Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Samweli Anaendeleza Ibada ya Kweli

Samweli Anaendeleza Ibada ya Kweli

Samweli Anaendeleza Ibada ya Kweli

NABII anawakaripia waamini wenzake ambao waliomba wapewe mfalme wa kibinadamu na anawahimiza wamtii Mungu. Ili kuonyesha kwamba ana mamlaka, nabii huyo anamwomba Yehova atokeze dhoruba kama ishara. Dhoruba za mvua hazitokei Israeli wakati huu wa mwaka, ambao ni wakati wa kuvuna ngano. Hata hivyo, Mungu analeta ngurumo na mvua. Hilo linawafanya watu wamwogope sana Yehova na mwakilishi wake, Samweli.—1 Samweli 12:11-19.

Nabii Samweli alikuwa mwandikaji pia. Masimulizi yake ya matukio yenye kusisimua ya kihistoria yanahusu kipindi cha miaka 330 hivi, nayo yanatia ndani shughuli za Waamuzi wa Israeli. Kwa mfano, simulizi la mtu halisi aliyeitwa Samsoni, mwanadamu mwenye nguvu zaidi aliyepata kuishi, limezungumziwa katika mashairi, nyimbo, michezo ya kuigiza, na sinema. (Waamuzi, sura ya 13–16) Samweli aliandika pia kuhusu Ruthu na Naomi, mama-mkwe wa Ruthu, ambao wote wawili walikuwa wajane maskini. Simulizi hilo la kweli ambalo lilikuwa na mwisho wenye furaha linasisimua sana pia.—Ruthu, sura ya 1–4.

Tunaweza kujifunza mambo gani kutokana na vitabu na maisha ya Samweli? Samweli aliendeleza ibada ya kweli jinsi gani?

Ujana Wake

Elkana, baba ya Samweli alikuwa mume mwenye upendo na alimwabudu Yehova. Hana, mke wa Elkana, alikuwa mwanamke imara kiroho. Katika nyumba ya Yehova huko Shilo, Hana ambaye alikuwa tasa alisali hivi kwa bidii na kuweka nadhiri: “Ee Yehova wa majeshi, ikiwa hakika utayaona mateso ya kijakazi wako, nawe kwa kweli unikumbuke, na ikiwa hutamsahau kijakazi wako na kwa kweli umpe kijakazi wako uzao wa kiume, mimi nitamtoa kwa Yehova siku zote za maisha yake, wala wembe hautapita juu ya kichwa chake.” (1 Samweli 1:1-11) Hilo lilimaanisha kwamba mtoto huyo angewekwa kando kwa ajili ya utumishi wa Yehova.

Hana alisali kimyakimya. Masimulizi hayo yanasema kwamba “midomo yake tu ndiyo ilikuwa ikitetemeka.” Kuhani Mkuu Eli alifikiri kimakosa kwamba Hana alikuwa amelewa na hivyo akamkaripia. Hata hivyo, kwa heshima Hana alimweleza hali yake, naye Eli akasema: “Nenda kwa amani, naye Mungu wa Israeli akupe ombi lako ambalo umemwomba.” Yehova alifanya hivyo, kwa kuwa masimulizi hayo yanaendelea kusema: “Ikawa mwishoni mwa mwaka kwamba Hana akachukua mimba, akamzaa mwana, akamwita jina lake Samweli, kwa maana alisema, ‘Nimemwomba kutoka kwa Yehova.’”—1 Samweli 1:12-20.

Samweli alilelewa katika “nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Mara tu Samweli alipoachishwa kunyonya, Hana alimleta kwenye nyumba ya Mungu huko Shilo na kumkabidhi kwa Kuhani Mkuu Eli. Chini ya mwongozo wa Eli, mvulana huyo “akawa mhudumu wa Yehova.” Shangwe kubwa ya Hana inaonyeshwa na maneno yake yenye kuchochea ambayo yaliandikwa na Samweli mwenyewe.—1 Samweli 2:1-11.

Ikiwa wewe ni mzazi, je, unawatia moyo watoto wako wafanye utumishi wa Yehova kuwa kazi yao maishani? Njia bora ya kutumia nguvu zetu ni kuendeleza ibada ya kweli.

Samweli alifanya mabadiliko mazuri yaliyomwezesha kuishi hekaluni. ‘Aliendelea kukua na kupendwa na Yehova na vilevile wanadamu.’ Alionyesha sifa za kimungu ambazo zilimfanya apendwe na wengine.—1 Samweli 2:21, 26.

