baada ya kuwapongeza wahitimu kwa sababu ya uchaguzi wao mzuri wa kiroho, alisema hivi: “Uchaguzi wenu umewaongoza kwenye maisha bora kabisa.”

Kisha, Anthony Morris, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, akazungumzia kichwa “Mvaeni Bwana Yesu Kristo,” ambacho kilitegemea Waroma 13:14. Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? ‘Kumvaa Bwana Yesu Kristo’ kunatia ndani “kuiga tabia za Bwana.” Hivyo, hilo linamaanisha kuiga mfano na mtazamo wa Yesu. “Yesu alifanya watu wajihisi wamestarehe,” msemaji akasema, “kwa sababu aliwajali kikweli, nao waliweza kutambua jambo hilo.” Halafu msemaji akaonyesha jinsi wanafunzi walivyokuwa wamejifunza mambo mengi katika Shule ya Gileadi, ‘ili waweze kufahamu kabisa akilini upana na urefu na kimo na kina’ cha kweli, kama vile andiko la Waefeso 3:18 linavyosema. Lakini akawakumbusha kuhusu mstari wa 19, unaosema: “Na kuujua upendo wa Kristo ambao unazidi ujuzi.” Ndugu Morris aliwahimiza wanafunzi hivi: “Mnapoendelea kujifunza kibinafsi, fikirieni jinsi mnavyoweza kuiga upendo na huruma za Kristo na ‘mmvae Bwana Yesu Kristo’ kikweli.”

Mashauri ya Mwisho Kutoka kwa Walimu wa Gileadi

Hotuba iliyofuata ilitolewa na Wallace Liverance, mwalimu wa Shule ya Gileadi. Kichwa cha hotuba yake kilitegemea andiko la Methali 4:7. Alisema kwamba ijapokuwa hekima kutoka kwa Mungu ni muhimu zaidi, tunapaswa pia ‘kujipatia uelewaji,’ ambao unatia ndani kuunganisha mambo mbalimbali ya hakika kisha kuona jinsi mambo hayo yanavyohusiana ili kupata maana kamili ya suala fulani. Msemaji alionyesha kwamba kujipatia uelewaji kunatuletea shangwe. Kwa mfano, katika siku za Nehemia, Walawi ‘walikuwa wakifafanua sheria’ na ‘kueleza maana yake.’ Baadaye, watu ‘wakashangilia sana, kwa maana walikuwa wameelewa maneno ambayo walijulishwa.’ (Nehemia 8:7, 8, 12) Ndugu Liverance alimalizia hivi: “Shangwe inatokana na kuelewa Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho.”

“Adui Yako Ni Nani Hasa?” ndicho kichwa cha hotuba iliyotolewa na Mark Noumair, mwalimu mwingine wa Shule ya Gileadi. Katika vita, askari-jeshi kadhaa wanauawa kimakosa na askari walio katika kikosi chao wenyewe. “Namna gani katika vita vya kiroho tunavyopigana?” akauliza. “Tusipokuwa waangalifu, tunaweza kuchanganyikiwa tusitambue maadui wetu ni nani hasa na tuwaumize askari-jeshi wenzetu.” Wivu unaweza kuwafanya watu fulani washindwe kuwatambua maadui wao. Ulimfanya Mfalme Sauli ajaribu kumuua Daudi, mwabudu mwenzake, lakini Wafilisti hasa ndio waliokuwa maadui wake. (1 Samweli 18:7-9; 23:27, 28) Kisha, msemaji akaendelea kusema: “Namna gani ikiwa mnatumika pamoja na mmishonari aliye na ustadi katika mambo mengi? Je, utamuumiza askari-jeshi mwenzako kwa kumchambua vikali, au utadumisha amani na kukubali kwamba wengine wana ustadi kuliko wewe katika mambo mbalimbali? Kukazia sana fikira udhaifu wa wengine kunaweza kutufanya tuchanganyikiwe na kushindwa kutambua ni nani hasa aliye adui yetu. Pigana na adui mwenyewe, Shetani.”

Mambo Yaliyoonwa Yenye Kupendeza na Mahojiano Yenye Kuelimisha

Sehemu iliyofuata yenye kichwa, “Fanya Kazi ya Mweneza-injili,” ilitolewa na Lawrence Bowen, mwalimu wa Shule ya Gileadi, nayo ilitia ndani mahojiano na mambo yaliyoonwa. Alisema kwamba “kazi kuu ya mmishonari aliyezoezwa katika Shule ya Gileadi ni kueneza habari njema, na wanafunzi wa darasa hili walifanya hivyo popote walipopata watu.” Mambo fulani yaliyoonwa yenye kupendeza yaliigizwa.

