Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Isaya—2

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Isaya—2

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Isaya—2

ISAYA alitimiza kwa uaminifu kazi yake akiwa nabii. Hukumu alizotangaza juu ya ufalme wa makabila kumi ya Israeli tayari zimetimia. Sasa ana ujumbe mwingine kuhusu wakati ujao wa Yerusalemu.

Jiji la Yerusalemu litaharibiwa, na wakaaji wake watachukuliwa mateka. Hata hivyo, uharibifu wake hautadumu. Baada ya muda, ibada ya kweli itarudishwa. Huo ndio ujumbe unaokaziwa hasa katika Isaya 36:1–66:24. * Tunaweza kufaidika kwa kuchunguza mambo yanayozungumziwa katika sura hizi kwa sababu zina unabii mwingi ambao unatimizwa katika siku zetu au utatimizwa hivi karibuni. Pia, sehemu hii ya kitabu cha Isaya ina unabii wenye kusisimua kuhusu Masihi.

“TAZAMA! SIKU ZINAKUJA”

(Isaya 36:1–39:8)

Katika mwaka wa 14 wa utawala wa Mfalme Hezekia (732 K.W.K.), Waashuru wanashambulia Yuda. Yehova anaahidi kulinda jiji la Yerusalemu. Tisho la kushambuliwa linakoma wakati malaika mmoja tu wa Yehova anapowaua askari-jeshi 185,000 Waashuru.

Hezekia ni mgonjwa. Yehova anajibu sala yake na kumponya, naye anamwongezea miaka 15 ya maisha. Mfalme wa Babiloni anapotuma wajumbe wampongeze, Hezekia anakosa hekima na kuwaonyesha hazina zake zote. Isaya anamjulisha Hezekia ujumbe huu wa Yehova: “Tazama! Siku zinakuja, na vyote vilivyo ndani ya nyumba yako na ambavyo mababu zako wameweka akiba mpaka leo hii kwa kweli vitachukuliwa kwenda Babiloni.” (Isaya 39:5, 6) Baada ya miaka mia moja na kitu, unabii huo unatimia.

Swali la Kimaandiko Lajibiwa:

38:8—“Vipandio” ambavyo kivuli kilifanywa kirudi nyuma juu yake vilikuwa nini? Kwa kuwa vifaa vya kupima mwendo wa jua vilitumiwa huko Misri na Babiloni katika karne ya nane K.W.K., huenda vipandio hivyo vilikuwa kipimo cha nyuzi katika kifaa ambacho huenda Ahazi, baba ya Hezekia alikuwa nacho. Au huenda kulikuwa na ngazi katika makao ya mfalme. Labda kivuli cha nguzo iliyokuwa kando ya ngazi hizo kilionekana kwenye ngazi hizo, na hivyo kutumiwa kupima wakati.

Mambo Tunayojifunza:

36:2, 3, 22. Ingawa Shebna aliachishwa kazi ya kuwa msimamizi-nyumba, aliruhusiwa kuendelea kumtumikia mfalme akiwa mwandishi wa yule aliyechukua mahali pake. (Isaya 22:15, 19) Tukiondolewa pendeleo fulani katika tengenezo la Yehova kwa sababu fulani, je, hatupaswi kuendelea kumtumikia Mungu katika pendeleo lolote analoruhusu?

37:1, 14, 15; 38:1, 2Wakati wa taabu, ni jambo la hekima kumfikia Yehova katika sala na kumtumaini kabisa.

37:15-20; 38:2, 3Jiji la Yerusalemu lilipotishwa na Waashuru, Hezekia alihangaikia hasa jinsi ambavyo kushindwa kwa jiji hilo kungeleta suto juu ya jina la Yehova. Alipojua kwamba ugonjwa wake ungesababisha kifo, Hezekia hakufikiria tu hali yake. Alihangaishwa zaidi alipofikiria jinsi ambavyo ukoo wa kifalme wa Daudi ungeathiriwa ikiwa angekufa bila mrithi. Pia, alihangaishwa kuhusu ni nani angewaongoza Waisraeli kupigana na Waashuru. Kama Hezekia, tunaona kutakaswa kwa jina la Yehova na kutimizwa kwa kusudi lake kuwa jambo muhimu zaidi kuliko wokovu wetu.

38:9-20. Wimbo huu wa Hezekia unatufundisha kwamba hakuna jambo muhimu kuliko kumsifu Yehova.

“ATAJENGWA UPYA”

(Isaya 40:1–59:21)

Mara tu baada ya kutabiri uharibifu wa Yerusalemu na Waisraeli kupelekwa utekwani huko Babiloni, Isaya anatabiri kuhusu kurudishwa kwa ibada ya kweli. (Isaya 40:1, 2) Andiko la Isaya 44:28 linasema: “[Yerusalemu] atajengwa upya.” Sanamu za miungu ya Babiloni zitabebwa kama “vifurushi.” (Isaya 46:1) Babiloni litaharibiwa. Yote hayo yanatimia baada ya karne mbili.

Yehova atamtoa mtumishi wake kuwa “nuru ya mataifa.” (Isaya 49:6) “Mbingu” au watawala wa Babiloni, “zitatawanywa vipande-vipande kama moshi,” na raia wake “watakufa kama chawa”; lakini ‘binti Sayuni aliye mateka atajifungua pingu za shingo yake.’ (Isaya 51:6; 52:2) Kwa wote ambao wanakuja kwake na kumsikiliza, Yehova anasema hivi: “Bila kusita mimi nitafanya pamoja nanyi agano linalodumu mpaka wakati usio na kipimo kuhusu fadhili zenye upendo kwa Daudi.” (Isaya 55:3) Kuishi kulingana na matakwa ya uadilifu ya Mungu kunaleta “furaha tele katika Yehova.” (Isaya 58:14) Kwa upande mwingine, makosa ya watu, ‘yanasababisha mgawanyiko kati yao na Mungu wao.’—Isaya 59:2.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

40:27, 28—Kwa nini taifa la Israeli lilisema: “Njia yangu imefichwa kutoka kwa Yehova, na haki kwa ajili yangu humkwepa Mungu wangu”? Huenda Wayahudi fulani huko Babiloni walifikiri kwamba Yehova hakuona jinsi walivyokuwa wakitendewa isivyo haki. Walikumbushwa kwamba Babiloni haikuwa mbali sana na Muumba wa dunia, ambaye hachoki wala kuzimia.

43:18-21—Kwa nini wahamishwa waliokuwa wakirudi waliambiwa ‘wasiyakumbuke mambo ya kwanza’? Hilo halikumaanisha kwamba walipaswa kusahau matendo ya Yehova ya zamani ya ukombozi. Badala yake, Yehova alitaka wamsifu kwa sababu ya “jambo jipya” ambalo wangejionea wenyewe, kama vile kusafiri kurudi Yerusalemu kwa usalama, labda kupitia njia ya moja kwa moja ya jangwani. “Umati mkubwa” unaotoka katika “dhiki kuu” utakuwa pia na sababu mpya na za kibinafsi za kumtukuza Yehova.—Ufunuo 7:9, 14.

49:6—Masihi ni “nuru ya mataifa” jinsi gani, hata ingawa huduma yake duniani ilikuwa tu kwa wana wa Waisraeli? Yesu ni nuru ya mataifa kwa sababu ya yale yaliyotukia baada ya kifo chake. Biblia inaonyesha kwamba andiko la Isaya 49:6 linawahusu wanafunzi wake. (Matendo 13:46, 47) Leo, Wakristo watiwa-mafuta, wakisaidiwa na umati mkubwa wa waabudu, wanatumika wakiwa “nuru ya mataifa,” wakiwaelimisha watu ‘kufika katika sehemu ya mwisho ya dunia.’—Mathayo 24:14; 28:19, 20.

