Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fundisha Yale Ambayo Biblia Inafundisha Hasa

Fundisha Yale Ambayo Biblia Inafundisha Hasa

Fundisha Yale Ambayo Biblia Inafundisha Hasa

“Mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha.”—MATHAYO 28:19, 20.

1. Biblia imesambazwa kwa kadiri gani?

NENO LA YEHOVA, Biblia Takatifu, ni mojawapo ya vitabu vya zamani sana na pia ni moja ya vitabu ambavyo vimesambazwa sana ulimwenguni. Imetafsiriwa kwa sehemu katika lugha zaidi ya 2,300. Zaidi ya asilimia 90 ya watu duniani wana Biblia katika lugha yao.

2, 3. (a) Kwa nini kuna mvurugo kuhusu mafundisho ya Biblia? (b) Tutazungumzia maswali gani?

2 Mamilioni ya watu wanasoma sehemu fulani ya Biblia kila siku. Wengine wamesoma Biblia nzima mara nyingi. Maelfu ya dini zinadai kwamba mafundisho yao yanategemea Biblia, lakini hazikubaliani kuhusu yale ambayo inafundisha. Mvurugo ni mkubwa hata zaidi kwa sababu wafuasi wa dini ileile hawaelewani hata kidogo. Kuna wale walio na mashaka kuhusu Biblia, chanzo chake, na umuhimu wake. Wengi wanaiona kuwa kitabu kitakatifu kinachotumiwa tu katika sherehe za kufanya nadhiri au kuapa kusema ukweli mahakamani.

3 Kwa kweli, Biblia ina maneno au ujumbe wenye nguvu wa Mungu kwa wanadamu. (Waebrania 4:12) Kwa hiyo, tukiwa Mashahidi wa Yehova tunataka watu wajifunze yale ambayo Biblia inafundisha. Tunafurahi kufanya kazi ambayo Yesu Kristo aliwapa wafuasi wake aliposema hivi: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha.” (Mathayo 28:19, 20) Katika huduma yetu ya hadharani, tunakutana na watu wanyoofu ambao wanaumia moyoni kwa sababu ya mvurugo wa kidini ambao umeenea sana ulimwenguni. Wanataka kujua ukweli kumhusu Muumba na wanatamani kujifunza yale ambayo Biblia inasema kuhusu kusudi la maisha. Acheni tuzungumzie maswali matatu ambayo yanawahangaisha watu wengi. Kuhusiana na kila swali, tutazungumzia mafundisho yasiyo sahihi ya viongozi wa kidini, kisha tutazungumzia yale ambayo Biblia inafundisha hasa. Maswali hayo ni: (1) Je, Mungu anatujali? (2) Kwa nini tupo hapa? (3) Inakuwaje tunapokufa?

Je, Mungu Anajali?

4, 5. Kwa nini watu wanafikiri kwamba Mungu hatujali?

4 Acheni tuanze na swali, Je, Mungu anatujali? Inasikitisha kwamba watu wengi wanafikiri kwamba Mungu hajali. Kwa nini wanafikiri hivyo? Sababu moja ni kwamba wanaishi katika ulimwengu uliojaa chuki, vita, na mateso. Wanasema, ‘Ikiwa Mungu anajali kikweli, bila shaka angezuia mambo hayo yenye kuhuzunisha yasitukie.’

5 Sababu nyingine inayowafanya watu wafikiri kwamba Mungu hatujali ni kwamba viongozi wa kidini wamewafanya wafikiri hivyo. Mara nyingi viongozi wa kidini wanasema nini msiba unapotokea? Mwanamke mmoja alipofiwa na watoto wake wawili wadogo katika aksidenti ya gari, kasisi wao alisema hivi: “Hayo yalikuwa mapenzi ya Mungu. Mungu alihitaji malaika wengine wawili.” Viongozi wa kidini wanaposema mambo kama hayo, kwa kweli wanamlaumu Mungu kwa sababu ya mambo mabaya yanayotukia. Hata hivyo, mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Yehova Mungu hasababishi kamwe mambo maovu. ‘Hasha, Mungu wa kweli hatendi kwa uovu.’—Ayubu 34:10.

6. Ni nani anayesababisha uovu na mateso ulimwenguni?

6 Basi, kwa nini kuna uovu na mateso mengi sana? Sababu moja ni kwamba kwa ujumla wanadamu wamemkataa Mungu kuwa Mtawala, hawataki kutii sheria na kanuni zake za uadilifu. Wanadamu wamejitiisha bila kujua chini ya Shetani, Mpinzani wa Mungu, kwa kuwa “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Kujua jambo hilo la hakika kunafanya iwe rahisi kwetu kuelewa kwa nini hali ni mbaya. Shetani ni mwovu, ana chuki, ni mdanganyifu, na mkatili. Kwa hiyo, tunapaswa kutarajia ulimwengu uwe kama mtawala wake. Haishangazi kwamba kuna uovu mwingi sana!