Sehemu mbili zilizofuata zilitolewa na Michael Burnett na Scott Shoffner, ambao ni washiriki wa familia ya Betheli. Waliwahoji washiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Australia, Barbados, Korea, na Uganda. Maelezo ya washiriki hao wa halmashauri za tawi yalionyesha jitihada kubwa inayofanywa ili kushughulikia mahitaji ya wamishonari, kutia ndani kuwaandalia makao mazuri na huduma za afya. Washiriki hao wa halmashauri za tawi walikazia kwamba wamishonari ambao wanafanikiwa wako tayari kubadilika kulingana na hali za mahali wanakotumika.

Umalizio Wenye Kuchochea

Hotuba ya msingi ya programu hiyo ilikuwa na kichwa “Mwogopeni Mungu na Kumpa Utukufu.” Hotuba hiyo ilitolewa na John E. Barr, mshiriki wa muda mrefu wa Baraza Linaloongoza. Alizungumzia andiko la Ufunuo 14:6, 7, ambalo linasema: “Nikamwona malaika mwingine akiruka katikati ya mbingu, naye alikuwa na habari njema ya milele ili aitangaze kuwa habari za furaha kwa wale wanaokaa duniani, na kwa kila taifa na kabila na lugha na watu, akisema kwa sauti kubwa: ‘Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika.’”

Ndugu Barr aliwahimiza wanafunzi wakumbuke mambo matatu kumhusu malaika huyo. Kwanza, alipaswa kutangaza habari njema ya milele ya kwamba Kristo sasa anatawala akiwa na mamlaka kamili ya Ufalme. Msemaji alisema: “Tuna hakika kabisa kwamba Yesu aliwekwa kuwa mfalme mwaka wa 1914. Hivyo, habari hizo za furaha zinapasa kutangazwa duniani pote.” Pili, malaika alisema: “Mwogopeni Mungu.” Msemaji alieleza kwamba wahitimu wanapaswa kuwasaidia wanafunzi wao wa Biblia wamheshimu na kumwogopa Mungu ili wasifanye jambo lolote linalomchukiza. Tatu, malaika aliamuru hivi: ‘Mpeni Mungu utukufu.’ “Msisahau,” akawahimiza wanafunzi, “tunatumikia ili kumletea Mungu utukufu, wala si kujiletea utukufu.” Kisha akizungumza kuhusu “saa ya hukumu,” Ndugu Barr alisema: “Wakati unaobaki kabla ya hukumu ya mwisho kutangazwa ni mfupi. Maisha ya watu yamo hatarini. Bado kuna watu wengi katika maeneo yetu wanaohitaji kusikia ujumbe wa habari njema kabla ya wakati kwisha.”

Huku wakikumbuka maneno hayo, wahitimu hao 56 walipewa diploma zao na kutumwa kwenye sehemu za mbali za dunia. Mioyo ya wahitimu na ya watu wengine wote waliohudhuria programu hiyo iliguswa sana na mashauri yenye kuchochea ambayo walipewa siku hiyo yenye kupendeza.

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi ambazo zimewakilishwa: 6

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 25

Idadi ya wanafunzi: 56

Wastani wa umri: 35.1

Wastani wa miaka katika kweli: 18.3

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13.9

[Picha katika ukurasa wa 18]

Darasa la 121 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Fox, Y.; Kunicki, D.; Wilkinson, S.; Kawamoto, S.; Consolandi, G.; Mayen, C. (2) Santiago, N.; Clancy, R.; Fischer, M.; de Abreu, L.; Davis, E. (3) Hwang, J.; Hoffman, D.; Wridgway, L.; Ibrahim, J.; Dabelstein, A.; Bakabak, M. (4)Peters, M.; Jones, C.; Ford, S.; Parra, S.; Rothrock, D.; Tatlot, M.; Perez, E. (5) de Abreu, F.; Kawamoto, S.; Ives, S.; Burdo, J.; Hwang, J.; Wilkinson, D. (6) Fox, A.; Bakabak, J.; Cichowski, P.; Forier, C.; Mayen, S.; Consolandi, E.; Wridgway, W. (7) Parra, B.; Perez, B.; Tatlot, P.; Santiago, M.; Ibrahim, Y.; Kunicki, C. (8) Burdo, C.; Cichowski, B.; Ives, K.; Ford, A.; Rothrock, J.; Hoffman, D.; Davis, M. (9) Peters, C.; Dabelstein, C.; Jones, K.; Clancy, S.; Fischer, J.; Forier, S.