53:10—Ni katika maana gani Yehova alipendezwa kumponda Mwana wake? Bila shaka, Yehova, Mungu mwenye huruma na fadhili, aliumia moyoni alipoona Mwana wake mpendwa akiteseka. Hata hivyo, Yehova alipendezwa na utii wa Yesu wa kutoka moyoni na yote ambayo yangetimizwa kupitia kuteseka na kufa kwake.—Methali 27:11; Isaya 63:9.

53:11—Ni ujuzi gani ambao kupitia huo Masihi “atawaletea watu wengi msimamo wa uadilifu”? Huo ni ujuzi ambao Yesu alipata kwa kuja duniani, kuwa mwanadamu, na kuteseka isivyo haki mpaka kifo. (Waebrania 4:15) Hivyo, alitoa dhabihu ya fidia, ambayo ilihitajiwa kuwasaidia Wakristo watiwa-mafuta na umati mkubwa wawe na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu.—Waroma 5:19; Yakobo 2:23, 25.

56:6—“Wageni” ni nani, nao ‘wanalishika agano la Yehova’ kwa njia gani? “Wageni” hao ni “kondoo wengine” wa Yesu. (Yohana 10:16) Wanalishika agano jipya kwa kutii sheria zinazohusiana na agano hilo, kuunga mkono kikamili mipango inayofanywa kupitia agano hilo, kula chakula kilekile cha kiroho pamoja na Wakristo watiwa-mafuta, na kuwaunga mkono katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi.

Mambo Tunayojifunza:

40:10-14, 26, 28. Yehova ni mwenye uwezo na mpole, mwenye nguvu-zote na hekima yote, naye ana uelewaji mwingi ambao hatuwezi kuelewa.

40:17, 23; 41:29; 44:9; 59:4. Mapatano ya kisiasa na sanamu ni “ubatili mtupu.” Hakuna faida yoyote ya kutumaini vitu hivyo.

42:18, 19; 43:8. Kupuuza Neno la Mungu lililoandikwa na kutosikiliza maagizo anayotoa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ni kuwa kipofu na kiziwi kiroho.—Mathayo 24:45.

43:25. Yehova anafuta makosa kwa ajili yake mwenyewe. Kuwekwa huru kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo na kupata uzima si muhimu kuliko kutakaswa kwa jina la Yehova.

44:8. Tunategemezwa na Yehova, ambaye ni imara na thabiti kama mwamba. Hatupaswi kamwe kuogopa kutoa ushahidi kuhusu Uungu wake!—2 Samweli 22:31, 32.

44:18-20. Kuabudu sanamu kunaonyesha kwamba mtu amepotoka moyoni. Hakuna chochote kinachopaswa kuchukua mahali pa Yehova katika moyo wetu.

46:10, 11. Uwezo wa kufanya ‘shauri lake mwenyewe lisimame,’ yaani, kutimiza kusudi lake, unathibitisha kabisa kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.

48:17, 18; 57:19-21. Tukimtumaini Yehova atuokoe, tukimkaribia, na tukitii amri zake, amani yetu itakuwa nyingi kama maji yanayotiririka mtoni na matendo yetu ya uadilifu yatakuwa mengi kama mawimbi ya bahari. Wale wasiotii Neno la Mungu ni kama “bahari inayorushwa-rushwa.” Hawana amani.

52:5, 6Wababiloni walikata kauli kimakosa kwamba Mungu wa kweli ni dhaifu. Hawakutambua kwamba watu wake Waisraeli walipelekwa utumwani kwa sababu Yehova alikuwa amewakasirikia. Wengine wanapopatwa na msiba, ni jambo la hekima kutokata kauli kwa haraka kuhusu kisababishi cha msiba huo.

52:7-9; 55:12, 13. Tuna angalau sababu tatu za kushiriki kwa shangwe katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Miguu yetu inawapendeza watu wanyenyekevu ambao wana njaa ya kiroho. Tunamwona Yehova “jicho kwa jicho,” yaani, tunakuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Pia, tunafanikiwa kiroho.