7. Ni sababu gani nyingine zinazofanya tuteseke?

7 Sababu nyingine inayofanya tuteseke ni kutokamilika kwa wanadamu. Wanadamu wenye dhambi wanapambana ili watawale, na mara nyingi mapambano hayo yanasababisha vita, uonevu, na kuteseka. Kwa kufaa, andiko la Mhubiri 8:9 linasema hivi: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” Sababu nyingine inayofanya tuteseke ni “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11) Mara nyingi, watu wanapata msiba kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa.

8, 9. Tunajua jinsi gani kwamba Yehova kwa kweli anatujali?

8 Inafariji kujua kwamba Yehova hasababishi kuteseka. Lakini je, kweli Mungu anajali mambo yanayotukia maishani mwetu? Jibu lenye kutia moyo kwa swali hilo ni ndiyo! Tunajua kwamba Yehova anajali kwa sababu katika Neno lake lililoongozwa kwa roho yake anatuambia kwa nini amewaacha wanadamu wafuate njia isiyofaa. Mungu amefanya hivyo kwa sababu ya masuala mawili: suala la enzi yake kuu na la utimilifu wa wanadamu. Kwa kuwa Yehova ni Muumba mweza-yote, si lazima atuambie kwa nini anawaacha wanadamu wateseke. Hata hivyo, anatuambia kwa sababu anatujali.

9 Fikiria sababu nyingine zinazothibitisha kwamba Mungu anatujali. ‘Aliumia moyoni mwake’ ubaya ulipojaa duniani katika siku za Noa. (Mwanzo 6:5, 6) Je, Mungu anahisi tofauti leo? Hapana, kwa kuwa yeye habadiliki. (Malaki 3:6) Anachukia ukosefu wa haki na anachukia kuona watu wakiteseka. Biblia inafundisha kwamba hivi karibuni Mungu ataondoa madhara yote ambayo yamesababishwa na utawala wa wanadamu na uvutano wa Ibilisi. Je, uthibitisho huo hautusadikishi kwamba Mungu anatujali?

10. Yehova anahisi namna gani kuhusu mateso yanayowapata wanadamu?

10 Viongozi wa kidini hawasemi ukweli kumhusu Mungu wanaposema kwamba misiba inayotupata ni mapenzi yake. Ukweli ni kwamba Yehova anatamani kukomesha mateso yanayowapata wanadamu. Andiko la 1 Petro 5:7 linasema: “Yeye anawajali ninyi.” Hivyo ndivyo Biblia inavyofundisha hasa!

Kwa Nini Tupo Hapa?

11. Mara nyingi dini za ulimwengu zinasema nini kuhusu maisha ya wanadamu duniani?

11 Acheni sasa tuzungumzie swali la pili ambalo linawahangaisha watu wengi, Kwa nini tupo hapa? Mara nyingi, dini za ulimwengu zinasema kwamba wanadamu ni wapita-njia tu hapa duniani. Wanaiona dunia yetu kuwa mahali pa kupumzikia tu, au jiwe la kukanyagia, wakiwa njiani kwenda kuishi mahali pengine. Viongozi fulani wa kidini wanafundisha uwongo wa kwamba siku moja Mungu ataiharibu dunia hii. Kwa sababu ya mafundisho kama hayo, watu wengi wamekata kauli kwamba ni afadhali waponde raha kabisa kwa sababu kifo tu ndicho kinawangojea. Biblia inafundisha nini hasa kuhusu kwa nini tupo hapa?

12-14. Biblia inafundisha nini kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia na wanadamu?

12 Mungu ana kusudi zuri sana kwa ajili ya dunia na wanadamu. “Hakuiumba tu [dunia] bila sababu” bali “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Kwa kuongezea, Yehova “ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Kujua mambo hayo kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia na wanadamu kunaweza kutusaidia kuelewa kwa nini tupo hapa.

13 Kitabu cha Mwanzo sura ya 1 na ya 2 kinaonyesha kwamba Yehova aliiumba dunia kwa njia nzuri sana ili wanadamu waishi humo. Kuelekea mwishoni mwa kipindi cha uumbaji kinachohusu dunia yetu, kila kitu kilikuwa “chema sana.” (Mwanzo 1:31) Mungu alimweka mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, katika bustani maridadi sana ya Edeni na kuwapa chakula kingi kizuri. Wanadamu hao wawili wa kwanza waliambiwa hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” Walipaswa kuzaa watoto wakamilifu, kupanua mipaka ya makao yao ya bustani duniani pote, na kuwatawala wanyama kwa upendo.—Mwanzo 1:26-28.

14 Kusudi la Yehova ni kwamba jamii ya wanadamu wakamilifu waishi duniani milele. Neno la Mungu linasema: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Kwa kweli, wanadamu waliumbwa ili wafurahie uzima wa milele katika Paradiso duniani. Hilo ndilo kusudi la Mungu, na hivyo ndivyo Biblia inavyofundisha hasa!

Inakuwaje Tunapokufa?

15. Dini nyingi za ulimwengu zinafundisha nini kuhusu hali yetu tunapokufa?

15 Sasa acheni tuzungumzie swali la tatu ambalo linawahangaisha watu wengi: Inakuwaje tunapokufa? Dini nyingi za ulimwengu zinafundisha kwamba kuna kitu fulani ndani ya mwili wa mwanadamu ambacho kinaendelea kuishi baada ya mwili kufa. Dini fulani bado zinashikilia wazo la kwamba Mungu anawaadhibu waovu kwa kuwatesa milele motoni. Lakini je, huo ni ukweli? Biblia inafundisha nini hasa kuhusu kifo?

16, 17. Kulingana na Biblia, wafu wako katika hali gani?

16 Neno la Mungu linasema hivi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe, wala hawana malipo tena.” Kwa kuwa wafu “hawajui lolote kamwe,” hawawezi kusikia, kuona, kuongea, kuhisi, au kufikiri. Hawapati malipo yoyote tena. Kwa nini? Kwa sababu hawawezi kufanya kazi yoyote! Zaidi ya hilo, “upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari zimepotea,” kwa kuwa hawawezi kuonyesha hisia yoyote.—Mhubiri 9:5, 6, 10.

17 Biblia inaeleza waziwazi na kwa njia rahisi hali ya wafu. Inasema kwamba wafu hawaendelei kuishi mahali fulani. Hakuna kitu kinachotoka ndani ya mwili wetu wakati wa kifo na kuendelea kuishi ili kizaliwe upya katika mwili mwingine, kama wanavyodai watu wanaoamini fundisho la kuzaliwa upya katika mwili mwingine. Tunaweza kueleza jambo hilo kupitia mfano huu: Maisha yetu ni kama moto. Moto unapozimika, hauendi popote. Haupo tena.

18. Mwanafunzi wa Biblia anapojifunza kwamba wafu hawajui lolote, anaweza kuelewa mambo gani?

18 Hebu fikiria matokeo ya kujua ukweli huo mmoja ulio rahisi lakini wenye nguvu. Mwanafunzi wa Biblia anapojifunza kwamba wafu hawajui lolote, ni rahisi kwake kukubali kwamba mababu zake waliokufa hawawezi kumsumbua hata iwe walikuwa wenye chuki kadiri gani walipokuwa hai. Pia, ataelewa mara moja kwamba wapendwa wake ambao wamelala usingizi katika kifo hawawezi tena kusikia, kuona, kuongea, kuhisi, au kufikiri. Kwa hiyo, haiwezekani kwamba wanateseka sana kwa upweke wakiwa toharani au motoni. Hata hivyo, Biblia inafundisha kwamba wafu ambao wamo katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa. Ni tumaini zuri kama nini!—Yohana 5:28, 29.

Kitabu Kipya Tunachohitaji Kutumia

19, 20. Tukiwa Wakristo, tuna daraka gani, na ni kifaa gani cha kujifunzia Biblia ambacho kimekusudiwa hasa kutumiwa katika huduma yetu?

19 Tumezungumzia maswali matatu tu ambayo yanawahangaisha watu wengi. Kuhusiana na kila swali, Biblia inafundisha mambo yaliyo wazi na rahisi kueleweka. Ni furaha iliyoje kuwafundisha kweli hizo watu ambao wanataka kujua yale ambayo Biblia inafundisha! Lakini kuna maswali mengine mengi muhimu na watu wanyoofu wanahitaji kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali hayo. Tukiwa Wakristo, tuna daraka la kuwasaidia kupata majibu ya maswali hayo.

20 Si rahisi kufundisha kweli za Kimaandiko kwa njia iliyo wazi na yenye kugusa moyo. Ili kutusaidia kufanya hivyo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alitayarisha kitabu ambacho kimekusudiwa hasa kutumiwa nasi katika huduma yetu ya Kikristo. (Mathayo 24:45-47) Kitabu hicho chenye kurasa 224 kinaitwa Biblia Inafundisha Nini Hasa?

21, 22. Ni mambo gani yenye kupendeza yaliyo katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?

