Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwanamume na Mwanamke Wana Wajibu Wenye Kuheshimika

Mwanamume na Mwanamke Wana Wajibu Wenye Kuheshimika

Mwanamume na Mwanamke Wana Wajibu Wenye Kuheshimika

YEHOVA MUNGU alimuumba Adamu kwanza, kisha Hawa. Kabla Hawa hajaumbwa, Adamu alipata uzoefu maishani. Wakati huo, Yehova alimpa Adamu maagizo fulani. (Mwanzo 2:15-20) Akiwa kama msemaji wa Mungu, Adamu alipaswa kumpa mke wake maagizo hayo. Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kwamba Adamu angeongoza katika mambo yote yaliyohusu ibada.

Kuna mpango kama huo katika kutaniko la Kikristo, nasi tunaweza kufaidika tukichunguza mpango huo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Simruhusu mwanamke . . . kuwa na mamlaka juu ya mwanamume, bali kuwa kimya. Kwa maana Adamu aliumbwa kwanza, kisha Hawa.” (1 Timotheo 2:12, 13) Hilo halimaanishi kwamba mwanamke anapaswa kunyamaza kabisa katika mikutano ya Kikristo. Kunyamaza kunamaanisha kutobishana na mwanamume. Hapaswi kudharau cheo chake, au kujaribu kulifundisha kutaniko. Wanaume wamepewa daraka la kusimamia na kufundisha kutaniko, lakini wanawake wanachangia sana mikutano ya Kikristo kwa kushiriki kwa njia mbalimbali.

Akitusaidia kuelewa wajibu wa wanaume na wa wanawake katika mpango wa Mungu, mtume Paulo aliandika hivi: “Mwanamume hakutoka katika mwanamke, bali mwanamke alitoka katika mwanamume . . . Tena, kuhusiana na Bwana mwanamke si bila mwanamume wala mwanamume si bila mwanamke [hakuna asiyemhitaji mwenzake]. Kwa maana kama vile mwanamke ametoka katika mwanamume, vivyo hivyo pia mwanamume amepitia katika mwanamke; lakini vitu vyote vimetoka kwa Mungu.”—1 Wakorintho 11:8-12.

Wanawake Wana Mapendeleo Mazuri

Chini ya Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli, wanawake walikuwa na mapendeleo yao nao walikuwa huru kutumia vipawa vyao. Kwa mfano, andiko la Methali 31:10-31 linazungumza kuhusu “mke mwenye uwezo,” ambaye ananunua vitambaa vizuri na kuwashonea watu wa nyumbani mwake mavazi bora. Hata, “ametengeneza mavazi ya ndani na kuyauza”! (Mstari wa 13, 21-24) “Kama meli za mfanyabiashara,” mwanamke huyo bora anatafuta chakula kizuri, hata ikiwa itamlazimu kwenda kuleta chakula hicho kutoka mbali. (Mstari wa 14) “Amefikiria shamba, akalinunua,” naye “amepanda shamba la mizabibu.” (Mstari wa 16) Kwa kuwa “biashara yake ni nzuri,” shughuli zake zinamletea faida. (Mstari wa 18) Zaidi ya ‘kuangalia shughuli za nyumba yake,’ mwanamke huyo mwenye bidii na anayemwogopa Yehova anawasaidia wengine bila uchoyo. (Mstari wa 20, 27) Haishangazi kwamba anasifiwa!—Mstari wa 31.

Sheria ambazo Yehova alitoa kupitia Musa ziliwapa wanawake nafasi nzuri ya kukua kiroho. Kwa mfano, katika Yoshua 8:35, tunasoma hivi: “Hakuna neno lolote kati ya yote ambayo Musa alikuwa ameamuru ambalo Yoshua hakusoma kwa sauti mbele ya kutaniko lote la Israeli, pamoja na wanawake na watoto wadogo na wakaaji wageni waliokuwa katikati yao.” Kumhusu kuhani Ezra, Biblia inasema hivi: “Akaleta sheria mbele ya kutaniko la wanaume na la wanawake na vilevile la wote wenye akili ya kutosha kuweza kusikiliza, katika siku ya kwanza ya mwezi wa saba. Naye akaendelea kusoma ndani ya kile kitabu kwa sauti mbele ya kiwanja cha watu wote kilichoko mbele ya Lango la Maji, kuanzia mapambazuko mpaka katikati ya mchana, mbele ya wanaume na wanawake na mbele ya wale wengine wenye akili; na watu wote wakasikiliza kwa makini kitabu cha sheria.” (Nehemia 8:2, 3) Wanawake walifaidika na usomaji huo wa Sheria. Pia, walishiriki sherehe za kidini. (Kumbukumbu la Torati 12:12, 18; 16:11, 14) La muhimu zaidi ni kwamba, kila mwanamke katika Israeli la kale angeweza kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova Mungu na kusali kwake.—1 Samweli 1:10.