Haiwezi kusemwa hivyo kuhusu Hofni na Finehasi, wana wasiofaa kitu wa Eli, ambao “hawakumtambua Yehova.” Walifanya uasherati na kujichukulia sehemu bora za dhabihu ambazo watu walileta hekaluni. Mungu alikuwa tayari amemtuma nabii ili atangaze adhabu ambayo Eli angetazamia, adhabu ambayo ilitia ndani kifo cha wanawe wawili. (1 Samweli 2:12, 15-17, 22-25, 27, 30-34) Yehova angemtumia Samweli kutoa ujumbe mwingine wa hukumu.

Samweli Anatumika Akiwa Nabii

Mungu alimwambia Samweli hivi: “Nawe unapaswa kumwambia [Eli] kwamba naihukumu nyumba yake mpaka wakati usio na kipimo kwa sababu ya kosa ambalo amelijua, kwa sababu wanawe wanamlaani Mungu, lakini yeye hakuwakemea.” Haikuwa rahisi kutoa ujumbe huo, na Eli alisisitiza kwamba Samweli asimfiche neno lolote la ujumbe huo. Hivyo, Samweli akamweleza yote ambayo Yehova alisema. Alihitaji ujasiri!—1 Samweli 3:10-18.

Samweli alipokomaa na kuwa mtu mzima, Waisraeli wote walijua kwamba alikuwa nabii wa Mungu. (1 Samweli 3:19, 20) Hukumu ambayo Samweli alitabiri ilianza wakati Waisraeli waliposhindwa kabisa na Wafilisti. Hofni na Finehasi walikufa vitani, nao Wafilisti wakalichukua sanduku la agano la Yehova. Alipopata habari kuhusu kifo cha wanawe na kuchukuliwa kwa Sanduku, Eli alianguka nyuma kutoka kwenye kiti chake, na shingo yake ikavunjika, naye akafa.—1 Samweli 4:1-18.

Miaka 20 baadaye, Samweli aliwahimiza Waisraeli waache ibada ya uwongo. Waliitikia kwa kuondoa sanamu zao, kwa kufunga, na kwa kuungama dhambi zao. Samweli alisali na kutoa toleo la kuteketezwa kwa ajili yao. Matokeo yalikuwa nini? Wafilisti waliposhambulia, Mungu aliwavuruga, na Waisraeli wakawashinda maadui hao. Kwa utegemezo wa Yehova, hali ya Waisraeli ikawa bora zaidi, nao wakatwaa tena maeneo yaliyokuwa yamechukuliwa na Wafilisti.—1 Samweli 7:3-14.

Bila shaka, Samweli aliendeleza ibada ya kweli. Kwa mfano, alihakikisha kwamba sehemu ya nyara zilizochukuliwa vitani zilitumiwa kutunza maskani. Alisaidia kupanga sherehe za Pasaka na utumishi wa Walawi ambao walitunza malango. (1 Mambo ya Nyakati 9:22; 26:27, 28; 2 Mambo ya Nyakati 35:18) Kila mwaka, Samweli alisafiri kutoka nyumbani kwake huko Rama, ili kwenda kuhukumu katika majiji mbalimbali. Alijulikana kuwa mtu mnyoofu na asiye na upendeleo. Kwa kuwa watu walimheshimu Samweli, aliweza kuwasaidia kiroho. (1 Samweli 7:15-17; 9:6-14; 12:2-5) Unyoofu na hali yake nzuri ya kiroho bila shaka iliwachochea wengi kufuata mfano wake. Je, maisha ya Samweli yanakuchochea pia?

Waisraeli Wanaomba Wapewe Mfalme

Alipokuwa amezeeka, Samweli aliwaweka rasmi wanawe, Yoeli na Abiya, wawe waamuzi. “Hawakutembea katika njia zake, bali walikuwa na mwelekeo wa kufuata faida isiyo ya haki na wakawa wakikubali rushwa na kupotosha hukumu.” Mwenendo wao uliwafanya wanaume wazee wa Israeli waombe wapewe mfalme. (1 Samweli 8:1-5) Hilo lilikuwa jambo baya machoni pa Samweli. Hata hivyo, aliposali kuhusu jambo hilo, Yehova alisema: “Hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi nisiwe mfalme juu yao.” (1 Samweli 8:6, 7) Mungu alimwambia Samweli akubali ombi la watu na awaonye kwamba chini ya utawala wa mfalme wangepoteza haki na uhuru fulani. Watu waliposisitiza, Yehova alifanya mpango ili Samweli amtie mafuta Sauli kuwa mfalme.—1 Samweli 8:6–22; 9:15-17; 10:1.