21 Kitabu hicho kilichotolewa kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya Mashahidi wa Yehova ya “Utii wa Kimungu” ya 2005/2006, kina mambo mbalimbali yenye kupendeza. Kwa mfano, kina utangulizi wa kurasa tano ambao unasaidia sana katika kuanzisha mafunzo ya Biblia. Inaelekea kwamba utaona ni rahisi kuzungumzia picha na maandiko yaliyo kwenye utangulizi wa kitabu hicho. Unaweza pia kutumia habari iliyo kwenye sehemu hiyo kuwaonyesha wanafunzi jinsi ya kupata sura na mistari ya Biblia.

22 Kimeandikwa kwa lugha rahisi na yenye kueleweka. Jitihada imefanywa ili kuugusa moyo wa mwanafunzi kwa kumshirikisha katika funzo inapowezekana. Mwanzoni mwa kila sura, kuna maswali kadhaa ya utangulizi na mwishoni mwa kila sura, kuna sanduku lenye kichwa, “Mambo Ambayo Biblia Inafundisha.” Sanduku hilo lina majibu ya Kimaandiko kwa maswali ya utangulizi. Kitabu hicho kina picha na maelezo mazuri ya picha na pia mifano ambayo itamsaidia mwanafunzi kuelewa mambo mapya. Ingawa sehemu kuu ya kitabu hicho ni rahisi sana, kuna nyongeza ambayo itakusaidia kuchunguza kwa undani zaidi vichwa 14 muhimu ikiwa mwanafunzi anahitaji habari zaidi.

23. Ni mapendekezo gani yanayotolewa kuhusu kutumia kitabu Biblia Inafundisha katika kuongoza mafunzo ya Biblia?

23 Kitabu Biblia Inafundisha kimekusudiwa kutusaidia kuwafundisha watu wenye viwango mbalimbali vya elimu na malezi mbalimbali ya kidini. Ikiwa mwanafunzi hana ujuzi wowote wa Biblia, huenda mkahitaji kutumia vipindi kadhaa vya funzo ili kumaliza sura nzima. Usizungumzie habari hiyo haraka-haraka, badala yake jitahidi kuugusa moyo wa mwanafunzi. Ikiwa haelewi mfano fulani uliotumiwa katika kitabu, fafanua mfano huo au tumia mfano mwingine. Jitayarishe vizuri, jitahidi kabisa kutumia kitabu hicho kwa njia nzuri, na usali ili Mungu akusaidie ‘kulitumia sawasawa neno la kweli.’—2 Timotheo 2:15.

Thamini Mapendeleo Yako Yenye Thamani Kubwa Sana

24, 25. Yehova amewapa watu wake mapendeleo gani yenye thamani kubwa sana?

24 Yehova amewapa watu wake mapendeleo yenye thamani kubwa sana. Ametuwezesha kujifunza kweli kumhusu. Hatupaswi kamwe kupuuza pendeleo hilo! Kwa kweli, Mungu amewaficha makusudi yake wenye kiburi na kuwafunulia wanyenyekevu. Yesu alisema hivi kuhusu jambo hilo: “Ninakusifu wewe hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye akili na umeyafunua kwa watoto.” (Mathayo 11:25) Ni heshima ya pekee sana kuhesabiwa miongoni mwa watu wanyenyekevu ambao wanamtumikia Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, Yehova.

25 Mungu ametupa pia pendeleo la kuwafundisha wengine kumhusu. Kumbuka kwamba watu wanaofundisha uwongo wamepotosha ukweli kumhusu Mungu. Kwa hiyo, watu wengi wana maoni yenye makosa kabisa kumhusu Yehova, kwa kuwa wanafikiri kwamba yeye hajali wala hana huruma. Je, uko tayari kurekebisha maoni hayo na unatamani kufanya hivyo? Je, unataka kuwasaidia watu wanyoofu kila mahali wajue ukweli kumhusu Mungu? Basi fanya yote unayoweza kuonyesha kwamba unamtii Mungu kwa kuhubiri na kuwafundisha wengine kwa bidii mambo ambayo Maandiko yanafundisha kuhusu habari mbalimbali muhimu. Wale wanaotafuta kweli wanahitaji kujifunza mambo ambayo Biblia inafundisha hasa.

Ungetoa Jibu Gani?

• Tunajua jinsi gani kwamba Mungu anatujali?

• Kwa nini tupo hapa duniani?

• Inakuwaje tunapokufa?

• Ni mambo gani yaliyo katika kitabu Biblia Inafundisha ambayo umefurahi kutumia?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 22]

Biblia inafundisha kwamba mateso yatakwisha

[Hisani]

Top right, girl: © Bruno Morandi/age fotostock; left, woman: AP Photo/Gemunu Amarasinghe; bottom right, refugees: © Sven Torfinn/Panos Pictures

[Picha katika ukurasa wa 23]

Waadilifu wataishi milele katika Paradiso