Katika karne ya kwanza W.K., wanawake waliomwogopa Mungu walikuwa na pendeleo la kumhudumia Yesu. (Luka 8:1-3) Mwanamke fulani alimtia Yesu mafuta kichwani na miguuni wakati wa chakula cha jioni huko Bethania. (Mathayo 26:6-13; Yohana 12:1-7) Wanawake walikuwa kati ya wale ambao Yesu aliwatokea baada ya kufufuliwa kwake. (Mathayo 28:1-10; Yohana 20:1-18) Baada ya Yesu kupanda mbinguni, kikundi cha wanafunzi 120 hivi ambacho kilikutana pamoja kilitia ndani “wanawake fulani na Maria mama ya Yesu.” (Matendo 1:3-15) Bila shaka, wengi wa wanawake hao au labda wote walikuwa katika chumba cha juu huko Yerusalemu siku ya Pentekoste 33 W.K. Siku hiyo, roho takatifu ilimiminwa juu ya wanafunzi hao wa Yesu nao wakaongea kimuujiza katika lugha mbalimbali.—Matendo 2:1-12.

Wanaume na wanawake walikuwa kati ya wale ambao unabii wa Yoeli 2:28, 29 ulitimizwa kuhusiana nao. Mtume Petro alitaja unabii huo siku ya Pentekoste: “[Mimi Yehova] nitaimimina sehemu ya roho yangu juu ya kila namna ya mwili, nao wana wenu na binti zenu watatoa unabii . . . Na hata juu ya watumwa wangu na juu ya wajakazi wangu nitaimimina sehemu ya roho yangu katika siku hizo.” (Matendo 2:13-18) Kwa muda fulani baada ya Pentekoste 33 W.K., wanawake Wakristo walipewa zawadi za roho. Waliongea na kutabiri katika lugha za kigeni. Huenda hawakutabiri mambo mapya, lakini walitangaza kweli za Kimaandiko.

Katika barua ambayo aliwaandikia Wakristo huko Roma, mtume Paulo anamsifu “Fibi dada yetu,” akimpendekeza kwao. Pia, anamtaja Trifaina na Trifosa, akiwaita “wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana.” (Waroma 16:1, 2, 12) Ingawa wanawake hao hawakuwekwa rasmi kuwa wazee au watumishi wa huduma katika kutaniko la Kikristo la mapema, wanawake hao na wengine wengi walikuwa na pendeleo la kuchaguliwa na Mungu ili washiriki pamoja na Mwana wake, Yesu Kristo, katika Ufalme wa mbinguni.—Waroma 8:16, 17; Wagalatia 3:28, 29.

Wanawake wanaomwogopa Mungu wana pendeleo kubwa sana leo! “Yehova mwenyewe anasema neno hili; wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa,” inasema Zaburi 68:11. Wanawake hao wanapaswa kupongezwa. Kwa mfano, ustadi wao wa kufundisha watu Biblia unawaongoza wengi wakubali mafundisho ya kweli yanayompendeza Mungu. Wanawake Wakristo walioolewa ambao wanawasaidia watoto wao kuwa waamini na ambao wanawaunga mkono waume zao walio na madaraka mengi kutanikoni wanastahili kusifiwa pia. (Methali 31:10-12, 28) Wanawake waseja pia wana sehemu yenye kuheshimika katika mpango wa Mungu, na wanaume Wakristo wanahimizwa ‘wawasihi wanawake wazee kama mama, wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.’—1 Timotheo 5:1, 2.

Migawo Mbalimbali ya Mwanamume

Mungu amempa mwanamume Mkristo wajibu naye anatazamiwa kuutimiza. Paulo alisema hivi: “Nataka mjue kwamba kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Wakorintho 11:3) Mwanamume pia ana kichwa. Kichwa chake ni Kristo. Bila shaka, mwanamume atatozwa hesabu na Kristo na hatimaye na Mungu. Naye Mungu anamtazamia mwanamume aongoze kwa upendo akiwa kichwa. (Waefeso 5:25) Imekuwa hivyo tangu wanadamu walipoumbwa duniani.

Biblia inaonyesha kwamba Mungu alimpa mwanamume migawo kulingana na cheo chake akiwa kichwa. Kwa mfano, Yehova alimwambia mwanamume Noa ajenge safina ili kuokoa uhai wakati wa Gharika. (Mwanzo 6:9–7:24) Mwanamume Abrahamu aliahidiwa kwamba kupitia uzao wake, familia na mataifa yote ya dunia yangejibariki. Kristo Yesu ndiye sehemu ya kwanza ya uzao huo. (Mwanzo 12:3; 22:18; Wagalatia 3:8-16) Mungu alimweka rasmi mwanamume Musa awaongoze Waisraeli kutoka Misri. (Kutoka 3:9, 10, 12, 18) Yehova alimtumia Musa kutoa mfumo wa sheria ambao unaitwa agano la Sheria au Sheria ya Musa. (Kutoka 24:1-18) Watu wote ambao waliandika Biblia walikuwa wanaume.

Akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu “alitoa zawadi katika [wanaume].” (Waefeso 1:22; 4:7-13) Anapoorodhesha sifa za waangalizi, Paulo anawataja wanaume. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9) Kwa hiyo, wanaume ndio wanaotumikia wakiwa waangalizi au wazee na watumishi wa huduma katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. (Wafilipi 1:1, 2; 1 Timotheo 3:8-10, 12) Wanaume tu ndio wanaopaswa kutumikia wakiwa wachungaji katika kutaniko la Kikristo. (1 Petro 5:1-4) Hata hivyo, kama tulivyoona, wanawake wamepewa na Mungu mapendeleo mazuri sana.

Wanafurahia Wajibu Wao

Wanaume na wanawake wanapata furaha wanapotimiza wajibu mbalimbali waliopewa na Mungu. Waume na wake wanapoiga mfano wa Kristo na wa kutaniko lake wanakuwa na ndoa zenye furaha. Paulo aliandika hivi: “Waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake . . . Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe.” (Waefeso 5:25-33) Hivyo, waume wanapaswa kuongoza, si kwa njia ya uchoyo, bali kwa njia ya upendo. Washiriki wa kutaniko la Kristo si wanadamu wakamilifu. Hata hivyo, Yesu anawapenda na kuwatunza. Vivyo hivyo, mume Mkristo anapaswa kumpenda na kumtunza mke wake.

Mke Mkristo “anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Anaweza kuiga mfano wa kutaniko katika jambo hilo. Andiko la Waefeso 5:21-24 linasema: “Jitiisheni kwa mmoja na mwenzake katika kumwogopa Kristo. Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko, yeye akiwa mwokozi wa mwili huu. Kwa kweli, kama kutaniko linavyojitiisha kwa Kristo, vivyo hivyo wanawake pia na wajitiishe kwa waume zao katika mambo yote.” Ingawa huenda nyakati nyingine mke akaona ni vigumu kujitiisha kwa mume wake, jambo hilo ‘linafaa katika Bwana.’ (Wakolosai 3:18) Itakuwa rahisi kwa mke kujitiisha kwa mume wake ikiwa atakumbuka kwamba kufanya hivyo kunampendeza Bwana Yesu Kristo.

Hata ikiwa mume wake si mwamini mwenzake, mke Mkristo anapaswa kujitiisha chini ya ukichwa wake. Mtume Petro anasema hivi: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.” (1 Petro 3:1, 2) Sara, ambaye alimheshimu mume wake, Abrahamu, alipewa pendeleo la kumzaa Isaka na kuwa nyanya ya Yesu Kristo. (Waebrania 11:11, 12; 1 Petro 3:5, 6) Hapana shaka kwamba Mungu atawapa thawabu wanawake ambao wanajiendesha kama Sara.

Wanaume na wanawake wanapotimiza wajibu wao waliopewa na Mungu, kunakuwa na amani na upatano. Hilo linawafanya waridhike na kuwa wenye furaha. Zaidi ya hilo, kufuata matakwa ya Kimaandiko kunamletea kila mmoja wao heshima inayoambatana na mapendeleo yao katika mpango wa Mungu.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Jinsi Wanavyoona Wajibu Waliopewa na Mungu

“Mume wangu anaongoza kwa njia ya upendo na fadhili akiwa kichwa,” anasema Susan. “Kwa kawaida, tunazungumza kuhusu maamuzi, na anapoamua jambo ambalo tutafanya au hatutafanya, ninajua kwamba ni kwa faida yetu. Mpango wa Yehova kuhusu wanawake Wakristo kwa kweli unanifurahisha na kuifanya ndoa yetu kuwa yenye nguvu. Tuna uhusiano wa karibu na tunashirikiana kutimiza miradi ya kiroho.”

Mwanamke fulani anayeitwa Mindy anasema hivi: “Wajibu ambao Yehova amewapa watumishi wake wanawake unatuhakikishia kwamba anatupenda. Ninaona kwamba kumtii na kumheshimu mume wangu na pia kumuunga mkono katika migawo yake kutanikoni ni njia yangu ya kuonyesha kwamba ninamthamini Yehova kwa sababu ya mpango huu.”

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kupatana na cheo cha mwanamume akiwa kichwa, Mungu alimpa Noa, Abrahamu, na Musa migawo mbalimbali

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa”