Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hatua Muhimu Katika Kutokeza Biblia za Lugha za Kiafrika

Hatua Muhimu Katika Kutokeza Biblia za Lugha za Kiafrika

Hatua Muhimu Katika Kutokeza Biblia za Lugha za Kiafrika

WASOMAJI wanyoofu wa Biblia huko Ulaya na Amerika Kaskazini walitambua zamani uhitaji wa kuwasaidia Waafrika walisome Neno la Mungu katika lugha zao wenyewe. Ili kutimiza lengo hilo zuri, watu wengi walikuja Afrika ili kujifunza lugha za Kiafrika. Wengine wao walibuni mfumo wa kuandika lugha fulani za Kiafrika na wakatunga kamusi. Kisha, wakaanza kutafsiri Biblia katika lugha nyingi za Kiafrika. Hiyo haikuwa kazi rahisi. Kitabu kimoja (The Cambridge History of the Bible) kinaeleza hivi: “Mtafsiri angechukua miaka kadhaa kutafuta neno ambalo lingefaa kutafsiri neno rahisi lililo muhimu sana katika mafundisho ya Kikristo.”

Mnamo 1857, Watswana walikuwa wa kwanza kupata Biblia nzima iliyotafsiriwa katika mojawapo ya lugha za Kiafrika ambazo mwanzoni hazikuwa na utaratibu wa kuandika. * Tafsiri hiyo yenye mabuku kadhaa, ilichapishwa na kutiwa jalada. Kisha, hatua kwa hatua, Biblia ikatafsiriwa katika lugha nyingine za Kiafrika. Tafsiri nyingi za Kiafrika zilikuwa na jina la Mungu, Yehova, katika Maandiko ya Kiebrania, au “Agano la Kale,” na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au “Agano Jipya.” Hata hivyo, matoleo yaliyorekebishwa, na tafsiri mpya zilichapishwa na watu mmoja-mmoja ambao hawakuliheshimu jina takatifu la Mtungaji wa Biblia, Yehova. Badala yake, walifuata utamaduni wa kishirikina wa Wayahudi wa kuliondoa jina la Mungu katika Biblia, na mahali pake kuweka majina ya cheo kama vile Mungu au Bwana. Hivyo, kukawa na uhitaji wa kuwaandalia watu wanaompenda Mungu barani Afrika, tafsiri ya Biblia ambayo inatumia jina la Mungu.

Tangu miaka ya 1980, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limefanya jitihada nyingi ili kutafsiri Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha kuu kadhaa za Kiafrika. Kwa sababu hiyo, leo mamia ya maelfu ya watu wanaopenda Biblia barani Afrika wanaweza kusoma Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha yao ya asili. Kufikia sasa, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikiwa nzima au sehemu, inapatikana katika lugha 17 za kienyeji barani Afrika.

Wasomaji wa Biblia hizo za lugha za Kiafrika wanafurahi kuwa na tafsiri inayotumia jina tukufu la Mungu, Yehova. Kwa mfano, Yesu aliposimama kwenye sinagogi huko Nazareti, alitangaza kazi aliyotumwa kufanya kwa kusoma sehemu ya kitabu cha kukunjwa cha Isaya, ambamo jina la Baba yake linapatikana. (Isaya 61:1, 2) Kulingana na Injili ya Luka kama ilivyotafsiriwa katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, Yesu alisoma hivi: “Roho ya Yehova iko juu yangu, kwa sababu alinitia mafuta kuwatangazia maskini habari njema, alinituma kuhubiri kuachiliwa huru kwa mateka na kupata kuona tena kwa vipofu, kuacha waliopondeka waende zao wakiwa wameachiliwa huru, kuhubiri mwaka wa Yehova wenye kukubalika.”—Luka 4:18, 19.

Hatua nyingine muhimu ya kutokeza Biblia katika lugha za Kiafrika ilifikiwa mnamo Agosti (Mwezi wa 8) 2005. Mwezi huo, nakala zaidi ya 76,000 za Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha mbalimbali zinazozungumzwa barani Afrika zilichapishwa na kutiwa jalada katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Afrika Kusini. Nakala hizo zilitia ndani Biblia 30,000 za lugha ya Kishona. Biblia hiyo ya Kishona ilitolewa kwenye Makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova ya “Utii wa Kimungu” nchini Zimbabwe.

Katika mwezi huo wa pekee, watu waliotembelea ofisi ya tawi ya Afrika Kusini walifurahia sana kuona Biblia mpya za lugha za Kiafrika zikichapishwa. “Nilifurahi sana na kusisimka kupata pendeleo la kushiriki katika kazi ya kutokeza Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika Kishona na katika lugha nyingine za Kiafrika,” anasema Nhlanhla, mwanabetheli anayefanya kazi ya kutia vitabu jalada. Bila shaka, hayo ndiyo maoni ya familia nzima ya Betheli ya Afrika Kusini.

Biblia mpya zitawafikia watu barani Afrika haraka zaidi na kwa gharama ya chini kuliko ilivyokuwa zilipokuwa zikichapishiwa katika nchi za ng’ambo na kusafirishwa kutoka huko. La muhimu zaidi ni kwamba, sasa Waafrika wana tafsiri sahihi inayotumia jina takatifu la Mtungaji mkuu wa Biblia, Yehova Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kufikia mwaka wa 1835, Biblia ilikuwa imetafsiriwa katika Kimalagasi, lugha ya Madagaska, na kufikia mwaka wa 1840, katika Kiamhara, lugha ya Ethiopia. Lugha ya Kimalagasi na ya Kiamhara zilianza kuandikwa muda mrefu kabla Biblia haijatafsiriwa katika lugha hizo.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Jina la Mungu katika Biblia ya Kitswana iliyochapishwa mwaka wa 1840

[Hisani]

Harold Strange Library of African Studies

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wageni kutoka Swaziland wanatazama Biblia mpya zinazochapishwa katika ofisi ya tawi ya Afrika Kusini