Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mzee wa Zaidi ya Miaka Mia Aliye na Kusudi Maishani

Mzee wa Zaidi ya Miaka Mia Aliye na Kusudi Maishani

Mzee wa Zaidi ya Miaka Mia Aliye na Kusudi Maishani

HIVI majuzi Elin alikuwa kati ya watu 60 nchini Sweden, ambao waliwekwa katika orodha ya watu wenye umri wa miaka 105 au zaidi. Yeye mwenyewe ana miaka 105. Ingawa anaishi katika makao ya wazee, Elin ana afya nzuri naye bado ni Shahidi anayetenda wa Yehova. Amekuwa mtendaji kwa miaka zaidi ya 60.

Kwa kuwahubiria wengine, Elin anafuata mfano wa mtume Paulo ambaye alihubiri akiwa katika kifungo cha nyumbani. Paulo aliwahubiria watu wote waliomtembelea. (Matendo 28:16, 30, 31) Vivyo hivyo, Elin anatumia kila nafasi kuongea na watu wanaosafisha makao yao, madaktari wa meno na madaktari wengine, watunzaji-nywele, wauguzi, na watu wengine anaokutana nao katika makao hayo. Anawahubiria kuhusu habari njema inayopatikana katika Biblia. Mara kwa mara, ndugu na dada wa kutaniko la Elin hata wanawaomba wanafunzi wao wa Biblia wamtembelee ili wafaidike kutokana na ujuzi na uzoefu wake.

Washiriki wa kutaniko ambalo Elin anashirikiana nalo wanavutiwa sana na uchangamfu wake na hamu yake ya kujua mambo. Shahidi mwenzake anasema hivi: “Elin ana uwezo mzuri wa kufuatana na utendaji mbalimbali wa kutaniko. Anakumbuka majina ya watoto wote na ya wale ambao wamehamia kutanikoni hivi karibuni.” Pia, Elin anajulikana sana kwa sababu ya ukaribishaji wake, ucheshi, na maoni yake mazuri kuhusu maisha.

Ni nini kinachomsaidia Elin kudumisha shangwe yake na kukazia akilini kusudi lake maishani? Yeye anasoma andiko moja la Biblia kila siku katika kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku, kinachochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia, akitumia miwani, anasoma sehemu fulani ya Biblia kila siku. Elin anajitayarisha kwa ajili ya mikutano ya kila juma ya Mashahidi wa Yehova, na ingawa hali yake ya kimwili inamzuia kuhudhuria mikutano hiyo, anasikiliza programu iliyorekodiwa ya mikutano. Kusoma kwa ukawaida Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia na kutoacha kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kunaweza kutusaidia kuwa na maisha yenye kusudi hata tukiwa na umri gani.—Zaburi 1:2; Waebrania 10:24, 25.