Samweli aliunga mkono mpango huo hata ingawa alikuwa na shaka kuuhusu. Baada ya Waisraeli kuwashinda Waamoni, aliwakusanya watu huko Gilgali ili kumfanya Sauli kuwa mfalme. (1 Samweli 10:17-24; 11:11-15) Samweli aliwasimulia kuhusu historia ya Israeli na kumhimiza mfalme na watu wamtii Yehova. Mungu alijibu sala ya Samweli kwa kuleta ngurumo na mvua kama ilivyotajwa mwanzoni. Mvua hiyo ilifanya watu wakiri kwamba walikosea kwa kumkataa Yehova. Walipomwomba Samweli asali kwa ajili yao, yeye alisema hivi: “Ni jambo lisilowaziwa, kwamba nimtendee Yehova dhambi kwa kuacha kusali kwa ajili yenu; nami nitawafundisha ninyi katika njia iliyo njema na iliyo sawa.” Huo ni mfano mzuri kama nini wa upendo mshikamanifu kwa Yehova na kwa watu wake! (1 Samweli 12:6-24) Je, wewe uko tayari kama Samweli kuunga mkono mipango ya kitheokrasi na kusali kwa ajili ya waamini wenzako?

Wafalme Wawili wa Kwanza wa Kibinadamu wa Israeli

Sauli alikuwa mtu mnyenyekevu aliyekubaliwa na Mungu. (1 Samweli 9:21; 11:6) Hata hivyo, baada ya muda, alipuuza mwelekezo wa Mungu. Kwa mfano, Samweli alimkaripia kwa sababu ya kukosa subira alipotoa dhabihu badala ya kungojea, kama alivyoamriwa. (1 Samweli 13:10-14) Sauli alipokosa kutii kwa kutomuua Mfalme Agagi wa Amaleki, Samweli alimwambia hivi: “Yehova ameurarua utawala wa kifalme wa Israeli kutoka kwako leo, naye hakika atampa mwenzako ambaye ni bora kuliko wewe.” Samweli mwenyewe akamuua Agagi kisha akaanza kumwombolezea Sauli.—1 Samweli 15:1-35.

Mwishowe, Yehova akamwambia Samweli hivi: “Ni mpaka wakati gani utamwombolezea Sauli, huku mimi, kwa upande mwingine, nimemkataa asitawale akiwa mfalme juu ya Israeli?” Hivyo, Yehova akamtuma Samweli Bethlehemu ili kumtia mafuta mwana wa Yese awe mfalme. Samweli aliwachunguza wana wa Yese mmoja baada ya mwingine mpaka Yehova alipoonyesha kwamba amemkubali Daudi, mwana wa mwisho wa Yese, atiwe mafuta. Siku hiyo, Samweli alijifunza jambo muhimu: “Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.”—1 Samweli 16:1-13.

Kwa kuwa kutotii kwa Sauli kulimtia Samweli uchungu, bila shaka alihuzunika zaidi kumwona akisitawisha chuki kumwelekea Daudi na kutaka kumuua! Ingawa alikabili majaribu hayo, Samweli aliendelea kuwa mwenye bidii hata alipokuwa amezeeka, naye alifanya yote aliyoweza katika utumishi wa Yehova.—1 Samweli 19:18-20.

Uvutano Mzuri wa Samweli

Samweli alipokufa, Waisraeli walimwombolezea nabii huyo mnyenyekevu na mwenye ujasiri ambaye alikuwa na uvutano mzuri katika maisha ya watu wengi. (1 Samweli 25:1) Samweli hakuwa mkamilifu, na nyakati nyingine alikosea katika maamuzi. Hata hivyo, ingawa alikuwa na udhaifu, Samweli alijitoa kikamili kwa Yehova naye alijitahidi bila kuchoka kuwasaidia wengine wafanye hivyo.

Mambo mengi yamebadilika tangu siku za Samweli, lakini masimulizi ya maisha yake yanatufunza mambo muhimu. Zaidi ya yote, Samweli aliendeleza na kuishi kupatana na ibada ya kweli ya Yehova. Je, hivyo ndivyo unavyofanya?

[Sanduku katika ukurasa wa 16]

FIKIRIA MAISHA YA SAMWELI

• Walee watoto wako katika “nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” kama vile wazazi wa Samweli walivyomfundisha neno la Mungu.—Waefeso 6:4.

• Watie moyo watoto wako wawe kama Samweli kwa kujiwekea mradi wa kumtumikia Yehova maishani.

• Alionyesha sifa za kimungu ambazo zilimfanya apendwe na wengine, na hivyo akatuwekea mfano mzuri.

• Samweli alifanya yote aliyoweza ili kuendeleza ibada ya kweli, nasi pia tunapaswa kufanya hivyo.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Samweli aliendeleza ibada ya kweli na alikuwa tayari kuwasaidia wengine kiroho