52:11, 12. Ili tustahili kuvichukua “vyombo vya Yehova,” yaani, maandalizi yake ya utumishi mtakatifu, tunapaswa kuwa safi kiroho na kiadili.

58:1-14. Ni ubatili mtu kujionyesha kwa unafiki kuwa mwenye ujitoaji na mwadilifu. Waabudu wa kweli wanapaswa kuzidi katika kuonyesha ujitoaji-kimungu wa kweli na matendo ya upendo wa kindugu.—Yohana 13:35; 2 Petro 3:11.

59:15b-19. Yehova anaona matendo ya wanadamu na anaingilia kati kwa wakati wake.

‘ATAKUWA TAJI LA UREMBO’

(Isaya 60:1–66:24)

Likitabiri kuhusu kurudishwa kwa ibada ya kweli katika nyakati za kale na katika siku zetu, andiko la Isaya 60:1 linasema: “Simama, Ee mwanamke, toa nuru, kwa maana nuru yako imekuja na utukufu wa Yehova umeangaza juu yako.” Sayuni “utakuwa taji la urembo mkononi mwa Yehova.”—Isaya 62:3.

Isaya anasali kwa Yehova kwa ajili ya wananchi wenzake ambao watatubu wakiwa uhamishoni huko Babiloni. (Isaya 63:15–64:12) Baada ya kuonyesha tofauti iliyopo kati ya watumishi wa kweli na wa uwongo, nabii huyo anatangaza jinsi Yehova atakavyowabariki wale wanaomtumikia.—Isaya 65:1–66:24.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

61:8, 9—“Agano linalodumu mpaka wakati usio na kipimo” ni nini, na “uzao” ni nani? Hilo ni agano jipya ambalo Yehova amefanya pamoja na Wakristo watiwa-mafuta. “Uzao” ni “kondoo wengine,” yaani, mamilioni ya watu ambao wanakubali ujumbe wao.—Yohana 10:16.

63:5—Ghadhabu ya Mungu inamtegemeza namna gani? Ghadhabu ya Mungu au hasira yake ya uadilifu ni hisia inayoweza kuongozwa. Ghadhabu yake inamtegemeza na kumchochea atekeleze hukumu zake za uadilifu.

Mambo Tunayojifunza:

64:6. Wanadamu wasio wakamilifu hawawezi kujiokoa wenyewe. Kuhusu kufanya upatanisho kwa ajili ya dhambi, matendo yao ya uadilifu ni kama tu mavazi yaliyochafuliwa.—Waroma 3:23, 24.

65:13, 14. Yehova anawabariki watumishi wake waaminifu, na kutosheleza kabisa mahitaji yao ya kiroho.

66:3-5. Yehova anachukia unafiki.

“Furahini”

Wayahudi waaminifu waliokuwa mateka huko Babiloni walifarijiwa sana na unabii uliohusu kurudishwa kwa ibada ya kweli! “Furahini,” anasema Yehova, “na muwe na shangwe milele katika hivi ninavyoumba. Kwa maana tazama, mimi ninaumba Yerusalemu kuwa sababu ya kushangilia na watu wake kuwa sababu ya kufurahi.”—Isaya 65:18.

Sisi pia tunaishi wakati ambapo giza linaifunika dunia na weusi mzito unayafunika mataifa. (Isaya 60:2) Tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Kwa hiyo, ujumbe wa Yehova wa wokovu ulio katika kitabu cha Biblia cha Isaya unatutia moyo sana.—Waebrania 4:12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kwa mazungumzo kuhusu Isaya 1:1–35:10, ona “Neno la Yehova Liko Hai—Mambo Makuu Katika Kitabu cha Isaya—1” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1 (Mwezi wa 12), 2006.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Je, unajua sababu kuu iliyomfanya Hezekia asali ili aokolewe asishambuliwe na Waashuru?

[Picha katika ukurasa wa 11]

“Jinsi inavyopendeza juu ya milima miguu ya yeye anayeleta habari njema!”