Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni katika maana gani mkutanishaji alimwona “mwanamume mmoja kati ya elfu moja” lakini hakumwona “mwanamke mmoja kati yao wote”?—Mhubiri 7:28.

Ili kuelewa vizuri maneno hayo yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu, tunapaswa kwanza kuelewa jinsi Yehova anavyowaona wanawake. Biblia inasema kwamba Ruthu, binti-mkwe wa mjane Naomi, alikuwa “mwanamke bora sana.” (Ruthu 3:11) Kulingana na Methali 31:10, mke mwema ‘ana thamani inayopita sana ile ya marijani.’ Hivyo basi, Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alimaanisha nini aliposema: “Nilifaulu kumwona mwanamume mmoja anayestahili heshima, lakini kati ya wanawake . . . sikumwona hata mmoja anayestahili heshima”?—Biblia Habari Njema.

Mistari mingine inaonyesha kwamba wanawake wengi walioishi siku za Sulemani walikuwa na viwango vya chini vya maadili. (Mhubiri 7:26) Inaelekea ilikuwa hivyo hasa kwa sababu ya wanawake wengi wageni waliomwabudu Baali. Hata Mfalme Sulemani alishawishiwa na wake wengi wageni aliokuwa nao. Biblia inasema: “Akawa na wake mia saba, binti za kifalme, na masuria mia tatu na mwishowe wake zake wakaugeuza moyo wake” ili kuabudu miungu ya uwongo. (1 Wafalme 11:1-4) Wanaume pia hawakuwa na maadili mema—mwanamume mmoja mwadilifu kati ya wanaume elfu moja, ilikuwa idadi ndogo sana. Sulemani anamalizia hivi: “Nimeona hili peke yake, ya kwamba Mungu wa kweli aliwafanya wanadamu wakiwa wanyoofu, lakini wao wenyewe wametafuta mipango mingi.” (Mhubiri 7:29) Kauli hiyo inahusu wanadamu wote, jamii ya wanadamu, wala haiwalinganishi wanaume na wanawake. Hivyo, maneno yaliyo katika Mhubiri 7:28 yanapaswa kuonwa kwa ujumla kuwa maelezo yanayohusu maadili ya watu wa siku za Sulemani.

Hata hivyo, mstari huo unaweza kuwa na maana nyingine. Unaweza pia kuwa wa kinabii, kwa kuwa hakuna mwanamke ambaye amewahi kumtii Yehova kikamilifu. Lakini mwanamume mmoja, Yesu Kristo, amefanya hivyo.—Waroma 5:15-17.

[Picha katika ukurasa wa 31]

“Mwanamume mmoja kati ya elfu moja”